Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Yehova Ni Nguvu Zangu”
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Oktoba 15
    • Mwenzi Mpya na Mgawo Mpya

      Katika mwaka wa 1945, nilitembelea London. Katika safari hiyo, nilitembelea Jumba la Makumbusho la Uingereza pamoja na mapainia wengine na Wanabetheli. Mmoja wao alikuwa Allan Coville, ambaye muda mfupi baadaye alihudhuria darasa la 11 la Gileadi. Alitumwa nchini Ufaransa na Ubelgiji.b Baadaye, nilipokuwa bado mmishonari nchini Thailand, aliniomba tufunge ndoa, nami nikakubali.

      Tulifunga ndoa huko Brussels, Ubelgiji mnamo Julai 9, 1955. Nilitamani sana kwenda kustarehe huko Paris baada ya arusi, kwa hiyo Allan alipanga tuhudhurie kusanyiko huko juma lililofuata. Hata hivyo, tulipofika tu, Allan aliombwa asaidie katika kutafsiri hotuba kwenye kusanyiko hilo. Kila siku, aliondoka asubuhi na tulirudi mahali pa kulala usiku sana. Hivyo, baada ya arusi tulienda Paris kustarehe, lakini mara nyingi nilimwona Allan kwa mbali tu, akiwa jukwaani! Hata hivyo, nilifurahi kumwona mume wangu akiwatumikia ndugu na dada zake, na sikuwa na shaka yoyote kwamba tukimtanguliza Yehova katika ndoa yetu, tutapata furaha ya kweli.

      Ndoa pia ilinifanya nihamie kwenye eneo jipya la kuhubiri huko Ubelgiji. Sikujua mengi kuhusu Ubelgiji isipokuwa tu kwamba vita vingi vilipiganwa huko, lakini muda si muda niligundua kwamba Wabelgiji wengi wanapenda amani. Kwa sababu ya mgawo huo, nililazimika pia kujifunza Kifaransa, lugha inayozungumzwa katika sehemu ya kusini ya nchi hiyo.

      Mwaka wa 1955 kulikuwa na wahubiri 4,500 hivi nchini Ubelgiji. Kwa miaka karibu 50, mimi na Allan tulitumika Betheli na katika kazi ya kusafiri. Katika miaka miwili na nusu ya kwanza, tulisafiri kwa baiskeli, tulipanda na kushuka milima, kukiwa na jua na kukiwa na mvua. Katika miaka hiyo yote, tulilala katika nyumba zaidi ya 2,000 za Mashahidi wenzetu! Mara nyingi nilikutana na ndugu na dada ambao walikuwa dhaifu kimwili lakini walimtumikia Yehova kwa nguvu zao zote. Mfano wao ulinitia moyo kutoacha utumishi wangu. Mwishoni mwa juma la ziara kutanikoni, sikuzote tulihisi tumejengwa. (Rom. 1:11, 12) Allan alikuwa rafiki wa kweli. Maneno ya Mhubiri 4:9, 10 ni ya kweli kabisa: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, . . . kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake”!

      Baraka za Kutumika kwa ‘Nguvu za Yehova’

      Kwa miaka mingi, mimi na Allan tumefurahia kuwasaidia watu wengi wamtumikie Yehova. Kwa mfano, katika mwaka wa 1983 tulitembelea kutaniko la Kifaransa huko Antwerp, ambako tulikaa na familia ambayo ilikuwa inaishi na Benjamin Bandiwila, ndugu kijana kutoka Zaire (sasa ni Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo). Benjamin alikuwa amehamia Ubelgiji kupata elimu ya juu. Alituambia hivi: “Ninawaonea wivu kwa sababu mmejitolea kabisa kumtumikia Yehova.” Allan akamjibu: “Unasema unatuonea wivu; lakini unafuatia elimu ya kilimwengu. Je, huoni kwamba hufanyi yale unayosema?” Maneno hayo ya waziwazi yalimfanya Benjamin afikirie maisha yake. Baadaye aliporudi Zaire, alianza kufanya upainia, na sasa yeye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi.

      Mwaka wa 1999, nilifanyiwa upasuaji wa kuondoa kidonda katika njia ya koo yangu. Tangu wakati huo, nimekuwa na uzito wa kilo 30 tu. Mimi kwa kweli ni ‘chombo dhaifu sana cha udongo.’ Hata hivyo, ninashukuru kwa sababu Yehova amenipa “nguvu zinazopita zile za kawaida.” Baada ya upasuaji, Yehova aliniwezesha kuambatana tena na Allan katika kazi ya kusafiri. (2 Kor. 4:7) Kisha, mnamo Machi 2004, Allan alikufa akiwa amelala. Ninamkosa sana, lakini ninafarijika kujua kwamba yuko katika kumbukumbu ya Yehova.

      Sasa nina umri wa miaka 83, na nimekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 63. Ningali ninahubiri kwa bidii, ninaongoza funzo la Biblia la nyumbani na kutumia nafasi ninazopata kila siku kutangaza kusudi zuri sana la Yehova. Nyakati nyingine, ninajiuliza hivi, ‘Ningeishi maisha ya aina gani kama singeanza kufanya upainia mwaka wa 1945?’ Wakati huo, ningetoa kisingizio kwamba siwezi kufanya upainia kwa sababu ya matatizo ya afya. Hata hivyo, ninafurahi sana kwamba nilianza upainia nikiwa kijana! Nimekuwa na pendeleo la kujionea mwenyewe kwamba tukimtanguliza Yehova anakuwa nguvu zetu.

  • “Yehova Ni Nguvu Zangu”
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Oktoba 15
    • b Simulizi la maisha la Ndugu Coville lilichapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Machi 15, 1961 (15/3/1961).

  • “Yehova Ni Nguvu Zangu”
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Oktoba 15
    • [Picha katika ukurasa wa 18]

      Nikiwa na mume wangu katika kazi ya kusafiri, mwaka wa 1956

      [Picha katika ukurasa wa 20]

      Nikiwa na Allan mwaka wa 2000

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki