-
Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 2Amkeni!—2010 | Desemba
-
-
WATU wa Mashariki ya Kati ya kale waliingiwa na baridi waliposikia neno Ashuru. Kulingana na kitabu cha Biblia cha Yona, nabii huyo alipopewa mgawo na Mungu ahubiri ujumbe wa hukumu huko Ninawi, mji mkuu wa Ashuru, alitoroka kuelekea upande mwingine! (Yona 1:1-3) Huenda alifanya hivyo kwa sababu Waashuru waliogopwa sana.
Historia Inayotegemeka
Nabii Nahumu wa Biblia alisema kwamba Ninawi lilikuwa “tundu la simba”na “jiji la umwagaji wa damu.” Aliongezea hivi: “Mawindo hayaondoki! Kuna sauti ya mjeledi na sauti ya mgongano wa gurudumu, na farasi anayetimua mbio na gari linalorukaruka. Mpanda-farasi, na kumetameta kwa upanga, na kumetameta kwa mkuki, na watu wengi waliouawa, na rundo kubwa la mizoga; wala hakuna mwisho wa maiti. Wanaendelea kujikwaa kati ya maiti zao.” (Nahumu 2:11; 3:1-3) Je, vitabu vya historia vinaunga mkono masimulizi hayo ya Biblia kuhusu Ashuru ya kale?
Kitabu Light From the Ancient Past kinasema kwamba Waashuru “walipigana kwa ustadi na ukatili, na waliwashinda adui zao kwa kutumia mbinu ya kuwaogopesha.” Maneno yanayofuata yanaonyesha jinsi mfalme Ashurnasirpal wa Pili wa Ashuru alivyojigamba kuwatendea wote waliompinga:
Mchongo wa mawe unaoonyesha wafungwa wakichunwa ngozi wakiwa hai
“Nilijenga nguzo kwenye lango la jiji lake, na kuwachuna ngozi wakuu wote waliokuwa wameasi, na nikafunika mnara huo kwa ngozi; wengine niliwatundika juu ya mnara, wengine nikawatundika juu ya miti kwenye mnara, . . . na nilikata miguu na mikono ya maofisa, wale maofisa wa kifalme waliokuwa wameasi. . . . Nikachoma kwa moto mateka wengi miongoni mwao, nami nikachukua mateka wengi walio hai.” Wachimbuzi wa vitu vya kale walipochimbua majumba ya kifalme ya Ashuru, walipata kuta zilizorembeshwa kwa michoro ya mateka wakitendewa kinyama.
-