-
Je, Inawezekana Kuamini Kuna Muumba?Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 1
-
-
Dini Zimeshindwa
Kwa kushangaza, dini ndiyo sababu kuu inayowafanya watu wasiamini kwamba kuna Mungu. Mwanahistoria Alister McGrath alieleza: “Kinachowafanya watu wasiamini kuwapo kwa Mungu ni chuki ambayo watu wamekuwa nayo kwa sababu ya maisha ya anasa na ya upotovu yaliyo katika dini kubwa.” Mara nyingi dini huonekana kama kisababishi cha vita na jeuri. Michel Onfray mwanafalsafa asiyeamini kwamba kuna Mungu aliandika jinsi inavyowezekana kwa kitabu kilekile cha kidini kutokeza aina mbili za watu, mtu wa kwanza “anajitahidi sana kuwa mtakatifu,” na yule mwingine “anatenda kwa ukatili wa kinyama,” yaani, ugaidi.
Watu wengi wana uchungu wanapokumbuka mambo yaliyotukia walipokuwa katika dini. Alipokuwa jeshini, Bertil, kijana kutoka Sweden alimsikia kasisi wa jeshi akitetea jeuri kwa kutumia onyo la Yesu kwamba wale wanaochukua upanga wataangamia kwa upanga. Kasisi huyo alisababu kwamba lazima kuwepo na mtu atakayeuchukua upanga, hivyo, lazima askari-jeshi awe mtumishi wa Mungu!—Mathayo 26:52.a
Bernadette, ambaye baba yake aliuawa nchini Ufaransa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, anakumbuka jinsi alivyokasirika kasisi aliposema hivi kwenye mazishi ya binamu yake mwenye umri wa miaka mitatu: “Mungu amemchukua mtoto huyu ili awe malaika.” Baadaye, Bernadette, alipata mtoto mlemavu na hakupata faraja yoyote kutoka kanisani.
Ciarán, ambaye alilelewa wakati wa kipindi chenye jeuri huko Ireland Kaskazini, alichukizwa sana na fundisho la moto wa mateso. Alikuwa akisema kwamba alichukizwa na Mungu yeyote ambaye alisababisha uovu na akamwambia Mungu ikiwa yupo, basi amuue. Si Ciarán tu aliyechukizwa na mafundisho hayo ya kidini yenye ukatili. Kwa kweli, huenda mafundisho ya dini yalichangia kuanzishwa kwa fundisho la mageuzi. Alister McGrath, alisema kwamba Darwin alianza kuwa na shaka kuhusu kuwapo kwa Mungu kwa sababu ya “kuchukizwa sana” na fundisho la moto wa mateso na si kwa sababu ya kuamini mageuzi. McGrath alisema pia kwamba Darwin “alihuzunishwa sana na kifo cha binti yake.”
Wengine huhusianisha dini na watu wasiotumia akili na wenye msimamo mkali. Irina, aliyekuwa amechoshwa na mahubiri yasiyo na maana na sala za kurudiwa-rudiwa anasimulia hivi: “Niliona kwamba watu wa kidini hawatumii akili.” Louis, ambaye alichukizwa sana na matendo ya kikatili yaliyochochewa na watu walioshikilia sana mambo ya kidini alikuwa na msimamo huu mkali: “Kwa miaka mingi niliona dini kuwa yenye kuchosha lakini sasa naona jinsi inavyowadhuru watu. Nilipinga vikali dini zote.”
-
-
Je, Inawezekana Kuamini Kuna Muumba?Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 1
-
-
Sababu Nyingine Zinazowafanya Watu Wasiwe na Imani
Watu wengi wanafundishwa kwamba mageuzi ni jambo hakika. Kwa mfano, Anila, alienda shuleni huko Albania ambako watu hawaamini kwamba kuna Mungu. “Shuleni tulifundishwa kwamba kuamini kwamba kuna Mungu ni upumbavu na ushamba,” anaeleza. “Nilijifunza mambo yenye kupendeza kuhusu mimea na vitu vingine vilivyo hai, lakini nilisema vyote vilitokea kwa mageuzi, kwa kuwa kufanya hivyo kulifanya tuonekane tunapatana na kufikiri kwa kisayansi.” Anakubali kwamba leo “uthibitisho uliotolewa ulipaswa kukubaliwa bila kupingwa.”
Uchungu unaweza pia kuwazuia watu fulani wasiamini kwamba kuna Mungu. Mara nyingi, Mashahidi wa Yehova hukutana na mtazamo kama huo wanapoenda nyumba kwa nyumba wakiwatolea watu tumaini la Biblia. Bertil, aliyetajwa hapo awali, alitembelewa na Shahidi fulani kijana. Bertil anakumbuka akijiambia hivi: ‘Mshupavu huyu amepotea sana!’ Anasema: “Nilimkaribisha ndani na kuanza kumshambulia kwa hoja kuhusu Mungu, Biblia, na dini.”
Gus anayeishi nchini Scotland, alitatizwa na ukosefu wa haki. Mwanzoni alikuwa mbishi na alikuwa akipinga alipozungumza na Mashahidi wa Yehova. Aliuliza maswali yanayofanana na yale ya nabii Mwebrania Habakuki, aliyemwambia Mungu hivi: “Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu?”—Habakuki 1:3.
Pia, wanadamu wametaabishwa kwa muda mrefu na wazo la kwamba Mungu hajali uovu uliopo. (Zaburi 73:2, 3) Simone de Beauvoir, mwandishi Mfaransa, alisema hivi wakati mmoja: “Ilikuwa rahisi kwangu kufikiri juu ya ulimwengu usio na muumba kuliko muumba anayekubali mambo yote yenye kupingana ya ulimwengu.”
-
-
Je, Inawezekana Kuamini Kuna Muumba?Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 1
-
-
“NILIPOWAZIA kwamba huenda kuna Muumba, wazo la kwamba kuna mtu aliye na nguvu za kuzuia kuteseka kwa wanadamu lakini hazitumii, lilinikasirisha sana!” Hivyo ndivyo alivyosema mtu fulani ambaye hapo awali hakuamini kwamba kuna Mungu na aliyewapoteza watu wa familia yake katika yale maangamizi makubwa yaliyotekelezwa na Wanazi. Si yeye tu aliye na hisia kama hizo.
Watu wengi wanapotendewa kikatili, inakuwa vigumu kwao kuamini kuna Mungu, au wanajifariji kwa kusema kwamba hakuna Mungu.
-