-
Je, Unaweza Kutegemea Mashauri ya Biblia?Amkeni!—2007 | Novemba
-
-
Je, Unaweza Kutegemea Mashauri ya Biblia?
‘Je, niamini kile ambacho mtu huyu ananieleza?’ Huenda ukajiuliza swali hilo mfanyabiashara anapojaribu kukuuzia gari lililotumika au mwanasiasa anapotoa ahadi kwenye kampeni ya uchaguzi. Hungependa kupoteza pesa au wakati wako kwa vitu au habari zenye thamani ndogo.
HUENDA ukajiuliza pia: ‘Je, Biblia ina kitu chochote chenye thamani ambacho ninaweza kujifunza? Nikisoma na kujifunza kitabu hicho, je, ninaweza kuwa na hakika kwamba wakati na jitihada zangu hazitapotea bure?’ Jibu la maswali hayo linapatikana katika mstari wa Biblia unaosema: “Hekima husimama au kuanguka kwa matokeo yake.” (Mathayo 11:19, Phillips) Naam, matokeo ambayo watu hupata kwa kutumia aina fulani ya mashauri, au “hekima,” huthibitisha ikiwa mashauri hayo yanafaa. Yafuatayo ni maelezo ya watu ambao walitumia wakati kujifunza Biblia. Maelezo yao yatakusaidia uamue ikiwa unapaswa kusoma na kujifunza kitabu hicho cha pekee.
Maswali Yanayohusu Kifo na Maisha Baada ya Kifo
Wakati fulani uliopita, mama ya Karen alikufa. Tangu alipokuwa mtoto, Karen, anayeishi Marekani aliamini kwamba watu wote wema wanapokufa wanaenda mbinguni. Imani hiyo haikumfariji sana. Alijiuliza hivi: ‘Kwa kuwa mama yangu sasa yuko mbinguni, anafananaje? Nitampataje nikifika huko? Je, nitafika huko? Nitakapokufa, je, kuna uwezekano kwamba nitakwenda mahali pengine?’
Karen alianza kujifunza Biblia kwa uangalifu pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alijifunza kwamba wafu hawako mbinguni lakini wamelala usingizi mzito. “Hawajui lolote kamwe,” linasema andiko la Mhubiri 9:5. Lakini, je, inawezekana amwone mama yake tena?
Maneno yafuatayo kutoka katika Biblia yalimpa faraja na tumaini: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Kristo] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Karen alijifunza kwamba Mungu wa Biblia kupitia Mwana wake, atawafufua wafu waishi hapahapa duniani. Karen alisema hivi: “Mafundisho ya Biblia yanayohusu kifo na ufufuo yanapatana na akili.”
Ni Ibada Gani Iliyo Sahihi?
Angela, msichana Mrumania alipokuwa na umri wa miaka 14, kasisi wa dini ya Pentekoste alimwombea ili apokee roho takatifu, naye akaanza kusema kwa lugha. Lakini wazazi wake walihisi kwamba mafundisho ya dini ya Pentekoste yanapingana na Biblia. Familia yao iliacha kwenda kanisani na ikaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.
Ingawa alivunjika moyo mwanzoni, baada ya muda mfupi Angela alianza kuona tofauti kati ya dini yake ya zamani na mafundisho ya Biblia. Kwa mfano, alisoma andiko la Yohana 17:3, ambalo linasema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” Angela alijifunza kwamba wale wanaopata upendeleo wa Mungu lazima kwanza wawe na ujuzi kumhusu. Angela alijiuliza hivi: “Ningepokeaje roho takatifu ya Mungu kwa njia ya pekee wakati sikuwa naelewa chochote kumhusu?” Anaendelea kusema: “Ninamshukuru Yehova kwa kunisaidia kupata njia inayofaa ya kumwabudu kupitia Neno lake lililoongozwa na roho.”
Shauri Linalobadili Maisha
“Nilikuwa mtu mwenye hasira sana,” anasema Gabriel, mwanamume kutoka India. “Nilipokasirishwa, ningepiga kelele, ningetupa-tupa vitu, na hata kuwaumiza watu. Funzo la Biblia lilinisaidia niweze kudhibiti hasira yangu. Sasa, hata hali iweje, ninaweza kujidhibiti.”
Gabriel alikuwa amesoma maandiko kama andiko la Methali 16:32, ambalo linasema hivi: “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu, naye anayezuia roho yake ni bora kuliko mtu anayeteka jiji.” Mwanamume mwingine aitwaye Dhiraj, ambaye pia ameweza kuidhibiti hasira yake, anaeleza hivi, “Andiko hilohilo lilinisaidia kuona kwamba kuongozwa na hasira ni ishara ya udhaifu lakini kuidhibiti hasira ni ishara ya kujiweza.”
Philip alikuwa mshiriki wa genge la uhalifu nchini Afrika Kusini. Alizoea kupigana, kuiba, na kutumia lugha chafu. Alifungwa jela kwa sababu ya makosa yake. Ijapokuwa alikuwa akiishi maisha mabaya, Philip alitamani kumjua Mungu. Baada ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, alisitawisha tamaa ya kumtumikia Mungu na akaamua kusafisha maisha yake. Aliacha mazoea yake mabaya na akakatisha uhusiano pamoja na rafiki zake wahalifu. Ni kweli gani za Biblia zilizomchochea kufanya mabadiliko hayo?
Mashahidi wa Yehova walimwonyesha maneno ya Yesu yanayopatikana katika andiko la Yohana 6:44, ambalo linasema hivi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” Philip anasema hivi: “Yehova aliona jambo fulani zuri ndani yangu naye akanivuta kwa watu wake, undugu mzuri kama nini!” Pia, Philip alithamini masimulizi ya Biblia kuhusu huruma za Yehova kuwaelekea watenda-mabaya wanaotubu. Philip anasema hivi: “Masimulizi hayo, yalinisaidia kuona jinsi Yehova alivyo na usawaziko anaposhughulika na wanadamu wasio wakamilifu wanaotubu.”—2 Samweli 12:1-14; Zaburi 51.
Mwanamume Mwaustralia aitwaye Wade alikuwa na zoea la kutumia kileo vibaya na dawa za kulevya, alicheza kamari, na alijihusisha sana katika upotovu wa kingono. Hata hivyo, hakupata furaha. Siku moja alikuwa na mazungumzo na Mashahidi wa Yehova na akakubali kujifunza Biblia. Wade alijifunza nini?
“Nilipendezwa sana na jinsi ambavyo Yesu aliwatendea wengine,” anasema Wade. “Yesu aliwaonyesha fadhili, aliwaonyesha huruma, na kuwapenda watu wote kutia ndani watoto. Kadiri nilivyojifunza ndivyo nilivyotaka kuwa kama yeye. Biblia ilinifundisha jinsi ya kuwa mwanamume halisi na jinsi ya kubadili utu wangu.” Vipi kuhusu matendo yote mabaya aliyofanya? Wade anaendelea kusema hivi: “Biblia ilinifundisha kwamba ikiwa ningetubu dhambi na kubadili mwenendo wangu, Mungu angenisamehe. Kwa kweli, nitaishi milele katika paradiso duniani. Hatimaye nilikuwa na matumaini!” (Mathayo 5:5) Wade alisafisha maisha yake na sasa anamwabudu Yehova akiwa na dhamiri safi.
Maelezo ambayo umetoka kuyasoma yametoka kwa watu ambao walitaka kuboresha hali zao za maisha. Walichunguza Biblia ili waone ikiwa mafundisho yake yangeweza kuwasaidia kushughulika na matatizo yao na kujibu maswali yao. Matokeo mazuri ambayo wamepata yanathibitisha kwamba wanaweza kutegemea mwongozo unaofaa unaopatikana katika Biblia. Wewe pia unaweza kutegemea mwongozo huo.
Maneno yaliyoongozwa na roho yanasema: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amepata hekima, na mtu anayepata utambuzi, kwa maana kuwa nayo kama mapato ni bora kuliko kuwa na mapato ya fedha na kuwa nayo kama mazao ni bora kuliko dhahabu yenyewe. Ina thamani kuliko marijani, na mapendezi yako mengine yote hayawezi kulinganishwa nayo. Urefu wa siku uko katika mkono wake wa kuume; na katika mkono wake wa kushoto kuna utajiri na utukufu. Njia zake ni njia za uzuri, na barabara zake zote ni amani. Ni mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika sana wataitwa wenye furaha.”—Methali 3:13-18.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]
JINSI BIBLIA ILIVYOMSAIDIA MFUNGWA
Mwanamume anayeitwa Bill alikuwa na ndoa yenye furaha sana. Lakini kabla ya kumaliza mwaka mmoja katika ndoa hiyo, alifungwa jela kwa sababu ya makosa aliyofanya miaka mingi mapema.
Baada ya kipindi fulani cha kuhuzunika kwa kupoteza uhuru wake, Bill aliamua kutumia miaka iliyofuata vizuri huko gerezani. Anasema hivi: “Niliketi kitandani nikisoma na kujifunza Biblia.” Pia, alianza kutenda kupatana na mambo aliyokuwa akijifunza. “Nilikuwa mwenye fadhili na urafiki kuwaelekea wafungwa wenzangu, ambao waliona kwamba sikutaka kushiriki katika mambo mabaya waliyofanya. Mara kwa mara wangesema hivi kunihusu: ‘Bill anataka kutumikia kifungo chake kwa njia tofauti, amjue Mungu na aielewe Biblia. Hatamsumbua mtu yeyote.’
“Kwa sababu ya sifa zangu, wafungwa wengine hawakunihusisha katika migogoro yao na hali nyingine zisizopendeza. Walinzi waligundua kwamba siwezi kuwasumbua. Wakaanza kupendekeza nifanye kazi ambazo zilinifanya nisihitaji kushirikiana na wafungwa wengine kwa muda mrefu. Kutenda kulingana na mambo niliyojifunza kulinilinda sana.”
Bill alihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova iliyofanywa gerezani na aliwaambia wafungwa wengine kuhusu mambo aliyojifunza. Alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova alipokuwa gerezani. Akikumbuka wakati huo, anasema: “Nilipoteza karibu miaka 50 ya maisha yangu, na sasa nilitaka kufanya marekebisho. Nina hakika kwamba njia bora zaidi ambayo mfungwa anaweza kufanya hivyo ni kwa kufuata mafundisho ya Biblia. Na njia ya kujifunza Biblia kwa usahihi ni kujifunza na Mashahidi wa Yehova. Ni dini yao tu inayofundisha ukweli wa Biblia. Hakuna anayeweza kupinga hilo.”
Sasa Bill ametoka gerezani na anashirikiana na kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova nchini Marekani. Yeye pamoja na mke wake wanaendelea kujifunza Neno la Mungu na kuishi kupatana na mafundisho yake. Wanathamini sana maneno yanayopatikana katika Isaya 48:17, 18: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake. Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.”
[Picha katika ukurasa wa 23]
Karen, Marekani
[Picha katika ukurasa wa 23]
Angela, Romania
[Picha katika ukurasa wa 24]
Dhiraj, India
[Picha katika ukurasa wa 24]
Gabriel, India
[Picha katika ukurasa wa 24, 25]
Philip na familia yake, Afrika Kusini
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wade, Australia
-
-
Wonyesho wa Kudumu wa Upendo wa MunguAmkeni!—2007 | Novemba
-
-
Wonyesho wa Kudumu wa Upendo wa Mungu
MAAJABU saba ya ulimwengu wa kale yaliitwa hivyo kwa sababu yaliwashangaza wanadamu. Hata hivyo, kati ya maajabu hayo ni piramidi tu zinazoonekana leo. Kwa upande mwingine, ingawa Biblia iliandikwa na watu wanyenyekevu kwa kutumia vifaa vinavyoweza kuharibika, bado ipo na imetufikia ikiwa sahihi. Tunaweza kuwa na uhakika kabisa katika kitabu hiki cha pekee.—Isaya 40:8; 2 Timotheo 3:16, 17.
Kwa kufanya mawazo yake yaandikwe, Yehova Mungu alihakikisha kwamba maneno yake yangetufikia bila kubadilishwa na kumbukumbu zisizo kamilifu za wanadamu. Isitoshe, lugha rahisi iliyotumiwa na waandikaji waliotumiwa na Mungu iliwawezesha wengi walio na elimu ya chini waielewe Biblia wanapoisoma. (Matendo 4:13) Je, hilo si jambo ambalo ungetarajia kutoka kwa Muumba na waandikaji wake walioongozwa na roho? Pia, Biblia imegawanywa sana kwa sababu Mungu anawapenda sana wanadamu popote walipo hata wawe wanazungumza lugha gani. (1 Yohana 4:19) Kwa kweli, Biblia imeenezwa sana si kwa sababu haina thamani bali kwa sababu ina thamani kubwa!
Biblia inafunua mengi zaidi kuhusu upendo wa Mungu. Kama vile tumeona katika habari zilizotangulia, Neno la Mungu linaeleza tulikotoka, kwa nini maisha ni mafupi na yamejaa taabu, na jinsi ambavyo Mungu atarekebisha hali hiyo kwa kutumia Ufalme wake. Pia tumechunguza mashauri mazuri sana ya Biblia kuhusu jinsi tunavyoweza kuwa na maisha yenye furaha na yenye kuridhisha hata sasa. (Zaburi 19:7-11; Isaya 48:17, 18) Zaidi ya yote, tumejifunza jinsi Muumba wetu atakavyosafisha jina lake kutokana na shutuma ambazo zimetokezwa na uwongo wa Shetani.—Mathayo 6:9.
Ni kitabu kipi kingine chenye thamani, chenye mawaidha yanayohusu wakati huu, chenye manufaa, na kilichojaa matumaini kwa ajili ya wanadamu wenye matatizo? Ndiyo, tofauti na maajabu saba ya ulimwengu wa kale yaliyojengwa ili kutukuza miungu ya uwongo au watu mashuhuri, Biblia ni wonyesho wa kudumu wa upendo wa Yehova usio na ubinafsi kwa ajili ya uumbaji wake wa kibinadamu.
Ikiwa hujafanya hivyo, mbona usichunguze Maandiko wewe mwenyewe? Kwa sasa, Mashahidi wa Yehova wanajifunza Biblia bila malipo na watu zaidi ya milioni sita ulimwenguni. Wanaliona kuwa pendeleo kuwasaidia watu wanyoofu wajionee kwamba Biblia ni Neno la Mungu linalotegemeka.—1 Wathesalonike 2:13.
-
-
Kwa nini niishi kupatana na viwango vya Biblia?Amkeni!—2007 | Novemba
-
-
Vijana Huuliza . . .
Kwa nini niishi kupatana na viwango vya Biblia?
UMEKETI shuleni ukila chakula cha mchana pamoja na wasichana wawili. Mmoja wao anamwangalia kijana fulani.
Msichana wa kwanza anakuambia: “Unajua kijana yule anakupenda. Nilitambua mara moja nilipoona jinsi anavyokutazama. Macho yake hayabanduki!”
Msichana wa pili anasogeza kichwa chake karibu na sikio lako na kusema kwa sauti ya chini: “Acha nikuambie! Hana mpenzi!”
Msichana wa pili anasema: “Ubaya ni kwamba mimi tayari nina mpenzi, la sivyo ningeanzisha uhusiano naye mara moja!”
Kisha msichana wa kwanza anakuuliza swali ambalo huwa linakukera.
“Kwa nini huna mpenzi?”
Ulijua tu atakuuliza swali hilo. Kwa kweli, unatamani kuwa na mpenzi. Lakini umeambiwa kwamba ni bora ungoje kwanza hadi uwe tayari kwa ndoa ndipo uanze kumtafuta mchumba. Kama tu haingekuwa . . .
“Ni kwa sababu ya dini yako, siyo?” msichana wa pili anasema.
Unajiuliza kimoyomoyo, ‘Amejuaje, kwani anaweza kusoma akili yangu?’
“Wewe ni Biblia, Biblia, Biblia, huna hata uhuru,” msichana wa kwanza anakudhihaki. “Kwani huwezi kujifurahisha nyakati nyingine?”
Umewahi kupatwa na hali kama hiyo? Je, watu wamekudhihaki kwa sababu ya kujaribu kuishi kupatana na viwango vya Biblia? Ulijibuje?
◼ Ulitetea viwango vyako vya maadili kwa uthabiti.
◼ Uliaibika, lakini ukaeleza imani yako kwa kadiri ulivyoweza.
◼ Uliamua kwamba marafiki wako hawakuwa wamekosea na kwamba ulikuwa ukikosa mambo mengi yanayoleta raha!
Je, umewahi kujiuliza swali hili, ‘Kweli kuna umuhimu wa kuishi kupatana na kanuni za Biblia?’ Msichana mmoja anayeitwa Deborah alikuwa na maoni kama hayo.a Anasema hivi: “Wasichana wengine wa rika langu wangefanya lolote watakalo. Ni kama hawakuwajibika kwa yeyote. Nilihisi viwango vya Biblia vimenibana. Uhuru ambao marafiki wangu walikuwa nao ulinivutia.”
Je, Ni Vibaya Kuwa na Mashaka?
Mwandikaji wa Biblia Asafu alipitia kipindi fulani maishani mwake ambapo alijiuliza ikiwa ni muhimu kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Mwandikaji huyo aliandika hivi: “Niliwaonea wivu wenye kujisifu, nilipokuwa nikiiona amani ya watu waovu.” Hata alisema: “Hakika nimeusafisha moyo wangu bure na kuiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia.”—Zaburi 73:3, 13.
Yehova Mungu anaelewa kwamba nyakati fulani watu wanaweza kuwa na mashaka kuhusu umuhimu wa kuishi kupatana na viwango vyake. Hiyo ndiyo sababu aliruhusu maneno ya Asafu yaandikwe katika Biblia. Mwishowe, Asafu aliamua kwamba kuishi kupatana na sheria ya Mungu ndiyo njia bora maishani. (Zaburi 73:28) Alifikia mkataa huo jinsi gani? Asafu alikuwa na hekima. Alifanya uamuzi huo, si kwa sababu ya kupatwa na misiba fulani, bali kwa kujifunza kutokana na makosa ya wengine. (Zaburi 73:16-19) Je, unaweza kufanya hivyo?
Jithibitishie Ukweli
Kinyume na Asafu, Mfalme Daudi alijifunza kutokana na hali ngumu alizopitia kwamba wale wanaopuuza viwango vya Mungu wanapatwa na madhara. Alifanya uzinzi pamoja na mke wa mtumishi wake, kisha akajaribu kuficha dhambi hiyo. Matokeo yakawa kwamba aliwaumiza watu wengine, kutia ndani Mungu, na akafadhaika sana. (2 Samweli 11:1–12:23) Baada ya Daudi kutubu, Yehova kupitia roho yake alimwongoza aeleze hisia zake kwa wimbo na akafanya maneno hayo yahifadhiwe katika Biblia kwa faida yetu. (Zaburi 51:1-19; Waroma 15:4) Kwa hiyo, ni jambo la hekima na linalopatana na Maandiko kujifunza kutokana na makosa ya watu wengine.
Ili kukusaidia uige mfano wa Asafu na uepuke makosa ya Daudi, fikiria maelezo ya vijana kutoka nchi kadhaa ambao kwa muda fulani walikataa viwango vya Biblia. Vijana hao walijihusisha na ngono kabla ya ndoa. Kama ilivyokuwa na Daudi, wao wametubu dhambi zao na sasa wana msimamo mzuri pamoja na Mungu. (Isaya 1:18; 55:7) Fikiria kile walichosema.
Amkeni!: Ni mambo gani yaliyochochea maoni na matendo yako?
Deborah: “Nilipokuwa shuleni niliona kila mtu akiwa na mpenzi, na walionekana kuwa na furaha. Nilipokuwa nao na kuwaona wakikumbatiana na kubusiana, niliona wivu na kujihisi mpweke. Nilijiruhusu kutumia wakati mwingi nikimfikiria kijana fulani niliyevutiwa naye. Hilo lilichochea tamaa ya kuwa naye na nilikuwa tayari kufanya chochote ili nitimize tamaa hiyo.”
Mike: “Nilisoma vitabu na kuona vipindi ambavyo vilitukuza ngono. Kuzungumza kuhusu ngono na marafiki wangu kuliamsha udadisi wangu. Kisha, nilipokuwa peke yangu na msichana nilifikiri kwamba ningeweza kumshika-shika bila kufanya ngono. Nilifikiri kwamba ningeweza kujizuia wakati wowote.”
Andrew: “Nilitazama ponografia (picha au habari za ngono) kwenye Intaneti. Nilianza kunywa kileo kwa wingi sana. Na nilihudhuria karamu pamoja na vijana ambao hawakuheshimu viwango vya maadili vya Biblia.”
Tracy: “Nilipokuwa na umri wa miaka 16, kuwa na mpenzi kulikuwa jambo muhimu zaidi maishani mwangu. Akilini nilijua kwamba kufanya ngono kabla ya ndoa ni dhambi, lakini sikuchukia jambo hilo. Sikukusudia kuwa na uhusiano wa kingono kabla ya ndoa, lakini hisia zangu zilizidi uwezo wangu wa kufikiri. Kwa muda, dhamiri yangu haikunisumbua.”
Amkeni!: Je, njia hiyo ya maisha ilikuletea furaha?
Deborah: “Mwanzoni, nilijihisi huru na nilifurahia kwamba sasa nilipendwa na watu wengine wa rika langu. Lakini hisia hizo hazikudumu. Nilianza kujiona kuwa mchafu, mwenye hatia, na asiye na maana. Nilijuta sana kwamba nilikuwa nimepoteza ubikira, kitu ambacho nisingekipata tena. Tangu wakati huo nimejiuliza mara nyingi, ‘Kwani nilifikiria mimi ni nani nisipatwe na madhara yoyote? Kwa nini—kwa nini nilipuuza viwango vyenye upendo vya Yehova?’”
Mike: “Nilianza kuhisi ni kama sehemu yangu fulani imekufa. Nilijaribu kupuuza jinsi matendo yangu yalivyowaathiri wengine, lakini singeweza. Ilihuzunisha kutambua kwamba katika kufuatia raha, nilikuwa nimewaumiza wengine. Nisingeweza kulala. Mwishowe, raha ya kufanya ngono haramu ilipotea, na mawazo yangu yalitawaliwa na hisia za maumivu na aibu.”
Andrew: “Ilianza kuwa rahisi zaidi kutenda kupatana na tamaa mbaya. Lakini wakati huohuo, nilikuwa nimelemewa na hisia za hatia na nilijichukia sana.”
Tracy: “Haikunichukua muda mrefu kutambua uhalisi wa mambo. Ukosefu wa adili katika ngono ulikuwa umeniharibia ujana wangu. Nilifikiri kwamba mimi na mpenzi wangu tungefurahia maisha. Lakini haikuwa hivyo. Mwishowe tuliumizana, tukasababishiana mateso na kuvunjika moyo. Nilikaa kitandani usiku mmoja baada ya mwingine nikilia na nikitamani kwamba ningefanya mambo kupatana na njia ya Yehova.”
Amkeni!: Ungewapa mashauri gani vijana wengine wanaojiuliza ikiwa viwango vya maadili vya Biblia vinabana?
Deborah: “Hutakuwa na maisha bora zaidi ukipuuza viwango vya Biblia. Hebu fikiria jinsi Yehova atakavyohisi ukifuata mashauri yake. Kisha ufikirie sana kuhusu matokeo ya kupuuza mashauri yake. Kumbuka, matendo yako hayakuathiri wewe tu. Yatawaathiri watu wengine. Ukipuuza mashauri ya Mungu, utajidhuru mwenyewe.”
Mike: “Ni kweli kwamba kijuujuu maisha ya vijana wenzako yanaonekana kuwa yanapendeza. Lakini chunguza mambo kwa undani zaidi. Yehova amekupa vitu vyenye thamani sana kwa kukuwezesha ujiheshimu na usiwe na lawama. Kutupa zawadi hizo kwa sababu huwezi kujizuia ni kujishusha sana. Zungumza na wazazi wako na watu wengine waliokomaa kuhusu matatizo yako. Ukikosea, funua jambo hilo mara moja na urekebishe makosa yako. Ukifanya mambo jinsi Yehova anavyotaka, utapata amani halisi.”
Andrew: “Usipokuwa na uzoefu, unaweza kufikiri kwamba vijana wenzako wana maisha yanayosisimua. Mtazamo wao utakuathiri. Kwa hiyo, chagua marafiki kwa hekima. Mtegemee Yehova, na utaepuka majuto mengi.”
Tracy: “Usijidanganye kwa kufikiri, ‘Jambo kama hilo haliwezi kunipata.’ Mama yangu aliniketisha chini na kuniambia waziwazi kwamba matendo yangu yatakuwa na matokeo mabaya. Niliudhika sana. Nilifikiri kwamba nilikuwa na hekima ya kutosha nisiweze kushawishiwa na mwenendo mbaya. Nilikuwa nimekosea. Ishi kupatana na viwango vya Yehova na ushirikiane na watu wanaofanya vivyo hivyo. Kufanya hivyo kutakuletea furaha zaidi.”
Je, Viwango vya Biblia Ni Pingu au Mkanda wa Usalama?
Iwapo vijana wenzako wanakudhihaki kwa sababu unajaribu kuishi kupatana na viwango vya Biblia, jiulize maswali yafuatayo: ‘Kwa nini hawataki kuishi kupatana na sheria za Biblia kuhusu maadili ya ngono? Je, wameisoma Biblia na kuchunguza faida zinazotokana na kutii amri za Mungu? Je, wamechunguza kwa uangalifu matokeo ya kupuuza viwango hivyo? Au badala yake, je, wanafuata tu kile ambacho kila mtu anafanya?’
Inaelekea kwamba unawafahamu watu ambao ‘wanafuata umati.’ (Kutoka 23:2) Je, hungependa kuwa na utu bora kuliko huo? Unaweza kuwaje tofauti? Kwa kufuata shauri la Biblia la ‘kujihakikishia mwenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ (Waroma 12:2) Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” na angependa uwe na furaha pia. (1 Timotheo 1:11; Mhubiri 11:9) Viwango vilivyo katika Biblia vipo kwa faida yako. Ni kweli kwamba unaweza kuviona kuwa pingu zinazozuia uhuru wako. Lakini ukweli ni kwamba viwango vya maadili vya Biblia ni kama mkanda wa usalama ndani ya gari unaomlinda msafiri asiumie.
Bila shaka, unaweza kuiamini Biblia. Ukichagua kuishi kupatana na viwango vyake, utamfurahisha Yehova na pia utajifaidi mwenyewe.—Isaya 48:17.
[Maelezo ya Chini]
a Majina katika makala hii yamebadilishwa.
-