Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wanaume—Je, Mnajitiisha Chini ya Ukichwa wa Kristo?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Mei 15
    • Wanaume—Je, Mnajitiisha Chini ya Ukichwa wa Kristo?

      “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.”—1 KOR. 11:3.

      1. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova ni Mungu mwenye utaratibu?

      ANDIKO la Ufunuo 4:11 linasema hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Kwa kuwa Yehova Mungu ni Muumba, yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote naye ana mamlaka juu ya vitu vyote alivyoumba. Tukiangalia mpangilio wa familia yake ya malaika, tunaona wazi kwamba Yehova “si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.”—1 Kor. 14:33; Isa. 6:1-3; Ebr. 12:22, 23.

      2, 3. (a) Yehova alimuumba nani kwanza? (b) Mwana mzaliwa wa kwanza ana cheo gani kikilinganishwa na cheo cha Baba?

      2 Mungu aliishi peke yake kwa miaka isiyohesabika kabla hajaumba kitu chochote. Yehova aliumba kwanza kiumbe wa roho anayeitwa “Neno” kwa sababu alikuwa Msemaji wake. Vitu vingine vyote viliumbwa kupitia huyo Neno. Baadaye, msemaji huyo alikuja duniani akawa mwanadamu mkamilifu ambaye aliitwa Yesu Kristo.—Soma Yohana 1:1-3, 14.

      3 Maandiko yanasema nini kuhusu cheo cha Mungu kikilinganishwa na cheo cha Mwana wake mzaliwa wa kwanza? Akiandika chini ya mwongozo wa roho takatifu, mtume Paulo anatuambia hivi: “Nataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Kor. 11:3) Kristo yuko chini ya ukichwa wa Baba yake. Ukichwa na kujitiisha ni mambo ya maana sana ili kuwe na amani na utaratibu kati ya viumbe wenye akili. Hata yule ambaye “kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa” anatakiwa ajitiishe chini ya ukichwa wa Mungu.—Kol. 1:16.

      4, 5. Yesu alihisi namna gani kuhusu cheo chake kikilinganishwa na cheo cha Yehova?

      4 Yesu alihisi namna gani kuhusu kujitiisha chini ya ukichwa wa Yehova na kuja duniani? Maandiko yanasema hivi: “Kristo Yesu, ambaye, ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu. Hapana, bali alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu. Zaidi ya hayo, alipojikuta katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.”—Flp. 2:5-8.

      5 Nyakati zote, Yesu alijitiisha kwa unyenyekevu chini ya mapenzi ya Baba yake. Yesu alisema hivi: “Mimi siwezi kufanya lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; . . . hukumu ninayotoa ni ya uadilifu, kwa sababu ninatafuta, si mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi yake aliyenituma.” (Yoh. 5:30) Pia, alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza [Baba yangu].” (Yoh. 8:29) Karibu mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alisema hivi katika sala kwa Baba yake: “Nimekutukuza duniani, nikiwa nimemaliza kazi ambayo umenipa niifanye.” (Yoh. 17:4) Ni wazi kwamba Yesu alitambua na kukubali ukichwa wa Mungu bila tatizo.

      Mwana Alifaidika kwa Kujitiisha Chini ya Baba

      6. Ni sifa gani nzuri sana ambazo Yesu alionyesha?

      6 Yesu alipokuwa duniani alionyesha sifa nyingi nzuri sana. Kwa mfano, alimpenda sana Baba yake. Alisema hivi: “Ninampenda Baba.” (Yoh. 14:31) Alionyesha pia upendo mkubwa kwa watu. (Soma Mathayo 22:35-40.) Yesu alikuwa mwenye fadhili na mwenye kujali, hakuwa mkali au hakuwakandamiza watu. Alisema hivi: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Watu wenye umri mbalimbali ambao walikuwa mfano wa kondoo, hasa wale waliokandamizwa na kuonewa, walifarijiwa sana na utu wenye kuvutia wa Yesu na ujumbe wake wenye kutia moyo.

      7, 8. Chini ya Sheria, mwanamke mwenye mtiririko wa damu aliwekewa vizuizi gani, lakini Yesu alimtendea jinsi gani?

      7 Fikiria jinsi Yesu alivyowatendea wanawake. Katika historia yote, wanaume wengi wamewatendea wanawake vibaya sana. Viongozi wa kidini katika Israeli la kale waliwatendea wanawake vivyo hivyo. Lakini Yesu aliwatendea wanawake kwa heshima. Tunaona hilo wazi kutokana na jinsi alivyomtendea mwanamke ambaye alikuwa na ugonjwa wa kutiririka damu kwa miaka 12. “Alikuwa ameumizwa sana” na matabibu au madaktari wengi na alikuwa ametumia mali zake zote ili aponywe. Hata hivyo, ingawa alijitahidi kabisa kupata matibabu ‘hali yake ilikuwa mbaya zaidi.’ Chini ya Sheria, alionwa kuwa asiye safi. Mtu yeyote aliyemgusa angekuwa pia asiye safi.—Law. 15:19, 25.

      8 Mwanamke huyo aliposikia kwamba Yesu anaponya wagonjwa, alijiunga na umati uliokuwa ukimzunguka, huku akisema hivi: “Nikiyagusa tu mavazi yake ya nje nitapona.” Alimgusa Yesu na mara moja akapona. Yesu alijua kwamba mwanamke huyo hakupaswa kugusa vazi lake. Hata hivyo, Yesu hakumkemea. Badala yake, alimtendea kwa fadhili. Alielewa jinsi mwanamke huyo alivyohisi baada ya kuwa mgonjwa kwa miaka mingi sana na alitambua kwamba mwanamke huyo alihitaji sana msaada. Yesu alimwambia hivi kwa huruma: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, na uwe na afya njema.”—Marko 5:25-34.

      9. Wanafunzi wa Yesu walipojaribu kuwazuia watoto kumkaribia, alitenda jinsi gani?

      9 Hata watoto walistarehe walipokuwa na Yesu. Pindi moja, watu walipomletea watoto, wanafunzi wake waliwakemea, inaonekana walifikiri kwamba Yesu hangetaka kusumbuliwa na watoto. Lakini Yesu hakuhisi hivyo. Simulizi hilo la Maandiko linatuambia hivi: “Alipoona hilo, Yesu akaghadhibika na kuwaambia [wanafunzi]: ‘Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.’” Kisha, “akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.” Yesu hakuvumilia tu kukaa na watoto; aliwakaribisha kwa uchangamfu.—Marko 10:13-16.

      10. Yesu alijifunza kutoka kwa nani sifa ambazo alionyesha?

      10 Yesu alijifunza kutoka kwa nani sifa ambazo alionyesha katika maisha yake duniani? Kabla ya kuwa mwanadamu, alimtazama Baba yake wa mbinguni kwa miaka mingi sana naye akajifunza njia zake. (Soma Methali 8:22, 23, 30.) Akiwa mbinguni, aliona jinsi Yehova alivyotumia ukichwa wake kwa njia ya upendo juu ya viumbe Wake wote naye akaiga sifa hiyo. Je, Yesu angeweza kufanya hivyo ikiwa hakuwa tayari kujitiisha? Alifurahia kujitiisha kwa Baba yake, naye Yehova alifurahi sana kuwa na Mwana anayejitiisha. Alipokuwa duniani, Yesu aliiga kikamili sifa bora za Baba yake wa mbinguni. Ni pendeleo kama nini kwetu kujitiisha kwa Kristo, Mtawala wa Ufalme wa mbinguni aliyewekwa rasmi na Mungu!

      Iga Sifa za Kristo

      11. (a) Tunapaswa kujitahidi sana kumwiga nani? (b) Kwa nini wanaume hasa walio katika kutaniko wanapaswa kujitahidi kumwiga Yesu?

      11 Watu wote katika kutaniko la Kikristo, hasa wanaume, wanapaswa kuendelea kujitahidi kuiga sifa za Kristo. Kama tulivyoona, Biblia inatangaza hivi: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.” Wanaume Wakristo wanapaswa kujitahidi kuiga kichwa chao, Kristo, kama vile Kristo alivyomwiga Mungu wa kweli ambaye ni Kichwa chake. Mtume Paulo alifanya hivyo alipogeuka na kuwa Mkristo. Aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Kor. 11:1) Naye mtume Petro alisema: “Mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Pet. 2:21) Himizo la kumwiga Kristo linawahusu hasa wanaume kwa sababu nyingine. Kwa sababu hao ndio wanaowekwa kuwa wazee na watumishi wa huduma. Kama Yesu alivyopata shangwe kwa kumwiga Yehova, ndivyo wanaume Wakristo wanavyopaswa kupata shangwe katika kumwiga Kristo na sifa zake.

      12, 13. Wazee wanapaswa kuwatendea jinsi gani kondoo walio chini ya utunzaji wao?

      12 Wazee katika kutaniko la Kikristo wana wajibu wa kujifunza kuwa kama Kristo. Petro aliwahimiza hivi wanaume wazee, au wazee wa kutaniko: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; wala si kama kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.” (1 Pet. 5:1-3) Wazee Wakristo hawapaswi kuwa madikteta, wenye kukandamiza au wasiojali kondoo, au kuwa wakali. Wanaiga mfano wa Kristo kwa kujitahidi kuwa wenye upendo, wenye kujali, wanyenyekevu, na kuwatendea kwa fadhili kondoo walio chini ya utunzaji wao.

      13 Wale wanaoongoza katika kutaniko ni wanaume wasio wakamilifu, na hivyo wanapaswa sikuzote kukumbuka udhaifu huo. (Rom. 3:23) Kwa hiyo, wanapaswa kuwa na hamu kubwa ya kujifunza kumhusu Yesu na kuiga upendo wake. Wanahitaji kutafakari kuhusu jinsi Mungu na Kristo wanavyoshughulika na watu na kisha wajitahidi kuwaiga. Petro anatuhimiza hivi: “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu wa akili kuelekeana ninyi wenyewe, kwa sababu Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”—1 Pet. 5:5.

      14. Wazee wanapaswa kuwaheshimu wengine kwa kadiri gani?

      14 Wanaume waliowekwa rasmi katika kutaniko wanapaswa kuonyesha sifa nzuri wanaposhughulika na kundi la Mungu. Andiko la Waroma 12:10 linasema hivi: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” Wazee na watumishi wa huduma wanawaheshimu wengine. Kama Wakristo wote kwa ujumla, wanaume hao hawapaswi ‘kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili wakiwaona wengine kuwa ni bora kuliko wao.’ (Flp. 2:3) Bila shaka, wale wanaoongoza wanapaswa kuwaona wengine kuwa ni bora kuliko wao. Wakifanya hivyo, wanaume hao waliowekwa rasmi watakuwa wakifuata shauri hili la Paulo: “Ingawa hivyo, sisi tulio na nguvu tunapaswa kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu, na tusiwe tukijipendeza wenyewe. Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake. Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.”—Rom. 15:1-3.

      ‘Kuwapa Wake Heshima’

      15. Waume wanapaswa kuwatendea wake zao namna gani?

      15 Sasa fikiria shauri la Petro kwa wanaume ambao wameoa. Aliandika hivi: “Enyi waume, endeleeni kukaa [na wake zenu] vivyo hivyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke.” (1 Pet. 3:7) Kumheshimu mtu kunamaanisha kumwona mtu huyo kuwa wa maana sana. Hivyo, utafikiria maoni, mahitaji, na mambo ambayo mtu huyo anataka na unaweza kukubali maoni yake ikiwa hakuna sababu yoyote nzuri ya kukataa maoni hayo. Hivyo ndivyo mume anavyopaswa kumtendea mke wake.

      16. Neno la Mungu linatoa onyo gani kwa waume kuhusu kuwaheshimu wake zao?

      16 Petro anapowaambia waume wawaheshimu wake zao, anaongezea onyo hili: “Kusudi sala zenu zisizuiwe.” (1 Pet. 3:7) Hilo linaonyesha wazi kwamba jinsi mwanamume anavyomtendea mke wake ni jambo zito machoni pa Yehova. Mume akikosa kumheshimu mke wake sala zake zinaweza kuzuiwa. Zaidi ya hayo, je, si ni kweli kwamba wake kwa ujumla wanaitikia vizuri wanapotendewa kwa heshima na waume zao?

      17. Mume anapaswa kumpenda mke wake kwa kadiri gani?

      17 Neno la Mungu linashauri hivi kuhusu mume kumpenda mke wake: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. . . . Kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo, kama vile Kristo pia anavyolitendea kutaniko . . . Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe.” (Efe. 5:28, 29, 33) Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kwa kadiri gani? Paulo aliandika hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Efe. 5:25) Ndiyo, mume anapaswa kuwa tayari hata kufa kwa ajili ya mke wake, kama vile Kristo alivyokufa kwa ajili ya wengine. Mume Mkristo anapomtendea mke wake kwa wororo, fadhili, uangalifu, na bila uchoyo, inakuwa rahisi zaidi kwa mke wake kujitiisha chini ya ukichwa wake.

      18. Ni msaada gani ambao wanaume wanaweza kupata ili watimize madaraka yao katika ndoa?

      18 Je, ni vigumu sana kwa waume kuwaheshimu wake zao kwa njia hiyo? Hapana, Yehova hangeweza kamwe kuwaambia wafanye jambo ambalo hawawezi kufanya. Zaidi ya hayo, waabudu wa Yehova wanaweza kupata nguvu kuu zaidi katika ulimwengu wote—roho takatifu ya Mungu. Yesu alisema hivi: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:13) Waume wanaweza kumwomba Yehova katika sala awape roho yake ili iwasaidie wanaposhughulika na wengine, kutia ndani wake zao.—Soma Matendo 5:32.

      19. Habari yetu inayofuata itazungumzia nini?

      19 Kwa kweli, wanaume wana daraka zito la kujifunza jinsi ya kujitiisha chini ya Kristo na kuiga ukichwa wake. Lakini namna gani wanawake, hasa wale walioolewa? Habari inayofuata itazungumzia jinsi wanavyopaswa kuona daraka lao katika mpango wa Yehova.

  • Wanawake—Kwa Nini Mjitiishe Chini ya Ukichwa?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Mei 15
    • Wanawake—Kwa Nini Mjitiishe Chini ya Ukichwa?

      “Kichwa cha mwanamke ni mwanamume.”—1 KOR. 11:3.

      1, 2. (a) Mtume Paulo aliandika nini kuhusu mpango wa Yehova wa ukichwa na kujitiisha? (b) Ni maswali au maulizo gani ambayo yatazungumziwa katika habari hii?

      YEHOVA ameweka utaratibu ambao mtume Paulo alitaja alipoandika kwamba “kichwa cha kila mwanamume ni Kristo” nacho “kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Kor. 11:3) Habari iliyotangulia ilionyesha kwamba Yesu aliona ni pendeleo na shangwe kujitiisha chini ya Kichwa chake, Yehova Mungu, na pia ilionyesha kwamba Kristo ndiye kichwa cha wanaume Wakristo. Kristo alikuwa mwenye fadhili, mpole, mwenye huruma, naye hakuwa mwenye uchoyo aliposhughulika na watu. Wanaume walio katika kutaniko wanahitaji kuwatendea wengine kwa njia hiyo, hasa wake zao.

      2 Hata hivyo, namna gani wanawake? Kichwa chao ni nani? Paulo aliandika: “Kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” Wanawake wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu? Je, bado wanapaswa kufuata kanuni hiyo ikiwa mume si mwamini? Je, kujitiisha chini ya ukichwa wa wanaume kunamaanisha kwamba mke anapaswa kunyamaza tu katika ndoa, na hapaswi kusema lolote maamuzi yanapofanywa? Mwanamke anajiletea sifa jinsi gani?

      “Nitamfanyia Msaidizi”

      3, 4. Kwa nini kufuata mpango wa ukichwa katika ndoa kuna faida?

      3 Mungu ndiye aliyeanzisha mpango wa ukichwa. Baada ya kumuumba Adamu, Yehova Mungu alisema: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.” Baada ya Hawa kuumbwa, Adamu alifurahi sana kupata mwenzi na msaidizi na akasema hivi: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu.” (Mwa. 2:18-24) Adamu na Hawa walikuwa na tarajio zuri ajabu la kuwa baba na mama wa jamii yote ya wanadamu wakamilifu, ambao wangeishi milele kwa furaha katika paradiso duniani.

      4 Kwa sababu ya uasi wa wazazi wetu wa kwanza, hali kamilifu katika bustani ya Edeni ilipotea. (Soma Waroma 5:12.) Lakini bado Mungu alimwona mume kuwa kichwa cha mke wake. Mume na mke wakifuata mpango huo kwa njia inayofaa, wanapata faida kubwa na furaha katika ndoa yao. Wanahisi kama Yesu alivyohisi kuhusu kujitiisha chini ya Kichwa chake, Yehova. Kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu ‘alifurahi mbele za Yehova wakati wote.’ (Met. 8:30) Kwa sababu ya hali ya kutokamilika, wanaume hawawezi tena kutumia ukichwa wao kwa njia kamilifu, nao wake hawawezi kujitiisha kwa ukamilifu. Hata hivyo, waume na wake wanapoendelea kujitahidi kadiri wanavyoweza, mpango wa ukichwa unaleta furaha kubwa zaidi katika ndoa wakati huu.

      5. Kwa nini wenzi wa ndoa wanapaswa kuchukua kwa uzito shauri la Waroma 12:10?

      5 Ili ndoa ifanikiwe ni lazima wenzi wa ndoa watumie shauri hili la Kimaandiko ambalo linawahusu Wakristo wote: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Rom. 12:10) Pia, mume na mke wanapaswa kujitahidi kabisa ‘kuwa wenye fadhili wao kwa wao, wenye huruma nyororo, wakisameheana kwa hiari.’—Efe. 4:32.

      Wakati Mwenzi wa Ndoa Si Mwamini

      6, 7. Matokeo yanaweza kuwa nini ikiwa mke Mkristo anajitiisha chini ya mume ambaye si mwamini?

      6 Namna gani ikiwa mwenzi wako wa ndoa si mtumishi wa Yehova? Katika visa vingi, mume ndiye asiye mwamini. Mke anapaswa kumtendea jinsi gani mume asiyemwamini? Biblia inajibu hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”—1 Pet. 3:1, 2.

      7 Neno la Mungu linamwambia mke aendelee kujitiisha chini ya mume ambaye si mwamini. Mwenendo wake mzuri unaweza kumchochea mume achunguze kile kinachomfanya mke wake ajiendeshe kwa njia nzuri hivyo. Na hilo linaweza kumfanya mume achunguze mafundisho ya mke wake Mkristo na mwishowe anaweza kukubali kweli.

      8, 9. Mke Mkristo anaweza kufanya nini ikiwa mume wake ambaye si mwamini hathamini mwenendo wake mzuri?

      8 Namna gani ikiwa mume ambaye si mwamini hathamini mwenendo mzuri wa mke wake? Maandiko yanamtia moyo mke Mkristo aonyeshe sifa za Kikristo nyakati zote, hata inapokuwa vigumu sana kufanya hivyo. Kwa mfano, tunasoma hivi kwenye 1 Wakorintho 13:4: “Upendo ni wenye ustahimilivu.” Hivyo basi, ni vizuri mke Mkristo aendelee kujiendesha kwa ‘unyenyekevu kamili wa akili na upole, na ustahimilivu,’ huku akivumilia hali hiyo kwa upendo. (Efe. 4:2) Kwa msaada wa nguvu ya utendaji ya Mungu, yaani, roho takatifu, tunaweza kuendelea kuonyesha sifa za Kikristo hata chini ya hali ngumu.

      9 Paulo aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Flp. 4:13) Roho ya Mungu inamwezesha mwenzi wa ndoa Mkristo kufanya mambo mengi ambayo hangeweza kufanya. Kwa mfano, akitendewa vibaya na mwenzi wake wa ndoa anaweza kushawishiwa kulipiza kisasi. Hata hivyo, Biblia inawaambia hivi Wakristo wote: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Rom. 12:17-19) Pia, andiko la 1 Wathesalonike 5:15 linatushauri hivi: “Angalieni kwamba mtu asimlipe mwingine yeyote ubaya kwa ubaya, bali sikuzote fuatilieni yaliyo mema kuelekea mtu na mwenzake na kwa wengine wote.” Kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova, tunaweza kufanya mambo ambayo hatuwezi kufanya kwa uwezo wetu. Inafaa kama nini kwetu kusali ili roho takatifu ya Mungu itupe nguvu tunazohitaji!

      10. Yesu alitenda jinsi gani watu waliposema au kumtendea kwa njia isiyo ya fadhili?

      10 Yesu aliweka mfano mzuri sana katika kushughulika na watu ambao walisema au kumtendea mambo mabaya. Andiko la 1 Petro 2:23 linasema: “Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.” Tunahimizwa tufuate mfano wake mzuri. Usikasirishwe na matendo mabaya ya wengine. Kama Wakristo wote wanavyoshauriwa, uwe ‘mwenye huruma nyororo, mnyenyekevu katika akili, usilipe ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano.’—1 Pet. 3:8, 9.

      Je, Mke Anapaswa Kunyamaza Tu Katika Ndoa?

      11. Wanawake fulani Wakristo watashiriki katika pendeleo gani kubwa?

      11 Je, kujitiisha kwa ukichwa wa mume kunamaanisha kwamba wanawake wanapaswa kunyamaza tu katika ndoa, na hawapaswi kusema jambo lolote kuhusu mambo ya familia au mambo mengine? Hapana. Yehova amewapa wanawake na pia wanaume mapendeleo mengi. Hebu fikiria pendeleo kubwa ambalo wale 144,000 wamepewa la kuwa wafalme na makuhani mbinguni chini ya Kristo atakapotawala juu ya dunia! Hesabu hiyo inatia ndani wanawake. (Gal. 3:26-29) Bila shaka, Yehova amewapa wanawake daraka la maana katika mpango wake wa mambo.

      12, 13. Toa mfano unaoonyesha kwamba wanawake walitoa unabii.

      12 Kwa mfano, katika nyakati za Biblia, wanawake fulani walitoa unabii. Andiko la Yoeli 2:28, 29 lilitabiri hivi: “Nitaimimina roho yangu juu ya kila namna ya mwili, na wana wenu na binti zenu watatoa unabii. . . . Na hata juu ya watumishi wa kiume na juu ya wajakazi katika siku hizo nitaimimina roho yangu.”

      13 Wanafunzi 120 hivi wa Yesu ambao walikusanyika katika chumba cha juu huko Yerusalemu katika siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., walitia ndani wanawake na wanaume pia. Roho ya Mungu ilimiminwa juu ya kikundi hicho chote. Ndiyo sababu Petro alitaja maneno yaliyotabiriwa na nabii Yoeli kuwahusu wanaume na wanawake pia. Petro alisema hivi: “Hili ndilo lililosemwa kupitia nabii Yoeli, ‘Na katika siku za mwisho,’ Mungu asema, ‘Nitaimimina sehemu ya roho yangu juu ya kila namna ya mwili, nao wana wenu na binti zenu watatoa unabii . . . ; na hata juu ya watumwa wangu na juu ya wajakazi wangu nitaimimina sehemu ya roho yangu katika siku hizo, nao watatoa unabii.’”—Mdo. 2:16-18.

      14. Wanawake walitimiza sehemu gani katika kueneza Ukristo katika karne ya kwanza?

      14 Katika karne ya kwanza, wanawake walitimiza sehemu ya maana sana katika kueneza Ukristo. Waliwahubiria wengine kuhusu Ufalme wa Mungu na walifanya mambo mengine yaliyohusiana na kazi ya kuhubiri. (Luka 8:1-3) Kwa mfano, mtume Paulo alimtaja Fibi kuwa “mhudumu wa kutaniko lililo katika Kenkrea.” Na alipotuma salamu kwa wafanyakazi wenzake, Paulo aliwataja wanawake fulani waaminifu kutia ndani “Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana.” Pia alimtaja “Persisi mpendwa wetu, kwa maana mwanamke huyo alifanya kazi nyingi katika Bwana.”—Rom. 16:1, 12.

      15. Wanawake wanatimiza sehemu gani katika kueneza Ukristo siku zetu?

      15 Katika siku zetu, kati ya watu milioni saba wanaohubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote, wengi wao ni wanawake wenye umri mbalimbali. (Mt. 24:14) Wengi kati ya wanawake hao ni wahudumu wa wakati wote, wamishonari, na Wanabetheli. Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Yehova mwenyewe anasema neno hili; wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.” (Zab. 68:11) Maneno hayo yamethibitika kuwa ya kweli! Yehova anathamini sehemu ambayo wanawake wanatimiza katika kutangaza habari njema na kutimiza makusudi yake. Bila shaka, takwa lake la kwamba wanawake wanapaswa kujitiisha halimaanishi kuwa wanapaswa kujitiisha kwa kunyamaza tu.

      Wanawake Wawili Ambao Hawakunyamaza Tu

      16, 17. Mfano wa Sara unaonyesha jinsi gani kwamba wanawake hawapaswi kunyamaza tu katika ndoa?

      16 Ikiwa Yehova anawapa wanawake mapendeleo mengi, je, waume hawapaswi kuzungumza na wake zao kabla ya kufanya maamuzi mazito? Ni jambo la hekima kwa waume kufanya hivyo. Maandiko yanataja wake fulani ambao walitoa maoni yao au walichukua hatua hata bila kuombwa maoni na waume zao. Fikiria mifano miwili.

      17 Sara, mke wa mzee wa ukoo Abrahamu, alizidi kumwambia amfukuze mke wake wa pili na mwana wake kwa sababu walikosa heshima. ‘Jambo hilo halikumpendeza Abrahamu hata kidogo,’ lakini si Mungu. Yehova alimwambia Abrahamu hivi: “Usiruhusu jambo lolote ambalo Sara anazidi kukuambia liwe lisilokupendeza juu ya huyo mvulana na juu ya kijakazi wako. Sikiliza sauti yake.” (Mwa. 21:8-12) Abrahamu alimtii Yehova, akamsikiliza Sara, naye akafanya jambo ambalo Sara aliomba.

      18. Abigaili alichukua hatua gani?

      18 Mfikirie pia Abigaili, mke wa Nabali. Daudi alipokuwa akimkimbia Mfalme Sauli mwenye wivu, alipiga kambi kwa muda karibu na makundi ya Nabali. Badala ya kuchukua kitu chochote kutoka katika vitu vingi vya mwanamume huyo tajiri, Daudi na wanaume wake walilinda mali yake. Hata hivyo, Nabali “alikuwa mkali na mwenye matendo mabaya,” naye ‘aliwakemea wanaume wa Daudi kwa sauti kali.’ Alikuwa “mtu asiyefaa kitu,” na ‘ukosefu wa akili ulikuwa pamoja naye.’ Wanaume wa Daudi walipoomba kwa heshima chakula kidogo, Nabali alikataa kuwapa. Abigaili alifanya nini aliposikia jambo lililotukia? Bila kumwambia Nabali, ‘alifanya haraka, akachukua mikate mia mbili na mitungi miwili mikubwa ya divai na kondoo watano na vipimo vitano vya sea vya nafaka iliyochomwa na keki mia moja za zabibu kavu na keki mia mbili za tini zilizoshinikizwa’ na kumpa Daudi na wanaume wake. Je, Abigaili alifanya jambo linalofaa? Biblia inasema: “Yehova akampiga Nabali, naye akafa.” Baadaye, Daudi alimwoa Abigaili.—1 Sam. 25:3, 14-19, 23-25, 38-42.

      ‘Mwanamke Anayejiletea Sifa’

      19, 20. Kwa kweli ni nini kinachomfanya mwanamke astahili kusifiwa?

      19 Maandiko yanampongeza mke anayefanya mambo kwa njia ya Yehova. Kitabu cha Biblia cha Methali kinamsifu “mke mwenye uwezo,” na kinasema hivi kumhusu: “Thamani yake inapita sana ile ya marijani. Moyo wa mume wake umemtegemea, wala hakuna faida inayokosekana. Amemthawabisha mume wake kwa mema, wala si kwa mabaya, siku zote za maisha yake.” Zaidi ya hayo, yeye “hufungua kinywa chake kwa hekima, na sheria ya fadhili zenye upendo ziko katika ulimi wake. Anaangalia shughuli za nyumba yake, wala hali mkate wa uvivu. Wanawe wamesimama na kumtangaza kuwa mwenye furaha, mume wake husimama, naye humsifu.”—Met. 31:10-12, 26-28.

      20 Kwa kweli ni nini kinachomfanya mwanamke astahili sifa? Methali 31:30 inasema: “Uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejiletea sifa.” Kumwogopa Yehova kunatia ndani kujitiisha kwa kupenda chini ya mpango wa ukichwa ulioanzishwa na Mungu. “Kichwa cha mwanamke ni mwanamume,” kama vile tu “kichwa cha kila mwanamume ni Kristo,” na “kichwa cha Kristo ni Mungu.”—1 Kor. 11:3.

      Mshukuru Mungu kwa Ajili ya Zawadi Ambayo Amekupa

      21, 22. (a) Wakristo waliofunga ndoa wana sababu gani za kumshukuru Mungu kwa ajili ya zawadi ya ndoa? (b) Kwa nini tunapaswa kuheshimu mipango ya Yehova ya mamlaka na ukichwa? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 17.)

      21 Wakristo waliofunga ndoa wana sababu nyingi sana za kumshukuru Mungu! Wanaweza kutembea bega kwa bega wakiwa wenzi wa ndoa wenye furaha. Wanapaswa hasa kumshukuru Mungu kwa kuwapa zawadi yenye baraka ya ndoa kwa sababu inawapa nafasi ya kuungana katika maisha na kutembea pamoja na Yehova. (Rut. 1:9; Mika 6:8) Akiwa ndiye Mwanzilishi wa ndoa, Yehova anajua kile tunachohitaji hasa ili tupate furaha katika ndoa. Sikuzote fanyeni mambo kwa njia yake, na ‘shangwe ya Yehova itakuwa ngome yenu,’ hata katika ulimwengu huu wenye misukosuko.—Neh. 8:10.

      22 Mume Mkristo ambaye anampenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe atatumia ukichwa wake kwa njia ya upole na fadhili. Atampenda kikweli mke wake, kwa kuwa mke huyo anayemwogopa Mungu atamuunga mkono na kumheshimu sana. Na jambo la maana hata zaidi ni kwamba ndoa yao ambayo ni mfano mzuri itamletea heshima Mungu wetu anayestahili kusifiwa, Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki