-
“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini MnyenyekevuMkaribie Yehova
-
-
Yehova Hukubali Sababu
13. Usemi “kukubali sababu” hutumiwa katika Biblia kumaanisha nini, na kwa nini sifa hiyo inamfaa kabisa Yehova?
13 Unyenyekevu wa Yehova unadhihirishwa na sifa nyingine yenye kupendeza—kukubali sababu. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wanadamu wengi wasiokamilika hawana sifa hiyo. Yehova yuko tayari kuwasikiliza viumbe wake wenye akili, na yuko tayari pia kukubali maoni yao maadamu hayakiuki kanuni zake za uadilifu. Usemi “kukubali sababu” hutumiwa katika Biblia kumaanisha kihalisi ‘kukubali maoni ya wengine.’ Hiyo pia ni sifa muhimu ya hekima ya Mungu. Andiko la Yakobo 3:17 lasema hivi: ‘Hekima ya kutoka juu ni yenye kukubali sababu.’ Yehova ambaye ni mwenye hekima kamilifu anakubali sababu kwa njia gani? Kwanza, yeye hujipatanisha na hali mbalimbali. Kumbuka kwamba jina lake linatufundisha kwamba Yeye hujisababisha kuwa chochote kinachohitajiwa ili kutimiza makusudi yake. (Kutoka 3:14) Je, hilo halionyeshi kwamba yeye hujipatanisha na hali na ni mwenye kukubali sababu?
14, 15. Ono la Ezekieli la gari la kimbingu la Yehova linatufunza nini kuhusu tengenezo Lake la kimbingu, na hilo linatofautianaje na mashirika ya wanadamu?
14 Kuna ono moja la Biblia linalotusaidia kuelewa kwa kadiri fulani jinsi Yehova anavyojipatanisha na hali mbalimbali. Nabii Ezekieli alipata ono la tengenezo la kimbingu la Yehova la viumbe wa roho. Aliona gari kubwa ajabu na Yehova mwenyewe ndiye anayelielekeza gari hilo daima. Lilienda kwa njia ya kustaajabisha sana. Magurudumu yake makubwa yenye pande nne, yalijaa macho hivi kwamba yaliweza kuona kila mahali na kusafiri kuelekea upande wowote ghafula bila kusimama wala kugeuka. Na gari hilo kubwa mno halikujikokota polepole kama gari lililotengenezwa na wanadamu. Liliweza kwenda kwa mwendo wa umeme, na hata kugeuka ghafula! (Ezekieli 1:1, 14-28) Naam, tengenezo la Yehova linaweza kujipatanisha kabisa na hali mbalimbali na kushughulikia mahitaji yanayotokea kama anavyofanya Mungu Mwenye Enzi Kuu na mweza-yote ambaye analiongoza.
15 Wanadamu hawawezi kamwe kujipatanisha kikamili na hali kwa njia hiyo. Mara nyingi wanadamu na mashirika yao hushikilia mno maoni yao bila kubadilika, na hawakubali sababu. Kwa mfano: Meli ya mafuta au garimoshi la kubeba mizigo laweza kuwa kubwa sana na lenye nguvu nyingi sana. Lakini je, garimoshi au meli inaweza kugeuka mara moja hali zikibadilika? Garimoshi la mizigo haliwezi kuepuka kitu fulani kinachoanguka kwenye reli yake. Haliwezi kusimama ghafula. Baada ya breki kufungwa, garimoshi lenye mizigo mizito laweza kwenda umbali wa kilometa mbili hivi kabla ya kusimama! Vivyo hivyo, huenda meli kubwa ya mafuta ikasafiri umbali wa kilometa nane baada ya injini kuzimwa. Hata injini zikiendeshwa kinyumenyume, bado meli hiyo inaweza kusonga mbele umbali wa kilometa tatu! Ndivyo ilivyo na mashirika ya wanadamu ambayo mara nyingi hushikilia sana sera zake na kutokubali mawazo mapya. Mara nyingi watu hukataa kubadilika kulingana na mahitaji na hali mpya kwa sababu ya kiburi. Mashirika mengi yamevunjika na hata serikali nyingi kupinduliwa kwa sababu ya kutobadilika kulingana na hali. (Mithali 16:18) Twaweza kushukuru kama nini kwamba Yehova na tengenezo lake ni tofauti sana na mashirika hayo ya wanadamu!
Jinsi Yehova Anavyokubali Sababu
16. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu aliposhughulika na Loti kabla ya kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora?
16 Fikiria tena kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora. Malaika wa Yehova alimpa Loti na familia yake maagizo yaliyo wazi kabisa: “Ujiponye mlimani.” Lakini maagizo hayo hayakumpendeza Loti. “Sivyo, bwana wangu!” akasihi. Akiamini kwamba angekufa kama angekimbilia milimani, Loti aliomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia mji wa karibu ulioitwa Soari. Kumbuka kwamba Yehova alikuwa amekusudia kuuangamiza mji huo. Isitoshe, Loti hakuwa na sababu nzuri ya kuogopa. Bila shaka Yehova angeweza kumlinda Loti huko milimani! Hata hivyo, Yehova alikubali ombi la Loti, hakuuangamiza mji wa Soari. Malaika akamwambia hivi Loti, “Tazama, nimekukubali hata kwa neno hili.” (Mwanzo 19:17-22) Je, jambo hilo halionyeshi kwamba Yehova ni mwenye kukubali sababu?
17, 18. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu kuhusiana na Waninawi?
17 Yehova hukubali pia toba ya kutoka moyoni. Sikuzote yeye huonyesha rehema na kutenda yaliyo sawa. Fikiria jambo lililotukia nabii Yona alipotumwa mji wa Ninawi wenye uovu na jeuri. Yona alitangaza ujumbe rahisi sana wa Mungu kotekote katika Ninawi: Mji huo mashuhuri ungeangamizwa baada ya siku 40. Lakini, mambo yalibadilika ghafula. Waninawi walitubu!—Yona, sura ya 3.
18 Tunajifunza jambo fulani tunapolinganisha jinsi Yehova alivyohisi na jinsi Yona alivyohisi hali ilipobadilika. Yehova alijipatanisha na hali hiyo mara moja, akawa Mwenye Kusamehe dhambi badala ya kuwa “mtu wa vita.”d (Kutoka 15:3) Lakini Yona hakuwa tayari kubadilika wala hakuonyesha rehema kama Yehova alivyofanya. Badala ya kukubali sababu kama Yehova, alikuwa kama garimoshi la mizigo au meli kubwa ya mafuta tuliyotaja awali. Alitaka mji huo uangamizwe tu kama alivyokuwa ametangaza. Hata hivyo, kwa subira Yehova alimfundisha nabii wake asiye na subira somo lisilosahaulika kuhusu kukubali sababu na kuonyesha rehema.—Yona, sura ya 4.
Yehova ni mwenye kukubali sababu na anajua udhaifu wetu
19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ni mwenye kukubali sababu kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye? (b) Mithali 19:17 inaonyeshaje kwamba Yehova ni Bwana ‘mwema na mwenye kukubali sababu,’ na kwamba unyenyekevu wake hauna kifani?
19 Mwishowe, Yehova ni mwenye kukubali sababu kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye. Mfalme Daudi alisema: “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:14) Yehova anajua udhaifu wetu na kasoro zetu kuliko tunavyojijua. Hatarajii kamwe tufanye mambo yanayozidi uwezo wetu. Biblia inasema kwamba mabwana fulani ni ‘wema na wenye kukubali sababu’ na wengine ni “wagumu kupendeza.” (1 Petro 2:18) Je, Yehova ni Bwana wa aina gani? Mithali 19:17 inasema: “Amhurumiaye maskini humkopesha BWANA.” Ni wazi kwamba bwana aliye mwema na mwenye kukubali sababu ndiye tu anayezingatia kila tendo la fadhili ambalo maskini wanafanyiwa. Isitoshe, andiko hilo pia linadokeza kwamba Muumba wa ulimwengu anajiona kuwa na deni kwa wanadamu duni wanaofanya matendo hayo ya rehema! Huo ni unyenyekevu usio na kifani.
20. Tuna uhakika gani kwamba Yehova husikiliza na kujibu sala zetu?
20 Hata leo Yehova ni mpole na mwenye kukubali sababu anaposhughulika na watumishi wake. Yeye husikiliza sala zetu za imani. Hatupaswi kukata kauli kwamba hajibu sala zetu kwa sababu hawatumi malaika waongee nasi. Kumbuka kwamba mtume Paulo alipowaomba waamini wenzake ‘waendeleze sala’ ili aweze kuachiliwa kutoka gerezani, aliongeza hivi: “Ili nipate kurudishwa kwenu karibuni zaidi.” (Waebrania 13:18, 19) Kwa hiyo, sala zetu zinaweza kwa kweli kumfanya Yehova atende jambo ambalo huenda hangetenda!—Yakobo 5:16.
21. Hatupaswi kuwa na maoni gani kuhusu unyenyekevu wa Yehova, lakini tunapaswa kumthamini kwa sababu gani?
21 Bila shaka, sifa zinazoonyesha unyenyekevu wa Yehova, yaani, upole, utayari wa kutusikiliza, subira, na kukubali sababu, hazimaanishi kwamba Yehova hulegeza kanuni zake adilifu. Huenda makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wakadhani kwamba wanakubali sababu wanapotekenya masikio ya wafuasi wao kwa kulegeza kanuni za Yehova za maadili. (2 Timotheo 4:3) Lakini mwelekeo wa wanadamu wa kuridhiana ili wapendwe haupatani kabisa na sifa ya Mungu ya kukubali sababu. Yehova ni mtakatifu; hawezi kamwe kupotosha kanuni zake adilifu. (Mambo ya Walawi 11:44) Basi, na tupende sifa ya Yehova ya kukubali sababu kwa kuwa inathibitisha unyenyekevu wake. Je, hufurahi sana kujua kwamba Yehova Mungu ni mnyenyekevu sana licha ya kwamba ana hekima isiyo na kifani katika ulimwengu wote? Inapendeza kama nini kumkaribia Mungu huyu mtukufu ambaye ni mpole, mwenye subira, na mwenye kukubali sababu!
-
-
“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini MnyenyekevuMkaribie Yehova
-
-
d Zaburi 86:5 inasema kwamba Yehova ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe.’ Zaburi hiyo ilipotafsiriwa katika Kigiriki, usemi “tayari kusamehe” ulitafsiriwa e·pi·ei·kesʹ, au “mwenye kukubali sababu.”
-