-
Tusalije kwa Mungu?Mnara wa Mlinzi—1996 | Julai 15
-
-
MWANAFUNZI alipoomba maagizo kuhusu sala, Yesu hakukataa kumpa. Kulingana na Luka 11:2-4, alijibu hivi: “Mnaposali, semeni: ‘Baba! Jina lako litukuzwe; utawala [“ufalme,” NW] wako ufike. Utupe daima chakula chetu cha kila siku. Utusamehe dhambi zetu, maana sisi tunawasamehe wote waliotukosea; na usitutie katika majaribu.’” (Habari Njema Kwa Watu Wote) Hiyo ndiyo ijulikanayo kwa kawaida kuwa Sala ya Bwana. Inajulisha habari nyingi sana.
-
-
Tusalije kwa Mungu?Mnara wa Mlinzi—1996 | Julai 15
-
-
Mwanzoni, neno la kwanza kabisa hutuambia ni nani apaswaye kuelekezewa sala zetu—Baba yetu. Ona kwamba Yesu hakuruhusu hata kidogo kusali kwa mtu mwingine, mfano, “mtakatifu,” au hata kwake mwenyewe. Kwa vyovyote, Mungu alikuwa ametangaza hivi: “Utukufu wangu sitampa mwingine, wala sitawapa sanamu sifa zangu.” (Isaya 42:8) Kwa hiyo sala zielekezwazo kwa kitu kingine chochote au mtu mwingine yeyote badala ya Baba yetu wa kimbingu hazisikiwi na yeye, hata mwabudu awe mwenye moyo mweupe kadiri gani. Katika Biblia, ni Yehova Mungu tu aitwaye “Msikiaji wa sala.”—Zaburi 65:2, NW.
Wengine huenda wakasema kwamba “watakatifu” hutenda wakiwa waombezi tu kwa Mungu. Lakini Yesu mwenyewe aliagiza hivi: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Nanyi mkiomba lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana.” (Yohana 14:6, 13) Kwa njia hiyo, Yesu aliondolea mbali lile wazo kwamba mtu yeyote aitwaye mtakatifu angeweza kutumikia katika fungu la mwombezi. Ona pia yale aliyosema mtume Paulo kumhusu Kristo: “Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” “Aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.”—Warumi 8:34; Waebrania 7:25.
Jina Ambalo Lazima Litukuzwe
Maneno yaliyofuata ya sala ya Yesu yalikuwa: “Jina lako litukuzwe.” Mtu angeweza kutukuzaje, yaani, kutakasa, au kuweka kando, jina la Mungu isipokuwa alilijua na alilitumia? Mungu anatambulishwa kwa jina lake la kibinafsi Yehova zaidi ya mara 6,000 katika “Agano la Kale.”
Kielezi-chini cha Kutoka 6:3 katika Douay Version ya Katoliki chasema hivi kuhusu jina la Mungu: “Watu fulani wa kisasa wametunga jina Yehova . . . , kwani matamshi ya kweli ya jina [la Mungu], ambalo liko katika maandishi ya Kiebrania, hayajulikani sasa, kwa sababu limekuwa halitumiwi kwa muda mrefu.” Kwa hiyo New Jerusalem Bible ya Katoliki hutumia jina Yahweh. Ingawa wasomi fulani hupendelea matamshi hayo, “Yehova” ndiyo njia moja halali na iliyofuatwa muda mrefu ya kutamka jina la kimungu katika Kiswahili. Lugha nyinginezo zina njia zazo zenyewe za kulitamka jina la kimungu. Jambo kuu ni kwamba twalitumia jina hilo ili tulitukuze. Je, kanisa lako limekufundisha kutumia jina Yehova katika sala?
Mambo Yafaayo ya Kutajwa Katika Sala
Halafu Yesu akawafundisha wanafunzi wake kusali: “Ufalme wako uje.” Gospeli ya Mathayo yaongezea maneno haya: “Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ufalme wa Mungu ni serikali mikononi mwa Yesu Kristo. (Isaya 9:6, 7) Kulingana na unabii wa Biblia, upesi utaondoa serikali zote za kibinadamu na kuleta muhula wa amani ya tufe lote. (Zaburi 72:1-7; Danieli 2:44; Ufunuo 21:3-5) Kwa hiyo Wakristo wa kweli hufanya kufika kwa huo Ufalme kuwa kichwa chenye kurudiwa-rudiwa katika sala zao. Je, kanisa lako limekufundisha kufanya hivyo?
-