-
Albania2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KUTAMBULIWA KISHERIA HATIMAYE!
Majuma kadhaa yaliyofuata, akina ndugu walitumia muda mwingi wakizungumza na wanasheria na maafisa wengine, wakijaribu kusajili kisheria kazi ya kuhubiri Ufalme. Tayari kikundi cha akina ndugu na watu wanaopendezwa kilichokuwa Tiranë kilikuwa kimetoa maombi rasmi, lakini sasa kulikuwa na serikali nyingine mamlakani, kwa hiyo, jitihada zilihitajiwa.
“Kila mahali tulipokwenda, tulikwenda kwa miguu,” akumbuka ndugu mmoja. “Tulipokuwa tukitembea mjini, tulikuwa tukikutana na waziri wa haki za kibinadamu, waziri wa mambo ya ndani, waziri wa haki, mkuu wa polisi, washiriki wa mahakama ya kikatiba, na watu wengine wenye mamlaka. Watu hao walikuwa na fadhili na walifurahi kwamba mambo yalikuwa yameanza kuwa mazuri. Tayari wengi wao walijua kuhusu ungjillorë. Hakukuwa na shaka kamwe kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiendesha shughuli zao nchini Albania.”
Kwa majuma kadhaa, maafisa walikuwa wamesema kwamba serikali itawasajili rasmi Mashahidi wa Yehova, lakini hakuna lolote lililofanywa. Hata hivyo, matumaini yalipatikana wakati Angelo Felio, ndugu kutoka Marekani mwenye asili ya Kialbania, alipotembelea familia yao mjini Tiranë. Alipokuwa Albania, Angelo aliandamana na ndugu hao kwenda kumwona mshauri wa waziri wa serikali aliyekuwa na mamlaka ya kutusajili rasmi. Mshauri huyo alifurahi alipojua kwamba familia ya Angelo inatoka katika eneo moja na familia yao.
“Kwenu ni wapi?” akamwuliza Angelo. Kwa kushangaza, wote walikuwa watu wa kijiji kimoja.
“Ukoo wenu?” akauliza.
Amini usiamini, walikuwa watu wa familia moja, lakini familia zao hazikuwa zimeonana kwa miaka mingi.
“Karatasi zenu ziko sawa, nami nilikuwa tayari kuwasaidia,” akasema. “Lakini sasa, sina budi kufanya hivyo, kwa kuwa wewe ni wetu!”
Siku chache baadaye, mshauri huyo akawakabidhi akina ndugu Oda Na. 100, iliyowatambua kisheria Mashahidi wa Yehova nchini Albania. Hatimaye, ibada ya Mungu wa kweli, Yehova, iliyokuwa imepigwa marufuku tangu 1939, ikatambuliwa kisheria na huru! “Hatuna maneno ya kufafanua tulivyohisi moyoni siku hiyo,” akina DiGregorio wakasema.
-
-
Albania2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 172]
Oda Na. 100 iliyowatambua kisheria Mashahidi wa Yehova
-