-
Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
MPANGO MPYA WA KUFANYA UPAINIA MSAIDIZI
Kulikuwa na msisimuko mkubwa ilipotangazwa kuwa mapainia wasaidizi wanaweza kutimiza takwa la saa 30 au 50 katika mwezi wa Aprili. Wengi ambao kwa kawaida hawangeweza kushiriki utumishi huo walifurahi sana kupata fursa hiyo. Maelfu ya wahubiri walichukua upainia msaidizi kwa mara ya kwanza, na wengi ambao walikuwa mapainia hapo awali walifurahi kufanya hivyo tena. Isitoshe, wahubiri wengi ambao hawakuweza kufanya upainia msaidizi walijitahidi sana kuongeza utumishi wao. Kulikuwa na matokeo gani?
Ofisi nyingi za tawi ziliripoti ongezeko lililozidi vilele vya hapo awali. Ulimwenguni, wahubiri 2,657,377 walichukua upainia msaidizi na idadi hiyo ni mara tano zaidi ya kilele cha mapainia wasaidizi cha mwaka uliotangulia! Asilimia 80 ya Wanabetheli wote duniani, yaani 16,292 kati ya Wanabetheli 20,290, walishiriki katika pendeleo hilo la utumishi. Je, haipendezi kujua kwamba watumishi wa Yehova walifanya mengi zaidi katika kazi ya kuhubiri mwezi wa Aprili kuliko mwezi mwingine wowote katika historia?
Zaidi ya mwaka mmoja tu baada ya tetemeko kubwa la nchi lililosababisha vifo vya watu 300,000 hivi, mwezi wa Aprili nchi ya Haiti iliripoti vilele vipya katika historia ya kazi ya kuhubiri nchini humo. Wahubiri 6,185 kati ya 17,009, walikuwa mapainia wasaidizi. Kampeni ya pekee ya kusambaza broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, ambayo karibuni imetolewa katika Kikrioli cha Haiti, iliwafariji sana na kuwapa tumaini watu waliokuwa wanaomboleza.
Mwezi wa Aprili, ndugu na dada zetu nchini Nigeria walikabili hali ngumu isiyo ya kawaida. Katika siku nne zilizotengwa kwa ajili ya uchaguzi (tatu zikiwa za Jumamosi), serikali iliwakataza watu kutembea nje kati ya saa moja asubuhi na saa kumi na moja jioni isipokuwa kwa sababu ya kupiga kura. Hata hivyo, wahubiri hawakukata tamaa. Kutaniko moja lilisema: “Tunawaandikia tukiwa na shangwe nyingi na mioyo iliyojaa uthamini kwa sababu ya wakati mzuri ambao tumefurahia mwezi huo.” Katika kutaniko lingine, 92 kati ya wahubiri 127 waliobatizwa walijiandikisha kuwa mapainia wasaidizi, kutia ndani wazee wote na watumishi wa huduma. Wanabetheli 555 kati ya washiriki wote 688 wa familia ya Betheli walifanya upainia msaidizi.
Walifaulu Licha ya Hali Ngumu. Jeannette, anayeishi katika eneo la vijijini lenye milima nchini Burundi, ametamani siku zote kuwa painia, lakini ana ugonjwa wa moyo unaomzuia kutembea mbali au kwenye maeneo yenye mwinuko sana. Jeannette alifurahi aliposikia kwamba takwa la saa kwa ajili ya mapainia wasaidizi katika mwezi wa Aprili limepunguzwa. Ili kumsaidia kutimiza tamaa yake ya kuwa painia, wazee walipanga ahubiri katika eneo lililo karibu na kwake. Zaidi ya hayo, mapainia na wahubiri waliongoza mafunzo yao ya Biblia nyumbani kwake. Kufikia mwisho wa mwezi, Jeannette alifurahi kwamba alikuwa ameanzisha mafunzo manne ya Biblia. “Ningependa kufanya upainia tena,” anasema, “na nina hakika kwamba Yehova atanisaidia.”
Katika kisiwa cha Grenada, dada mmoja kijana ambaye ni kiziwi alifanya upainia licha ya matatizo yanayofanya iwe vigumu kwake kutembea. Anasema, “Ilikuwa vigumu sana kutembea mbali hadi kwenye kituo cha basi ili kupata gari la kwenda kwenye mkutano wa utumishi.” Isitoshe, dada huyo hakuwa na kazi, na alimwomba Yehova kwa bidii amsaidie. Alitenda kulingana na sala zake na akawa akijiruzuku kwa kuuza vitu vilivyofumwa kwa kroshia na vito vinavyotengenezwa kwa mkono. Alisema hivi baadaye: “Nilishiriki kikamili kazi ya kuhubiri na ndugu walinitegemeza na kunitia moyo sana. Hilo liliniletea furaha ya kweli!”
Toshi, dada mwenye umri wa miaka 101 nchini Japani, alifurahi kujiandikisha kuwa painia msaidizi mwezi wa Aprili. Kwa kuwa hawezi kwenda nje ya makao anayoishi, yeye huhubiri kwa kuandika barua au kuwahubiria watu wanaofanya kazi hapo. Anaeleza: “Kwa kuwa nina tatizo la kusikia, mimi huzungumza kwa sauti ya juu. Kwa hiyo, hata watu walio katika ujirani wanaweza kunisikia.”
Felix, ndugu anayeishi Kosta Rika na ambaye amepooza mikono na miguu aliamua kuwa painia msaidizi. Angefanyaje hivyo? Aliwekewa meza ya vitabu nje ya nyumba yake ili awahubirie wapita-njia. Mwisho wa mwezi, Felix alikuwa amechoka lakini alihisi ameburudika kiroho na alifurahi kuanzisha mafunzo manne ya Biblia.
Wahubiri wengi wachanga walifurahia pia kushiriki katika utendaji wa pekee mwezi huo. Kwa mfano, huko Hispania, Sandra mwenye umri wa miaka 11 na kaka yake, Alejandro, mwenye umri wa miaka 7, walitaka kuongeza utumishi wao. Walichochewa na bidii ya ndugu wa kutaniko lao na mfano mzuri wa wazazi wao, na wakatamani kuwa mapainia wasaidizi. Wangefanyaje hivyo ilhali hawajabatizwa? Wote wawili walipanga ratiba ya kutumia wakati sawa na wa wazazi wao katika utumishi, na kujitayarisha kwa kuwa na vipindi vya mazoezi wakati wa jioni ya Ibada ya Familia. Wazazi wao walifikiri kwamba kadiri mwezi ulivyosonga, watoto hao wangechoka. Lakini watoto hao hawakuyumba-yumba. Kufikia Aprili 30, wote katika familia hiyo walikuwa wametimiza mradi wao wa saa 30 isipokuwa Alejandro, ambaye bado alihitaji saa tatu. Hivyo, akaenda kuhubiri na baba yake ili atimize lengo lake la mwezi huo. Walifurahi kama nini kuwa na wakati mzuri na kufanya mengi wakiwa familia iliyoungana!
“Nilisali kila siku,” asema Jean, “kwamba mimi na mume wangu, Philip, tuweze kuhubiri saa 30.” Hata hivyo, Philip, ambaye awali alikuwa mwangalizi wa wilaya hadi alipodhoofishwa na ugonjwa unaoathiri ubongo wake, alilazwa hospitalini nchini Hispania, akiwa hata hawezi kusema. Aliwasiliana tu kwa macho, akiyafumba na kufumbua mara moja ili kusema ndiyo na mara mbili ili kusema la.
“Nilipomwambia kuhusu upainia msaidizi,” Jean aendelea kusema, “alionyesha kwamba yeye pia angependa kuwa painia msaidizi.” Lakini angetimizaje mradi huo?
Miezi iliyokuwa imepita, Jean na Philip waliwahubiria wagonjwa, watu wa familia waliowatembelea, na wafanyakazi hospitalini. “Mwezi wa Aprili, tulipanga kuhubiri hapo hospitalini kwa saa moja hivi kwa siku Philip alipokuwa macho, na angeshiriki katika mazungumzo hayo kwa kufumba na kufumbua macho.”
Hata hivyo ilipofika Machi, Philip alipelekwa kwenye wadi ya wagonjwa wasiopaswa kuchangamana na wengine. Lakini, yeye na Jean waliweza kufuata ratiba yao kwa kuwahubiria wafanyakazi wa hospitali kwa dakika chache mara tofauti-tofauti kwa siku. Mmoja wa wauguzi aliyekubali kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? alimtazama Philip machoni na kumwahidi kuwa angerudi kesho yake ili asome maandiko. Aliporudi, Jean alimwomba asome Yohana 17:3 na akamuuliza maoni yake kuhusu andiko hilo. Waliendelea kwa njia hiyo, naye Philip alionyesha kwa macho kama jibu la muuguzi huyo ni sahihi au la. Hata wakati ambapo hakufanya kazi katika wadi hiyo, muuguzi huyo wa kike alikuja kumhakikishia Philip kwamba alikuwa akimwomba Yehova ili awe na uhusiano wa karibu pamoja Naye.
Watumishi wa Yehova wanaona utendaji huo ulioongezeka kuwa njia ya kuonyesha upendo wao kwa jirani zao, kuonyesha shukrani kwa dhabihu ya Yesu Kristo, na kuonyesha kwamba wanajitoa kwa Baba yao wa mbinguni. Wanatazamia kwa hamu mwezi wa Machi 2012, ambapo watapata fursa nyingine ya kutimiza takwa la saa 30 au 50 katika kazi ya kuhubiri.
-
-
Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
Mambo Waliyosema Kuhusu Upainia Msaidizi:
• “Ilikuwa mara ya kwanza maishani mwangu kufanya upainia msaidizi. Sijui niseme nini kuonyesha jinsi ninavyothamini pendeleo hili!”
• “Asanteni sana kwa mpango huu mpya. Umetuletea shangwe nyingi sana.”
• “Mpango huo ulikuwa wa pekee sana katika historia ya kutaniko letu.”
• “Kuwa na mapainia wasaidizi wengi sana kumechangia roho ya amani na umoja kutanikoni.”
• “Lazima Har–Magedoni iwe imekaribia sana!”—Mtu fulani ambaye si Shahidi aliyeona bidii yetu katika mwezi wa Aprili.
-