-
Albania2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
MWANZO MZURI—KISHA MATATIZO
Ingawa Halmashauri ya Nchi ilijitahidi kuendeleza ibada safi, matatizo yalikuwa njiani. Mwaka wa 1963, Melpo Marks alimwandikia John, ndugu yake, kwamba ndugu wawili wa Halmashauri ya Nchi, Leonidha Pope na Luçi Xheka, hawakuwa “pamoja na familia zao” na kwamba mikutano haifanywi. Baadaye kukawa na fununu kwamba Spiro Vruho yuko hospitalini, naye Leonidha Pope na Luçi Xheka ni wagonjwa, andiko la Matendo 8:1, 3 lilirejelewa, ambapo Sauli wa Tarso aliwatia Wakristo gerezani. Ni nini kilichokuwa kikiendelea?
Leonidha Pope, Luçi Xheka, na Sotir Ceqi walikuwa wakifanya kazi katika kiwanda fulani ambapo washiriki wa Chama cha Kikomunisti walifanya mkutano na wafanyakazi wote, wakipigia debe dhana za Kikomunisti. Siku moja, kulipokuwa na mazungumzo kuhusu mageuzi, Leonidha na Luçi walisimama na kusema: “Hapana! Mwanadamu hakutokana na nyani!” Siku iliyofuata walichukuliwa na kutenganishwa na familia zao, na kupelekwa kufanya kazi uhamishoni katika miji ya mbali, adhabu ambayo huitwa internim (korokoroni) na Waalbania. Luçi alipelekwa katika milima ya Gramsh. Kwa kuwa waliamini kwamba Leonidha ndiye “mkubwa” wao, walimpeleka katika milima ya Burrel, yenye mawe-mawe na baridi kali. Miaka saba ilipita kabla ya kurudi nyumbani kwao, Tiranë.
Kufikia Agosti 1964, karibu mikutano yote iliacha kufanywa. Ripoti chache zilizopokewa zilionyesha kwamba ndugu hao walikuwa chini ya uchunguzi mkali wa Sigurimi. Stempu moja ilikuwa na ujumbe huu: “Mwombeni Bwana kwa niaba yetu. Nyumba zinapekuliwa. Hawaturuhusu kujifunza. Watatu wako korokoroni.” Mwanzoni, ilidhaniwa kwamba ndugu Pope na Xheka walikuwa wameachiliwa, kwa kuwa wao tu ndio waliojua mbinu hiyo ya kuandika chini ya stempu. Hata hivyo, baadaye ilikuja kujulikana kwamba Frosina, mke wa Luçi, ndiye aliyekuwa ametuma ujumbe huo.
Akina ndugu waliokuwa wakiongoza hawakuwako. Nao waliobaki hawakuweza kuwasiliana kwa sababu ya upelelezi wa Sigurimi. Hata hivyo, ndugu waliokuwa korokoroni waliwatolea ushahidi mzuri mtu yeyote waliyekutana naye. Watu wa Gramsh walikuwa wakisema: “Ungjillorë [wainjilisti] wako hapa. Hawajiungi na jeshi, lakini wanatujengea madaraja na kurekebisha majenereta.” Sifa nzuri ya ndugu hao ilijulikana kwa miaka mingi.
-
-
Albania2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Marufuku ilipoondolewa mwaka wa 1992, Frosina alikuwa mmoja wa Mashahidi tisa waliobatizwa ambao walikuwa wamebaki Albania.
-