-
Mwige Kristo Unapokuwa na MamlakaMnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 1
-
-
Yesu Kristo Amepewa “Mamlaka Yote”
Fikiria mfano wa Yesu Kristo. Kabla tu ya kwenda mbinguni, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mathayo 28:18) Je, maneno hayo yaliwaogopesha wanafunzi hao? Je, walihisi kwamba sasa Yesu angekuwa kama Makaisari wa Roma ambao walikuwa wakikomesha migawanyiko au maasi kimabavu?
Masimulizi ya Biblia hayasemi hivyo! Yesu Kristo hutumia mamlaka kama Baba yake. Ingawa Yehova ndiye Mweza-Yote na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, yeye hutaka raia zake wamtumikie kwa hiari wala si kumtii bila kufikiri, kwa kuogopa, au kama watumwa. (Mathayo 22:37) Yehova hatumii kamwe mamlaka yake vibaya. Jambo hilo linaonyeshwa na maono yenye kusisimua ambayo nabii Ezekieli aliona.
Katika maono hayo, Ezekieli aliona viumbe wanne wa kimalaika ambao walitetea enzi kuu ya Mungu. Kila mmoja wao alikuwa na nyuso nne. Ezekieli aliandika hivi: “Na mfano wa nyuso zao, hao wanne walikuwa na uso wa mwanadamu na uso wa simba upande wa kuume, na hao wanne walikuwa na uso wa ng’ombe-dume upande wa kushoto; hao wanne pia walikuwa na uso wa tai.” (Ezekieli 1:10) Nyuso hizo nne zinawakilisha sifa nne kuu za Mungu ambazo anasawazisha kikamilifu. Neno la Mungu linataja sifa hizo kuwa: upendo, ambao unawakilishwa na uso wa mwanadamu; haki, ambayo inawakilishwa na uso wa simba; na hekima, ambayo inawakilishwa na uso wa tai. Sifa hizo tatu hutumiwa pamoja na sifa ya nne ya nguvu, ambayo inawakilishwa na uso wa ng’ombe-dume. Mambo hayo yanamaanisha nini? Maono hayo yanaonyesha kwamba sikuzote Yehova hutumia nguvu zake zisizo na kikomo na mamlaka yake kupatana na zile sifa nyingine zake kuu.
Kwa kumwiga Baba yake, sikuzote Yesu Kristo alitumia mamlaka yake kupatana kabisa na upendo, hekima, na haki. Wanafunzi wa Yesu waliburudika sana walipotumikia chini ya mamlaka yake. (Mathayo 11:28-30) Upendo ndio sifa kuu zaidi inayomtambulisha Yehova Mungu na Yesu Kristo, bali si nguvu wala mamlaka!—1 Wakorintho 13:13; 1 Yohana 4:8.
-
-
Mwige Kristo Unapokuwa na MamlakaMnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 1
-
-
Namna gani ikiwa una mamlaka ya kadiri fulani katika kutaniko la Kikristo? Ili uone ikiwa unatumia mamlaka yako vizuri, jichunguze ukitumia kanuni zifuatazo kutoka kwa Yehova Mungu ambazo Yesu Kristo alituwekea mfano wa kuzitumia.
“Mtumwa wa Bwana . . . anahitaji kuwa mpole kwa wote, . . . akiendelea kujizuia chini ya uovu, akiwafundisha kwa upole wale wasio na mwelekeo unaofaa.”—2 Timotheo 2:24, 25.
Watu fulani katika kutaniko la mapema la Kikristo walikuwa na mamlaka nyingi. Kwa mfano, Timotheo angeweza ‘kuwaamuru watu fulani wasifundishe fundisho tofauti.’ (1 Timotheo 1:3) Hata hivyo, hapana shaka kwamba Timotheo aliiga sifa za Mungu katika mambo yote aliyofanya, kwa kuwa alifuata shauri la Paulo la kufundisha “kwa upole” na “kuwa mpole kwa wote” akiwa mwangalizi katika kutaniko la Kikristo. Kwa kuwa Timotheo alikuwa kijana, alipaswa kuwatendea wazee kama mwana mwenye heshima na kuwatendea vijana kama ndugu anayejali. (1 Timotheo 5:1, 2) Kupitia utunzaji huo wenye upendo, kutaniko la Kikristo huwa kama familia yenye upendo na uchangamfu wala si kama kampuni yenye ubaridi na isiyojali.—1 Wakorintho 4:14; 1 Wathesalonike 2:7, 8.
“Watawala wa mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu hutumia mamlaka juu yao. Hivyo sivyo ilivyo katikati yenu; bali yeyote anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu.”—Mathayo 20:25, 26.
Madikteta wa ulimwengu “hupiga ubwana” juu ya watu wengine kwa kuwashurutisha raia zao na kusisitiza wafanye mambo kwa njia fulani, nao huwatisha kwamba wataadhibiwa wasipotii. Hata hivyo, Yesu Kristo alikazia kwamba inafaa kuwatumikia wengine na si kuwashurutisha. (Mathayo 20:27, 28) Sikuzote aliwajali wanafunzi wake na aliwatendea kwa upendo. Ukifuata kielelezo cha Yesu, itakuwa rahisi kwa wengine kushirikiana nawe. (Waebrania 13:7, 17) Itakuwa rahisi kwao pia kufanya mengi zaidi ya yale unayowaomba wafanye, na watayafanya kwa hiari bali si kwa kuhisi kwamba wanalazimishwa.—Mathayo 5:41.
“Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si . . . kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.”—1 Petro 5:2, 3.
Leo, waangalizi wanatambua kwamba watatoa hesabu kwa ajili ya hali ya kiroho ya wote katika kutaniko. Wanachukua daraka hilo kwa uzito. Wanapolitunza kundi la Mungu, wao hujitahidi kufanya hivyo kwa hiari, kwa hamu, na kwa upendo. Kama mtume Paulo, wao hujitahidi sana kujenga na kuimarisha imani ya wale walio chini yao, badala ya kuwa mabwana wa imani yao.—2 Wakorintho 1:24.
Shauri linapohitajiwa, wazee hulitoa kwa roho ya upole ili kumrekebisha mkosaji au kumsaidia Mkristo mwenzao kufanya maendeleo ya kiroho. Wao hukumbuka maneno haya ya mtume Paulo: “Akina ndugu, hata mtu akijikwaa katika kosa fulani kabla ya yeye kulijua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole, huku kila mmoja wenu akiendelea kujiangalia, ili wewe pia usije ukajaribiwa.”—Wagalatia 6:1; Waebrania 6:1, 9-12.
“Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari . . . Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:13, 14.
Wewe huwatendeaje wale wasiofuata kwa ukamili kanuni za Kikristo? Je, wewe hutambua kwamba wao si wakamilifu kama Yehova na Yesu Kristo wanavyotambua? (Isaya 42:2-4) Au je, wewe husisitiza sheria katika kila jambo? (Zaburi 130:3) Kumbuka kwamba inafaa kuonyesha upole inapowezekana na kuwa thabiti wakati tu inapohitajiwa. Ukiwatendea wale walio chini ya mamlaka yako kwa upendo, utaweza kuwaamini sana nao pia watakuamini.
Ikiwa umepewa mamlaka yoyote, jitahidi sana kumwiga Yehova Mungu na Yesu Kristo unapoitumia.
-