-
Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa Baada ya Ukosefu wa Uaminifu?Amkeni!—1997 | Aprili 8
-
-
Kwa kufikiria maumivu makali kama hayo, mtu aweza kuuliza, ‘Je, uzinzi lazima ukomeshe ndoa?’ Siyo lazima. Maneno ya Yesu kuhusu uzinzi yaonyesha kwamba mwenzi mwaminifu ana chaguo la Kimaandiko kutaliki lakini hawajibiki kufanya hivyo. Baadhi ya wenzi huamua kujenga upya na kuimarisha kile ambacho kiliharibiwa, kwa kufanya mabadiliko yahitajiwayo—ingawa uzinzi hauna udhuru.
Bila shaka, ni bora kufanya mabadiliko ya lazima katika uhusiano wa ndoa wakati wenzi wote wawili ni waaminifu kwa kila mmoja. Lakini, hata kama ukosefu wa uaminifu umetokea, baadhi ya wenzi wasio na hatia huchagua kuhifadhi ndoa. Badala ya kutegemeza uamuzi kwa kufikiria eti mambo yote yatakuwa sawa, mwenzi asiye na hatia apaswa kupima matokeo yatakayotokea. Bila shaka atafikiria mahitaji ya watoto wake na pia hali yake mwenyewe ya kiroho, kihisia-moyo, kimwili, na mahitaji ya kifedha.b Atakuwa mwenye hekima kufikiria pia ikiwa ndoa yake ina uwezekano wa kuokolewa.
Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa?
Kabla ya kujaribu kujenga upya nyumba iliyoharibiwa na kimbunga, mjenzi lazima apime ikiwa inaweza kujengwa upya. Hali kadhalika, kabla ya kujaribu kujenga upya uhusiano ambao umeharibiwa na ukosefu wa uaminifu, wenzi—hasa mwenzi asiye na hatia—atataka kuchanganua vizuri uwezekano wa kurudishwa kwa ukaribu na itibari katika ndoa.
Jambo la kufikiriwa ni ikiwa mwenzi mwenye kosa aonyesha toba ya moyo mweupe au badala ya hivyo, bado afanya uzinzi “moyoni wake.” (Mathayo 5:27, 28) Ingawa aahidi kubadilika, je, anasita kukomesha mara moja uhusiano wake usio wa adili? (Kutoka 20:14; Mambo ya Walawi 20:10; Kumbukumbu la Torati 5:18) Je, bado aendelea kuwaangalia wanawake wengine kwa kuwatamani? Je, amlaumu mke wake kwa sababu ya uzinzi wake? Ikiwa ndivyo, juhudi za kurudisha itibari kwa ndoa zaelekea hazitafanikiwa. Kwa upande mwingine, ikiwa akomesha uhusiano huo haramu, akubali daraka kwa kosa lake, na aonyesha kujitoa kabisa katika kuijenga upya ndoa, mke wake aweza kuona msingi wa kutumaini kwamba itibari ya kweli yaweza kurudishwa siku moja.—Mathayo 5:29.
Pia, je, mwenzi mwaminifu asamehe kwa kupenda kwake mwenyewe? Hii haina maana kwamba hapaswi kueleza hisia zake za kuumizwa sana kwa habari ya kile kilichotokea au kwamba ajifanye kama hakuna kitu chochote kimebadilika. Humaanisha kwamba katika wakati ufaao, atajitahidi kuondoa uchungu mkuu wa moyo. Msamaha kama huo huchukua wakati lakini waweza kusaidia kuanzisha msingi imara ambao juu yao ndoa yaweza kujengwa upya.
-
-
Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa Baada ya Ukosefu wa Uaminifu?Amkeni!—1997 | Aprili 8
-
-
a Kuna sababu za msingi zinazofanya mtu aweze kuchagua kutaliki mwenzi aliye mzinzi. Kwa mazungumzo zaidi juu ya jambo hili, ona “Maoni ya Biblia: Uzinzi—Kusamehe au Kutosamehe?” katika toleo la Amkeni! la Agosti 8, 1995.
-