-
Mradi Mpya wa Mwisho AntaktikaAmkeni!—2000 | Julai 22
-
-
Mradi Mpya wa Mwisho Antaktika
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA AUSTRALIA
SEHEMU fulani za Antaktika zaweza kuwa baridi sana, asema mwandishi mmoja, hivi kwamba “ukiangusha ufito wa feleji waweza kuvunjika kama kioo, . . . na ukivuta samaki kutoka kwenye shimo ndani ya barafu kwa muda wa sekunde tano ataganda . . . na kuwa mgumu kabisa.” Kwa sababu ya hali zake za kipekee na zisizo za kawaida, uzuri usio na mimea yoyote—nyakati nyingine unaokamilishwa na nuru yenye kuvutia kutoka kusini—Antaktika ni kama ulimwengu mwingine.
Lakini Antaktika ni sehemu ya ulimwengu huu. Kwa hakika, imelinganishwa na maabara kubwa ya asili ya kuchunguza dunia na angahewa lake, na vilevile mabadiliko ya kimazingira, kutia ndani yale yanayosababishwa na wanadamu. Wanasayansi wanazidi kuhangaika wanapofikiria uchunguzi huo. Wameona matukio mapya yenye kuogofya katika Maeneo ya Ncha za Kusini, na yanadokeza kwamba hali si shwari kabisa. Lakini kwanza, acheni tuone kwa nini Antaktika ni bara la pekee.
Kwanza, Antaktika—bara lililojitenga zaidi na mabara mengine ulimwenguni—ni bara la utofautiano. Lina uzuri mwingi kupindukia na halijavurugwa na utendaji wa wanadamu lakini halikaliki. Ndiyo sehemu yenye upepo zaidi ulimwenguni, yenye baridi zaidi, hata hivyo huathirika kwa urahisi. Ndilo bara lenye mvua ndogo zaidi kuliko bara jinginelo, lakini barafu yake ni asilimia 70 ya maji yasiyo na chumvi katika sayari yetu. Barafu hiyo iliyo na kimo cha meta 2,200 hufanya Antaktika kuwa bara refu zaidi duniani, likiwa na wastani wa meta 2,300 juu ya usawa wa bahari. Pia ndilo bara la tano kwa ukubwa duniani, na bado Antaktika halina wakazi wa kudumu isipokuwa usubi, aina fulani ya nzi asiye na mabawa mwenye urefu unaozidi sentimeta moja.
Ni Kama Kuzuru Mihiri!
Unapojasiria kutembea katika sehemu za ndani-ndani za Antaktika, utaona viumbe wakizidi kupungua, hasa ufikapo maeneo yanayoitwa mabonde makavu. Majangwa hayo ya nchani yenye ukubwa wa kilometa mraba 3,000 yapo hasa kwenye Milima ya Transantarctic—mfululizo wa safu za milima unaovuka bara hilo na kufikia urefu wa meta 4,300 katika sehemu fulani. Dhoruba za barafu hupita katikati ya mabonde makavu na kukausha mara moja theluji ambayo huenda ikaanguka. Wanasayansi wanaamini kwamba mabonde hayo yaliyopo duniani yanafanana na Mihiri. Kwa sababu hiyo, yalionwa kuwa eneo linalofaa kujaribia vifaa vya angani kabla ya kurusha chombo Viking kwenye Mihiri.
Na bado, hata mabonde makavu yana viumbe hai! Ndani ya miamba yenye kuvuja, katika mianya midogo ya hewa, huishi aina fulani za bakteria, mwani, na kuvu zilizo sugu. Hutegemea tu unyevu kidogo sana ili kuishi. Nje ya makao yao yasiyo ya kawaida kuna miamba iliyo ukiwa inayoitwa ventifact, yenye umbo la ajabu na inayong’aa sana kwa sababu ya kupigwa na pepo zisizokoma za Antaktika kwa karne nyingi.
Lilipewa Jina Kabla ya Kugunduliwa
Tangu siku za wanafalsafa Wagiriki wa kale, ilidhaniwa kwamba kuna ardhi kubwa sana upande wa kusini. Kwa mfano, Aristotle, alidai kwamba kuna uhitaji wa kuwa na bara la kusini ili kusawazisha ardhi iliyojulikana kuwa katika Kizio cha Kaskazini. Kitabu Antarctica—Great Stories From the Frozen Continent chasema kwamba “kwa kuwa kizio cha kaskazini kilikuwa chini ya kundi la nyota la Arktos, Dubu, kwa hiyo, Aristotle (384-322 KWK) alisababu kwamba ardhi isiyojulikana kuelekea upande wa kusini lazima iwe Antarktikos—yaani, kinyume kabisa”—au upande unaoelekeana. Hivyo, kwa kweli Antaktika ni tofauti kwa sababu, ilipewa jina miaka 2,000 hivi kabla haijagunduliwa!
Mwaka wa 1772, mvumbuzi Mwingereza Kapteni James Cook aliabiri kuelekea kusini ili kutafuta lile bara lililodaiwa lilikuwa kusini. Aliingia kwenye visiwa vinavyopigwa na upepo mkali na vilima vikubwa vya barafu, au “visiwa vya barafu,” kama alivyoviita. “Baadhi yake,” aliandika, “vilikuwa na mzunguko upatao kilometa tatu, na urefu wa meta 20, na bado mawimbi ya bahari yalikuwa na nguvu kiasi cha kubeba vilima hivyo.” Akiwa ameazimia, Cook aliendelea kusafiri upande wa kusini, na katika Januari 17, 1773, meli zake, Resolution na Adventure, zikawa vyombo vya kwanza vya baharini kupata kuvuka Mzingo wa Antaktiki. Cook aliendesha chombo chake kwa kukwepa barafu ya baharini mpaka alipozuiwa hatimaye. “Singeweza kuona chochote upande wa kusini ila barafu,” akaandika katika kifaa chake cha kurekodia mwendo na safari ya meli. Kwa kweli, alikuwa amebakisha mwendo wa kilometa 120 tu kufika kwenye ardhi ya Antaktiki alipogeuka na kurudi nyuma.
Kwa hiyo ni nani aliyekuwa wa kwanza kuona Antaktika? Kwa kweli, ni nani aliyekuwa wa kwanza kufika huko? Hakuna mtu aliye na hakika kufikia leo hii. Huenda hata ilikuwa ni wavuvi wa nyangumi au wawindaji wa sili, kwa kuwa Cook aliporudi nyumbani, na kuripoti kwamba kulikuwa na sili, pengwini, na nyangumi wengi, wavuvi walikimbia hima-hima kwenye eneo hilo.
Damu Kwenye Barafu
Cook “aligundua kundi kubwa zaidi la wanyama wa mwitu ulimwenguni, na alikuwa mtu wa kwanza kujulisha ulimwengu juu ya wanyama hao,” akaandika Alan Moorehead katika kitabu chake The Fatal Impact. “Kuhusu wanyama wanaoishi Antaktika,” asema Moorehead, “[matokeo] yalikuwa ni maangamizi makubwa.” Kitabu Antarctica—Great Stories From the Frozen Continent chasema: “Kuelekea mwisho wa karne ya kumi na nane, kuvua sili katika kizio cha kusini kulifanana sana na hekaheka za kutafuta dhahabu iliyogunduliwa. Mahitaji ya ngozi ya sili huko China na Ulaya yameongezeka sana hivi kwamba sili wote waliokuwapo walitoweka na hivyo kukatisha tamaa wawindaji wa sili, ambao sasa walihitaji kwenda kutafuta sehemu mpya za kuwinda zenye makazi yasiyoporwa ya wanyama hao.”
Baada ya wawindaji wa sili kuharibu kabisa riziki yao, wavuvi wa nyangumi walianza kupora bahari. “Hakuna mtu atakayepata kujua ni nyangumi na sili wangapi waliouawa katika bahari ya kusini,” aandika Moorehead. “Je, ni milioni kumi au milioni hamsini? Hakuna haja ya kuhesabu; mauaji yaliendelea mpaka hakukuwa na chochote cha kuua.”
Hata hivyo, leo, sheria za kimataifa hulinda mimea na wanyama wote wa Antaktiki. Kwa kuongezea, kukosekana kwa wanyama-wawindaji wa ardhini pamoja na chakula kingi sana cha baharini hufanya pwani ya Antaktiki iwe mahali salama kwa ajili ya wanyama wa mwitu. Lakini kuna ishara za mashambulizi yasiyoonekana waziwazi huko Antaktika, ambazo huenda zisikomeshwe na mikataba ya kimataifa.
[Sanduku katika ukurasa wa 15]
NCHA ZILIZOELEKEANA
Ijapokuwa zinafanana kwa kiasi fulani, Ncha ya Kaskazini na Ncha ya Kusini ni ‘ncha zilizoelekeana kabisa’ katika njia nyingi kuliko tu mahali zilipo. Fikiria yafuatayo.
Eneo lote lililo karibu zaidi na Ncha ya Kaskazini lina barafu na bahari, ilhali Ncha ya Kusini iko karibu na sehemu ya kati ya bara la tano kwa ukubwa duniani.
Ncha ya Kaskazini imezungukwa na nchi zenye watu wengi za Amerika, Asia, na Ulaya, ilhali Antaktika imezingirwa na bahari kubwa, ambayo kwa kweli ndiyo yenye tufani zaidi katika sayari.
Makumi ya maelfu ya familia huishi karibu na Mzingo wa Aktiki, ambao pia ni makao ya maelfu ya mimea na wanyama. Hata hivyo hakuna mwanadamu aliye mwenyeji wa Antaktika. Viumbe hai pekee walio wa asili ya huko ni mwani, bakteria, kuvumwani, kuvu, aina mbili za maua, na aina chache za wadudu.
“Antaktika imeitwa bara linalodundadunda,” chasema kichapo Encyclopædia Britannica, “kwa sababu ya ongezeko la barafu linalotukia kila mwaka na kupungua kwa pwani zenye barafu upande wa mbele.” Kwenye kilele chake, mwamba wa barafu huenea umbali wa kilometa 1,600 mbali na bahari. Kupanuka na kunywea huko ni mara sita zaidi ya mwamba wa barafu wa Aktiki, jambo linaloifanya Antaktika iathiri zaidi halihewa ulimwenguni pote.
-
-
Antaktika Bara Lililo HatariniAmkeni!—2000 | Julai 22
-
-
Antaktika Bara Lililo Hatarini
WANAANGA wanapotazama dunia kutoka angani, chasema kitabu Antarctica: The Last Continent, sehemu yenye kutokeza zaidi ya sayari yetu ni bamba la barafu la Antaktika. “Hung’aa kama taa kubwa nyeupe iliyo sehemu ya chini ya ulimwengu,” wakaripoti wanaanga hao.
Antaktika iliyo na ukubwa wa kilometa za kyubiki 30,000,000 ni kama mashine ya kutengenezea barafu inayotoshana na bara nzima. Theluji huanguka ardhini na kurundamana ili kufanyiza barafu. Nguvu za uvutano hufanya barafu itiririke polepole kuelekea pwani, na huko huingia baharini na kufanyiza miamba mikubwa sana ya barafu.—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 18.
Miamba ya Barafu Inayopungua
Hata hivyo, katika miaka ya majuzi, kuyeyuka kunakoongezeka kumepunguza ukubwa wa miamba kadhaa ya barafu, na mingine imetoweka kabisa. Mwaka 1995 sehemu yenye ukubwa wa kilometa za mraba 1,000 kati ya Mwamba wa Barafu wa Larsen wenye ukubwa wa kilometa 1,000 iliporomoka na kuvunjika na kuwa maelfu ya vilima barafu, kulingana na ripoti moja.
Eneo ambalo limeathiriwa kufikia sasa na kupungua kwa barafu ni Peninsula ya Antaktiki. Katika miaka 50 iliyopita, mwendelezo wa safu ya milima ya Andes ya Amerika Kusini, ambayo ni peninsula yenye umbo la S imepata ongezeko la joto la nyuzi Selsiasi 2.5. Tokeo ni kwamba Kisiwa cha James Ross, ambacho wakati mmoja kilizingirwa na barafu, sasa chaweza kuzungukwa. Kupungua kwa barafu kumetokeza pia ongezeko kubwa la mimea.
Kwa kuwa mahali ambapo pameyeyuka sana ni kwenye eneo la Peninsula ya Antaktiki pekee, wanasayansi fulani hawasadiki kwamba jambo hilo ladhihirisha kuongezeka kwa joto ulimwenguni pote. Hata hivyo, kulingana na uchunguzi mmoja wa Norway, barafu ya Aktiki inapungua pia. (Kwa sababu Ncha ya Kaskazini haipo penye ardhi, barafu nyingi ya Aktiki ni ya baharini.) Kulingana na uchunguzi huo, mabadiliko hayo yote yanalingana kabisa na utabiri kuhusu kuongezeka kwa joto ulimwenguni pote.
Lakini Antaktika hutimiza mengi zaidi kuliko kupatwa tu na mabadiliko ya halijoto. Bara hilo limeelezwa kuwa “eneo muhimu ambalo huelekeza sana tabia ya nchi ulimwenguni.” Ikiwa ndivyo, basi huenda halihewa ya wakati ujao ikaathiriwa iwapo bara hilo litaendelea kubadilika.
Kwa sasa, juu ya Antaktika kuna shimo lenye ukubwa maradufu ya Ulaya kwenye tabaka la ozoni la angahewa. Ozoni ambayo ni aina fulani ya oksijeni, hukinga dunia dhidi ya mnururisho hatari wa urujuanimno ambao huharibu macho na kusababisha kansa ya ngozi. Kwa sababu ya kuongezeka kwa mnururisho, watafiti katika Antaktika lazima walinde ngozi yao kutokana na jua na kuvaa miwani ya jua yenye rangi ya pekee inayoakisi nuru ili kulinda macho yao. Wakati ujao itajulikana wanyama wa mwituni wa Antaktika watakuwa wameathiriwa kwa kadiri gani.
Bara Linaloathiriwa kwa Urahisi —Tembea kwa Uangalifu
Huenda kichwa kilicho juu kikawakaribisha ifaavyo wageni Antaktika. Kwa nini? Kuna sababu kadhaa, kulingana na Tarafa ya Australia ya Antaktiki. Kwanza, kwa sababu ya uhusiano sahili wa ikolojia ya Antaktika, mazingira yake yaweza kuathiriwa kwa urahisi sana. Pili, mimea hukua polepole sana hivi kwamba alama ya wayo kwenye tuta la kuvumwani yaweza kuonekana miaka kumi baadaye. Mimea iliyoharibika au kudhoofika haiwezi kustahimili pepo kali za Antaktika, zinazoweza kuharibu mimea mingi sana. Tatu, baridi kali mno hufanya vitu vichukue miongo mingi kuoza. Nne, bila kujua watu wanaweza kuleta viumbe wadogo mno kwenye bara hili lililojitenga na linaloweza kuathiriwa kwa urahisi. Hatimaye, mahali ambapo watalii na wanasayansi huzuru mara nyingi ni kingo za pwani—maeneo yanayowafaa sana wanyama na mimea. Kwa kuwa maeneo hayo ni asilimia 2 hivi ya ardhi, ni rahisi kuelewa kwa nini hivi karibuni Antaktika itakuwa na msongamano wa watu. Hilo lazusha swali, ni nani anayesimamia bara hili kubwa?
Ni Nani Anayetawala Antaktika?
Ijapokuwa nchi saba zinadai kumiliki visehemu katika Antaktika, bara zima kwa ujumla ni la pekee kwa sababu halina mtawala aliyeteuliwa wala raia. “Antaktika ndilo bara pekee duniani kutawaliwa na mikataba ya kimataifa tu,” yaripoti Tarafa ya Australia ya Antaktiki.
Mkataba wa Antaktika ulitiwa sahihi na serikali 12 na ukaanza kutumika Juni 23, 1961. Tangu wakati huo, idadi ya mataifa wanachama imekua na kuzidi 40. Lengo la mkataba huo ni “kuhakikisha kwamba kwa masilahi ya wanadamu wote, Antaktika itaendelea kutumiwa milele kwa makusudi ya amani pekee na haitakuwa mahali pa mizozo ya kimataifa.”
Katika Januari 1998 Kumbukumbu la Kulinda Mazingira lililotangulia Mkataba wa Antaktika likawa sheria ya kimataifa. Kumbukumbu hilo limepiga marufuku uchimbaji wote wa madini katika Antaktika kwa angalau miaka 50. Pia limeteua bara hilo na mifumikolojia ya viumbe wa majini kuwa “hifadhi ya asili iliyotolewa kwa ajili ya amani na sayansi.” Shughuli za kijeshi, majaribio ya silaha, na kutupwa kwa mabaki ya nyuklia yamepigwa marufuku. Hata vigari vya kutelezea juu ya theluji vinavyokokotwa na mbwa vimepigwa marufuku pia.
Mkataba wa Antaktiki umesifiwa kuwa “mfano wa ushirikiano wa kimataifa usio na kifani.” Hata hivyo, bado kuna matatizo mengi yanayohitaji kutatuliwa, kutia ndani utawala. Mathalani, ni nani atakayehakikisha kwamba mkataba huo unafuatwa, na jinsi gani? Na mataifa wanachama yatakabilianaje na ongezeko la haraka la watalii—ambao ni tisho kwa ikolojia ya Antaktika inayoweza kuathiriwa kwa urahisi? Katika miaka ya majuzi zaidi ya watalii 7,000 wanaosafiri kwa meli wamezuru Antaktika kila mwaka, na idadi hiyo yatarajiwa kurudufika baada ya muda mfupi.
Huenda kukatokea magumu mengine wakati ujao. Mathalani, itakuwaje wanasayansi watakapopata madini yenye thamani au mafuta? Je, mkataba huo utazuia shughuli za kibiashara na uchafuzi ambao mara nyingi husababishwa na shughuli hizo? Mikataba yaweza kubadilishwa, kutia ndani Mkataba wa Antaktika. Kwa hakika, Kifungu cha 12 kinaruhusu mkataba huo “kurekebishwa wakati wowote chini ya makubaliano ya wote Waliohusika Kuanzisha Mkataba huo.”
Bila shaka, hakuna mkataba unaoweza kulinda Antaktika dhidi ya uchafuzi kutoka kwa nchi za kisasa zilizositawi kiviwanda. Itasikitisha kama nini iwapo “taa nyeupe” maridadi iliyo sehemu ya chini ya ulimwengu itachafuliwa kwa sababu ya pupa na kukosa ujuzi kwa wanadamu! Kudhuru Antaktika ni kuwadhuru wanadamu. Somo tunalopata kutokana na Antaktika ni kwamba dunia nzima—sawa na mwili wa binadamu—ni mfumo unaotegemeana, ulioratibiwa kikamilifu na Muumba ili kuendeleza uhai na kutufurahisha.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]
MWAMBA WA BARAFU NI NINI?
Juu kabisa kwenye sehemu za ndani za Antaktika, vijito vya barafu vinavyofanyizwa na theluji inayoanguka, hutiririka kuelekea pwani—vingine hutiririka kwa umbali wa kilometa moja hivi kwa mwaka, kulingana na picha za karibuni kutoka kwa rada za setilaiti. Vijito vingi vya barafu huungana kama mito na kufanyiza mito mikubwa sana ya barafu. Inapofika baharini, mito hiyo iliyoganda huelea juu ya maji na kufanyiza miamba ya barafu, mwamba ulio mkubwa zaidi ni Mwamba wa Barafu wa Ross (ulioonyeshwa). Una vijito vya barafu au barafuto zisizopungua saba, na unatoshana na Ufaransa na sehemu nyingine zina unene wa kilometa moja hivi.a
Chini ya hali za kawaida, miamba ya barafu haipungui. Barafuto zinapoongeza barafu zaidi kwenye mwamba, tabaka la nje la mwamba husukumwa mbali zaidi na bahari, kama vile dawa ya meno hufinywa kutoka kwenye tyubu. Kufikia hapo hatimaye vipande vikubwa huvunjika (hatua inayoitwa calving), na vipande hivyo huwa vilima vya barafu. Vilima fulani vya barafu vina “ukubwa upatao kilometa za mraba 13,000,” chasema kichapo The World Book Encyclopedia. Hata hivyo, katika miaka ya karibuni calving imeongezeka na miamba ya barafu imepungua, mingine imetoweka kabisa. Ijapokuwa hivyo, viwango vya bahari haviongezeki. Kwa nini? Kwa sababu miamba ya barafu tayari inaelea, na kutwaa nafasi ya maji kwa uzito wao. Lakini iwapo barafu kwenye ardhi ya Antaktika ingeyeyuka, ingekuwa sawa na kumwaga maji kutoka kwa tangi lenye ukubwa wa kilometa kyubiki 30,000,000 baharini! Viwango vya bahari vingeongezeka kwa meta 65 hivi!
[Maelezo ya Chini]
a Miamba ya barafu ni tofauti na barafu ya baharini. Barafu ya baharini huanza kama vipande vya barafu vinavyoelea na kujitokeza baharini wakati wa baridi kali maji yanapoganda. Kisha vipande hivyo huungana na kufanyiza barafu ya baharini. Mambo huwa kinyume wakati wa kiangazi. Vilima vya barafu havitokani na barafu ya baharini, lakini, hutokana na miamba ya barafu.
[Picha]
Miamba mikubwa ya barafu yavunjika karibu na Mwamba wa Barafu wa Ross. Hapa mwamba wa barafu una urefu wa takriban meta 65 juu ya usawa wa bahari
[Hisani]
Tui De Roy
[Picha katika ukurasa wa 20]
Kitoto cha sili aina ya “weddell”
[Hisani]
Picha: Commander John Bortniak, NOAA Corps
-