-
‘Nendeni Mkafanye Wanafunzi, Mkiwabatiza’Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 1
-
-
Wakati wa ubatizo, wale wanaotaka kubatizwa huulizwa maswali mawili ya msingi, nao hujibu kwa kusema ndiyo. Kwa kuwa Yesu alikazia kwamba ‘neno letu Ndiyo linapaswa kumaanisha Ndiyo, na Siyo yetu, Siyo,’ inafaa sote tuchunguze kwa makini maana ya maswali hayo mawili ya ubatizo.—Mathayo 5:37.
Toba na Wakfu
5. Swali la kwanza la ubatizo linakazia hatua gani mbili muhimu?
5 Katika swali la kwanza la ubatizo, yule anayetaka kubatizwa huulizwa ikiwa ametubu kuhusiana na mambo aliyofanya zamani na ikiwa amejiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake. Swali hilo linakazia hatua mbili muhimu ambazo mtu anahitaji kuchukua kabla ya kubatizwa, yaani, toba na wakfu.
6, 7. (a) Kwa nini ni lazima wote wanaotaka kubatizwa watubu? (b) Ni lazima mtu afanye mabadiliko gani baada ya kutubu?
6 Kwa nini ni lazima mtu atubu kabla ya kubatizwa? Mtume Paulo anaeleza hivi: “Wakati fulani sisi sote tulijiendesha . . . kupatana na tamaa za mwili wetu.” (Waefeso 2:3) Kabla ya kupata ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu, tuliishi kupatana na ulimwengu, kulingana na maadili yake na viwango vyake. Maisha yetu yaliongozwa na mungu wa mfumo huu, Shetani. (2 Wakorintho 4:4) Hata hivyo, baada ya kujua mapenzi ya Mungu, tunaazimia kuishi “si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.”—1 Petro 4:2.
7 Maisha hayo mapya huleta faida nyingi. Kwanza kabisa, yanatuwezesha kuwa na uhusiano wenye thamani pamoja na Yehova, ambao Daudi aliulinganisha na mwaliko wa kuingia katika “hema” la Mungu na “mlima [wake] mtakatifu.” Hilo ni pendeleo kubwa ajabu! (Zaburi 15:1) Yehova hamkaribishi mtu yeyote bali anawakaribisha wale tu ‘wanaotembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wao.’ (Zaburi 15:2) Kwa kuwa tulikuwa katika hali mbalimbali kabla ya kujifunza kweli, ili tutimize matakwa hayo huenda tukalazimika kufanya mabadiliko fulani katika mwenendo na utu wetu. (1 Wakorintho 6:9-11; Wakolosai 3:5-10) Kile kinachomchochea mtu afanye mabadiliko hayo ni toba, yaani, kujutia kabisa maisha yetu ya zamani na kuazimia kwa bidii kumpendeza Yehova. Toba humwongoza mtu ageuke kabisa, yaani, aache maisha ya kilimwengu ya ubinafsi na kufuata njia inayompendeza Mungu.—Matendo 3:19.
8. Sisi hujiwekaje wakfu, na kujiweka wakfu kunahusianaje na ubatizo?
8 Katika sehemu ya pili ya swali la kwanza la ubatizo, wale wanaotaka kubatizwa huulizwa ikiwa wamejiweka wakfu kwa Yehova ili wafanye mapenzi yake. Wakfu ni hatua muhimu ambayo inapaswa kutangulia ubatizo. Hatua hiyo hufanywa kupitia sala, na katika sala hiyo tunaeleza tamaa yetu ya kutoa maisha yetu kwa Yehova kupitia Kristo. (Waroma 14:7, 8; 2 Wakorintho 5:15) Kisha, Yehova anakuwa Bwana wetu na Mmiliki wetu, nasi tunafurahia kufanya mapenzi ya Mungu kama Yesu. (Zaburi 40:8; Waefeso 6:6) Ahadi hiyo nzito inayotolewa kwa Yehova hufanywa mara moja tu. Hata hivyo, kwa kuwa tunajiweka wakfu faraghani, siku ya ubatizo tunafanya tangazo la hadharani ili kuwaonyesha watu wote kwamba tumechukua hatua hiyo nzito ya kujiweka wakfu kwa Baba yetu wa mbinguni.—Waroma 10:10.
9, 10. (a) Mapenzi ya Mungu yanahusisha nini? (b) Maofisa wa Nazi walitambuaje kwamba tumejiweka wakfu?
9 Kuiga kielelezo cha Yesu cha kufanya mapenzi ya Mungu kunahusisha nini? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.” (Mathayo 16:24) Hapa Yesu alitaja mambo matatu ambayo ni lazima tuyafanye. Kwanza, ‘tunajikana’ wenyewe, yaani, tunaacha mielekeo yetu ya ubinafsi ya kutokamilika, na badala yake tunakubali shauri na mwongozo wa Mungu. Pili, ‘tunauchukua mti wetu wa mateso.’ Katika siku za Yesu, mti wa mateso uliwakilisha aibu na kuteseka. Kwa kuwa sisi ni Wakristo, tunakubali kuteseka kwa ajili ya habari njema. (2 Timotheo 1:8) Ingawa watu katika ulimwengu wanaweza kutudhihaki au kutushutumu, sisi ‘hudharau aibu’ kama Kristo, nasi tunapata furaha kwa kujua kwamba tunampendeza Mungu. (Waebrania 12:2) Mwishowe, tunamfuata Yesu “sikuzote.”—Zaburi 73:26; 119:44; 145:2.
10 Inapendeza kwamba hata wapinzani fulani hutambua kuwa Mashahidi wa Yehova wamejiweka wakfu kwa Mungu ili wamtumikie kwa moyo wote. Kwa mfano, katika kambi ya mateso ya Buchenwald wakati wa utawala wa Nazi huko Ujerumani, Mashahidi waliokataa kukana imani yao walipaswa kutia sahihi taarifa hii iliyochapishwa: “Bado mimi ni Mwanafunzi wa Biblia mwaminifu, nami sitavunja kamwe kiapo changu mbele za Yehova.” Bila shaka, maneno hayo yanaonyesha wazi mtazamo wa watumishi wote waaminifu wa Mungu waliojiweka wakfu!—Matendo 5:32.
Kutambulishwa Kuwa Mmoja wa Mashahidi wa Yehova
11. Mtu anayebatizwa anapata pendeleo gani?
11 Katika sehemu ya kwanza ya swali la pili, yule anayetaka kubatizwa huulizwa ikiwa anaelewa kwamba ubatizo wake unamtambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kubatizwa, anakuwa mhudumu aliyewekwa rasmi ambaye anatambulishwa kwa jina la Yehova. Hilo ni pendeleo kubwa na daraka zito. Isitoshe, linamwezesha yule anayebatizwa awe na tazamio la kupata wokovu wa milele, maadamu anabaki mwaminifu kwa Yehova.—Mathayo 24:13.
12. Heshima ya kutambulishwa kwa jina la Yehova huleta daraka gani?
12 Bila shaka, ni heshima kubwa sana kutambulishwa kwa jina la Mungu mweza-yote, Yehova. Nabii Mika alisema hivi: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) Hata hivyo, heshima hiyo huleta daraka fulani. Tunahitaji kuishi kwa njia inayoleta heshima kwa Yehova, yule ambaye tunatambulishwa kwa jina lake. Paulo aliwakumbusha Wakristo huko Roma kwamba ikiwa mtu hatendi yale anayohubiri, jina la Mungu “linafanyiwa makufuru,” au kuchafuliwa.—Waroma 2:21-24.
13. Kwa nini watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu wana daraka la kutoa ushahidi kuhusu Mungu wao?
13 Mtu anapokuwa Shahidi wa Yehova, anakubali pia daraka la kutoa ushahidi kuhusu Mungu wake. Yehova aliwaalika watu wa taifa la Israeli waliojiweka wakfu wawe mashahidi wake, ili watoe ushahidi kuhusu Uungu wake wa milele. (Isaya 43:10-12, 21) Lakini taifa hilo lilishindwa kutimiza daraka hilo, na mwishowe likapoteza kabisa kibali cha Yehova. Leo, Wakristo wa kweli wanajivunia pendeleo la kutoa ushahidi kumhusu Yehova. Tunafanya hivyo kwa sababu tunampenda na tunatamani jina lake litakaswe. Je, kweli tunaweza kunyamaza huku tukijua ukweli kuhusu Baba yetu wa mbinguni na kusudi lake? Tunahisi kama mtume Paulo, wakati aliposema: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!”—1 Wakorintho 9:16.
14, 15. (a) Tengenezo la Yehova hutusaidiaje kufanya maendeleo ya kiroho? (b) Ni maandalizi gani yanayotusaidia kiroho?
14 Katika swali la pili, yule anayetaka kubatizwa anakumbushwa pia kuhusu daraka lake la kushirikiana na tengenezo la Yehova linaloongozwa kwa roho. Hatuwezi kujitenga na wengine tunapomtumikia Mungu, nasi tunahitaji kusaidiwa, kutegemezwa, na kutiwa moyo na “ushirika mzima wa akina ndugu.” (1 Petro 2:17; 1 Wakorintho 12:12, 13) Tengenezo la Mungu linatimiza daraka muhimu katika maendeleo yetu ya kiroho. Linaandaa habari nyingi za Biblia zilizochapishwa ambazo zinatusaidia kuongeza ujuzi sahihi, kutenda kwa hekima tunapokabili matatizo, na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Kama mama anayehakikisha kwamba mtoto wake amelishwa vizuri na kutunzwa, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huandaa chakula tele cha kiroho kwa wakati unaofaa ili tufanye maendeleo ya kiroho.—Mathayo 24:45-47; 1 Wathesalonike 2:7, 8.
15 Kwenye mikutano ya kila juma, watu wa Yehova huzoezwa na kutiwa moyo wawe Mashahidi wa Yehova waaminifu. (Waebrania 10:24, 25) Shule ya Huduma ya Kitheokrasi hutufundisha kuzungumza mbele ya watu, na Mkutano wa Utumishi hutuzoeza kutangaza ujumbe wetu kwa njia yenye matokeo. Tunapohudhuria mikutano yetu na kujifunza kibinafsi habari za Biblia zilizochapishwa, tunaona roho ya Yehova ikifanya kazi ili kuongoza tengenezo lake. Kupitia maandalizi hayo yanayotolewa kwa ukawaida, Mungu hutuonyesha hatari, hutuzoeza kuwa wahudumu stadi, na kutusaidia tuendelee kukesha kiroho.—Zaburi 19:7, 8, 11; 1 Wathesalonike 5:6, 11; 1 Timotheo 4:13.
-
-
‘Nendeni Mkafanye Wanafunzi, Mkiwabatiza’Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 1
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]
Yale Maswali Mawili ya Ubatizo
Kwa msingi wa dhabihu ya Yesu Kristo, je, umetubu dhambi zako na kujiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake?
Je, unaelewa kwamba wakfu na ubatizo wako unakutambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova anayeshirikiana na tengenezo la Mungu linaloongozwa na roho?
-