Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Hujui Ni Wapi Itafanikiwa!
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Julai 15
    • Mfano wa Chachu

      9, 10. (a) Yesu alikazia jambo gani katika mfano wa chachu? (b) Katika Biblia, mara nyingi chachu inawakilisha nini, na tutazungumzia swali gani linalohusiana na jinsi Yesu alivyotumia neno chachu?

      9 Nyakati nyingine wanadamu hawawezi kuona ukuzi. Katika mfano unaofuata, Yesu anakazia jambo hilo. Anasema hivi: “Ufalme wa mbinguni ni kama chachu, ambayo mwanamke alichukua na kuitia katika vipimo vikubwa vitatu vya unga, mpaka tonge lote likachacha.” (Mt. 13:33) Chachu hiyo inawakilisha nini, nayo inahusiana jinsi gani na ukuzi wa Ufalme?

      10 Katika Biblia, mara nyingi chachu inatumiwa kuwakilisha dhambi. Mtume Paulo alionyesha maana hiyo ya chachu alipozungumza kuhusu uvutano mpotovu wa mtenda-dhambi fulani katika kutaniko la jiji la kale la Korintho. (1 Kor. 5:6-8) Je, Yesu alikuwa sasa akitumia chachu kuwakilisha ukuzi wa kitu kisichofaa?

      11. Chachu ilitumiwa jinsi gani zamani katika Israeli?

      11 Kabla ya kujibu swali hilo, tunahitaji kukumbuka mambo matatu ya kweli. Kwanza, ingawa Yehova hakuruhusu chachu itumiwe katika sherehe ya Pasaka, nyakati nyingine alikubali dhabihu ambazo zilikuwa na chachu. Chachu ilitumiwa katika matoleo ya ushirika ya kuonyesha shukrani, ambayo mtu alitoa kwa kupenda ili kumshukuru Yehova kwa sababu ya baraka zake nyingi. Mlo huo uliwaletea shangwe wale walioushiriki.—Law. 7:11-15.

      12. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Biblia inavyotumia mifano?

      12 Pili, ingawa nyakati nyingine kitu fulani katika Maandiko kinaweza kuwakilisha jambo lisilofaa, nyakati nyingine kitu hichohicho kinaweza kutumiwa kuwakilisha jambo linalofaa. Kwa mfano, katika 1 Petro 5:8, Shetani anafananishwa na simba, kuonyesha kwamba yeye ni hatari na mkatili. Lakini katika Ufunuo 5:5, Yesu anafananishwa na simba—“Simba ambaye ni wa kabila la Yuda.” Katika mfano huo wa pili, simba anatumiwa kuwakilisha haki yenye ujasiri.

      13. Mfano wa Yesu wa chachu unaonyesha nini kuhusu ukuzi wa kiroho?

      13 Tatu, katika mfano wa Yesu, hakusema kwamba chachu iliharibu tonge lote la unga, na kuufanya usiweze kutumiwa. Alikuwa tu akizungumzia njia ya kawaida ya kuoka mikate. Mwanamke huyo aliongeza kimakusudi chachu, na matokeo yakawa mazuri. Chachu hiyo ilitiwa katika tonge lote la unga. Hivyo, mwanamke huyo hangeweza kuona chachu hiyo ikifanya kazi. Hilo linatukumbusha mtu aliyepanda mbegu na kulala usingizi usiku. Yesu alisema kwamba “mbegu huota na hukua na kuwa ndefu, naye [mtu huyo] hajui ni jinsi gani hasa.” (Marko 4:27) Hiyo ni njia rahisi kama nini ya kuonyesha jinsi mtu anavyokua kiroho hatua kwa hatua kwa njia isiyoonekana! Huenda mwanzoni tusione ukuzi huo, lakini mwishowe matokeo yake yanaonekana wazi.

      14. Ni jambo gani kuhusu kazi ya kuhubiri linalokaziwa na uhakika wa kwamba chachu inachachusha tonge lote?

      14 Wanadamu hawaoni ukuzi huo, lakini unaenea duniani pote. Hilo ni jambo lingine linalokaziwa na mfano wa chachu. Chachu inachachusha tonge lote, ‘vipimo vyote vitatu vikubwa vya unga.’ (Luka 13:21) Kama chachu, kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ambayo imetokeza ukuzi huo wa kiroho imepanuka hivi kwamba ujumbe wa Ufalme unahubiriwa sasa “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; Mt. 24:14) Ni pendeleo kubwa kama nini kuchangia ukuzi huo wenye kustaajabisha wa kazi ya Ufalme!

  • Hujui Ni Wapi Itafanikiwa!
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Julai 15
    • Kama ile chachu isiyoonekana ilivyoenea katika tonge lote, nyakati nyingine ukuzi huo hauonekani waziwazi wala kueleweka, lakini unatukia!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki