-
Kuzaliwa Upya—Jinsi Gani?Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 1
-
-
Yesu alisema: “Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:5) Hivyo, mtu anazaliwa tena kwa maji na roho. Lakini maneno “maji na roho” yanarejelea nini?
Maana ya “Maji na Roho”
Kwa kuwa Nikodemo alikuwa msomi wa Dini ya Kiyahudi, hapana shaka alijua jinsi Maandiko ya Kiebrania yanavyotumia maneno “roho ya Mungu”—nguvu za utendaji za Mungu zinazoweza kuwafanya watu watende maajabu. (Mwanzo 41:38; Kutoka 31:3; 1 Samweli 10:6) Kwa hiyo, Yesu alipotumia neno “roho,” Nikodemo alielewa kwamba alimaanisha roho takatifu, yaani, nguvu za utendaji za Mungu.
Yesu alimaanisha nini alipotaja maji? Angalia matukio yanayotangulia na yanayofuata mazungumzo ya Yesu na Nikodemo. Yanaonyesha kwamba Yohana Mbatizaji na wanafunzi wa Yesu walibatiza kwa maji. (Yohana 1:19, 31; 3:22; 4:1-3) Ubatizo huo ulijulikana sana huko Yerusalemu. Kwa hiyo, Yesu alipotaja maji, Nikodemo alitambua kwamba alikuwa akizungumza kuhusu maji ya ubatizo bali si maji tu kwa ujumla.a
Kubatizwa “kwa Roho Takatifu”
Ikiwa “kuzaliwa kwa maji” kunahusiana na kubatizwa kwa maji, ‘kuzaliwa kwa roho’ kunamaanisha nini? Kabla ya mazungumzo ya Nikodemo na Yesu, Yohana Mbatizaji alikuwa ametangaza kwamba maji na pia roho ingetumika katika kubatiza. Alisema: “Mimi niliwabatiza ninyi kwa maji, lakini yeye [Yesu] atawabatiza ninyi kwa roho takatifu.” (Marko 1:7, 8) Mwandikaji wa Injili anayeitwa Marko anataja wakati wa kwanza ambapo ubatizo wa aina hiyo ulifanywa. Anaandika: “Baada ya siku hizo Yesu akaja kutoka Nazareti ya Galilaya, Yohana akambatiza katika Yordani. Mara moja alipopanda kutoka majini akaona mbingu zikifunguka, na roho ikashuka juu yake kama njiwa.” (Marko 1:9, 10) Yesu alipozamishwa katika Mto Yordani, alibatizwa kwa maji. Mara alipopokea roho kutoka mbinguni, alibatizwa kwa roho takatifu.
Miaka mitatu hivi baada ya kubatizwa, Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake hivi: “Ninyi mtabatizwa kwa roho takatifu siku chache baadaye.” (Matendo 1:5) Walibatizwa kwa roho wakati gani?
Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wa Yesu wapatao 120 walikuwa wamekusanyika katika nyumba fulani huko Yerusalemu. “Ghafula kukatokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote ambamo walikuwa wameketi. Nao wakaona ndimi kama za moto . . . , nao wote wakajazwa roho takatifu.” (Matendo 2:1-4) Siku hiyohiyo, watu wengine huko Yerusalemu walihimizwa wabatizwe kwa maji. Mtume Petro aliuambia umati hivi: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.” Watu hao walifanya nini? “Wale waliokubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo wakabatizwa, na katika siku hiyo nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa.”—Matendo 2:38, 41.
Kubatizwa kwa Njia Mbili
Ubatizo wa maji na wa roho takatifu unafunua nini kuhusu kuzaliwa upya? Unaonyesha kwamba mtu anahitaji kubatizwa kwa njia mbili ili azaliwe upya. Ona kwamba Yesu alibatizwa kwanza kwa maji. Kisha akapokea roho takatifu. Vivyo hivyo, wanafunzi wa kwanza walibatizwa kwanza kwa maji (baadhi yao na Yohana Mbatizaji), kisha wakapokea roho takatifu. (Yohana 1:26-36) Pia, wale wanafunzi wapya 3,000 walibatizwa kwanza kwa maji, kisha wakapokea roho takatifu.
Tunapozingatia kwamba wanafunzi wapya walibatizwa kwa njia mbili siku ya Pentekoste 33 W.K., tutatarajia mtu azaliwe upya kwa njia gani leo? Katika njia ileile ambayo mitume wa Yesu na wanafunzi wake wa kwanza walizaliwa upya. Kwanza mtu anatubu dhambi zake, anageuka na kuacha mwenendo mbaya, anajiweka wakfu kwa Yehova ili kumwabudu na kumtumikia, na kuonyesha hadharani kwamba amejiweka wakfu kwa kubatizwa kwa maji. Kisha, Mungu akimchagua kuwa mtawala katika Ufalme Wake, anamtia mafuta kwa roho takatifu. Mtu mwenyewe ndiye anayechukua hatua ya kwanza ya kubatizwa kwa maji, lakini Mungu ndiye anayechukua hatua ya pili ya kumbatiza kwa roho. Hivyo, mtu anazaliwa upya anapobatizwa katika njia zote mbili.
Lakini kwa nini Yesu alitumia maneno ‘kuzaliwa kwa maji na roho’ alipozungumza na Nikodemo? Alikuwa akikazia kwamba hali ya wale wanaobatizwa kwa maji na kwa roho inabadilika sana. Habari inayofuata inazungumzia badiliko hilo linalotokana na kuzaliwa upya.
[Maelezo ya chini]
a Vivyo hivyo, pindi moja mtume Petro alisema hivi kuhusu watu waliotaka kubatizwa: “Je, mtu yeyote anaweza kuyakataza maji?”—Matendo 10:47.
-
-
Kuzaliwa Upya—Kunatimiza Nini?Mnara wa Mlinzi—2009 | Aprili 1
-
-
Kuzaliwa Upya—Kunatimiza Nini?
KWA nini Yesu alitumia maneno ‘kuzaliwa kwa roho’ alipozungumzia kubatizwa kwa roho takatifu? (Yohana 3:5) Neno “kuzaliwa” linapotumiwa kwa njia ya mfano linamaanisha “mwanzo.” Hivyo, maneno “kuzaliwa upya” yanamaanisha “mwanzo mpya.” Kwa hiyo, maneno ya mfano “kuzaliwa” na “kuzaliwa upya” yanakazia kwamba uhusiano kati ya Mungu na wale wanaobatizwa kwa roho takatifu utakuwa na mwanzo mpya. Badiliko hilo katika uhusiano linatokea jinsi gani?
Alipoeleza jinsi Mungu anavyowatayarisha wanadamu ili watawale mbinguni, mtume Paulo alitumia mfano wa familia. Aliwaandikia Wakristo wa siku zake kwamba ‘wangefanywa kuwa wana’ na kwa hiyo Mungu angewatendea “kama wana.” (Wagalatia 4:5; Waebrania 12:7) Ili kuona jinsi mfano wa kufanywa kuwa mwana unavyomsaidia mtu kuelewa badiliko linalotokea mtu anapobatizwa kwa roho takatifu, fikiria tena ule mfano wa mwanamume kijana anayetaka kujiunga na shule ya wanafunzi ambao ni watoto wa wenyeji.
Badiliko Linalotokana na Kufanywa Kuwa Mwana
Katika mfano huo, kijana huyo hawezi kujiunga na shule hiyo kwa sababu yeye si mwenyeji. Sasa, wazia kwamba siku moja, badiliko kubwa linatokea. Kijana huyo anafanywa kuwa mwana kisheria na baba katika familia ya wenyeji. Jambo hilo linaleta mabadiliko gani kwa yule kijana? Kwa sababu amefanywa kuwa mwana, sasa anaweza kuwa na haki sawa na vijana wenyeji—kutia ndani haki ya kujiunga na ile shule. Kufanywa kuwa mwana kisheria kumebadili kabisa maisha yake.
Jambo hilo linafanana na yale yanayowapata wale wanaozaliwa upya, ingawa kwa njia kubwa zaidi. Fikiria mambo kadhaa yanayofanana. Yule kijana katika mfano atakubaliwa katika ile shule mradi tu atimize takwa la kujiunga na shule hiyo, yaani, kuwa mwenyeji kisheria. Lakini hawezi kutimiza takwa hilo bila msaada. Vivyo hivyo, wanadamu fulani watakuwa watawala katika Ufalme wa Mungu, au serikali ya mbinguni, mradi tu watimize takwa la kuingia humo, yaani, “kuzaliwa tena.” Hata hivyo, hawawezi kutimiza takwa hilo bila msaada kwa sababu Mungu ndiye anayefanya mtu azaliwe upya.
Ni nini kilichobadili hali ya yule kijana? Kufanywa kuwa mwana kisheria. Bila shaka, asili ya kijana yule haikubadilika alipofanywa kuwa mwana, bado alikuwa mtu yuleyule. Hata hivyo, baada ya kufanywa kuwa mwana kisheria, hali ya kijana huyo ilibadilika. Alikuwa na mwanzo mpya, kana kwamba amezaliwa upya. Alikubaliwa kuwa mwana kisheria, jambo lililompa haki ya kujiunga na ile shule na pia kuwa mtoto wa familia ya yule baba aliyemfanya kuwa mwana.
Vivyo hivyo, Yehova alibadili hali ya wanadamu wasio wakamilifu kwa kuanzisha mpango wa kisheria wa kuwafanya kuwa watoto wake. Mtume Paulo aliyekuwa mmoja wa watoto hao aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Mlipokea roho ya kufanywa kuwa wana, roho ambayo kupitia hiyo tunapaaza sauti: ‘Abba, Baba!’ Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu.” (Waroma 8:15, 16) Ndiyo, kwa kufanywa kuwa wana, Wakristo hao walifanywa kuwa sehemu ya familia ya Mungu, au “watoto wa Mungu.”—1 Yohana 3:1; 2 Wakorintho 6:18.
Kusema kweli, asili ya wale ambao Mungu aliwafanya kuwa wana haikubadilika, kwa kuwa bado walikuwa watu wasio wakamilifu. (1 Yohana 1:8) Hata hivyo, kama Paulo alivyoendelea kueleza, baada ya matakwa ya kisheria ya kufanywa kuwa wana kutimizwa, hali yao ilibadilika. Wakati huohuo, roho ya Mungu iliwapa usadikisho wenye nguvu sana kwamba wangeishi mbinguni pamoja na Kristo. (1 Yohana 3:2) Usadikisho huo waliopewa na roho takatifu uliwafanya wawe na maoni tofauti kabisa kuhusu maisha. (2 Wakorintho 1:21, 22) Ndiyo, walikuwa na mwanzo mpya—walizaliwa upya kwa njia ya mfano.
-