-
Njia ya Upendo Haishindwi KamweMnara wa Mlinzi—1999 | Februari 15
-
-
9. Biblia hutoa vielelezo gani vyenye kuonya vya watu waliotafuta masilahi yao wenyewe?
9 Upendo “hautafuti masilahi yao wenyewe.” (1 Wakorintho 13:5) Mtu mwenye upendo hatumii wengine kwa hila ili afanye atakayo. Biblia ina vielelezo vyenye kuonya kuhusu jambo hilo. Kutoa kielezi: Twasoma juu ya Delila, Yezebeli, na Athalia—wanawake waliotumia wengine kwa hila kwa ajili ya makusudi yao wenyewe ya kibinafsi. (Waamuzi 16:16; 1 Wafalme 21:25; 2 Mambo ya Nyakati 22:10-12) Kulikuwa pia na Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi. Alikuwa akiwaendea wale waliokuja Yerusalemu ili kupata hukumu na kwa hila kusingizia kwamba nyumba ya mfalme haikupendezwa kikweli na matatizo yao. Kisha, alikuwa akisema waziwazi kwamba kile ambacho kwa hakika nyumba ya mfalme ilihitaji ni mwanamume mwenye moyo mkunjufu kama yeye! (2 Samweli 15:2-4) Bila shaka, Absalomu alitafuta masilahi yake mwenyewe wala si ya wenye kuonewa. Akitenda akiwa mfalme wa kujiteua, alishawishi mioyo ya wengi. Lakini baada ya muda, Absalomu alishindwa vibaya sana. Alipokufa, hata hakuonwa kuwa alistahili kuzikwa kwa heshima.—2 Samweli 18:6-17.
10. Twaweza kuonyeshaje kwamba tunaangalia masilahi ya wengine?
10 Hilo ni onyo kwa Wakristo leo. Huenda kiasili tukawa na uwezo wa kushawishi, tuwe wanaume au wanawake. Huenda ikawa rahisi kwetu kufanya tutakayo, kwa kutawala mazungumzo au kuwadhoofisha wale walio na maoni tofauti kwa kusisitiza maoni yetu zaidi. Hata hivyo, ikiwa tuna upendo wa kweli, basi tutaangalia masilahi ya wengine. (Wafilipi 2:2-4) Hatutatumia wengine ili kujinufaisha au kuendeleza mawazo yenye shaka kwa sababu ya uzoefu au wadhifa wetu katika tengenezo la Mungu, kana kwamba maoni yetu ndiyo tu yastahiliyo kufikiriwa. Badala ya hivyo, tutakumbuka mithali hii ya Biblia: “Kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.”—Mithali 16:18.
-
-
Njia ya Upendo Haishindwi KamweMnara wa Mlinzi—1999 | Februari 15
-
-
11. (a) Twaweza kuonyesha upendo wenye fadhili na wenye adabu kwa njia zipi? (b) Twaweza kuonyeshaje kwamba hatushangilii ukosefu wa uadilifu?
11 Paulo pia aliandika kwamba upendo ni “wenye fadhili” na kwamba “haujiendeshi bila adabu.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Naam, upendo hautaturuhusu tutende kwa njia ya ufidhuli, isiyo na adabu, au isiyo na staha. Badala yake, tutafikiria hisia za wengine. Kwa kielelezo, mtu mwenye upendo ataepuka kufanya mambo ambayo yangesumbua dhamiri za wengine. (Linganisha 1 Wakorintho 8:13.)
-
-
Njia ya Upendo Haishindwi KamweMnara wa Mlinzi—1999 | Februari 15
-
-
12, 13. (a) Twapaswa tutendeje mtu anapotukosea? (b) Taja vielelezo vya Biblia ili kuonyesha kwamba hata hasira inayostahili yaweza kutufanya tutende bila hekima.
12 Paulo aandika kwamba upendo “haupati kuwa wenye kuchokozeka” (“si wenye hamaki,” Phillips). (1 Wakorintho 13:5) Kwa kweli, ni jambo la kawaida tu kwetu wanadamu wasio wakamilifu kufadhaika au kuwa na kiasi fulani cha hasira ya kisasi mtu anapotukosea. Hata hivyo, ingekuwa makosa kuweka kinyongo kwa muda mrefu au kuendelea katika hali ya kuchokozeka. (Zaburi 4:4; Waefeso 4:26) Ikiwa hali hiyo haitarekebishwa, hata hasira inayostahili yaweza kutufanya tutende bila hekima, naye Yehova aweza kutulaumu kwa kufanya hivyo.—Mwanzo 34:1-31; 49:5-7; Hesabu 12:3; 20:10-12; Zaburi 106:32, 33.
13 Watu fulani wameruhusu kutokamilika kwa wengine kuathiri uamuzi wao wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo au kushiriki katika huduma ya shambani. Hapo awali wengi wao walifanya pigano kali kwa ajili ya imani, labda wakivumilia upinzani wa familia, dhihaka kutoka kwa wafanyakazi wenzao, na kadhalika. Wamevumilia vizuizi hivyo kwa sababu wameviona kuwa majaribu ya uaminifu-maadili, na kwa kweli ndivyo ilivyo. Lakini ni nini kitokeacho wakati Mkristo mwenzako asemapo au kufanya jambo lisilopendeza? Je, hilo pia si jaribu la uaminifu-maadili? Bila shaka ndiyo, kwa kuwa tukiendelea katika hali ya kuchokozeka twaweza “kuruhusu mahali kwa ajili ya Ibilisi.”—Waefeso 4:27.
-
-
Njia ya Upendo Haishindwi KamweMnara wa Mlinzi—1999 | Februari 15
-
-
14, 15. (a) Yamaanisha nini ‘kuweka hesabu ya ubaya’? (b) Twaweza kumwigaje Yehova kwa kuwa wenye kusamehe?
14 Akiwa na sababu nzuri, Paulo aongeza kusema kwamba upendo “hauweki hesabu ya ubaya.” (1 Wakorintho 13:5) Hapa anatumia neno litumikalo katika uwekaji wa hesabu, kwa wazi akidokeza tendo la kuandika kosa hilo katika daftari ya hesabu ili lisisahaulike. Je, ni jambo lenye upendo kuweka rekodi ya kudumu akilini kuhusu neno au tendo lenye kuumiza, kana kwamba tutahitaji kulirejezea wakati fulani ujao? Twaweza kuwa wenye furaha kama nini kwamba Yehova hatuchunguzi kwa njia hiyo isiyo na rehema! (Zaburi 130:3) Naam, tunapotubu, yeye hufuta kabisa makosa yetu.—Matendo 3:19.
15 Twaweza kumwiga Yehova katika jambo hilo. Hatupaswi kuwa wenye hisia nyepesi kupita kiasi mtu anapoonekana kuwa anatudharau. Ikiwa sisi ni wepesi wa kuudhika, huenda tukawa tunajiumiza zaidi ya vile mtu aliyetuudhi angeweza kutuumiza. (Mhubiri 7:9, 22) Badala yake, twahitaji kukumbuka kwamba upendo “huamini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Bila shaka, hakuna yeyote kati yetu atakaye kudanganywa kwa urahisi, wala haitupasi kushuku kupita kiasi nia za ndugu zetu. Inapowezekana, na tumchukulie yule mwingine kuwa alikuwa na nia nzuri.—Wakolosai 3:13.
-