-
Kukosa Uaminifu—matokeo Yenye KuhuzunishaAmkeni!—1999 | Aprili 22
-
-
Huenda ukajiuliza, ‘Je, kupatana ndilo suluhisho letu?’ ‘Au je, nitaliki?’ Hasa ndoa inapokuwa na mikazo, waweza kuchochewa kufikia mkataa wa haraka kwamba talaka ndiyo suluhisho kwa matatizo yenu. Huenda ukasababu kwamba ‘kwa vyovyote, Biblia huruhusu talaka kwa msingi wa kukosa uaminifu katika ndoa.’ (Mathayo 19:9) Kwa upande mwingine, huenda ukasababu kwamba Biblia haisisitizi juu ya talaka. Kwa hiyo, waweza kuhisi kwamba ingekuwa bora kutafuta upatanisho, kujenga upya ndoa na kuiimarisha.
Kumtaliki au kutomtaliki mwenzi asiye mwaminifu ni uamuzi wa kibinafsi. Lakini unaweza kujuaje jambo la kufanya? Kwanza, tafadhali chunguza baadhi ya mambo yanayoweza kukusaidia kuamua ikiwa kupatana kunawezekana.
-
-
Je, Kupatana Kwawezekana?Amkeni!—1999 | Aprili 22
-
-
Je, Kupatana Kwawezekana?
“Ni rahisi kuanza kutafuta talaka kwa ghafula,” chasema kitabu “Couples in Crisis,” “lakini lazima kuwe na ndoa nyingi ambazo kwa msingi zinafaa na ambazo zingeweza kufanikiwa ikiwa matatizo yangetatuliwa.”
MAONI hayo yapatana na fundisho la Yesu Kristo la kale kuhusu talaka. Ijapokuwa alisema kwamba mwenzi asiye na hatia anaruhusiwa kuchukua talaka kwa msingi wa kukosa uaminifu katika ndoa, hakusema kwamba ilikuwa lazima kufanya hivyo. (Mathayo 19:3-9) Huenda mwenzi mwaminifu akawa na sababu za kutaka kuokoa ndoa. Huenda mume mkosaji akawa bado anampenda mke wake bado.a Huenda akawa ni mume mwenye kujali na baba mwenye kujitoa anayeandaa mahitaji ya familia yake kwa kudhamiria. Kwa kufikiria mahitaji yake na yale ya watoto, huenda mwenzi mwaminifu akaamua kutafuta kupatana badala ya talaka. Ikiwa ndivyo, ni mambo gani yanayoweza kufikiriwa, na magumu ya kujenga ndoa upya yanaweza kukabiliwaje kwa mafanikio?
Kwanza ujue kwamba wala talaka wala kupatana si rahisi. Zaidi ya hayo, kumsamehe tu mwenzi mzinzi hakuelekei kutatatua matatizo ya msingi katika ndoa. Kwa kawaida ili kuokoa ndoa, kujichunguza kwa undani, mawasiliano ya waziwazi, na kazi ngumu hutakikana. Mara nyingi wenzi wa ndoa hupuuza kiasi cha wakati kinachotakikana na jitahada zinazotakikana kujenga upya ndoa iliyovunjika. Hata hivyo, wengi wamevumilia na kama tokeo wamekuwa na ndoa zilizo imara.
Maswali ya Kujibiwa
Ili kufanya uamuzi unaotegemea habari fulani, mwenzi mwaminifu anapaswa kuchanganua hisia zake na mambo tofauti-tofauti anayoweza kuchagua. Huenda akafikiria mambo yafuatayo: Je, anataka kurudi? Je, amekomesha kabisa kufanya uzinzi, au anasitasita kukomesha uhusiano huo? Je, ameomba radhi? Ikiwa ndivyo, je, ametubu kikweli, amejuta kwa moyo mweupe kuhusu jambo alilofanya? Au je, anaelekea kunilaumu kwa kosa lake? Je, anajuta kikweli kwa madhara ambayo amesababisha? Au badala ya hivyo, amefadhaika tu kwa sababu uhusiano wake haramu umefunuliwa na kuvurugwa?
Vipi kuhusu wakati ujao? Je, ameanza kurekebisha mitazamo na matendo yalioongoza kwenye uzinzi? Je, ameazimia kwa dhati kutorudia kosa hilo? Au bado ana mwelekeo wa kucheza kimahaba na kuwa na uhusiano wa kihisia-moyo usiofaa na watu wa jinsia tofauti? (Mathayo 5:27, 28) Je, amejitoa kikamili kujenga ndoa upya? Ikiwa ndivyo, anafanya nini kuhusu jambo hilo? Majibu yafaayo kwa maswali haya yaweza kuwa msingi wa kuamini kwamba inawezekana kurudisha uhusiano wa ndoa.
-