-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Leonard (Len) Helberg, mwangalizi wa mzunguko aliyetembelea Pago Pago mwaka huo asimulia mambo aliyojionea:
“Wamishonari walikuwa wakikaa katika nyumba kubwa iliyokuwa juu ya duka kubwa la zamani. Upande mmoja, ng’ambo ya kijito, kulikuwa na baa, nao mabaharia walipenda kujiburudisha humo wakati wa jioni. Walipolewa na kuanza kusababisha vurugu barabarani, polisi wa kijiji hicho, ambaye alikuwa mfupi lakini ngangari, angejipenyeza katikati ya umati huo akiwa na sigara yake mdomoni huku akivurumisha makonde huku na huku ili kutenganisha pande mbili zinazozozana. Upande wa nyuma wa nyumba hiyo, kutoka katika kanisa lililokuwa likipakana na nyumba yetu kulikuwa na kelele za mahubiri ya kuwatisha watu kuhusu moto wa mateso. Tukiwa kwenye varanda upande wa mbele, tulikuwa tukiona umati wa watu ukikusanyika karibu na benki mara moja kwa mwezi siku ya mshahara. Wamishonari kutoka katika makanisa, walikuja kutoka pande zote za kisiwa hicho ili kukusanya fungu la kumi kutoka kwa waumini wao kabla hawajatumia mishahara yao.”
Katika mazingira hayo yenye vituko, watu wengi walipendezwa na mambo ya kiroho. Len anaeleza: “Mmishonari mmoja alikuwa akianza mahubiri saa 12 asubuhi kwa kuongoza funzo la Biblia katika kibanda cha kunyolea kilichokuwa karibu na nyumba yao, kabla kinyozi huyo kufungua kazi. Baada ya hapo, angejifunza na mwokaji mikate, kabla ya kununua mkate ambao angerudi nao nyumbani kwa ajili ya kiamsha-kinywa. Baadaye siku hiyo, ndugu huyohuyo alijifunza na kikundi cha wafungwa katika jela iliyokuwa katika kijiji hicho.”
-
-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Katika ziara yake ya majuma manne nchini Samoa ya Marekani mwaka wa 1955, Len alionyesha jumla ya watu 3,227 filamu hiyo katika maonyesho 15 tofauti-tofauti, wastani wa watu 215 hivi kwa kila onyesho.
Len akumbuka: “Kabla ya kila onyesho, tulizunguka kwa gari kijiji kizima tukitawanya vikaratasi vilivyokuwa na matangazo kuhusu filamu hiyo. Wakati huohuo tulipaaza sauti, ‘Kuna sinema ya bure leo,’ na kutaja mahali ambapo sinema hiyo itaonyeshwa.”
-