-
Urembo Ulio Bora ZaidiAmkeni!—2004 | Desemba 22
-
-
Umuhimu wa Urembo wa Ndani
Biblia hutuhakikishia kwamba Muumba wetu, Yehova Mungu, huthamini sana urembo wa ndani. Hebu ona mifano kadhaa.
Yehova alipomwambia nabii Samweli achague mfalme kwa ajili ya Israeli miongoni mwa wana wa Yese, nabii huyo alivutiwa na Eliabu ambaye alikuwa na sura nzuri. Samweli alisema: “Hakika huyu ndiye aliyechaguliwa na Bwana.” Lakini Yehova akamwambia Samweli: “Usifikiri ni Eliabu kwa sababu tu yeye ni mrefu na mwenye sura nzuri. Sijamchagua yeye. Watu huwahukumu wengine kulingana na sura yao, lakini mimi huwahukumu watu kulingana na yale yaliyo katika mioyo yao.”—1 Samweli 16:6, 7, Contemporary English Version.
Daudi, mwana wa mwisho, ndiye aliyechaguliwa kuwa mfalme. Ingawa inasemekana Daudi alikuwa na “macho yenye kupendeza” na “mwenye sura nzuri,” huenda hakuvutia sana kama ndugu zake wakubwa. Lakini “roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu ya Daudi kuanzia siku hiyo na kuendelea.” Ingawa Daudi hakuwa mkamilifu na alitenda dhambi nzito, alijulikana kuwa mtu mwenye moyo mzuri na alikuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu hadi alipokufa. (1 Samweli 16:12, 13) Bila shaka, Mungu alivutiwa naye hasa kwa sababu ya urembo wake wa ndani.
Kwa upande mwingine, mfikirie Absalomu, mwana wa Daudi. Japo alikuwa na sura nzuri sana, alikuwa mtu mwenye kuchukiza. Biblia inasema hivi kumhusu: “Basi, kwa kulinganisha na Absalomu, hakuna mwanamume aliyekuwa na sura nzuri sana katika Israeli yote kuweza kusifiwa sana hivyo. Hakuwa na kasoro yoyote, kuanzia wayo wa mguu wake mpaka kipaji cha kichwa chake.” (2 Samweli 14:25) Hata hivyo, tamaa ya makuu ya Absalomu ilimchochea kumwasi baba yake na kunyakua ufalme. Hata alilala na masuria wa baba yake. Hivyo, Mungu akamkasirikia, naye akafa kwa maumivu mengi.—2 Samweli 15:10-14; 16:13-22; 17:14; 18:9, 15.
Je, wewe huvutiwa na Absalomu? Bila shaka huvutiwi naye. Kwa ujumla, alikuwa mtu mwenye kuchukiza. Sura yake nzuri haikufunika kiburi na ukosefu wake wa uaminifu, wala haikumzuia asiangamie. Kwa upande mwingine, Biblia inataja mifano mingi ya watu wenye hekima na wenye kuvutia bila kufafanua lolote kuhusu sura yao. Ni wazi kwamba urembo wao wa ndani ndio uliokuwa muhimu zaidi.
-
-
Urembo Ulio Bora ZaidiAmkeni!—2004 | Desemba 22
-
-
Hata hivyo, tunaweza kusitawisha sifa nzuri ambazo hutuwezesha kuwa warembo kwa ndani. Biblia inasema hivi: “Uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejiletea sifa.” Kwa upande mwingine, Biblia huonya hivi: “Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, ndivyo alivyo mwanamke mwenye umbo la kupendeza lakini anayegeuka na kuacha kuwa na akili.”—Methali 11:22; 31:30.
Neno la Mungu hutusaidia kuthamini “yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.” (1 Petro 3:4) Bila shaka, urembo huo wa ndani ni bora zaidi ya urembo wa nje. Naam, sote tunaweza kuwa warembo kwa ndani.
-