-
Ni Nani Atakayeutawala Ulimwengu?Sikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
Kuelimishwa na Aristotle kulikoma ghafula mwaka wa 340 K.W.K. wakati ambapo mwana-mfalme huyo mwenye umri wa miaka 16 alirudi Pella akatawale Makedonia kwa kuwa baba yake hakuwako. Upesi, mrithi huyo wa kiti cha ufalme akaonyesha uhodari wake kivita. Alilikomesha haraka Maedi, kabila la Thrasi lililoasi, akateka jiji lao kuu mara moja, na kupaita mahali hapo Alexandroúpolis, kutokana na jina lake mwenyewe, jambo lililomfurahisha sana Philip.
KUENDELEA NA USHINDI
Aleksanda alirithi kiti cha ufalme cha Makedonia mwaka wa 336 K.W.K., akiwa na umri wa miaka 20 Philip alipouawa. Akiingia Asia kupitia Hellespont (paitwapo Dardanelles leo) mapema Mei mwaka wa 334 K.W.K., Aleksanda alianzisha kampeni ya ushindi akiwa na jeshi dogo lakini hodari la askari-jeshi 30,000 wa miguu na askari wapanda-farasi 5,000. Wahandisi, mabwana-pima, wasanifuujenzi, wanasayansi, na wanahistoria waliandamana na jeshi lake.
Kwenye Mto Granicus upande wa kaskazini magharibi mwa Asia Ndogo (leo inaitwa Uturuki), Aleksanda alishinda vita yake ya kwanza dhidi ya Uajemi. Katika kipindi cha majira ya baridi kali cha wakati huo alishinda sehemu ya magharibi ya Asia Ndogo. Katika masika ya mwaka wa 333 K.W.K. vita vingine vya kukata maneno dhidi ya Uajemi vilipiganwa Issus, upande wa kusini-mashariki mwa Asia Ndogo. Akiwa na jeshi la watu wapatao nusu milioni, Mfalme mkuu wa Uajemi, Dario wa Tatu, akaja kupigana na Aleksanda. Akiwa na uhakika kupita kiasi, Dario akaja pia na mama yake, mke wake, na washiriki wengine wa familia yake ili washuhudie kile ambacho kilipaswa kuwa ushindi mkubwa ajabu. Lakini Waajemi hawakuwa tayari kukabili shambulio la Wamakedonia la ghafula na lenye nguvu. Majeshi ya Aleksanda yalilishinda kabisa jeshi la Uajemi, na Dario akakimbia, akaiacha familia yake mikononi mwa Aleksanda.
Badala ya kuwafuata Waajemi waliokuwa wakikimbia, Aleksanda alielekea kusini kandokando ya Pwani ya Mediterania, akishinda vituo vilivyotumiwa na meli zenye nguvu za Uajemi. Lakini Tiro, kisiwa kilichokuwa jiji, kilikinza uvamizi. Akiwa ameazimia kulishinda, Aleksanda alianza mazingiwa yaliyodumu miezi saba. Wakati wa mazingiwa hayo ndipo Dario alipotoa ahadi iliyotajwa awali. Mambo yaliyoahidiwa yalikuwa yenye kuvutia sana hivi kwamba Parmenio, mshauri ambaye Aleksanda alimtumaini, aripotiwa kuwa alisema: ‘Ningalikuwa Aleksanda, ningalikubali.’ Lakini jenerali huyo mchanga akajibu hivi: ‘Hata mimi ningefanya hivyo, ikiwa ningekuwa Parmenio.’ Akikataa kufanya mapatano, Aleksanda aliendelea na mazingiwa na kuharibu Tiro mwezi wa Julai mwaka wa 332 K.W.K.
Akiliacha Yerusalemu, lililosalimu amri mbele zake, Aleksanda alisonga mbele kuelekea kusini, na kushinda Gaza. Wakiwa wamechoshwa na utawala wa Uajemi, Misri ilimkaribisha kama mwokozi. Huko Memphis, aliwapendeza makuhani wa Misri kwa kumtolea dhabihu mungu Apis mwenye sura ya fahali. Alianzisha pia jiji la Aleksandria, ambalo baadaye lilishindana na Athene likiwa kituo cha kujifunza nalo bado laitwa hivyo.
Kisha, Aleksanda akageuka kuelekea kaskazini-mashariki, akipitia Palestina na kuelekea Mto Tigris. Mwaka wa 331 K.W.K., alipigana vita kubwa ya tatu dhidi ya Uajemi, huko Gaugamela, karibu na magofu ya Ninewi. Huko, askari-jeshi 47,000 wa Aleksanda walilishinda nguvu jeshi la Uajemi lililopangwa upya la angalau askari-jeshi 250,000! Dario alikimbia na baadaye akauawa na watu wake mwenyewe.
Akiwa amesisimuka kwa sababu ya ushindi, Aleksanda aligeuka na kuelekea kusini na kulitwaa Babiloni, jiji kuu la Uajemi la wakati wa majira ya baridi kali. Pia alimiliki majiji makuu huko Susa na Persepolisi, akanyakua hazina kubwa ya Uajemi na kuyachoma makao makuu ya mfalme Shasta. Hatimaye, jiji kuu la Ecbatana likaanguka mikononi mwake. Mshindi huyo wa haraka akatiisha sehemu iliyosalia ya milki ya Uajemi, akienda mbali upande wa mashariki hadi Mto Indus, ulio katika Pakistan ya leo.
Alipovuka Indus, mpakani mwa mkoa wa Uajemi uitwao Taxila, Aleksanda alikutana na mpinzani mgumu sana, Porus, mtawala wa India. Aleksanda alipigana vita yake kubwa ya nne na ya mwisho dhidi yake mwezi wa Juni mwaka wa 326 K.W.K. Jeshi la Porus lilitia ndani askari-jeshi 35,000 na tembo 200, ambao waliwaogofya farasi wa Wamakedonia. Vita hivyo vilikuwa vikali na watu wengi walikufa, lakini majeshi ya Aleksanda yakashinda. Porus alisalimu amri na kujiunga nao.
Zaidi ya miaka minane ilikuwa imepita tangu jeshi la Makedonia livuke na kuingia Asia, nao askari-jeshi walikuwa wachovu na walitamani kurudi nyumbani. Wakiwa wamechoshwa na vile vita vikali dhidi ya Porus, walitaka kurudi nyumbani. Ingawa alisitasita mwanzoni, Aleksanda alikubali waliyotaka. Kwa kweli, Ugiriki ilikuwa imekuwa serikali ya ulimwengu. Koloni za Ugiriki zikiwa zimeanzishwa katika nchi zilizoshindwa, lugha na utamaduni wa Kigiriki zikaenea kotekote katika milki hiyo.
-
-
Ni Nani Atakayeutawala Ulimwengu?Sikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
USHINDI MBALIMBALI WA ALEKSANDA
MAKEDONIA
MISRI
Babiloni
Mto Indus
-