-
Jinsi ya Kuepuka Hatari za IntanetiAmkeni!—2004 | Desemba 8
-
-
Hatari za Vituo vya Maongezi
Mazungumzo kwenye vituo vya Intaneti hupoteza wakati mwingi sana, na kusababisha familia nyingi zivunjike. Mwanamume mmoja aliandika hivi kuhusu kiasi cha wakati ambacho mke wake hutumia kwenye kompyuta: “Mara tu anapofika nyumbani kutoka kazini, yeye huwasha kompyuta na anaweza kuitumia kwa saa tano au zaidi. Hilo limeathiri sana ndoa yetu.” Naam, kutumia Intaneti hukuzuia usifanye mambo na familia yako.
Angela Sibson, ambaye ni mshauri mkuu katika shirika moja la kutoa mashauri ya ndoa linaloitwa Relate, anasema kwamba Intaneti ni “njia ya kuanzisha uhusiano na watu wengine. Uhusiano huo unaweza kuimarika sana na kuvunja uhusiano mwingine wowote ambao mtu alikuwa nao mbeleni.” Mazungumzo ya kirafiki katika kituo cha mazungumzo cha Intaneti yanaweza kubadilika haraka na kuwa hatari. Wakiwa na nia ya kufanya matendo ya ukosefu wa adili, watu walio na “ujanja wa moyo” hutumia “ulimi laini” kuwaambia watu wengine mambo yanayowavutia. (Methali 6:24; 7:10) Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 26 anayeitwa Nicola, ambaye anaishi Uingereza, alidanganywa wakati mmoja kwenye Intaneti. Anasema hivi: “Aliniambia mara nyingi kwamba ananipenda. Alirudia-rudia kuniambia jinsi nilivyokuwa mrembo, nami nikadanganyika.” Dakt. Al Cooper, ambaye ni mwandishi wa kitabu Sex and the Internet: A Guidebook for Clinicians, anasema kwamba tunahitaji “kuwatahadharisha watu kuhusu hatari ya mzaha wa kimahaba unaoanzishwa katika kituo cha Intaneti na ambao mara nyingi husababisha talaka.”
Watoto hasa ndio wanaokabili hatari kubwa zaidi ya kudhulumiwa na “wahalifu wa ngono wanaotumia kompyuta.” Watu ambao hufanya ngono na watoto hutumia “maneno yaliyopotoka” na “hila ya midomo” kuwashawishi watoto wasio na ujuzi. (Methali 4:24; 7:7) Wao huwatayarisha watoto kwa ajili ya matendo machafu kwa kuwaelekezea sana fikira, kuwaonyesha upendo na fadhili nyingi, na hivyo kumfanya mtoto ajihisi kuwa ni wa maana sana. Ni kana kwamba wanajua mambo yanayompendeza mtoto, kutia ndani muziki na mambo anayofurahia kufanya. Wao hukazia sana matatizo madogo ambayo mtoto hukabili nyumbani na hivyo kumfanya aichukie familia yao. Ili watosheleze tamaa yao mbaya, watu hao wanaweza kuwatumia watoto tiketi za kusafiri. Matokeo huwa mabaya sana.
-
-
Jinsi ya Kuepuka Hatari za IntanetiAmkeni!—2004 | Desemba 8
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20, 21]
Jihadhari na Vituo vya Maongezi vya Intaneti!
Mwanamke mmoja ambaye ni polisi wa upelelezi anayeshughulikia uhalifu katika Intaneti alimkaribisha mwandishi wa Amkeni! aone hatari zilizopo katika vituo vya maongezi kwenye Intaneti. Alifungua kituo kimoja na kujifanya eti yeye ni msichana mwenye umri wa miaka 14. Baada ya sekunde chache tu, watu kadhaa walikiandikia kituo hicho. Watu hao waliuliza maswali kama vile: “Unatoka wapi?” “Wewe ni msichana au mvulana?” “Je, tunaweza kuzungumza?” Majibu fulani yalitoka kwa washukiwa kadhaa wa uhalifu wa ngono waliokuwa wakitafutwa na polisi. Hiyo inaonyesha jinsi ilivyo rahisi kwa watu wanaofanya ngono na watoto kuanza mazungumzo na mtoto wako katika kituo cha Intaneti!
Wazazi fulani hudhani kwamba watoto wao wako salama wanapowasiliana katika vituo hivyo vya maongezi eti kwa sababu watu wote wanaotumia kituo hicho wanaweza kuona mambo yanayoandikwa wakati mazungumzo yanapoendelea. Hata hivyo, baada ya kuanza kuwasiliana katika kituo hicho unaweza kukaribishwa uwe na mazungumzo ya watu wawili pekee. Tume ya Intaneti ya Kuwalinda Watoto ya Uingereza inaonya hivi kuhusu zoea hilo: “Unapofanya hivyo ni kama unajitenga na watu kwenye karamu na kuingia katika chumba cha faragha ili uzungumze na mtu usiyemjua.”
Ni muhimu pia kwa wazazi kuelewa kwamba kusudi la watu wanaofanya ngono na watoto si kuzungumza na mtoto tu. Hati iliyotayarishwa na Internet Crime Forum iliripoti hivi: “Baada ya kuwasiliana katika kituo cha maongezi, watu wanaofanya ngono na watoto wanaweza kuendeleza uhusiano na mtoto kupitia njia nyingine za mawasiliano, kama vile barua-pepe na simu (za mkononi).” Ripoti ya Shirika la Ujasusi la Marekani inasema hivi: “Ingawa mhalifu wa ngono anayetumia kompyuta hufurahia kuzungumza na mtoto, huenda akakabili matatizo mbalimbali. Wengi hupenda kumpigia mtoto simu. Wao hupenda kuzungumza na watoto juu ya ngono kupitia simu, nao hujitahidi kupanga wakati ambapo watakutana ili kufanya ngono.”
Ili kutimiza jambo hili, kwa kawaida mhalifu wa ngono anayetumia kompyuta atampatia mtoto namba yake ya simu. Iwapo mtoto wako atampigia simu, mhalifu huyo atatambua namba ya simu ya mtoto. Wahalifu fulani wana namba ambazo hazitozwi chochote au wanaweza kumwambia mtoto apige simu kwa njia ambayo gharama italipwa na anayepigiwa. Wengine hata wamewanunulia watoto simu za mkononi. Pia, wahalifu wanaweza kuwatumia watoto barua, picha, na zawadi.
Sio watoto peke yao wanaoathiriwa. Hivi karibuni, mwanamume mmoja alitumia usemi laini kuwabembeleza wanawake sita huko Uingereza, naye akafanikiwa kuwavutia wote kwa wakati uleule. Mwanamke mmoja mrembo anayeitwa Cheryl, mwenye umri wa miaka 27, ambaye ni mwanafunzi aliyehitimu katika chuo kikuu, ni mmoja kati ya watu walioathiriwa. Alisema hivi: “Sijui niseme nini. Uhusiano wetu kupitia Intaneti ulikuwa wa ndani sana hivi kwamba uliongoza maisha yangu.”
Jenny Madden mwanzilishi wa Women in Cyberspace alisema hivi: “Wanawake huvutiwa kuwasiliana kupitia Intaneti kwa sababu hakuna anayeangalia sura yao. Lakini hilo hufanya iwe rahisi kwao kutumiwa vibaya kwa sababu watu wanapowasiliana kupitia vituo vya maongezi, wao huwa na mwelekeo wa kufunua siri zao nyingi haraka sana.”
Katika uchunguzi mmoja uliofanywa na Beatriz Avila Mileham wa Chuo Kikuu cha Florida, mwanamume mmoja alisema hivi: “Ninahitaji tu kufungua kompyuta yangu na kupata maelfu ya wanawake ninaoweza kuchagua.” Mileham alisema hivi: “Karibuni Intaneti itakuwa njia kuu ya kuwa na uhusiano wa kingono nje ya ndoa.” Dakt. Al Cooper, mhariri wa kitabu Sex and the Internet: A Guidebook for Clinicians alisema hivi: “Wataalamu nchini kote wanasema kwamba uhusiano wa kingono kupitia kompyuta ni kisababishi kikuu cha matatizo ya ndoa.”
Kwa kufikiria hoja hizo muhimu, ni jambo la hekima kujihadhari tunapotumia Intaneti. Zungumza na watoto wako na uwafundishe jinsi wanavyoweza kujilinda dhidi ya hatari hizo. Ukiwa na ujuzi, unaweza kuepuka hatari za Intaneti.—Mhubiri 7:12.
-