-
Zoeeni Kufanya Mambo Ambayo MmejifunzaMnara wa Mlinzi—2002 | Septemba 15
-
-
Kataa “Hadithi Zisizo za Kweli”
8. (a) Shetani anajaribuje kuvunja imani yetu leo? (b) Paulo anatoa onyo gani katika 2 Timotheo 4:3, 4?
8 Shetani hujaribu kuvunja uaminifu wetu wa maadili kwa kutilia shaka mambo ambayo tumefundishwa. Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo waasi-imani na wengine hujaribu kuharibu imani ya wale wasio na ujuzi. (Wagalatia 2:4; 5:7, 8) Nyakati nyingine wao hutumia vyombo vya habari kueneza habari zisizo za kweli au hata uwongo mtupu kuhusu utaratibu ambao watu wa Yehova hufuata na makusudi yao. Paulo alionya kwamba watu wengine wangekengeushwa waache kweli. Aliandika: “Kutakuwako kipindi cha wakati ambapo hawatachukuliana na fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajirundikia walimu kwa ajili yao wenyewe ili wapate kutekenywa masikio yao; nao watageuzia mbali masikio yao kuacha kweli, lakini watageuzwa kando kwenye hadithi zisizo za kweli.”—2 Timotheo 4:3, 4.
9. Inawezekana Paulo alimaanisha nini alipotaja “hadithi zisizo za kweli”?
9 Badala ya kushika kiolezo cha maneno yenye afya, wengine walivutiwa na “hadithi zisizo za kweli.” Hadithi hizo ni zipi? Labda Paulo alimaanisha hekaya kama zile zinazopatikana katika kitabu kinachoitwa Tobiti cha Apokrifa.a Inawezekana hadithi zisizo za kweli zilitia ndani mambo ya kusisimua yaliyokisiwa tu. Kisha kuna wale ambao “kwa kupatana na tamaa zao wenyewe” huenda walidanganywa akili na wale ambao walikuwa wakipuuza kanuni za Mungu au waliokuwa wakiwachambua wenye kuongoza kutanikoni. (3 Yohana 9, 10; Yuda 4) Hata yawe ni mambo gani yaliyohusika, inaonekana wengine walipendelea habari zisizo za kweli badala ya kweli ya Neno la Mungu. Kisha wakaacha kufanya mambo waliyojifunza, wakaangamia kiroho.—2 Petro 3:15, 16.
10. Hadithi zisizo za kweli siku hizi ni zipi, na Yohana alionyeshaje uhitaji wa kujihadhari?
10 Leo, tunaweza kuepuka kuvutiwa na hadithi zisizo za kweli ikiwa tunachunguza na kuchagua kwa uangalifu mambo tunayosikiliza na kusoma. Kwa mfano, mara nyingi vyombo vya habari huonyesha matendo machafu. Watu wengi huendeleza dhana ya kwamba mambo ya Mungu hayajulikani au hata kudai kwamba hakuna Mungu. Wachambuzi wa Biblia wanadai kwamba Biblia haikuandikwa kwa mwongozo wa Mungu. Na waasi-imani wa siku hizi huendelea kujaribu kutilia shaka imani ya Wakristo ili kuivunja. Mtume Yohana alionya hivi kuhusu hatari inayofanana na hiyo ambayo ilitokezwa na manabii wasio wa kweli katika karne ya kwanza: “Wapendwa, msiamini kila usemi uliopuliziwa, lakini jaribuni semi zilizopuliziwa ili kuona kama hizo zatokana na Mungu, kwa sababu manabii wengi wasio wa kweli wameenda kuingia katika ulimwengu.” (1 Yohana 4:1) Basi tunahitaji kujihadhari.
11. Taja njia moja ya kujijaribu na kuona kama tuko katika imani.
11 Paulo aliandika hivi kuhusu habari hiyo: “Fulizeni kujijaribu kama nyinyi mumo katika imani.” (2 Wakorintho 13:5) Mtume huyo alituhimiza tuendelee kujijaribu ili tuone kama tunafuata mafundisho yote ya Kikristo. Ikiwa tuna mwelekeo wa kusikiliza wale wanaolalamika-lalamika, tunahitaji kujichunguza kupitia sala. (Zaburi 139:23, 24) Je, sisi hukosoa-kosoa watu wa Yehova? Ikiwa ndivyo, kwa nini? Je, ni kwa sababu mtu fulani ametuudhi kwa maneno au kwa matendo? Ikiwa ndivyo, je, tunachukulia jambo hilo kwa njia inayofaa? Dhiki yoyote tunayokabili katika mfumo huu ni ya muda tu. (2 Wakorintho 4:17) Hata kama tunapata jaribu fulani kutanikoni, mbona tuache kumtumikia Mungu? Ikiwa jambo fulani limetuudhi, je, haingefaa tujitahidi kwa kadiri tunavyoweza kulisuluhisha na kuliacha mkononi mwa Yehova?—Zaburi 4:4; Mithali 3:5, 6; Waefeso 4:26.
12. Waberoya walituwekeaje mfano mzuri?
12 Badala ya kuwa wachambuzi, na tudumishe maoni mazuri ya kiroho kuhusu habari tunayojifunza katika funzo la binafsi na katika mikutano ya kutaniko. (1 Wakorintho 2:14, 15) Na badala ya kutilia shaka Neno la Mungu, inafaa tuwe na maoni kama yale ya Waberoya wa karne ya kwanza ambao waliyachunguza Maandiko kwa makini. (Matendo 17:10, 11) Basi, na tufanye yale ambayo tunajifunza, tukatae hadithi zisizo za kweli na kushikamana na kweli.
13. Tunawezaje kueneza hadithi zisizo za kweli pasipo kujua?
13 Kuna aina nyingine ya hadithi isiyo ya kweli ambayo tunahitaji kujihadhari nayo. Kuna habari nyingi za kusisimua zinazoenezwa hasa na barua-pepe (E-mail) kupitia kompyuta. Inafaa tujihadhari na habari kama hizo, na hasa kama hatujui chanzo chake. Hata kama Mkristo mwenye sifa nzuri ndiye aliyetutumia jambo fulani lililoonwa au masimulizi fulani, inawezekana kwamba hata yeye alisimuliwa tu habari hizo. Hiyo ndiyo sababu inafaa tujihadhari tusisimulie au kueneza habari ambazo hazijathibitishwa. Haingefaa kusimulia “hekaya zisizo za kimungu,” au “hadithi zisizo za kweli ambazo huhalifu kilicho kitakatifu.” (1 Timotheo 4:7; New International Version) Kwa kuwa sisi pia tuna wajibu wa kuzungumza mambo yaliyo kweli, ni vizuri tuepuke jambo lolote linaloweza kutufanya tueneze bila kukusudia habari zisizo za kweli.—Waefeso 4:25.
-
-
Zoeeni Kufanya Mambo Ambayo MmejifunzaMnara wa Mlinzi—2002 | Septemba 15
-
-
a Inawezekana kitabu Tobiti kiliandikwa karne ya tatu K.W.K., nacho kimejaa hadithi zenye ushirikina kuhusu Myahudi aitwaye Tobia. Ilisemekana kwamba alikuwa na uwezo wa kupata nguvu za kuponya na za kuondosha mashetani akitumia moyo, nyongo, na ini la samaki fulani mwenye kutisha.
-