-
Je, Uovu Umeshinda?Mnara wa Mlinzi—2003 | Januari 15
-
-
Baadaye, katika siku za mzee wa ukoo Ayubu, Shetani alitokeza suala jingine. Huku akitaka kuvunja uaminifu wa Ayubu kwa Mungu, Shetani alisema: “Ngozi kwa ngozi, naam, yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake.” (Ayubu 2:4) Hilo lilikuwa dai la ujumla na linaloweza kutilika shaka kama nini! Kwa kutumia neno la ujumla “mtu” badala ya kutaja jina la Ayubu, Shetani alitilia shaka uaminifu wa kila mtu. Kwa kweli, alidai hivi: “Mtu atafanya chochote awezacho ili kuokoa uhai wake. Nikipewa nafasi, ninaweza kugeuza kila mtu amwache Mungu.”
-
-
Je, Uovu Umeshinda?Mnara wa Mlinzi—2003 | Januari 15
-
-
Je, Kweli Shetani Anaweza Kugeuza Kila Mtu Amwache Mungu?
Je, Shetani amefaulu kuthibitisha dai lake kwamba anaweza kugeuza kila mtu amwache Mungu? Katika sura ya 11 ya kitabu cha Biblia cha Waebrania, mtume Paulo anataja wanaume na wanawake kadhaa waaminifu walioishi kabla ya Ukristo. Kisha anasema: “Wakati utakosekana kwangu nikiendelea kusimulia juu ya Gideoni, Baraki, Samsoni, Yeftha, Daudi na vilevile Samweli na wale manabii wengine.” (Waebrania 11:32) Paulo anataja watumishi hao waaminifu wa Mungu kuwa ‘wingu kubwa la mashahidi.’ (Waebrania 12:1) Neno la Kigiriki lililotumiwa hapa “wingu” halimaanishi wingu lenye umbo na ukubwa fulani hususa, bali ladokeza wingu lisilo na umbo hususa linalotanda na kufunika anga. Mfano huo unafaa kwa sababu watumishi wa kale waliokuwa waaminifu kwa Mungu ni wengi sana kama wingu linalotanda na kufunika anga. Naam, kwa karne nyingi, watu wengi sana wameamua kwa hiari yao kuwa waaminifu kwa Yehova Mungu.—Yoshua 24:15.
Vipi wakati wetu? Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wameongezeka na kuzidi milioni sita licha ya mnyanyaso na upinzani mkali waliopata katika karne ya 20. Watu wengine wapatao milioni tisa wanashirikiana na Mashahidi, na wengi wao wanachukua hatua hususa ya kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu.
Jibu bora kabisa kwa dai la Shetani kwamba anaweza kugeuza watu wamwache Yehova lilitolewa na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Hata maumivu makali aliyopata kwenye mti wa mateso hayakuvunja uaminifu wake. Kabla Yesu hajafa, alisema hivi kwa sauti kubwa: “Baba, ndani ya mikono yako naikabidhi roho yangu.”—Luka 23:46.
Shetani anatumia mbinu zote alizo nazo kutia ndani vishawishi na mnyanyaso wa moja kwa moja ili kuwavuta wanadamu upande wake. Yeye hujitahidi kuwashawishi watu wamwache Mungu kwa kutumia “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha.” (1 Yohana 2:16) Pia Shetani ‘amepofusha akili za wasioamini, ili mmuliko wa habari njema yenye utukufu juu ya Kristo, usipate kung’aa kwa kupenya.’ (2 Wakorintho 4:4) Naye Shetani hutumia vitisho na hofu ya wanadamu ili kutimiza mradi wake.—Matendo 5:40.
Hata hivyo, wale walio upande wa Mungu hawashindwi na Ibilisi. Wamepata kumjua Yehova Mungu na ‘kumpenda kwa moyo wao wote na kwa nafsi yao yote na kwa akili yao yote.’ (Mathayo 22:37) Naam, uaminifu thabiti wa Yesu Kristo na wa wanadamu wengine wengi unathibitisha kabisa kwamba Shetani Ibilisi ameshindwa.
-