Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Amani ya Kristo Inawezaje Kudhibiti Mioyoni Mwetu?
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Septemba 1
    • Tunapokuwa na Mahangaiko Mengi

      8. Ni baadhi ya mambo gani yanayosababisha hangaiko, na hangaiko laweza kutokeza nini?

      8 Hangaiko ni jambo halisi kabisa maishani katika “siku [hizi] za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Ni kweli kwamba Yesu alisema: “Komeni kuwa wenye kuhangaikia nafsi zenu kuhusu ni nini mtakachokula au juu ya miili yenu kuhusu ni nini mtakachovaa.” (Luka 12:22) Lakini si mahangaiko yote yanayosababishwa na kutafuta vitu vya kimwili. Loti ‘alitaabishwa sana’ na ukosefu wa adili wa Sodoma. (2 Petro 2:7) Paulo ‘alihangaikia sana makutaniko yote.’ (2 Wakorintho 11:28) Yesu alikuwa na maumivu makali sana usiku uliotangulia kifo chake hivi kwamba “jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka kwenye ardhi.” (Luka 22:44) Bila shaka, si mahangaiko yote yanayoonyesha kwamba mtu ana imani dhaifu. Hata hangaiko liwe linasababishwa na nini, likizidi na kuendelea kwa muda mrefu, linaweza kutukosesha amani. Wengine wamekuwa na mahangaiko mengi sana hivi kwamba wamehisi hawawezi kuendelea kutimiza majukumu yao ya kumtumikia Yehova. Biblia husema: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha.” (Mithali 12:25) Tunaweza kufanya nini basi, ikiwa tuna mahangaiko mengi sana?

      9. Ni baadhi ya hatua gani madhubuti zinazoweza kuchukuliwa ili kupunguza hangaiko, lakini ni mambo gani yanayosababisha hangaiko ambayo hatuwezi kuyaondoa?

      9 Katika hali fulani, huenda tukafaulu kuchukua hatua madhubuti. Ikiwa hangaiko letu linasababishwa na ugonjwa, litakuwa jambo la busara kulishughulikia, ingawa mtu binafsi ndiye anayepaswa kuamua mambo hayo.a (Mathayo 9:12) Ikiwa tumelemewa na majukumu mengi, tunaweza kuwakabidhi wengine baadhi ya majukumu hayo. (Kutoka 18:13-23) Hata hivyo, vipi juu ya watu kama vile wazazi ambao wana majukumu mazito wasiyoweza kuwakabidhi watu wengine? Namna gani Mkristo anayeishi na mwenzi mpinzani? Namna gani familia inayokabili hali ngumu sana za kiuchumi au inayoishi katika sehemu yenye vita? Bila shaka, hatuwezi kuondoa mambo yote yanayosababisha hangaiko katika mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, tunaweza kudumisha amani ya Kristo mioyoni mwetu. Jinsi gani?

      10. Mkristo anaweza kupunguza hangaiko katika njia gani mbili?

      10 Njia moja ni kutafuta faraja kutoka kwa Neno la Mungu. Mfalme Daudi aliandika hivi: “Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako zaifurahisha roho yangu.” (Zaburi 94:19) “Faraja” anayotoa Yehova inaweza kupatikana katika Biblia. Kusoma kwa ukawaida Kitabu hicho kilichopuliziwa kutatusaidia tudumishe amani ya Kristo mioyoni mwetu. Biblia husema: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Vivyo hivyo, Paulo aliandika hivi: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Kusali kwa bidii na kwa ukawaida kutatusaidia kudumisha amani yetu.

      11. (a) Yesu alituwekea kielelezo gani kizuri kuhusu sala? (b) Tuoneje sala?

      11 Yesu alikuwa kielelezo kizuri kuhusiana na habari hii. Katika pindi fulani, alizungumza kwa sala na Baba yake wa kimbingu kwa muda wa saa nyingi kwa wakati mmoja. (Mathayo 14:23; Luka 6:12) Sala ilimsaidia kuvumilia majaribu makali zaidi. Usiku uliotangulia kifo chake, maumivu yalizidi sana. Alifanyaje? Alisali “kwa bidii zaidi.” (Luka 22:44) Naam, Mwana mkamilifu wa Mungu alikuwa mtu wa sala. Basi wafuasi wake wasio wakamilifu wana uhitaji mkubwa hata zaidi wa kuwa na zoea la kusali. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake ‘wasali sikuzote wala wasikate tamaa.’ (Luka 18:1) Sala ni mawasiliano halisi na muhimu pamoja na Yule anayetujua vyema zaidi ya tunavyojijua wenyewe. (Zaburi 103:14) Ikiwa tutadumisha amani ya Kristo mioyoni mwetu, ‘tutasali bila kukoma.’—1 Wathesalonike 5:17.

  • Amani ya Kristo Inawezaje Kudhibiti Mioyoni Mwetu?
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Septemba 1
    • a Nyakati nyingine, hangaiko linaweza kusababishwa au kuzidishwa na ugonjwa, kama vile mshuko-moyo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki