-
Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 7Amkeni!—2011 | Mei
-
-
Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 7
Serikali Kuu ya Saba ya Ulimwengu
Hii ni habari ya mwisho katika mfululizo wenye habari saba katika matoleo ya “Amkeni!” yenye kufuatana yanayozungumzia serikali saba kuu za ulimwengu zinazotajwa katika historia ya Biblia. Kusudi lake ni kuonyesha kwamba Biblia inategemeka na imeongozwa na roho ya Mungu na ujumbe wake unatoa tumaini kwamba mateso yanayosababishwa na utawala mkatili wa wanadamu yatakwisha.
TUNAISHI katika wakati wa pekee sana na wenye matukio muhimu—wakati wa kutokea kwa serikali kuu ya saba inayotajwa katika historia ya Biblia. Isitoshe, serikali hiyo peke yake ndiyo inayosalia ikiwa unabii katika Biblia, kwa kuwa serikali zile nyingine sita sasa ni sehemu ya historia ya Biblia. Kuhusu serikali hizo saba, au “wafalme,” Biblia ilitabiri hivi: “Kuna wafalme saba: watano wameanguka, mmoja yuko, yule mwingine bado hajafika, lakini atakapofika lazima adumu kwa muda mfupi.”a—Ufunuo 17:10.
Zaidi ya miaka 1,900 hivi iliyopita, wakati maneno hayo yalipoandikwa, watano kati ya “wafalme,” au milki saba za kisiasa, ‘zilikuwa zimeanguka.’ Zilikuwa Misri, Ashuru, Babiloni, Muungano wa Umedi na Uajemi, na Ugiriki. Maneno “mmoja yuko” yalirejelea Roma. Lakini Roma haingetawala milele. Kungekuwa na milki nyingine moja, lakini unabii huo ulisema: “Bado ha[i]jafika.” Kama Biblia ilivyotabiri, ‘mfalme’ wa saba aliibuka! Milki hiyo ilikuja kuwa gani? Je, itatawala mpaka wakati usiojulikana? Ikiwa sivyo, itafikia kikomo chake kwa njia gani? Biblia inatupa majibu.
Unabii Unaotegemeka
Serikali ya saba ilianza kujitokeza wakati ambapo Uingereza, ambayo ilikuwa sehemu ya kaskazini-magharibi ya Milki ya Roma, ilipoanza kupata nguvu. Kufikia miaka ya 1760, kisiwa hicho kilikuwa kimeibuka na kuwa Milki ya Uingereza yenye nguvu. Utajiri na nguvu za Uingereza ziliendelea kuongezeka, hivi kwamba katika karne ya 19, ikawa ndiyo nchi tajiri na yenye nguvu zaidi duniani. “Milki ya Uingereza,” kinasema kitabu kimoja, “ilikuwa ndiyo milki kubwa zaidi kuwahi kuonekana ulimwenguni. Ilikuwa na watu milioni 372 na ilienea katika eneo lenye ukubwa wa maili zaidi ya milioni 11 za mraba [kilomita milioni 28 za mraba].”
Hata hivyo, vita vya kwanza vya ulimwengu (1914-1918) vilifanya Uingereza iwe na uhusiano wa pekee na Marekani ambayo hapo awali ilikuwa koloni yake. Matokeo yakawa nini? Mahali pa Milki ya Uingereza pakachukuliwa na muungano wa Uingereza na Marekani, na muungano huo wa nchi mbili zinazotumia Kiingereza na zinazofanana katika njia nyingi ukawa serikali kuu ya ulimwengu ambayo ipo hadi sasa.—Ona sanduku “Muungano wa Pekee.”
Unabii wa Ufunuo 17:10 unafanana na unabii mwingine unaopatikana katika kitabu cha Danieli. Danieli aliandika kuhusu ‘sanamu kubwa’ ambayo Mfalme Nebukadneza wa Babiloni aliona katika maono aliyopewa na Mungu. (Danieli 2:28, 31-43) Danieli alimfunulia mtawala huyo kwamba sehemu za mwili za sanamu hiyo ziliwakilisha mfuatano wa milki za kisiasa zilizoanza na Babiloni ambayo ndiyo iliyokuwa serikali kuu ya ulimwengu wakati huo. (Misri na Ashuru tayari zilikuwa zimetawala na kutoweka.) Historia sasa inathibitisha mambo yafuatayo:
Kichwa cha dhahabu kiliwakilisha Milki ya Babiloni.
Kifua na mikono ya fedha ilifananisha Muungano wa Umedi na Uajemi.
Tumbo na mapaja ya shaba yaliwakilisha Ugiriki ya kale.
Miguu ya chuma ilifananisha Milki ya Roma.
Nyayo zenye mchanganyiko wa chuma na udongo zilifananisha hali ya kisiasa na kijamii isiyo na umoja ambayo ingekuwapo wakati wa utawala wa serikali ya ulimwengu ya Uingereza na Marekani.
Kulingana na Ufunuo 17:10, serikali kuu ya saba ya ulimwengu ‘lazima idumu kwa muda mfupi.’
-
-
Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 7Amkeni!—2011 | Mei
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 17]
MUUNGANO WA PEKEE
Katika mkutano ambao Rais Barack Obama wa Marekani na Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron walifanya pamoja na waandishi wa habari mnamo Julai (Mwezi wa 7) 2010, rais huyo wa Marekani alitangaza hivi: “Lazima tukazie jambo hili. Marekani na Uingereza wana uhusiano wa pekee sana. Tunafurahia urithi uleule. Tuna viwango vilevile. . . . Zaidi ya yote, muungano wetu unafanikiwa kwa sababu tuna malengo yaleyale. . . . Marekani na Uingereza zinapoungana pamoja, watu wetu—na watu wote ulimwenguni—wanakuwa na usalama na ufanisi zaidi. Kwa ufupi, Marekani haina rafiki mwingine wa karibu na mwenye nguvu zaidi kuliko Uingereza.”
-