Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kukosa Uaminifu—matokeo Yenye Kuhuzunisha
    Amkeni!—1999 | Aprili 22
    • Kukosa Uaminifu—matokeo Yenye Kuhuzunisha

      “Nimeondoka,” ikasema sauti kwenye simu—labda hayo ndiyo maneno yaliyokuwa yenye kuvunja moyo zaidi ambayo Pata aliwahi kuambiwa na mume wake. “Singeweza kuamini usaliti huo,” asema. “Jambo ambalo nilikuwa nimehofu zaidi—kwamba mume wangu angeniacha na kuchukua mwingine—likawa ukweli mchungu.”

      PAT mwenye umri wa miaka 33 alitaka kufanikisha ndoa yao; mume wake alikuwa amemhakikishia kwamba hangemwacha kamwe. “Tulikuwa tumeahidi kukaa pamoja, hata kuwe na matatizo gani,” akumbuka Pat. “Nilisadiki kwamba alikuwa mnyoofu. Kisha . . . aliniacha. Sasa nimeachwa peke yangu—sina hata paka kipenzi nimebaki mpweke kabisa!”

      Hiroshi hatasahau kamwe siku ambayo mama yake aligunduliwa kuwa na uhusiano wa kingono nje ya ndoa. “Nilikuwa na umri wa miaka 11 tu,” akumbuka. “Mama aliingia ndani ya nyumba mbiombio akiwa na hasira. Baba alikuwa nyuma yake, akisema, ‘Usifanye haraka. Acha tuzungumzie jambo hili.’ Ningeweza kuhisi kwamba jambo baya sana lilikuwa limetukia. Baba alivunjika moyo kabisa. Hajapata kurudia tena hali yake ya kawaida. Kwa kuongezea, hakuwa na mtu wa kumtumaini. Hivyo alikuja kwangu. Ebu wazia: mtu mwenye umri wa miaka 40 hivi akimwendea mwanaye mwenye umri wa miaka 11 ili afarijiwe na kuonyeshwa hisia-mwenzi!”

      Hata ziwe ni kashfa za kimapenzi ambazo zimevuruga familia za kifalme, wanasiasa, mashujaa wa sinema, na viongozi wa kidini au uwe ni usaliti na machozi katika familia zetu wenyewe, kukosa uaminifu katika ndoa kwaendelea kusababisha majonzi mengi. Kichapo The New Encyclopædia Britannica, chasema, “inaonekana kwamba uzinzi ni jambo linalokubalika ulimwenguni pote, na katika visa fulani ni wa kawaida kama ndoa.” Watafiti fulani wanakadiria kwamba kati ya watu wapatao asilimia 50 hadi 75 wakati fulani walikosa uaminifu. Mtafiti wa mambo ya ndoa Zelda West-Meads asema kwamba ingawa mara nyingi kukosa uaminifu hakugunduliwi, “uthibitisho mwingi waonyesha kwamba kuna ongezeko la kukosa uaminifu.”

      Hisia Nyingi Kwelikweli

      Ingawa takwimu za kukosa uaminifu na talaka zinashtua, hazifunui madhara kamili yanayowapata watu katika maisha yao ya kila siku. Mbali na hasara kubwa za kifedha, fikiria hisia nyingi sana zinazohusika katika takwimu hizo—machozi mengi sana, na mvurugo unaopita kiasi, kihoro, hangaiko, na maumivu makali sana, na vilevile siku nyingi kupindukia ambazo washiriki wa familia hukosa usingizi. Huenda watu wanaopatwa na masaibu haya wakaendelea kuishi, lakini inaelekea watabaki na maumivu ya kihisia-moyo kwa muda mrefu. Maumivu na madhara hayo hayaishi kwa urahisi.

      “Kwa kawaida mvunjiko wa ndoa hutokeza hisia-moyo nyingi sana,” chaeleza kitabu How to Survive Divorce, “zinakuwa nyingi sana hivi kwamba nyakati fulani hutisha kukuvuruga usijiendeshe kwa busara. Unapaswa kufanya nini? Unapaswa kutenda namna gani? Utakabilianaje na tatizo hilo? Huenda ukayumbayumba kati ya kuwa na uhakika na kuwa na shaka, kati ya kukasirika na kuhisi ukiwa na hatia au kati ya kuwa na itibari na kushuku.”

      Hivyo ndivyo Pedro alivyohisi baada ya kupata habari kwamba mke wake alikosa uaminifu. “Kukosa uaminifu kunapotokea,” aungama hivi, “ndipo hisia-moyo nyingi sana zenye kutatanisha humlemea mtu.” Huwa vigumu sana kwa wahasiriwa kuelewa ile hali ya kuvunjika moyo—sembuse watu wasiohusika, wasioelewa vema hali hiyo. Pat adai kwamba “hakuna mtu yeyote anayeelewa kikweli jinsi ninavyohisi. Ninapofikiri juu ya mume wangu akiwa na mwanamke mwingine, mimi huhisi maumivu halisi ya kimwili, kuumwa ambako ni vigumu kuelezea mtu yeyote.” Aongezea hivi: “Kuna nyakati fulani ambapo mimi huhisi kana kwamba ninashikwa na kichaa. Siku moja ninahisi kana kwamba ninaweza kudhibiti hali; siku inayofuata nahisi siwezi. Siku moja mimi humkosa; siku inayofuata hukumbuka njama zote, udanganyi wote na kutwezwa kote alikofanya.”

      Hasira na Hangaiko

      “Nyakati fulani,” akiri mtu mmoja ambaye mwenzi wake alikosa uaminifu, “hisia-moyo inayokukumba ni hasira tu.” Si ghadhabu tu kuhusu kosa lililofanywa na madhara yaliyosababishwa. Badala ya hivyo, kama alivyoeleza mwandishi mmoja wa habari, ni “uchungu wa moyo kuhusu ndoa ambayo ingekuwa nzuri, lakini ikaharibiwa.”

      Pia hisia za kutojistahi na kutofaa huwa jambo la kawaida. Pedro akiri hivi: “Unakuwa na hisia hizi: ‘Je, sivutii vya kutosha? Je, nina kasoro kwa njia fulani?’ Unaanza kujichanganua ili upate kosa.” Katika kitabu chake To Love, Honour and Betray, Zelda West-Meads, wa Baraza la Kitaifa la Mashauri ya Ndoa la Uingereza, atoa uthibitisho huu: “Mojawapo ya mambo magumu zaidi kukabiliana nayo . . . ni kutojistahi.”

      Hatia na Mshuko-Moyo

      Kwa kawaida hisia-moyo hizi hufuatiwa kwa haraka na hisia nyingi za hatia. Mke mmoja aliyekata tamaa asema: “Nafikiri wanawake husumbuliwa sana na hatia. Unajilaumu mwenyewe na kujiuliza: ‘Ni jambo gani baya nililofanya?’”

      Mwanamume mmoja aliyesalitiwa afunua jambo jingine analoliita hisia-moyo zinazobadilika kwa ghafula. Aeleza hivi: “Mshuko-moyo unakuwa jambo jipya ambalo hutokea kama halihewa mbaya.” Mwanamke mmoja anakumbuka kwamba baada ya kuachwa na mume wake, hakuna siku hata moja ambayo hakulia. “Naweza kukumbuka waziwazi siku ya kwanza ambayo sikulia majuma kadhaa baada ya kuachwa,” asimulia. “Miezi kadhaa ilipita kabla sijamaliza juma moja bila kulia. Siku na majuma ambayo sikulia yakawa matukio muhimu yaliyoashiria kurudia hali yangu ya kawaida.”

      Udanganyifu Maradufu

      Jambo wasilotambua watu wengi ni kwamba mara nyingi mzinzi anakuwa amemwumiza sana mwenzi wake maradufu. Katika njia gani? Pat atupatia dokezo: “Ilikuwa vigumu kwa upande wangu. Hakuwa tu mume wangu bali pia rafiki yangu—rafiki bora zaidi—kwa miaka mingi.” Ndiyo, katika visa vingi mke humwendea mume wake ili kupata utegemezo matatizo yanapotokea. Sasa, hajawa tu chanzo cha matatizo yenye kufadhaisha bali pia ameacha kuwa chanzo cha msaada kinachohitajiwa sana. Katika tendo moja, amesababisha maumivu makali na kumnyang’anya mke wake mtu wa kutumaini.

      Tokeo ni kwamba, mojawapo ya mambo yanayowalemea wenzi wasio na hatia ni hisi ya kina kirefu ya kusalitiwa na kuvunjwavunjwa kwa imani. Mshauri mmoja wa ndoa aeleza sababu kwa nini usaliti wa ndoa waweza kusababisha madhara makubwa sana ya kihisia-moyo: “Tunajitoa sana sisi wenyewe, matumaini yetu, miradi na mataraja yetu, kwa ndoa . . . , tukitafuta mtu fulani tunayeweza kumwitibari kikweli, mtu tunayehisi tunaweza kumtegemea sikuzote. Itibari hiyo inapopotezwa kwa ghafula, inaweza kuwa kama nyumba iliyojengwa kwa karata inayoanguka ghafula.”

      Kwa wazi, kama inavyosemwa katika kitabu How to Survive Divorce, wahasiriwa “wanahitaji msaada kuchanganua mabadiliko makubwa ya kihisia-moyo . . . Huenda wakahitaji msaada wa kuamua ni mambo gani watakayofanya na jinsi ya kuyafanya.” Lakini mambo hayo ni yapi?

      Huenda ukajiuliza, ‘Je, kupatana ndilo suluhisho letu?’ ‘Au je, nitaliki?’ Hasa ndoa inapokuwa na mikazo, waweza kuchochewa kufikia mkataa wa haraka kwamba talaka ndiyo suluhisho kwa matatizo yenu. Huenda ukasababu kwamba ‘kwa vyovyote, Biblia huruhusu talaka kwa msingi wa kukosa uaminifu katika ndoa.’ (Mathayo 19:9) Kwa upande mwingine, huenda ukasababu kwamba Biblia haisisitizi juu ya talaka. Kwa hiyo, waweza kuhisi kwamba ingekuwa bora kutafuta upatanisho, kujenga upya ndoa na kuiimarisha.

      Kumtaliki au kutomtaliki mwenzi asiye mwaminifu ni uamuzi wa kibinafsi. Lakini unaweza kujuaje jambo la kufanya? Kwanza, tafadhali chunguza baadhi ya mambo yanayoweza kukusaidia kuamua ikiwa kupatana kunawezekana.

  • Je, Kupatana Kwawezekana?
    Amkeni!—1999 | Aprili 22
    • Je, Kupatana Kwawezekana?

      “Ni rahisi kuanza kutafuta talaka kwa ghafula,” chasema kitabu “Couples in Crisis,” “lakini lazima kuwe na ndoa nyingi ambazo kwa msingi zinafaa na ambazo zingeweza kufanikiwa ikiwa matatizo yangetatuliwa.”

      MAONI hayo yapatana na fundisho la Yesu Kristo la kale kuhusu talaka. Ijapokuwa alisema kwamba mwenzi asiye na hatia anaruhusiwa kuchukua talaka kwa msingi wa kukosa uaminifu katika ndoa, hakusema kwamba ilikuwa lazima kufanya hivyo. (Mathayo 19:3-9) Huenda mwenzi mwaminifu akawa na sababu za kutaka kuokoa ndoa. Huenda mume mkosaji akawa bado anampenda mke wake bado.a Huenda akawa ni mume mwenye kujali na baba mwenye kujitoa anayeandaa mahitaji ya familia yake kwa kudhamiria. Kwa kufikiria mahitaji yake na yale ya watoto, huenda mwenzi mwaminifu akaamua kutafuta kupatana badala ya talaka. Ikiwa ndivyo, ni mambo gani yanayoweza kufikiriwa, na magumu ya kujenga ndoa upya yanaweza kukabiliwaje kwa mafanikio?

      Kwanza ujue kwamba wala talaka wala kupatana si rahisi. Zaidi ya hayo, kumsamehe tu mwenzi mzinzi hakuelekei kutatatua matatizo ya msingi katika ndoa. Kwa kawaida ili kuokoa ndoa, kujichunguza kwa undani, mawasiliano ya waziwazi, na kazi ngumu hutakikana. Mara nyingi wenzi wa ndoa hupuuza kiasi cha wakati kinachotakikana na jitahada zinazotakikana kujenga upya ndoa iliyovunjika. Hata hivyo, wengi wamevumilia na kama tokeo wamekuwa na ndoa zilizo imara.

      Maswali ya Kujibiwa

      Ili kufanya uamuzi unaotegemea habari fulani, mwenzi mwaminifu anapaswa kuchanganua hisia zake na mambo tofauti-tofauti anayoweza kuchagua. Huenda akafikiria mambo yafuatayo: Je, anataka kurudi? Je, amekomesha kabisa kufanya uzinzi, au anasitasita kukomesha uhusiano huo? Je, ameomba radhi? Ikiwa ndivyo, je, ametubu kikweli, amejuta kwa moyo mweupe kuhusu jambo alilofanya? Au je, anaelekea kunilaumu kwa kosa lake? Je, anajuta kikweli kwa madhara ambayo amesababisha? Au badala ya hivyo, amefadhaika tu kwa sababu uhusiano wake haramu umefunuliwa na kuvurugwa?

      Vipi kuhusu wakati ujao? Je, ameanza kurekebisha mitazamo na matendo yalioongoza kwenye uzinzi? Je, ameazimia kwa dhati kutorudia kosa hilo? Au bado ana mwelekeo wa kucheza kimahaba na kuwa na uhusiano wa kihisia-moyo usiofaa na watu wa jinsia tofauti? (Mathayo 5:27, 28) Je, amejitoa kikamili kujenga ndoa upya? Ikiwa ndivyo, anafanya nini kuhusu jambo hilo? Majibu yafaayo kwa maswali haya yaweza kuwa msingi wa kuamini kwamba inawezekana kurudisha uhusiano wa ndoa.

      Mawasiliano Muhimu

      “Pasipo mashauri,” asema mwandishi mmoja wa Biblia, “makusudi hubatilika.” (Mithali 15:22) Kwa hakika inakuwa hivyo mwenzi asiye na hatia anapohitaji kuzungumza kuhusu ukosefu huo wa uaminifu pamoja na mwenzi wake. Bila kuingilia mambo ya ndani sana isivyo lazima, wangeweza kuwa na mazungumzo yaliyo wazi na ya umakini ambayo yangeweza kutokeza ukweli kuhusu kilichotokea na kumaliza kutoelewana. Jambo hili laweza kuzuia wenzi wasizidi kutengana kwa sababu ya kutoelewana na kuwa na uchungu wa moyo wa muda mrefu. Ni kweli kwamba mume na mke wataona mazungumzo hayo kuwa yenye kutia uchungu. Lakini wengi wameona kwamba yanachangia fungu muhimu katika hatua ya kuaminiana tena.

      Hatua nyingine muhimu kuelekea kupatana kwa njia yenye matokeo ni kujaribu kutambua sehemu zenye matatizo katika ndoa—mambo ambayo huenda wenzi wote wawili wakahitaji kuyafanyia kazi. Zelda West-Meads, ashauri hivi: “Baada ya kuzungumzia hali zenye kuhuzunisha, baada ya kuamua kwamba kwa kweli jambo hilo limemalizika, kwamba bado mnataka kubaki katika ndoa, tatueni kosa lililotokea na kuifanya upya ndoa [hiyo].”

      Labda mlichukuliana kivivihivi. Huenda mlipuuza shughuli za kiroho. Labda hamkuwa mkitumia wakati wa kutosha pamoja. Labda hukumwonyesha mwenzi wako upendo mwingi, shauku nyororo, pongezi, na heshima aliyohitaji. Kukadiria upya miradi na maadili yenu mkiwa pamoja kutachangia fungu kubwa kuwaleta karibu zaidi na kutazuia kukosa uaminifu wakati ujao.

      Kufanyia Kazi Msamaha

      Kujapokuwa jitihada za moyo mweupe, huenda mwenzi aliyekosewa asione likiwa jambo rahisi kumsamehe mume wake, sembuse mwanamke yule mwingine. (Waefeso 4:32) Ingawa hivyo, inawezekana kuachilia mbali uchungu wa moyo hatua kwa hatua. Kitabu kimoja cha marejezo chashauri kwamba “mwenzi mwaminifu anapaswa kutambua kwamba wakati hufika ambapo wanahitaji kuacha kufikiria mambo hayo na kuanza maisha upya.” “Ni muhimu kutoendelea kutaja dhambi za zamani za mwenzi wako ili ku[mwa]dhibu kila mara mnapobishana.”

      Wenzi wengi wameona kwamba kwa kujitahidi kupunguza au kuondoa hisia zenye uchungu mwingi, hatimaye wameacha kuhisi uhasama kuelekea mkosaji. Hiyo ni hatua ya maana katika kujenga ndoa upya.

      Jifunze Kumwamini Tena

      “Je, tutaweza kuaminiana tena?” akasema kwa maumivu mwanamke mmoja mwenye wasiwasi. Hangaiko lake ni halali kwa sababu udanganyifu wa mzinzi umeharibu—au angalau ukadhuru vibaya sana—kuaminiana. Kama vile chombo cha kuwekea maua chenye thamani, ni rahisi kuvunja tumaini lakini ni vigumu kulijenga. Uhakika ni kwamba wenzi wanapaswa kuaminiana na kustahiana, si kuendeleza tu uhusiano bali kuufanya usitawi.

      Kwa kawaida itatia ndani kujifunza kumwamini mtu tena. Badala ya kudai kuaminiwa bila kujali hisia za mwenzake, mwenzi mwenye hatia anaweza kusaidia kujenga upya imani kwa kuwa wazi na kufuatia haki kabisa kuhusu utendaji wake. Wakristo wanatiwa moyo ‘waweke mbali ukosefu wa lililo kweli na kusema kweli’ mtu na mwenzake. (Waefeso 4:25) Ili kuaminiwa tena, huenda hapo mwanzoni “ukampa [mwenzi] wako ratiba sahihi kuhusu mipango yako hasa,” asema Zelda West-Meads. “Mwambie [mwenzi] wako mahali unapoenda, wakati utakaporudi na uhakikishe kwamba upo mahali uliposema utakuwapo.” Mipango ikibadilika, umwarifu.

      Huenda kujistahi tena kukahitaji wakati na jitihada. Mwenzi mwenye hatia anaweza kusaidia kwa kuwa mwenye shauku nyingi na mwenye kupongeza sana—akimwambia mke wake mara nyingi kwamba anathaminiwa na kupendwa. Mshauri wa ndoa anayeheshimiwa ashauri hivi: “Mpe sifa kwa yote anayofanya.” (Mithali 31:31, Today’s English Version) Mke pia kwa upande wake, anaweza kujistahi tena kwa kufikiria mambo fulani maishani ambayo yeye hufanya vyema.

      Inahitaji Wakati

      Kwa kufikiria maumivu makali sana yanayosababishwa na kukosa uaminifu, haishangazi kwamba baada ya miaka mingi inawezekana kumbukumbu zilizo dhahiri na zenye kuhuzunisha zikawako. Hata hivyo, maumivu yanapopungua hatua kwa hatua, unyenyekevu, saburi, na uvumilivu kwa upande wa wote zitasaidia kujenga upya imani na staha.—Waroma 5:3, 4; 1 Petro 3:8, 9.

      “Maumivu mabaya sana ya miezi michache ya kwanza hayadumu,” chatoa uhakikisho kitabu To Love, Honour and Betray. “Hatimaye [hu]pungua . . . Hatimaye unakuta kwamba siku, majuma, miezi na hata miaka inaweza kupita bila wewe kuyafikiria.” Unapoendelea kutumia kanuni za Biblia katika ndoa yako na kutafuta msaada na mwongozo wa Mungu, bila shaka utapata matokeo yenye kutuliza ya “amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora.”—Wafilipi 4:4-7, 9.

      “Ninapokumbuka,” aripoti Pedro, “jambo hilo limebadili mwendo wa maisha yetu. Bado twahitaji kufanya marekebisho machache kwa ndoa yetu mara kwa mara. Lakini tumeokoka masaibu hayo. Bado tumefunga ndoa. Na tuna furaha.”

      Lakini vipi ikiwa mwenzi asiye na hatia hana sababu ya kumsamehe yule asiye mwaminifu? Au vipi ikiwa anamsamehe mwenzi wake (kwa kiwango cha kuachilia uchungu wa moyo) na bado akiwa na sababu halali aamua kuchukua talaka inayokubaliwa na Biblia?b Talaka inaweza kumdai mtu mambo gani? Twakukaribisha ufikirie mambo yanayohusika katika talaka, na vilevile jinsi ambavyo wengine wamekabiliana nayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ili kusahilisha mambo, kwa ujumla tutamtaja mwenzi mwaminifu kuwa mke. Hata hivyo, kanuni zinazozungumziwa pia zawahusu waume ambao wake zao si waaminifu.

      b Tafadhali ona makala “Maoni ya Biblia: Uzinzi—Kusamehe au Kutosamehe?” katika toleo la Amkeni! la Agosti 8, 1995.

      [Sanduku katika ukurasa wa 6]

      MSAADA WA MAANA

      Kwa kufikiria mambo mengi yanayoweza kuzingatiwa, huenda ikanufaisha kutafuta msaada kutoka kwa mshauri mwenye uzoefu na usawaziko. Kwa kielelezo, Mashahidi wa Yehova, wanaweza kuwafikia wazee wa kutaniko walio na fadhili na huruma.—Yakobo 5:13-15.

      Washauri, marafiki, na jamaa wanatiwa moyo wasisisitize juu ya mapendezi yao wenyewe au kutetea au kulaumu uamuzi uliochukuliwa wa ama talaka iliyo na msingi wa Kimaandiko ama kupatana. Mwanamke mmoja Mkristo aliyetalikiwa anasihi hivi: “Toeni tu utegemezo mwingi, na mtuache tuamue la kufanya.”

      Shauri lapaswa kutegemea Biblia peke yake. “Msiwaambie jinsi wanavyopaswa kuhisi au wasivyopaswa kuhisi,” adokeza mtu mmoja aliyetalikiwa. “Badala ya hivyo, waruhusuni wajieleze kwa uhuru.” Hisia-mwenzi, shauku ya kidugu, na huruma nyororo zitasaidia kupunguza majeraha makubwa sana yaliyosababishwa na usaliti wa ndoa. (1 Petro 3:8) Mshauri mwenye uzoefu alisema hivi: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.”—Mithali 12:18.

      Mume mmoja mwaminifu asema hivi: “Nilihitaji mtu mwenye kunielewa, maneno ya kufariji, na kutiwa moyo.” “Na mke wangu alitamani kupata mwelekezo hususa na kupongezwa kwa jitihada alizokuwa akifanya—msaada unaoonekana ambao ungemsaidia aendelee.”

      Ikiwa baada ya kufikiria sana kwa uangalifu na kwa sala mtu aamua kumtaliki mwenzi wake au kutengana akiwa na sababu ya Kimaandiko, shauri lisitolewe katika njia inayoweza kumfanya mtu huyo ahisi kuwa na hatia. Badala ya hivyo, mtu huyo aweza kusaidiwa ashinde hisia za hatia zisizo na msingi.

      “Ikiwa wataka kuwa chanzo bora cha kutoa faraja,” asema mhasiriwa mmoja, “usisahau kamwe hisia-moyo za kibinadamu zenye kina kirefu zinazohusika.”

      [Sanduku katika ukurasa wa 7]

      SABABU INAYOFANYA WENGINE WASIACHANE

      Katika jumuiya nyingi, kuna wake ambao hawana chaguo jingine ila kubaki na mume mzinzi asiyetubu. Kwa kielelezo, wanawake fulani Wakristo wanaoishi katika maeneo yenye ­mizozo au yenye kiwango cha chini cha kiuchumi wamebaki pamoja na mume asiye mwaminifu kwa ndoa ambaye huendelea kutunza watu wa nyumba yake katika mambo fulani-fulani, hata ingawa huenda asiwe mwamini. Kama tokeo, wana makao, ulinzi unaohitajiwa, mapato yenye kutegemeka, na uthabiti wa kiasi fulani wa kuwa na baba nyumbani—hata ingawa huenda asiwe mwaminifu. Wamesababu kwamba kwa kubaki pamoja, ijapokuwa si jambo linalopendeza au lililo rahisi, kumewawezesha—katika hali zao hususa—kudhibiti maisha yao kwa kiwango kikubwa kuliko jinsi ambavyo wangefanya ikiwa wangeng’ang’ana kivyao.

      Baada ya kuvumilia hali hiyo—nyakati nyingine kwa miaka mingi—baadhi ya wake hawa hatimaye wamepata shangwe ya kuona waume wao wakibadili njia zao na kuwa Wakristo waaminifu na wenye upendo.—Linganisha 1 Wakorintho 7:12-16.

      Kwa hiyo, wale wanaoamua kubaki na mwenzi—hata ikiwa si mwenye kutubu—hawapaswi kuchambuliwa. Wamelazimika kufanya uamuzi mgumu na wanapaswa kupewa msaada wowote na utegemezo wanaohitaji.

      [Sanduku katika ukurasa wa 8]

      NI NANI MWENYE KULAUMIKA?

      Ni kweli kwamba katika visa fulani huenda kutokamilika kwa mwenzi kuwe kulichangia mkazo katika uhusiano, lakini Biblia husema kwamba “kila mmoja hujaribiwa kwa kuvutwa na kutongozwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetungika mimba, huzaa dhambi; nayo, dhambi, wakati imetimilika, hutokeza kifo.” (Yakobo 1:14, 15) Ijapokuwa kunaweza kuwa na mambo mbalimbali yanayochangia uzinzi, ‘tamaa ya mtu mwenyewe’ ndiyo hasa kisababishi cha msingi. Ikiwa kasoro za mwenzi husababisha matatizo ya ndoa, kwa hakika kufanya uzinzi si njia ya kuzitatua.—Waebrania 13:4.

      Badala yake, matatizo ya ndoa yanaweza kutatuliwa mume na mke wakitumia daima kanuni za Biblia. Inatia ndani “kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.” Pia wanapaswa kudumu katika kudhihirisha sifa kama vile “shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu.” La maana zaidi, wanapaswa ‘kujivika wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.’—Wakolosai 3:12-15.

  • Kuchagua Talaka
    Amkeni!—1999 | Aprili 22
    • Kuchagua Talaka

      “Mwenzi wako wa ndoa akifa, watu wanaelewa hali yako hata ikiwa hukuwa mwenzi wa ndoa aliye bora. Lakini mume wako akikuacha—wengine, hufikiri hukuwa mke mwema. Tafadhali, tafadhali, NISAIDIENI!”—Msomaji wa Amkeni! katika Afrika Kusini.

      KUKOSA uaminifu na talaka ni mambo yanayoweza kufadhaisha sana. Hata ingawa wengi wamepata sababu za kupatana na wenzi wao na kuhifadhi ndoa yao, wengine wana sababu halali za kufanya uchaguzi unaokubalika na Mungu wa kumtaliki mwenzi mzinzi. (Mathayo 5:32; 19:9) Kwa kielelezo, usalama, hali ya kiroho, na hali nzuri ya ujumla ya mke mwaminifu pamoja na watoto wake yaweza kuwa hatarini. Huenda pia akawa na wasiwasi kuhusu kuambukizwa maradhi yanayopitishwa kingono. Au labda amemsamehe mwenzi wake kwa kufanya uzinzi, lakini hakuna msingi wa kutumaini kwamba kuaminiana halisi kwaweza kupatikana tena na kwamba anaweza kuendelea kuishi pamoja naye akiwa mume wake.

      “Huu ulikuwa uamuzi mgumu zaidi mai­shani mwangu,” akakiri mke mmoja aliyefadhaika. Ni uamuzi mgumu kwelikweli—si kwa sababu tu kusalitiwa husababisha maumivu makali bali pia talaka huleta matokeo ya muda mrefu yatakayoathiri maisha yake yote. Kwa hiyo, kama mke apaswa kumtaliki au kutomtaliki mwenzi wake asiye mwaminifu huo ni uamuzi wa kibinafsi. Haki ya mwenzi huyo inayoungwa mkono na Biblia kuhusu uamuzi huo yapaswa kuheshimiwa na wengine.

      Ingawa hivyo, kwa kusikitisha watu wengi hufanya haraka kutaliki wenzi wao kabla ya kuhesabu gharama vizuri. (Linganisha Luka 14:28.) Ni mambo gani yanayotiwa ndani katika kuchagua talaka?

      Ikiwa Kuna Watoto

      “Mara nyingi mahitaji ya watoto husahauliwa au hupuuzwa na wazazi ambao hujizamisha katika matatizo yao,” chasema kitabu Couples in Crisis. Hivyo, unapofikiria kumtaliki mwenzi wako, kumbuka hali ya kiroho na hali njema ya watoto wako. Watafiti wengi wanasema kwamba kadiri talaka iwavyo ya amani, ndivyo yaelekea watoto hawatateseka sana. Hata chini ya hali ngumu, upole utamsaidia mtu ‘asipigane, bali awe mwanana kuelekea wote, akijizuia mwenyewe chini ya uovu.’—2 Timotheo 2:24, 25.a

      Mtu akichagua kutaliki, yapasa ikumbukwe kwamba ni mume na mke—si watoto—wanaotalikiana. Bado watoto wanahitaji Mama na Baba. Bila shaka, kwaweza kukawa na hali zinazopita kiasi, kama vile mtoto anapokuwa katika hatari ya kutendwa vibaya. Lakini tofauti za kidini au za kibinafsi hazipasi kutumiwa kuzuia watoto wasipate manufaa ya kuwa na wazazi wawili.

      Kwa kuongezea, jambo linalohitaji kufikiriwa ni hisia-moyo za watoto zinazoweza kuathirika kwa urahisi na uhitaji wa kupewa uhakikishio, upendo, na shauku ya kutosha. “Upendo huu unapoendelezwa,” chasema kitabu kimoja, “utawaandalia msingi wa kukabiliana na hali hiyo mpya.” Pia, kuhangaikia mahitaji yao ya kiroho ya kila siku kwaweza kuwasaidia wadumishe hali imara.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Mathayo 4:4.

      Mambo ya Kifedha na ya Kisheria

      Bila kuepukika talaka humnyang’anya kila mwenzi kiasi fulani cha mapato na mali, hali-njema ya kiasi fulani, na labda makao yaliyotunzwa vizuri. Kwa kuwa huenda mtu akahitaji kushughulikia matumizi yaliyoongezeka kwa mapato yaliyopungua, ni jambo la hekima kupanga bajeti iliyo halisi kulingana na mambo ya kutangulizwa kifedha. Msukumo wa kutaka kulipia hasara na maumivu ya kihisia-moyo kwa kutumia fedha nyingi zaidi au kuwa na deni wapaswa kuepukwa.

      Ikiwa uamuzi unafikiwa wa kutalikiana, ni lazima pia mtu pamoja na mwenzi wake waamue namna watakavyoshughulika na akaunti za pamoja za benki. Kwa kielelezo, ili kuzuia matumizi mabaya ya fedha katika akaunti za pamoja za benki, huenda likawa jambo la hekima kumwomba meneja wa benki aombe sahihi za wenzi wote wawili wanapotaka kutoa fedha hadi kila mmoja atakapokuwa na akaunti yake mwenyewe.

      Pia ni jambo la busara kuweka rekodi nzuri za mapato na matumizi, unapojitayarishia majadiliano ya fedha utakazokuwa unapewa kwa matumizi. Katika nchi nyingi pia, ni takwa la kisheria kwamba watu wawaeleze wasimamizi wa kodi kuhusu badiliko la hali yao.

      Kwa kuongezea, watu wengi zaidi hunufaika kwa kutafuta mashauri kutoka kwa mtaalamu wa mambo ya kisheria—mtu ambaye ana uzoefu hususa katika masuala ya talaka. Nchi fulani huruhusu wapatanishi wawasaidie wenzi washirikiane kufikia makubaliano ya pamoja na ya amani, ambayo baadaye huthibitishwa rasmi na mahakama ya kisheria. Hasa katika visa vinavyohusisha watoto, wazazi wengi hupendelea kutafuta huduma za mtaalamu asiye na upendeleo. Badala ya kujipatia faida kubwa za kimwili, wazazi hunuia kupunguza kuhitilafiana na kuumizana. Vitu fulani vya kimwili kwa kweli havistahili kumfanya mtu ateseke kihisia-moyo na kutumia fedha nyingi.

      Uhusiano Uliobadilika

      “Hatupaswi kudharau mfadhaiko na ukosefu wa uhakika ambao watu wengi huhisi kuhusu marafiki wao waliotalikiana,” asema mtafiti mmoja. Hata ikiwa mwenzi mwaminifu anachukua hatua kulingana na haki zake za kisheria, kiadili, na Kimaandiko, huenda kukawa na wengine watakaomwona kuwa kisababishi cha kuvunjika kwa ndoa. Huenda wakaonyesha hivyo kwa kumsalimu kwa ubaridi hadi kufikia hatua ya kumwepuka waziwazi. Lililo baya hata zaidi, ni kwamba waandamani wa karibu wa zamani waweza kumwonyesha uhasama wa waziwazi.

      Kwa kweli wengi hawatambui mtu huhitaji utegemezo kiasi gani anapotaliki; huenda wakafikiri kwamba barua fupi au kadi inatosha. Hata hivyo, kwa kawaida kuna marafiki ambao “huonyesha hisia-mwenzi zinazofaa,” chasema kitabu Divorce and Separation, “na watakutembelea kuona ikiwa unataka mtu wa kuandamana naye mahali popote, unataka ufanyiwe jambo fulani au ikiwa unataka kuzungumza tu.” Kwa kweli, wakati huo maishani, mtu huhitaji, kama Biblia isemavyo, “rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.”—Mithali 18:24.

      Kujaribu Kurudia Hali ya Kawaida

      Miaka 16 baada ya kutalikiana, mama mmoja akiri hivi: “Bado kuna nyakati ambazo ninahisi upweke kwelikweli—hata ninapokuwa na watu wengine.” Yeye hukabilianaje na hali hiyo? “Nimebuni utaratibu wa kufanya mambo mengi,” akumbuka, “kwa kuwa na shughuli nyingi kazini, kumtunza mwana wangu, na kutunza nyumba yangu. Pia nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, na kushiriki itikadi zangu pamoja na majirani, na kuwafanyia wengine mambo. Kufanya hivyo kulisaidia sana.”

      Tarehe na nyakati fulani za mwaka zaweza kuamsha kumbukumbu na hisia-moyo zenye kuhuzunisha: siku ambayo kukosa uaminifu kulifunuliwa, wakati alipotoka nyumbani, ta­rehe ya kesi ya mahakamani. Matukio yenye furaha ambayo wenzi walishiriki—kama vile kwenda likizo na ukumbusho wa kila mwaka wa arusi—yaweza kuwa mambo yaliyo magumu kushughulika nayo kihisia-moyo. “Mimi hushughulika na siku hizo kwa kupanga nitumie wakati pamoja na familia yangu au na marafiki wa karibu wanaofahamu hali yangu,” asema Pat. “Sisi hufanya mambo yatakayofuta mawazo ya zamani na kuwa na kumbukumbu mpya. Lakini mimi hupata msaada mkubwa zaidi kupitia uhusiano wangu na Yehova—nikijua kwamba yeye huelewa ninavyohisi.”

      Usikate Tumaini

      Wenzi wasio na hatia ambao hutumia kanuni za Biblia na kuamua kufuatia haki waliyopewa na Mungu ya kumtaliki mwenzi mzinzi hawapaswi kuhisi hatia au kuhofu kwamba Yehova amewatupa. Mwendo wa udanganyifu wa mwenzi mzinzi—ambao umesababisha “kulia na kuugua”—ndio humchukiza Mungu. (Malaki 2:13-16) Hata Yehova, Mungu mwenye “huruma nyororo,” anajua jinsi ambavyo mtu huhisi anapokataliwa na mpendwa wake. (Luka 1:78; Yeremia 3:1; 31:31, 32) Basi, uwe na hakika kwamba, “BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake.”—Zaburi 37:28.

      Bila shaka, ingekuwa afadhali ikiwa hapo mwanzoni kukosa uaminifu katika ndoa na matokeo yake mabaya yangeepukwa. Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia,b ambacho ni mwongozo unaotumika wa familia, kinasaidia watu wengi ulimwenguni pote kujenga ndoa zenye furaha na kuepuka kukosa uaminifu katika ndoa. Kina sura zinazohusu kujenga ndoa yenye furaha, kuwazoeza watoto, na kukabiliana na matatizo ya ndoa. Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au wachapishaji wa gazeti hili watafurahi kuandaa habari zaidi.

      [Maelezo ya Chini]

      a Habari zaidi yaweza kupatikana katika mfululizo wa makala “Malezi ya Mtoto—Ni Maoni Gani Yaliyosawazika?” katika toleo la Amkeni! la Desemba 8, 1997, na kwenye makala “Kusaidia Watoto wa Talaka,” ya Aprili 22, 1991, Kiingereza.

      b Kimechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

      [Sanduku katika ukurasa wa 10]

      WATOTO HAWASTAHILI KUWA NA WAZAZI WALIOTALIKIANA

      Mwaka wa 1988 Diana aliyekufa, Binti-Mfalme wa Wales, alisema kwamba katika Uingereza peke yake, kila siku watoto 420 hushuhudia wazazi wao wakitalikiana. Thuluthi moja ya watoto hao wana umri unaopungua miaka mitano. Kwa kuhuzunisha, asilimia 40 hivi ya watoto hao hupoteana kabisa na mmoja wa wazazi wao baada ya talaka.

      Kinyume cha vile watu wengi hufikiri, “ni watoto wachache sana wa wazazi waliotalikiana hukubali mvunjiko huo,” asema mwandishi anayeheshimiwa wa masuala ya afya na ya kitiba. “Watoto wengi wangependelea kuona wazazi wao wakiishi pamoja hata ikiwa hali ya familia ni ngumu.” Hata ikiwa wenzi walibishana sana wakati kukosa uaminifu kulipogunduliwa, hawakupaswa kufikia kwa haraka mkataa wa kwamba kuvunja ndoa kungeleta hali bora kwa watoto. Kufanya mabadiliko katika mtazamo na tabia yao kwaweza kuwafanya waendelee kuishi pamoja kwa hali-njema ya familia nzima.

      “Waume wanaofanya ngono za ovyo-ovyo,” asema mwandishi Pamela Winfield, “wanapaswa kufikiri juu ya maumivu watakayosababishia watoto wao nyumba yao itakapovunjika kufuatia upumbavu wao.”

      [Sanduku katika ukurasa wa 11]

      JE, MUNGU HUCHUKIA TALAKA ZOTE?

      “Jambo lililonitia wasiwasi zaidi,” akiri Pat, “lilikuwa wazo la kwamba ‘BWANA huchukia kuachana.’ Sikuzote akilini mwangu nilikuwa nikijiuliza, ‘Je, ninafanya jambo linalompendeza Yehova?’”

      Acheni tutazame muktadha wa Malaki 2:16 ili kujibu swali hilo. Katika siku za Malaki yawezekana wanaume wengi Waisraeli walikuwa wakiwataliki wake zao, ili kuoa wanawake wapagani, wachanga zaidi. Mungu alishutumu mwenendo huu wenye udanganyifu na hila. (Malaki 2: 13-16) Kwa sababu hiyo, jambo analochukia Mungu ni mtu kumtupilia mbali mwenzi wake kwa sababu isiyo na msingi ili kuchukua mwenzi mwingine. Mtu anayefanya uzinzi kwa njia ya udanganyifu na kisha ama anamtaliki mwenzi wake ama anamsonga mwenzi wake amtaliki anakuwa amefanya dhambi yenye hila na yenye kuchukiza.

      Hata hivyo, mistari hii haishutumu talaka zote. Hili laweza kuthibitishwa na maneno ya Yesu: “Yeyote yule atalikiye mke wake, ila kwa sababu ya uasherati, na kuoa mwingine afanya uzinzi.” (Mathayo 19:9) Hapa Yesu alikiri kwamba uasherati ni msingi unaokubalika wa kutaliki Kimaandiko—kwa kweli, ndio msingi pekee unaokubalika ili kufunga ndoa tena. Mwenzi asiye na hatia aweza kuamua kumsamehe mwenzi aliyekosea. Hata hivyo, mtu anayeamua kutumia taarifa ya Yesu kama msingi wa kumtaliki mwenzi mzinzi hafanyi jambo linalomchukiza Yehova. Mungu huchukia mwenendo wa mwenzi wa ndoa wa kukosa uaminifu na wenye udanganyifu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki