Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kujenga Pamoja Duniani Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kutimiza Uhitaji wa Majumba ya Kusanyiko

      Kwa muda wa miaka iliyopita, vifaa vya aina nyingi vimetumiwa kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko. Mashahidi wa Yehova wamekodi mahali kama vile majumba ya umma, shule, majumba ya maonyesho, mabohari ya silaha, viwanja vya michezo, na viwanja vya maonyesho. Katika sehemu chache, vifaa bora sana vilipatikana kwa bei nafuu. Mara nyingi zaidi, wakati na jitihada nyingi vilitakwa ili kusafisha mahali, kuandaa vikuza-sauti, kujenga jukwaa, na kusafirisha viti. Nyakati nyingine mapatano yalifutwa dakika ya mwisho. Kadiri idadi ya makutaniko ilivyoongezeka, ikawa vigumu zaidi na zaidi kupata mahalimahali pafaapo pa kutosha. Ni jambo gani lingeweza kufanywa?

      Kwa mara nyingine tena, suluhisho lilikuwa kwamba Mashahidi wa Yehova wawe na mahali pao wenyewe. Hiyo ingehusisha kurekebisha upya majengo yenye kufaa na kujenga mapya. La kwanza la Majumba ya Kusanyiko kama hayo katika Marekani lilikuwa jumba la maonyesho katika Long Island City, New York, lililorekebishwa upya na likaanza kutumiwa na Mashahidi wa Yehova mwishoni-mwishoni mwa 1965.

      Karibu wakati uleule, Mashahidi kwenye kisiwa cha Guadeloupe cha Karibea walikuwa wakichora ramani ya Jumba la Kusanyiko la kutimiza mahitaji yao. Walihisi kwamba ingefaidi ikiwa wangekuwa na makusanyiko ya mzunguko katika sehemu nyingi tofauti-tofauti. Lakini miji iliyo mingi haikuwa na vifaa vilivyokuwa vikubwa vya kutosha. Kwa hiyo Mashahidi walijenga muundo uwezao kubebeka uliofanyizwa kwa vyuma na paa ya aluminiamu, kitu ambacho kingetosha kwa watu 700 na ambacho kingeweza kujengwa popote palipokuwa na ardhi iliyokuwa tambarare kidogo. Walilazimika kuongezea ukubwa wa jumba hilo tena na tena, mpaka lilipofikia kuweza kutoshea watu 5,000. Ebu fikiria kusafirisha, kujenga, na kubomoa tani 30 za vifaa kwa kila kusanyiko! Hilo Jumba la Kusanyiko lilijengwa na kubomolewa mara kadhaa kwa mwaka kwa muda wa miaka 13, mpaka ilipokuwa vigumu kupata ardhi kwa ajili ya jumba lenye kubebeka, ikawa lazima kununua ardhi na kujenga Jumba la Kusanyiko la kudumu, ambalo sasa hutumika kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko na mikusanyiko ya wilaya.

      Katika sehemu chache, miradi ya Jumba la Kusanyiko ilitumia majengo yaliyokuwako. Katika Uingereza, katika Hays Bridge, Surrey, shule yenye majengo mengi ya miaka 50 ilinunuliwa na kurekebishwa upya. Iko katika uwanja wa hektari 11 katika sehemu nzuri ya mashambani. Yaliyokuwa hapo zamani majengo ya sinema na bohari la bidhaa za viwanda yalijengwa yakiwa na umbo jipya na kuanza kutumiwa katika Hispania; kiwanda cha nguo kisichotumika katika Australia; jumba la dansi katika Quebec, Kanada; jumba la michezo ya kuvingirisha matufe katika Japani; bohari la bidhaa katika Jamhuri ya Korea. Yote hayo yalijengwa upya na kuwa Majumba ya Kusanyiko yenye kuvutia ambayo yangeweza kutumika vyema kuwa vitovu vikubwa vya elimu ya Biblia.

      Majumba ya Kusanyiko mengine yalikuwa mapya kabisa, yakiwa yamejengwa toka chini hadi juu. Lile umbo la pembenane la aina yalo la jumba katika Hellaby, South Yorkshire, Uingereza, pamoja na uhakika wa kwamba kazi iliyo nyingi ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea lilitokeza makala katika jarida la Taasisi ya Uhandisi wa Ujenzi. Jumba la Kusanyiko katika Saskatoon, Saskatchewan, katika Kanada, lilikusudiwa litoshee watu 1,200; lakini wakati kuta za ndani zinaposimamishwa mahali pazo, jengo hilo laweza kutumiwa likiwa Majumba ya Ufalme manne yakiwa upande kwa upande. Jumba la Kusanyiko la Haiti (lililotangulia kujengwa na kusafirishwa kutoka Marekani) lilikuwa wazi katika pande mbili ili wale walioketi ndani waweze kupashwa baridi daima na pepo zilizoko—kitulizo chenye kukaribishwa katika jua kali la Haiti. Jumba katika Port Moresby, Papua New Guinea, lilibuniwa kwa njia ya kwamba sehemu za kuta zingeweza kufunguka kama milango ili kuweza kutoshea umati mkubwa kuliko ule ambao ungeweza kutoshea ndani.

      Uamuzi wa kujenga Jumba la Kusanyiko haufanywi na kikundi cha waangalizi ambao baada ya hapo hutarajia kila mtu mwingine auunge mkono. Kabla ya Jumba la Kusanyiko jipya lolote kujengwa, Sosaiti huhakikisha kwamba uchanganuzi wa uangalifu umefanywa kuhusu uhitaji walo na ni mara ngapi litatumiwa. Ufikirio hutolewa si kwa idili ya wenyeji kwa ajili ya mradi bali pia mahitaji ya ujumla shambani. Jambo hilo huzungumzwa pamoja na makutaniko yote yatakayohusika, ili kuhakikisha tamaa na uwezo wa akina ndugu wa kuutegemeza.

      Hivyo, kazi ianzapo, Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo wanaiunga mkono kabisa. Pesa za kila mradi hutolewa na Mashahidi wenyewe. Mahitaji ya kifedha huelezwa, lakini michango ni ya kujitolea na watoaji hawajulikani ni kina nani. Mipango ya uangalifu hutangulia kufanywa, na ujenzi hunufaika kutokana na ujuzi uliokwisha kupatikana katika kujenga Majumba ya Ufalme na, mara nyingi, kutoka kwa miradi ya Majumba ya Kusanyiko katika sehemu nyingine. Inapohitajiwa, pande fulani za kazi zinaweza kupewa wafanyakazi wa mkataba wa kulipwa, lakini kazi iliyo nyingi kwa kawaida hufanywa na Mashahidi wenye idili. Hiyo inaweza kupunguza nusu ya gharama.

      Kukiwa na jamii ya wafanyakazi wenye stadi na wengine ambao hutoa wakati na vipawa vyao, kwa kawaida ujenzi wote husonga mbele kwa haraka. Ujenzi fulani waweza kuhitaji zaidi ya mwaka. Lakini kwenye Kisiwa cha Vancouver katika Kanada, katika 1985, wenye kujitolea kama 4,500 walikamilisha Jumba la Kusanyiko la meta za mraba 2,300 kwa siku tisa tu. Jengo hilo latia ndani pia Jumba la Ufalme liwezalo kutoshea watu 200 kwa matumizi ya makutaniko ya mahali hapo. Katika New Caledonia, kafyu iliwekwa na serikali katika 1984 kwa sababu ya msukosuko wa kisiasa, hata hivyo wenye kujitolea kama 400 walifanya kazi kwenye Jumba la Kusanyiko wakati ule, na lilikamilishwa kwa miezi minne tu. Karibu na Stockholm, Sweden, Jumba la Kusanyiko zuri, lenye kufaa, likiwa na viti 900 vya mbao za oki vyenye matakia, lilijengwa kwa miezi saba.

      Nyakati nyingine jitihada zenye kuendelea katika mahakama zimehitajiwa ili kupata ruhusa ya kujenga hayo Majumba ya Kusanyiko. Ndivyo ilivyokuwa katika Kanada katika Surrey, British Columbia. Wakati uwanja uliponunuliwa, matakwa ya kisheria ya eneo yaliruhusu ujenzi wa mahali kama hapo pa ibada. Lakini wakati ramani zilipopelekwa kwenye baraza, katika 1974, Baraza la Wilaya ya Surrey lilipitisha sheria ikisema kwamba makanisa na majumba ya kusanyiko yangeweza kujengwa tu katika Eneo la P-3—eneo lisilokuwako! Hata hivyo, makanisa 79 yalikuwa yamejengwa katika manispaa hiyo katika wakati uliopita bila matata. Jambo hilo lilipelekwa mahakamani. Maamuzi mengi yenye kupendelea Mashahidi wa Yehova yalitolewa. Wakati kizuizi cha maofisa wenye chuki zisizo na msingi kilipoondolewa hatimaye, wafanyakazi wa kujitolea walifuatia ujenzi huo kwa idili kubwa hivi kwamba waliukamilisha kwa miezi kama saba. Kama ilivyokuwa kwa habari ya Nehemia katika jitihada zake za kujenga upya kuta za Yerusalemu la kale, walihisi kwamba ‘mkono wa Mungu ulikuwa juu yao’ ili wakamilishe kazi hiyo.—Neh. 2:18.

      Wakati Mashahidi wa Yehova katika Marekani waliponunua Stanley Theater katika Jersey City, New Jersey, jengo hilo lilikuwa katika daftari ya mkoa ya mahali pa kihistoria. Ijapokuwa jumba hilo lilikuwa katika hali mbaya yenye kuhitaji marekebisho, lilikuwa na uwezekano mzuri sana wa kutumika likiwa Jumba la Kusanyiko. Hata hivyo, wakati Mashahidi walipotaka kufanya marekebisho yaliyohitajiwa, maofisa wa jiji walikataa kutoa ruhusa. Meya hakutaka Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo; yeye alikuwa na mipango mingine kwa ajili ya jengo hilo. Hatua ya kisheria ilihitajiwa ili kuzuia maofisa wasitumie mamlaka yao kinyume cha sheria. Mahakama ilitoa uamuzi wenye kupendelea Mashahidi. Upesi baada ya hapo, wakazi wa eneo hilo walipiga kura kumwondoa meya huyo katika cheo chake. Kazi kwenye jumba ilisonga mbele kwa haraka. Tokeo lilikuwa Jumba la Kusanyiko zuri sana lililotoshea watu zaidi ya 4,000. Ni mahali ambapo wanabiashara na wakazi wa jiji hilo pia huonea fahari.

      Wakati wa miaka 27 iliyopita, katika sehemu nyingi za dunia, Majumba ya Kusanyiko yenye kuvutia na yenye kufaa yamejengwa na Mashahidi wa Yehova ili kutumika kuwa vitovu vya elimu ya Biblia. Majumba kama hayo yanapatikana kwa hesabu zenye kuongezeka katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika, na nch za Mashariki, pamoja na visiwa vingi. Katika nchi fulani—kwa kielelezo, Nigeria, Italia, na Denmark—Mashahidi wa Yehova wamejenga hata vifaa vya kudumu vilivyo vikubwa zaidi katika mahali peupe ambavyo vinaweza kutumiwa kwa ajili ya mikusanyiko yao ya wilaya.

  • Kujenga Pamoja Duniani Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Picha katika ukurasa wa 330]

      Majumba ya Kusanyiko ya Mashahidi wa Yehova

      Ili kuwa na mahali pa makusanyiko yao ya pindi kwa pindi, Mashahidi wa Yehova katika baadhi ya maeneo wameona kuwa jambo lenye kufaa kujenga Majumba ya Kusanyiko yao wenyewe. Kazi iliyo nyingi hufanywa na Mashahidi wenyeji. Hapa pana machache tu ya majumba hayo yaliyokuwa yakitumiwa katika miaka ya mapema ya 1990

      Uingereza

      Venezuela

      Italia

      Ujerumani

      Kanada

      Japani

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki