-
Albania2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
MGAWO AMBAO HAUKUTAZAMIWA
Michael na Linda DiGregorio walikuwa wamishonari katika Jamhuri ya Dominika. Babu na nyanya ya Michael ni baadhi ya Waalbania waliobatizwa Boston, miaka ya 1920, naye Michael alijua Kialbania kwa kiasi fulani. Kwa hiyo, Ndugu na Dada DiGregorio walipoamua kutembelea familia yao nchini Albania mwaka wa 1992, waliuliza Baraza Linaloongoza ikiwa wanaweza kukutana na akina ndugu watakapokuwa nchini humo kwa siku tatu. Walishangaa Baraza Linaloongoza lilipowaomba wabaki Albania kwa miezi mitatu, wasaidie kupanga kazi ya kuhubiri.
Katika ofisi ya tawi huko Roma, ndugu kutoka Ugiriki na Italia waliwapasha habari akina DiGregorio kuhusu hali nchini Albania na kuwaonyesha picha za baadhi ya akina ndugu wa Albania, kutia ndani Vasil Gjoka. Ndugu na Dada DiGregorio waliposafiri kwenda Tiranë mwezi wa Aprili 1992, kwa mara nyingine tena Waalbania waliokuwa ugenini waliruhusiwa kurudi nchini. Hata hivyo, bado kulikuwa na migogoro ya kisiasa, nao watu walikuwa na wasiwasi kuhusu wakati ujao.
Michael na Linda walipokuwa wakitembea kutoka katika uwanja wa ndege, familia ya Michael ilikuja mbio kuwalaki. Wakati huohuo, Michael akamtambua Vasil Gjoka, aliyekuwa ameelezwa kwamba akina DiGregorio wanawasili siku hiyo.
“Wewe nenda na familia,” Michael akamwambia Linda, “naja sasa hivi.”
Baada ya kumkumbatia Linda, watu wa familia wakabeba mizigo ya akina DiGregorio na kuharakisha kuelekea kwenye magari, huku Michael akienda haraka kukutana na Vasil.
“Nitarudi Tiranë Jumapili,” Michael akamwambia Vasil akiwa na haraka, “tutaonana.”
Koço, mtu wa familia ya Michael iliyokuwa Albania, ambaye hakujua kwamba Michael na Linda ni Mashahidi wa Yehova, akamwendea haraka na kumwambia: “Unafanya nini? Hatuzungumzi na watu tusiowajua!”
Walipokuwa wakisafiri katika njia zenye kupinda-pinda kuelekea Korçë, akina DiGregorio wakaona jinsi nchi hiyo ilivyokuwa tofauti kabisa na Karibea. “Kila kitu kilikuwa kimezeeka, chenye rangi ya kahawia au kijivu-jivu, na kimejaa vumbi,” akumbuka Michael. “Kulikuwa na seng’enge kila mahali. Watu walionekana hoi. Magari yalikuwa machache sana. Madirisha yalikuwa yamevunjika. Wakulima walikuwa wakilima kwa majembe. Mambo yalikuwa vilevile yalivyokuwa zamani za akina babu na nyanya! Tulihisi kana kwamba tumerudi enzi hizo!”
“MUNGU ALIKUWA NANYI KATIKA SAFARI YENU”
Koço alikuwa na kitu fulani alichokuwa ameficha kwa muda mrefu, naye alitaka kumwonyesha Michael. Nyanya ya Michael alipokufa, familia iliyokuwa Boston iliandikia familia iliyokuwa Albania barua ndefu. Kurasa kumi za kwanza zilizungumzia hasa mambo ya kifamilia, lakini kuelekea mwisho wa barua hiyo, familia hiyo ilieleza kuhusu ufufuo.
“Polisi waliichunguza barua hiyo,” Koço akamwambia Michael, “na kusoma kurasa chache za kwanza. Kisha wakachoka na kusema: ‘Chukueni! Ni mambo ya kifamilia tu!’ Niliposoma sehemu ya mwisho, nilifurahi sana kusikia kuhusu Mungu!”
Ndipo Michael akaeleza kwamba yeye na Linda ni Mashahidi wa Yehova, kisha akamhubiria Koço kwelikweli.
Kama ilivyokuwa nyakati za Biblia, Waalbania huhisi kwamba ni jukumu lao kuwatunza na kuwalinda wageni wao. Kwa hivyo, Koço akasisitiza kwamba ataambatana na Michael na Linda kwenda Tiranë.
“Tulipofika Tiranë, hatukuipata nyumba ya Vasil,” akumbuka Michael, “kwa sababu barabara hazikuwa na majina. Kwa hiyo, Koço akapendekeza tuulizie kwenye ofisi ya posta.”
“Aliporudi kutoka posta,” asema Linda, “Koço alikuwa ameduwaa, nasi tukaenda moja kwa moja hadi nyumbani kwa Vasil.”
Baadaye, Koço akaeleza: “Nilipoingia posta na kumuulizia Vasil, waliniambia: ‘Mtu huyo ni mtakatifu! Una habari amepatwa na nini? Tiranë nzima, hakuna mtu mwadilifu kama huyo!’ Niliposikia hivyo, nikajua kwamba Mungu alikuwa nanyi katika safari yenu! Siwezi kuwazuia!”
KUPANGA MAMBO TIRANË
Vasil alifurahi sana kuwaona akina DiGregorio, nao walizungumza kwa saa nyingi. Jioni ndipo Vasil alipowaeleza kwamba Jani Komino, aliyekuwa amefungwa pamoja na Nasho Dori, alikufa asubuhi hiyo. Kwa nini Vasil hakwenda kwenye mazishi ya ndugu huyo mpendwa aliyekuwa rafiki yake mkubwa? “Kwa sababu,” akaeleza, “nilikuwa nasubiri mtu aliyetumwa na Baraza Linaloongoza.”
Michael na Linda walihitaji kukaa Tiranë, hata hivyo, serikali ya wakati huo haikuwaruhusu wageni kukaa mjini. Wangefanya nini?
“Tuliacha mambo mikononi mwa Yehova,” asema Michael, “na hatimaye tukapata nyumba ndogo ya kukaa.”
“Wenye nyumba ndio waliokuwa na ufunguo,” akumbuka Linda, “nao waliingia na kutoka wapendavyo. Isitoshe, tulikuwa tukipita katika nyumba ya mwingine ili kuingia kwetu. Lakini angalau, nyumba yetu haikuwa njiani, nasi hatukutaka kuwa hadharani sana.”
Akina DiGregorio waliwasikiliza kwa saa nyingi ndugu wazee wa Tiranë wakisimulia majaribu waliyokuwa wamevumilia. Hata hivyo, mojawapo ya matatizo ni kwamba baadhi ya ndugu hao hawakuaminiana.
“Kivyake, kila mmoja alikuwa mwaminifu,” akumbuka Michael, “hata hivyo walishuku uaminifu wa wenzao. Hata hivyo, ijapokuwa hawakuwa na uhusiano wa karibu kati yao, hawakujitenga nasi. Baada ya kuzungumzia hali hiyo kwa utulivu, walikubali kwamba jambo kuu ni kulitangaza jina la Yehova. Waliungana katika upendo na kuwa na matumaini kuhusu wakati ujao.”
-
-
Albania2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 167]
Michael na Linda DiGregorio
-