-
Je, Unashiriki Katika Kufanya Mikutano ya Kikristo Iwe Yenye Kujenga?Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 15
-
-
Mikutano Ambayo Inakusudiwa ‘Kujenga, Kutia Moyo, na Kufariji’
13. (a) Mikutano yetu inapaswa kuwa na matokeo gani kwa wale wanaohudhuria? (b) Ni swali gani ambalo ni muhimu sana kwa wazee?
13 Paulo anasema kwamba kusudi la maana la mikutano ya kutaniko ni ‘kuwajenga, kuwatia moyo, na kuwafariji’ wale wanaohudhuria.c (1 Kor. 14:3) Wazee Wakristo leo wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba sehemu zao za mikutano zinawatia moyo kikweli akina ndugu na dada na kuwafariji? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze mkutano ambao Yesu aliongoza muda mfupi baada ya kufufuliwa.
14. (a) Ni mambo gani yaliyotukia kabla ya mkutano ambao ulipangwa na Yesu? (b) Kwa nini ni wazi kwamba mitume walifarijiwa ‘Yesu alipokaribia na kusema nao’?
14 Kwanza, angalia mambo ambayo yalitukia kabla ya mkutano huo. Kabla tu ya Yesu kuuawa, mitume ‘walimwacha na kukimbia,’ na kama ilivyotabiriwa, ‘walitawanyika na kwenda kila mmoja kwenye nyumba yake.’ (Marko 14:50; Yoh. 16:32) Kisha, baada ya Yesu kufufuliwa, aliwaalika mitume wake walioshuka moyo wahudhurie mkutano wa pekee.d Basi, “wale wanafunzi kumi na mmoja wakaingia Galilaya mpaka kwenye mlima ambako Yesu alikuwa amewafanyia mpango.” Walipofika, ‘Yesu alikaribia na kusema nao.’ (Mt. 28:10, 16, 18) Wazia jinsi mitume walivyofarijiwa wakati Yesu alipochukua hatua hiyo! Yesu alizungumzia mambo gani?
15. (a) Yesu alizungumzia mambo gani, lakini hakuzungumza kuhusu nini? (b) Mkutano huo ulikuwa na matokeo gani kwa mitume?
15 Yesu alianza kwa kutangaza hivi: “Nimepewa mamlaka yote.” Kisha, akawapa mgawo: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.” Mwishowe, akawahakikishia hivi kwa upendo: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote.” (Mt. 28:18-20) Lakini je, uliona jambo ambalo Yesu hakufanya? Hakuwakemea mitume wake; wala hakutumia mkutano huo kutilia shaka nia yao au kuwafanya wahisi kwamba wana hatia zaidi kwa kutaja udhaifu wa imani ambao walionyesha kwa muda mfupi. Badala yake, Yesu aliwahakikishia tena upendo wake na wa Baba yake kwa kuwapa mgawo mzito. Njia ambayo Yesu alitumia ilikuwa na matokeo gani kwa mitume? Walijengwa, walitiwa moyo, na kufarijiwa sana hivi kwamba muda mfupi baada ya mkutano huo, walianza tena “kufundisha na kutangaza habari njema.”—Mdo. 5:42.
16. Wazee Wakristo leo wanaiga mfano wa Yesu jinsi gani wanapoongoza mikutano ambayo ni chanzo cha burudisho?
16 Leo, wazee wanamwiga Yesu kwa kuona mikutano kuwa nafasi za kuwahakikishia waamini wenzao kwamba Yehova ana upendo wa kudumu kuelekea watu wake. (Rom. 8:38, 39) Hivyo, wanaposhughulikia sehemu zao katika mikutano, wazee wanakazia sifa nzuri za ndugu zao, bali si udhaifu wao. Hawatilii shaka nia ya ndugu zao. Badala yake, maneno yao yanaonyesha wazi kwamba wanawaona waamini wenzao kuwa watu mmoja-mmoja ambao wanampenda Yehova na wanaotaka kufanya mambo yaliyo sawa. (1 The. 4:1, 9-12) Bila shaka, nyakati nyingine huenda wazee wakahitaji kutoa mashauri ya kulirekebisha kutaniko kwa ujumla, lakini ikiwa ni watu wachache tu wanaohitaji kurekebishwa, kwa kawaida ni vizuri kuzungumza faraghani na wale wanaohusika na kuwapa mashauri hayo. (Gal. 6:1; 2 Tim. 2:24-26) Wazee wanapotoa hotuba mbele ya kutaniko lote, kusudi lao ni kutoa pongezi wakati wowote inapofaa kufanya hivyo. (Isa. 32:2) Wanajitahidi kuzungumza kwa njia ambayo inawafanya wote waliohudhuria wahisi kwamba wameburudishwa na kutiwa nguvu baada ya mkutano.—Mt. 11:28; Mdo. 15:32.
-
-
Je, Unashiriki Katika Kufanya Mikutano ya Kikristo Iwe Yenye Kujenga?Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 15
-
-
c Kamusi moja (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words) ikieleza tofauti kati ya maneno “tia moyo” na neno “fariji,” inasema kwamba neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “fariji” linamaanisha “wororo wa hali ya juu zaidi kuliko [kutia moyo].”—Linganisha na Yohana 11:19.
-