-
“Kwa Nini Mtoto Wangu Amebadilika Sana?”Amkeni!—2008 | Juni
-
-
“Kwa Nini Mtoto Wangu Amebadilika Sana?”
Scott na Sandraa walipigwa na butwaa binti yao mwenye umri wa miaka 15 alipoingia sebuleni. Nywele zake zilizokuwa za rangi ya dhahabu, sasa zilikuwa nyekundu! Mazungumzo yaliyofuata yaliwaacha midomo wazi.
“Je, tulikupa ruhusa ya kutia rangi nywele zako?”
“Kwa kweli, hamkusema sipaswi kufanya hivyo.”
“Mbona hukutuuliza?”
“Kwa sababu nilijua mngekataa!”
SCOTT na Sandra wanaweza kuthibitisha kwamba miaka ya kubalehe ni kipindi cha msukosuko—si kwa vijana tu bali pia kwa wazazi wao. Kwa kweli, baba na mama wengi hawako tayari kukabiliana na mabadiliko makubwa yanayotokea mtoto wao anapobalehe. “Binti yetu alibadilika bila kuonyesha dalili zozote,” anakumbuka Barbara, mama mmoja huko Kanada. “Nilijiuliza, ‘Kwa nini mtoto wangu amebadilika sana?’ Ni kana kwamba alichukuliwa tukiwa usingizini na tukaletewa mtoto tofauti!”
Kwa kweli, mambo yaliyompata Barbara yamewapata wengine pia. Fikiria yale ambayo wazazi katika sehemu mbalimbali ulimwenguni waliwaambia waandishi wa Amkeni!
“Alipofikia umri wa kubalehe, kwa ghafula mwana wangu alianza kushikilia sana maoni yake na kutilia shaka zaidi mamlaka yetu.”—Lia, Uingereza.
“Binti zetu walianza kujihangaikia sana, hasa kuhusu sura yao.”—John, Ghana.
“Mwana wangu alitaka kujifanyia maamuzi. Hakutaka kuambiwa la kufanya.”—Celine, Brazili.
“Binti yetu hakutaka tena tumkumbatie wala kumbusu.”—Andrew, Kanada.
“Wavulana wetu walianza kuwa washindani sana. Badala ya kukubali maamuzi yetu, waliyapinga na kubishana nasi kuyahusu.”—Steve, Australia.
“Binti yangu alificha hisia zake. Alijifungia katika ulimwengu wake mwenyewe, naye alikasirika nilipojaribu kumtia moyo anifunulie hisia zake.”—Joanne, Mexico.
“Watoto wetu walikuwa na mwelekeo wa kuficha matendo na maoni yao na walitaka faragha zaidi. Badala ya kuwa nasi, mara nyingi walipendelea kuwa na marafiki wao.”—Daniel, Filipino.
Ukiwa mzazi wa kijana anayebalehe, huenda ukaona kwamba baadhi ya maelezo yaliyo hapo juu yanapatana sana na hali zako. Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba jitihada zako za kumwelewa “mgeni” huyo aliye kati yenu, yaani, mwana au binti yenu zinaweza kufanikiwa. Biblia inaweza kukusaidia. Jinsi gani?
Hekima na Uelewaji
Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Jipatie hekima, jipatie uelewaji.” (Methali 4:5) Sifa hizo mbili ni muhimu unaposhughulika na kijana anayebalehe. Unahitaji uelewaji si ili tu kufahamu tabia zake bali pia kutambua yale hasa yanayompata mtoto wako. Pia unahitaji hekima ili kumsaidia kwa mafanikio kijana wako awe mtu mzima anayetegemeka.
Usifikiri kwamba mwana au binti yako hakuhitaji kwa sababu inaonekana kuwa hamna uhusiano wa karibu kama zamani. Ukweli ni kwamba, vijana wanaobalehe wanahitaji—na hata wanataka—wazazi wao wajihusishe na maisha yao katika kipindi hicho kigumu. Uelewaji na hekima zitakusaidiaje kuandaa mwongozo huo?
[Maelezo ya Chini]
a Majina katika mfululizo huu yamebadilishwa.
-
-
Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Uelewaji UnavyohusikaAmkeni!—2008 | Juni
-
-
Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Uelewaji Unavyohusika
Tuseme unatembelea nchi ya kigeni na huzungumzi lugha ya wenyeji wa nchi hiyo. Hapana shaka kwamba itakuwa vigumu kuwasiliana nao—lakini hilo halimaanishi hamwezi kuwasiliana. Kwa mfano, kamusi inaweza kukusaidia kujifunza semi za msingi katika lugha hiyo. Au mtu fulani anaweza kutafsiri mazungumzo yenu ili mweze kuelewana.
NYAKATI nyingine, huenda wazazi wanaolea vijana wakahisi kwamba wamo katika hali kama hiyo. Sawa na lugha ya kigeni, huenda ikawa vigumu kuelewa tabia za vijana wanaobalehe—lakini hilo halimaanishi kwamba haziwezi kueleweka. Siri ya mafanikio ni wazazi wajaribu kuelewa hasa kinachotukia katika kipindi hicho cha ukuzi chenye msisimko na kinachotatanisha.
Kiini cha Tabia za Vijana
Kijana anapotaka kujitegemea, nyakati nyingine hilo halimaanishi kwamba anataka kuasi. Kumbuka, Biblia inasema kwamba baada ya muda, “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Ili kujitayarisha kwa ajili ya majukumu mazito watakapokuwa watu wazima, vijana wanahitaji angalau uzoefu fulani wa kufanya maamuzi.
Chunguza kile ambacho huenda kikawa kiini cha tabia zilizoonwa na wazazi walionukuliwa katika makala iliyotangulia.
Lia, huko Uingereza, alisema hivi: “Kwa ghafula mwana wangu alianza kushikilia sana maoni yake na kutilia shaka zaidi mamlaka yetu.”
Kama watoto wadogo, vijana huuliza tena na tena, “Kwa nini?” Hata hivyo, huenda vijana wasitosheke na jibu fupi. Kwa sababu gani? Mtume Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa . . . nikifikiri kama mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Vijana wanapositawisha uwezo wao wa kufikiri, wanahitaji maelezo zaidi ili “nguvu zao za ufahamu” zizoezwe.—Waebrania 5:14.
John huko Ghana, alisema hivi: “Binti zetu walianza kujihangaikia sana, hasa kuhusu sura yao.”
Iwe ukuzi wa haraka unaotukia wakati wa kubalehe utaanza mapema, kwa kuchelewa, ama utaanza kwa wakati hususa, unawafanya vijana wahangaikie sura yao kupita kiasi. Wasichana wanaweza kusisimkia umbo lao jipya au kuwa na wasiwasi kulihusu, au wanaweza pia kuwa na hisia zote mbili. Isitoshe, wanapokuwa na chunusi—na wanapoanza kutumia vipodozi—ni rahisi kuelewa ni kwa nini vijana wanatumia muda mrefu zaidi kujitazama kwenye kioo kuliko muda wanaotumia kujifunza.
Daniel, huko Filipino, alieleza: “Watoto wetu walikuwa na mwelekeo wa kuficha matendo na maoni yao na walitaka faragha zaidi. Badala ya kuwa nasi, mara nyingi walipendelea kuwa na marafiki wao.”
Kuficha siri kunaweza kuwa hatari. (Waefeso 5:12) Hata hivyo, faragha si kuficha siri. Hata Yesu alitambua umuhimu wa kutafuta “mahali pasipo na watu ili awe peke yake.” (Mathayo 14:13) Pia, kadiri vijana wanavyokua, wanahitaji faragha—na wanataka watu wazima waheshimu faragha hiyo. Kiwango fulani cha faragha kinawasaidia vijana wawaze na kuwazua. Huo ni uwezo muhimu utakaowafaa sana watakapokuwa watu wazima.
Hali kadhalika, kujifunza jinsi ya kuanzisha urafiki ni sehemu ya ukuzi. Ni kweli kwamba “mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Hata hivyo, Biblia inasema hivi pia: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Kujifunza jinsi ya kuanzisha na kudumisha urafiki unaofaa ni uwezo muhimu watakaotumia hata watakapokuwa watu wazima.
Wakikabili mojawapo ya hali hizo, ingefaa wazazi wajitahidi kujipatia uelewaji ili wasielewe vibaya tabia za vijana wao. Bila shaka, mbali na uelewaji wanapaswa kuwa na hekima, yaani, uwezo wa kushughulikia hali kwa njia itakayoleta matokeo bora zaidi. Wazazi wa vijana wanaobalehe wanaweza kufanyaje hivyo?
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Vijana wanapositawisha uwezo wao wa kufikiri, wanahitaji maelezo zaidi kuhusu sheria za familia
-
-
Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Hekima InavyohusikaAmkeni!—2008 | Juni
-
-
Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Hekima Inavyohusika
“Tunajaribu sana kuwapa mwongozo mwana na binti yetu, lakini ni kama tunawakemea daima kwa sababu fulani. Nyakati nyingine hatujui ikiwa tunawafanya wajiamini au wasijiamini. Ni vigumu sana kuwa na usawaziko.”—George na Lauren, Australia.
KUMLEA kijana anayebalehe si kazi rahisi. Mbali na kukabiliana na matatizo mapya yanayotokezwa na mtoto wao, huenda wazazi wakahuzunika au kuwa na wasiwasi kwa sababu mwana au binti yao anakua. “Kutambua kwamba watoto wetu watatuacha siku moja ni wazo lenye kuhuzunisha,” anakiri Frank, baba mmoja huko Australia. “Si rahisi kukubali kwamba si wewe unayeongoza maisha yao sasa.”
Lia, aliyenukuliwa mapema katika mfululizo huu, anakubaliana na hilo. “Ni vigumu kumtendea mwanangu kama mtu mzima, kwa kuwa bado namwona tu kuwa mvulana wangu mdogo,” anasema. “Ni kana kwamba alianza shule jana tu!”
Ingawa ni vigumu kukubali hilo, ukweli ni kwamba vijana wanaobalehe si watoto tena. Wao ni watoto wanaozoezwa kuwa watu wazima na wazazi wao ni walimu na wachocheaji wao. Hata hivyo, kama George na Lauren waliotajwa hapo juu, wazazi wana uwezo wa kumsaidia kijana ajiamini au asijiamini. Wazazi wanaweza kuonyeshaje usawaziko unaofaa? Biblia ina mashauri yanayosaidia. (Isaya 48:17, 18) Acheni tuchunguze mifano fulani.
Mawasiliano Mazuri Ni Muhimu
Biblia inawaambia Wakristo wawe ‘wepesi kuhusu kusikia’ na ‘wasiwe wepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) Ijapokuwa shauri hilo linafaa unaposhughulika na watoto wa umri wowote ule, kusikia—au kusikiliza—ni muhimu hasa unaposhughulika na vijana wanaobalehe. Na huenda hilo likahitaji jitihada nyingi.
“Nilihitaji kuboresha ustadi wangu wa kuwasiliana na wana wangu walipokuwa matineja,” anasema Peter, baba mmoja huko Uingereza. “Wavulana wetu walipokuwa wachanga, mimi na mke wangu tuliwaambia walichopaswa kufanya, nao walitii. Lakini kwa kuwa sasa wamekua, tunahitaji kujadiliana, kuzungumza kwa undani, na kuwaacha watumie uwezo wao wa kufikiri kuchanganua mambo. Kwa ufupi, tunahitaji kuufikia moyo.”—2 Timotheo 3:14.
Ni muhimu kusikiliza hasa maoni yanapotofautiana. (Methali 17:27) Danielle anayeishi Uingereza, alijionea ukweli wa jambo hilo. Anasema hivi: “Nilikuwa na tatizo na mmoja wa binti zangu kuhusu jinsi alivyonijibu nilipomwambia afanye chochote. Lakini aliniambia kwamba sikuzote nilikuwa nikimfokea na kumwamrisha. Tulitatua tatizo hilo kwa kuketi na nikamsikiliza naye akanisikiliza kikweli. Alieleza jinsi nilivyokuwa nikizungumza naye na jinsi nilivyomfanya ahisi, nami nikamweleza maoni na hisia zangu.”
Danielle aligundua kwamba kuwa “mwepesi kuhusu kusikia” kulimsaidia kutambua kiini cha tatizo. “Sasa ninajitahidi kumtendea binti yangu kwa subira,” anasema, “nami ninajitahidi kuzungumza naye wakati ambapo sijakasirika.” Aliongeza hivi: “Uhusiano wetu unakuwa bora.”
Methali 18:13 inasema: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” Greg, baba mmoja huko Australia, alijionea ukweli wa jambo hilo. “Nyakati nyingine matatizo kati yetu na watoto wetu hutokea wakati ambapo mimi na mke wangu tunawakemea watoto wetu badala ya kuwasikiliza kwanza na kutambua jinsi wanavyohisi,” anasema. “Hata ikiwa hatukubaliani kabisa na mitazamo yao, tumeona kwamba ni muhimu sana kuwaruhusu wafunue hisia zao kabla ya kuwarekebisha au kuwashauri inavyohitajika.”
Uhuru Mwingi Kadiri Gani?
Huenda kisababishi kikubwa zaidi cha matatizo kati ya wazazi na vijana wanaobalehe kikahusiana na suala la uhuru. Kijana anapaswa kupewa uhuru mwingi kadiri gani? Kuhusu uhuru, baba mmoja alisema hivi: “Mara nyingine, mimi huhisi kwamba binti yangu akionja asali atachonga mzinga.”
Kwa wazi, kuwapa vijana uhuru usio na mipaka kutakuwa na matokeo mabaya. Kwa kweli, Biblia inaonya kwamba “mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.” (Methali 29:15) Vijana wa umri wowote ule wanahitaji mwongozo thabiti, na inapohusu kutekeleza sheria za familia wazazi wanapaswa kuwa wenye upendo lakini imara. (Waefeso 6:4) Wakati huohuo, vijana wanapaswa kupewa kiasi fulani cha uhuru ili wawe tayari zaidi kufanya maamuzi ya hekima baadaye maishani.
Kwa mfano, fikiria jinsi ulivyojifunza kutembea. Mwanzoni, ulipokuwa mtoto mchanga, ulibebwa. Muda si muda, ulianza kutambaa kisha kutembea. Bila shaka, kutambaa au kutembea kunaweza kumhatarisha mtoto mdogo. Hivyo, wazazi wako walikuwa waangalifu sana na huenda walikuwekea vizuizi fulani ili usikaribie maeneo hatari, kama vile ngazi. Hata hivyo, walikuruhusu utembee peke yako na baada ya kuanguka mara kadhaa, hatimaye ulifaulu kutembea bila matatizo.
Kupata uhuru kunahusisha hatua kama hizo. Mwanzoni, kwa njia ya mfano wazazi wanawabeba watoto wao wachanga kwa kuwafanyia maamuzi. Baadaye, kadiri watoto wanavyokomaa, wazazi wanawaruhusu watambae kwa kujifanyia maamuzi fulani. Wakati huohuo wanawawekea vijana vizuizi ambavyo vinawalinda kutokana na madhara. Kadiri watoto wao wanavyokomaa, ndivyo wazazi wanavyowaruhusu “watembee” peke yao. Kisha watakapokuwa watu wazima, watakuwa na uwezo kamili wa ‘kubeba mzigo wao wenyewe.’—Wagalatia 6:5.
Kujifunza Kutokana na Mfano wa Biblia
Kwa wazi, akiwa na umri wa miaka 12, Yesu alikuwa amepewa uhuru fulani na wazazi wake, lakini hakuutumia vibaya. Badala yake, ‘aliendelea kujitiisha’ kwa wazazi wake na “akazidi kufanya maendeleo katika hekima na ukuzi wa kimwili, akipata kibali kwa Mungu na wanadamu.”—Luka 2:51, 52.
Ukiwa mzazi, unaweza kujifunza kutokana na mfano huo kwa kuwapa watoto wako uhuru zaidi kadiri wanavyoonyesha wanaweza kuutumia vizuri. Kuhusiana na hilo, fikiria yale ambayo wazazi fulani wamesema kuhusu mambo waliyojionea.
“Nilikuwa nikiingilia sana shughuli za watoto wangu. Lakini baadaye, nilianza kuwafundisha kanuni mbalimbali na kuwaacha wafanye uamuzi kupatana na yale waliyojifunza. Baada ya hapo, niliona kwamba walianza kufikiria kwa makini zaidi maamuzi yao.”—Soo Hyun, Korea.
“Nyakati zote mimi na mume wangu huwa na wasiwasi kuhusu kuwapa watoto wetu uhuru, lakini hatujaacha hilo lituzuie kuwaruhusu watumie uhuru wanaostahili kwa njia inayofaa.”—Daria, Brazili.
“Nimegundua kwamba ni muhimu kumpongeza mwana wangu ambaye ni tineja anapotumia vizuri uhuru ninaompa. Pia mimi hufanya yale ninayomwambia afanye. Kwa mfano, mimi humwambia ninakoenda na ninachofanya. Pia ikiwa nitachelewa, mimi humjulisha.”—Anna, Italia.
“Katika nyumba yetu tunasisitiza kwamba wana wetu hawana haki ya kujitegemea lakini wanapaswa kuthibitisha kwamba wanaweza kutegemeka.”—Peter, Uingereza.
Kukabili Matokeo
Biblia inasema hivi: “Ni jambo jema kwa mwanamume kuchukua nira wakati wa ujana wake.” (Maombolezo 3:27) Mojawapo ya njia bora ya kijana kujichukulia nira ya wajibu ni kujionea mwenyewe ukweli wa taarifa hii: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6:7.
Wakiwa na nia nzuri, huenda wazazi fulani wakawakinga vijana wao kutokana na matokeo ya matendo yasiyo ya hekima. Kwa mfano, tuseme kwamba kwa kununua vitu asivyohitaji mvulana fulani anajiingiza katika deni. Atajifunza nini ikiwa Baba na Mama watalipa deni hilo? Kwa upande mwingine, mvulana huyo angejifunza nini ikiwa wazazi wake wangemsaidia kupanga jinsi atakavyojilipia deni hilo?
Wazazi hawafaidi watoto wao hata kidogo wanapowakinga kutokana na matokeo ya tabia zao za kutokuwa waangalifu. Badala ya kuwatayarisha kwa ajili ya maisha ya utu uzima, kufanya hivyo kunawafundisha kwamba nyakati zote kutakuwa na mtu wa kuwaondoa matatani, kuwatatulia matatizo wanayojiletea, na kuwafunikia makosa yao. Inafaa zaidi kuwaacha vijana wavune walichopanda na wajifunze kutatua matatizo yao. Hiyo ni sehemu muhimu ya ‘kuzoeza nguvu zao za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’—Waebrania 5:14.
“Mtu Anayebadilika na Kukomaa”
Hapana shaka kwamba wazazi wa vijana wanaobalehe wana kazi ngumu. Nyakati fulani, huenda watafadhaika na kutokwa na machozi wanapojitahidi kuwalea watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.
Mwishowe, kulea watoto kwa mafanikio hakumaanishi kuwadhibiti, bali kunamaanisha kuwafundisha na kukazia kanuni zinazofaa mioyoni mwao. (Kumbukumbu la Torati 6:6-9) Bila shaka ni rahisi kusema hivyo kuliko kutenda. “Tunashughulika na mtu anayebadilika na kukomaa,” anasema Greg, aliyenukuliwa mapema. “Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kuendelea kumfahamu mtu huyo mpya na kujirekebisha ili kupatana naye.”
Jitahidi kufuata kanuni za Biblia zilizozungumziwa katika makala hii. Uwe na usawaziko kuhusu yale unayotazamia kutoka kwa watoto wako. Lakini usimwachie kamwe mtu mwingine wajibu wako wa kuwa kielelezo kikuu maishani mwao. Biblia inasema: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.”—Methali 22:6.
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Kupata uhuru ni kama kujifunza kutembea—unapatikana hatua kwa hatua
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Kabla ya kuwa kijana, Yesu alipewa uhuru fulani
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
“Kusisitiza Mamlaka Yako”
Hata ingawa kijana wako anaweza kukasirishwa na sheria unazoweka hilo halimaanishi kwamba unapaswa kulegeza mamlaka yako. Kumbuka, vijana wanaobalehe hawana ujuzi maishani na bado wanahitaji mwongozo.—Methali 22:15.
Katika kitabu chake New Parent Power! John Rosemond anaandika hivi: “Ni rahisi kwa wazazi kukubali washinikizwe na msukosuko wa kihisia wa watoto wao na kuanza kuwapa uhuru zaidi kuliko wanavyostahili ili kuepuka magombano. Lakini wazazi hawapaswi kamwe kufanya hivyo. Huo ndio wakati wa kusisitiza mamlaka yao, si wakati wa kuwaachilia watoto wapuuze mamlaka hiyo. Ingawa hapana shaka watapinga wazo hilo, huo pia ndio wakati wa watoto kutambua kwamba wazazi wao wako tayari kushika usukani.”
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Kuwapa Uhuru Zaidi
Mara nyingi vijana hutaka uhuru mwingi kuliko wanavyostahili. Wakati huohuo, wazazi fulani huwapa uhuru mdogo kuliko wanavyoweza. Usawaziko unaweza kupatikana jinsi gani? Kwanza huenda ukataka kuchunguza orodha iliyo hapa chini. Mwana au binti yako ni mwenye kutegemeka katika mambo gani?
□ Kuchagua marafiki
□ Kuchagua mavazi
□ Kutumia pesa vizuri
□ Kurudi nyumbani kwa wakati uliowekwa
□ Kumaliza kazi za nyumbani
□ Kumaliza kazi za shule
□ Kuomba msamaha unapokosea
□ Mengine ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․
Ikiwa tayari kijana wako anaonyesha ukomavu katika baadhi ya mambo yaliyo hapo juu, kwa nini usifikirie njia fulani za kumpa uhuru zaidi?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Waruhusu wafunue hisia zao kabla ya kuwarekebisha au kuwashauri inavyohitajika
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Wazazi wanapaswa kuwazoeza watoto wao kuwa wenye kutegemeka
-