-
“Alitupenda Sisi Kwanza”Mkaribie Yehova
-
-
Tendo Kuu Zaidi la Upendo
4. Askari Mroma alipataje kujua kwamba Yesu hakuwa mtu wa kawaida, naye alikata kauli gani?
4 Askari Mroma aliyesimamia mauaji ya Yesu alipigwa na bumbuazi alipoona giza lililotokea kabla ya Yesu kufa na tetemeko kubwa la dunia lililotokea baadaye. Alisema hivi: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Mathayo 27:54) Ni wazi kwamba Yesu hakuwa mtu wa kawaida. Askari huyo aliunga mkono mauaji ya Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu Mwenyezi! Mwana huyo alipendwa na Baba yake kwa kadiri gani?
5. Ni mfano gani umetolewa ili kutusaidia kuelewa kwamba Yehova na Mwanaye wamekuwa pamoja mbinguni kwa muda mrefu sana?
5 Biblia inamwita Yesu “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” (Wakolosai 1:15) Hebu fikiria—Mwana wa Yehova alikuwapo kabla ya ulimwengu kuumbwa. Basi, Mwana huyo alikaa na Baba yake kwa muda gani? Wanasayansi fulani wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo kwa muda wa miaka bilioni 13. Huo ni muda usiowazika, sivyo? Ili kuwasaidia watu waelewe muda ambao wanasayansi wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo, jengo moja lenye mitambo ya kuigiza miendo ya sayari lina chati ya tarehe yenye urefu wa meta 110. Wageni wanapotembea kando ya chati hiyo, kila hatua wanayopiga inawakilisha miaka ipatayo milioni 75 ya muda ambao ulimwengu umekuwapo. Alama ndogo inayolingana na unene wa unywele wa mwanadamu imewekwa mwishoni mwa chati hiyo ili kuwakilisha muda ambao wanadamu wameishi duniani! Lakini, hata ikiwa makisio hayo ni sahihi, urefu wa chati hiyo hauwezi kamwe kuwakilisha umri wa Mwana wa Yehova! Alikuwa akifanya kazi gani wakati huo wote?
6. (a) Mwana wa Yehova alikuwa akifanya nini kabla ya kuwa mwanadamu? (b) Yehova na Mwanaye wanaunganishwa na kifungo cha aina gani?
6 Mwana huyo alifurahi kutumiwa na Baba yake akiwa “stadi wa kazi.” (Mithali 8:30) Biblia inasema hivi: “Na bila yeye [Mwana] hata kitu kimoja hakikuja kuwako.” (Yohana 1:3) Kwa hiyo Yehova na Mwanaye walishirikiana kuumba vitu vingine vyote. Walikuwa na kazi zenye kuvutia na kufurahisha kwelikweli. Watu wengi hukubali kwamba mzazi na mtoto hupendana sana. Na upendo “ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Basi, ni nani kati yetu anayeweza kuelewa kwa ukamili nguvu za kifungo ambacho kimekuwapo kwa muda mrefu hivyo? Ni wazi kwamba Yehova Mungu na Mwanaye wameunganishwa na kifungo cha upendo chenye nguvu kuliko kifungo chochote kile.
7. Yesu alipobatizwa, Yehova alionyeshaje hisia zake kumwelekea?
7 Hata hivyo, Baba alimtuma Mwanaye duniani ili azaliwe akiwa mwanadamu. Kwa hivyo, Yehova hakuweza kushirikiana kwa ukaribu na Mwanaye mpendwa huko mbinguni kwa miaka kadhaa. Akiwa mbinguni, Yehova alipendezwa sana kumtazama Yesu akikua hadi akawa mwanamume mkamilifu. Yesu alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi. Tunajua jinsi Yehova Baba yake alivyohisi kumhusu, hata alisema moja kwa moja kutoka mbinguni: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Bila shaka Baba ya Yesu alifurahi sana kumwona akifanya kwa uaminifu yote yaliyotabiriwa, mambo yote ambayo alipaswa kufanya!—Yohana 5:36; 17:4.
8, 9. (a) Yesu alitendewaje Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., na Baba yake wa mbinguni alihisije? (b) Kwa nini Yehova alimruhusu Mwanaye ateseke na kufa?
8 Hata hivyo, Yehova alihisije Nisani 14, mwaka wa 33 W.K.? Alihisije Yesu aliposalitiwa na kukamatwa na umati usiku? Alihisije Yesu alipoachwa na rafiki zake na kushtakiwa isivyo haki? Alihisije Yesu alipodhihakiwa, kutemewa mate, na kupigwa ngumi? Alihisije alipopigwa mijeledi iliyochanachana mgongo wake? Alihisije mikono na miguu yake ilipopigiliwa misumari kwenye mti, kisha akaachwa akiwa amening’inia huku watu wakimtukana? Baba alihisije Mwanaye mpendwa alipokuwa akimlilia kwa maumivu makali? Yehova alihisije Yesu alipokata pumzi, na kwa mara ya kwanza kabisa tangu mwanzo wa uumbaji wote, Mwanaye mpendwa akakoma kuwapo?—Mathayo 26:14-16, 46, 47, 56, 59, 67; 27:38-44, 46; Yohana 19:1.
’Mungu alitoa Mwana wake mzaliwa pekee’
9 Hatuna la kusema. Kwa kuwa Yehova ana hisia, hatuwezi kamwe kueleza uchungu ambao alihisi kwa sababu ya kifo cha Mwanaye. Lakini tunaweza kueleza kusudi la Yehova la kuruhusu jambo hilo litukie. Kwa nini Baba ya Yesu alijiruhusu kupatwa na uchungu huo? Yehova anatueleza jambo la kupendeza katika Yohana 3:16—mstari huu wa Biblia ni muhimu sana hivi kwamba umeitwa Injili ndogo. Andiko hilo lasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” Kwa hiyo, Yehova alifanya hivyo kwa sababu ya upendo. Zawadi ambayo Yehova alitoa—kumtuma Mwanaye ateseke na kufa kwa ajili yetu—ndiyo tendo kuu zaidi la upendo ambalo limewahi kufanywa.
-
-
“Alitupenda Sisi Kwanza”Mkaribie Yehova
-
-
12 A·gaʹpe ni upendo unaoongozwa na kanuni. Si hisia tunayokuwa nayo bila kufikiri. Upendo huo unatia ndani mambo mengi, unahusisha fikira na una kusudi fulani. Zaidi ya yote, upendo wa a·gaʹpe hauna ubinafsi. Kwa mfano, soma tena Yohana 3:16. Ni “ulimwengu” upi ambao Mungu aliupenda sana hivi kwamba akamtoa Mwanaye mzaliwa-pekee? Ulimwengu huo ni wanadamu wanaoweza kukombolewa. Unatia ndani watu wengi ambao wanaendelea kutenda dhambi maishani. Je, Yehova anampenda kila mtu kama alivyompenda Abrahamu mwaminifu, aliyekuwa rafiki yake? (Yakobo 2:23) La, lakini kwa upendo, Yehova anawatendea watu wote mema hata kwa hasara yake. Anataka watu wote watubu na kubadili njia zao. (2 Petro 3:9) Wengi hufanya hivyo. Naye hufurahi kuwa rafiki yao.
-