Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mtu Anapotaka Kuendelea Kunywa
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Januari 1
    • Hata mtu anapokunywa kupita kiasi akiwa peke yake, haikosi watu wengine wataathiriwa, na mara nyingi matokeo yanakuwa yenye kuhuzunisha.b Ulevi unahusika mara nyingi mtu anapotukanwa au kupigwa, mtu anaposhambuliwa au kuuawa, na vilevile misiba inapotokea barabarani au kazini. Ulevi pia unasababisha matatizo mengi ya afya na hasara kubwa ya pesa kwa jamii kila mwaka. Isitoshe, mtu mmoja-mmoja, familia, na watoto wanaathiriwa sana kihisia.

  • Maoni ya Mungu Kuhusu Pombe
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Januari 1
    • Matokeo Mabaya ya Kunywa Kupita Kiasi

      Pombe inaweza kumnufaisha mtu kwa kadiri fulani, hata hivyo, inabadili sana jinsi akili na mwili unavyofanya kazi. Kunywa pombe kupita kiasi kunaweza kusababisha matatizo yafuatayo:

      Akili ya mtu anayekunywa pombe kupita kiasi inaathiriwa hivi kwamba ‘hawezi kufikiri vizuri.’ (Methali 23:33, Today’s English Version) Allen aliyekuwa akinywa pombe kupita kiasi, ambaye anatajwa katika makala ya kwanza, anasema hivi: “Ulevi sugu si kasoro ya mwili tu; bali pia ni kasoro ya maoni na mtazamo wa mtu. Hajali jinsi anavyowaumiza watu wengine.”

      Huenda mtu anayekunywa pombe kupita kiasi akashindwa kujizuia. Biblia inaonya hivi: “Divai na divai tamu ndivyo vinavyoondoa kusudi jema.” (Hosea 4:11) Jinsi gani? Tunapokunywa pombe huenda tukashindwa kuzuia mawazo na tamaa ambazo kwa kawaida tunazidhibiti, huenda hata tukaanza kuziona kuwa sawa na zenye kutamanika. Azimio letu la kufanya yaliyo sawa linaweza kudhoofika. Pombe inaweza kudhoofisha pia azimio letu la kudumisha mwenendo mzuri, na hivyo kusababisha madhara makubwa ya kiroho.

      Kwa mfano, John aligombana na mke wake, akatoka kwa hasira, na kuingia katika baa. Alikuwa amekunywa kiasi fulani cha pombe ili apoe wakati mwanamke fulani alipomjia. Baada ya kunywa pombe zaidi, John alitoka pamoja na mwanamke huyo na akafanya uzinzi naye. Baadaye, John alijuta sana kufanya jambo ambalo hangefanya kamwe kama hangekuwa amekunywa pombe.

      Mtu anayekunywa pombe kupita kiasi huenda akashindwa kudhibiti usemi na matendo. “Ni nani aliye na taabu sikuzote? Ni nani anayegombana na kupigana?” Biblia inajibu: “Kila mtu anayekaa mpaka usiku wa manane ili kuendelea kunywa.” (Methali 23:29, 30, Contemporary English Version) Mtu anayekunywa kupita kiasi anaweza kusikia kana kwamba “yuko baharini akiwa na kichefuchefu, na akining’inia juu ya mlingoti wa meli inayorushwa huku na huku baharini.” (Methali 23:34, TEV) Mwanamume ambaye amekunywa kupita kiasi huenda akaamka akiwa “na majeraha katika mwili mzima, hata asikumbuke jinsi alivyoumia.”—Methali 23:35, CEV.

      Afya ya mtu anayekunywa kupita kiasi inaweza kuathiriwa. “Mwishowe [pombe] huuma kama nyoka; huchoma kama nyoka mwenye sumu.” (Methali 23:32, BHN) Wanasayansi wamethibitisha kwamba methali hiyo ya kale ni ya kweli. Pombe inaweza kumwathiri mtu kama sumu hatari kwa kusababisha kansa mbalimbali, uvimbe na magonjwa mengine ya ini, ugonjwa wa kongosho, kiwango cha chini cha sukari katika damu ya watu wanaougua kisukari, kiharusi, ugonjwa wa moyo, na pia inaweza kuathiri kijusi. Hayo ni kati ya matatizo mengi yanayoweza kumpata mtu anayekunywa pombe nyingi. Hata mtu anayekunywa pombe kupita kiasi mara moja tu anaweza kupoteza fahamu au kufa. Lakini madhara makubwa zaidi ya kunywa kupita kiasi hayatajwi katika vitabu vya tiba.

      Madhara yaliyo makubwa zaidi. Mtu anayekunywa pombe nyingi anapatwa na madhara ya kiroho, hata kama hajalewa. Maneno haya ya Biblia ni wazi: “Ole wao wanaoamka asubuhi na mapema ili watafute tu kileo, wanaokawia mpaka giza la jioni sana hivi kwamba divai inawawasha!” Kwa nini? Isaya anaeleza madhara ya kiroho yanayotokana na kunywa kupita kiasi: “Hawauangalii utendaji wa Yehova, wala hawakuiona kazi ya mikono yake.”—Isaya 5:11, 12.

      Neno la Mungu linatushauri tusiwe “kati ya watu wanaokunywa divai mno.” (Methali 23:20) Wanawake wazee wanaonywa wasiwe “watumwa wa divai nyingi sana.” (Tito 2:3) Kwa nini? Pole kwa pole, bila kutambua, mtu anaanza kunywa pombe nyingi zaidi, mara nyingi zaidi. Hatimaye, yule anayekunywa huenda akafikiria sana pombe na kuwaza, ‘Asubuhi itafika wakati gani, ili niendelee kunywa?’ (Methali 23:35, CEV) Watu wanaokunywa pombe wako katika hali mbaya sana wanapotamani kunywa pombe asubuhi ili wapate nafuu baada ya kulewa usiku.

      Biblia inaonya kwamba wale wanaokunywa “divai kupita kiasi,” au kushiriki katika “karamu za kupindukia, [na] mashindano ya kunywa . . . watatoa hesabu kwake yeye aliye tayari kuhukumu wale walio hai na wale walio wafu.” (1 Petro 4:3, 5) Naye Yesu alionya hivi kuhusu siku zetu zenye hatari: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku [ya Yehova] iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki