-
Je, Tuitegemee au Tusiitegemee?Amkeni!—2007 | Novemba
-
-
Je, Tuitegemee au Tusiitegemee?
“Usitumaini mbao zilizooza,” akaandika William Shakespeare, mwandishi wa tamthilia Mwingereza. Kwa kweli, kabla ya kukanyaga mbao za mashua, unapaswa kuhakikisha kwamba hazijaoza.
MANENO ya Shakespeare yanapatana na maneno ya Mfalme Sulemani mwenye hekima wa Israeli la kale ambaye aliandika hivi miaka 3,000 hivi iliyopita: “Mujinga anaamini kila neno: lakini mwenye akili anaangalia sana namna anavyokwenda.” (Methali 14:15, Zaire Swahili Bible) Naam, ni mjinga tu ambaye atakubali kila kitu anachosikia, akifanya maamuzi na kutenda kupatana na mashauri au mafundisho yasiyo na msingi. Kutegemea vitu visivyofaa, kama tu kukanyaga mbao zilizooza, kunaweza kutuletea msiba. Huenda ukajiuliza, ‘Je, kuna mwongozo wowote ambao kwa kweli tunaweza kuutegemea?’
Mamilioni ya watu ulimwenguni pote hutegemea kabisa kitabu kimoja cha kale. Kitabu hicho ni Biblia Takatifu. Wanategemea kitabu hicho kiongoze hatua zao. Maamuzi yao yanategemea mashauri ya kitabu hicho na matendo yao yanapatana na mafundisho yake. Je, watu hao wanakanyaga mbao zilizooza? Jibu la swali hilo linategemea sana jibu la swali lingine, Je, kuna sababu nzuri za kuitegemea Biblia? Toleo hili la pekee la Amkeni! linachunguza uthibitisho uliopo.
Toleo hili la Amkeni! halijakusudiwa kukulazimisha uwe na imani au maoni fulani ya kidini. Badala yake, limekusudiwa kuonyesha uthibitisho wenye nguvu ambao umewasadikisha mamilioni ya watu kwamba wanaweza kuitegemea Biblia. Baada ya kusoma makala zinazofuata, unaweza kujiamulia ikiwa unaweza kuitegemea Biblia.
Unapaswa kuchunguza habari hii kwa uzito. Kwa kweli, ikiwa Biblia ni chanzo chenye kutegemeka cha kupata mwongozo kutoka kwa Muumba wetu, basi utafaidika ikiwa wewe na wapendwa wako mtachunguza kile ambacho Biblia inasema.
Hata hivyo, acheni kwanza tutaje mambo fulani ya hakika kuhusu Biblia. Kwanza kabisa, Biblia ni kitabu cha pekee.
-
-
Kitabu cha PekeeAmkeni!—2007 | Novemba
-
-
Kitabu cha Pekee
“Biblia ndicho kitabu kilichogawanywa kwa wingi zaidi katika historia.”—The World Book Encyclopedia.
ZAIDI ya miaka 550 iliyopita, mwandishi Mjerumani, Johannes Gutenberg alianza uchapishaji kwa kutumia mashini ya kuchapishia yenye herufi zinazopangwa. Kitabu cha kwanza muhimu alichochapisha kilikuwa Biblia.a Tangu wakati huo mabilioni ya vitabu kuhusu habari mbalimbali vimechapishwa. Hata hivyo, Biblia ndicho kitabu cha pekee zaidi kati ya hivyo vyote.
◼ Inakadiriwa kwamba zaidi ya Biblia bilioni 4.7 (ikiwa nzima au sehemu yake) zimechapishwa. Hiyo ni mara tano zaidi ya idadi ya nakala za kitabu Quotations From Chairman Mao, ambacho ndicho kitabu cha pili kugawanywa kwa wingi zaidi.
◼ Hivi karibuni, zaidi ya nakala milioni 50 za Biblia au sehemu zake ziligawanywa kwa mwaka mmoja tu. “Kila mwaka, Biblia ndicho kitabu ambacho huuzwa zaidi,” inasema ripoti moja katika gazeti The New Yorker.
◼ Biblia imetafsiriwa katika zaidi ya lugha 2,400 ikiwa nzima au kwa sehemu. Angalau sehemu fulani ya Biblia inapatikana katika lugha zinazozungumzwa na zaidi ya asilimia 90 ya wanadamu.
◼ Karibu nusu ya waandikaji wa Biblia walikamilisha kazi yao ya kuandika kabla ya kuzaliwa kwa Mchina mashuhuri na mwenye hekima, Confucius, na Siddhārtha Gautama, mwanzilishi wa Ubudha.
◼ Biblia imekuwa na uvutano mkubwa sana katika sanaa, kutia ndani baadhi ya michoro, muziki, na fasihi zinazojulikana sana ulimwenguni.
◼ Biblia imeokoka licha ya kupigwa marufuku na serikali mbalimbali, kuteketezwa na wapinzani wa kidini, na kushambuliwa na wachambuzi. Hakuna kitabu kingine ambacho kimepata upinzani mkubwa kadiri hiyo na kikaokoka.
Mambo hayo ambayo yametajwa ni yenye kuvutia sana, sivyo? Hata hivyo, habari zenye kupendeza na takwimu pekee hazithibitishi kwamba Biblia ni yenye kutegemeka. Sasa, tutachunguza sababu tano zinazowasadikisha mamilioni ya watu kwamba Biblia ni kitabu kinachostahili kutegemewa.
[Maelezo ya Chini]
a Biblia ya Gutenberg ilikuwa tafsiri ya Kilatini nayo ilikamilika mwaka wa 1455 hivi.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Mashini ya kuchapishia ya Gutenberg na ukurasa wa Biblia yake
[Hisani]
Press: Courtesy American Bible Society; page: © Image Asset Management/age fotostock
-
-
1. Ni Sahihi KihistoriaAmkeni!—2007 | Novemba
-
-
Sababu za Kuitegemea Biblia
1. Ni Sahihi Kihistoria
Ni vigumu kukiamini kitabu ambacho kina mambo yasiyo sahihi. Wazia ukisoma kitabu cha kisasa cha historia ambacho kinaonyesha kwamba Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipiganwa katika miaka ya 1800 au kinachosema rais wa Marekani ni mfalme. Je, kasoro hizo hazingefanya ukitilie shaka kitabu hicho?
HAKUNA mtu ambaye amefaulu kupinga usahihi wa historia ya Biblia. Biblia hutaja watu na matukio halisi.
Watu. Kuhusu Pontio Pilato, yule gavana Mroma wa Yudea ambaye alimtoa Yesu ili atundikwe, wachambuzi wa Biblia walitia shaka ikiwa aliwahi kuishi. (Mathayo 27:1-26) Uthibitisho wa kwamba wakati fulani Pilato aliwahi kuwa mtawala wa Yudea ulipatikana katika jiwe [1] lililogunduliwa kwenye jiji la bandarini la Kaisaria katika Bahari ya Mediterania mnamo 1961.
Kabla ya mwaka wa 1993, hakukuwa na ushuhuda nje ya Biblia uliounga mkono maisha ya Daudi, yule mchungaji kijana mwenye ujasiri aliyekuja kuwa mfalme wa Israeli. Lakini mwaka huo, wachimbaji wa vitu vya kale walipata jiwe la volkano [2], katika eneo fulani upande wa kaskazini mwa Israeli linalofikiriwa kuwa la karne ya tisa K.W.K., na wataalamu wanasema lina maneno “Nyumba ya Daudi” na “mfalme wa Israeli.”
Matukio. Kwa muda mrefu hadi nyakati za hivi karibuni, wasomi wengi walishuku usahihi wa simulizi la Biblia la taifa la Edomu kupigana na Waisraeli nyakati za Daudi. (2 Samweli 8:13, 14) Walisema kwamba Edomu ilikuwa jamii ya wafugaji wakati huo na haikuwa na mpangilio wala nguvu za kutosha kuweza kuwatisha Waisraeli mpaka muda mrefu baadaye. Hata hivyo, uchimbuzi uliofanywa hivi karibuni unaonyesha kwamba “Edomu ilikuwa jamii iliyo na nguvu na yenye mpangilio karne kadhaa mapema [tofauti na ilivyodhaniwa mapema], kama ilivyoonyeshwa katika Biblia,” inaeleza makala moja katika jarida Biblical Archaeology Review.
Vyeo vinavyofaa. Kulikuwa na watawala mbalimbali katika karne 16 ambazo Biblia iliandikwa. Nyakati zote Biblia hutumia cheo kinachofaa inapomtaja mtawala fulani. Kwa mfano, Biblia hutaja kwa usahihi inapomrejezea Herode Antipa kuwa “mtawala wa wilaya” na Galio kuwa “liwali.” (Luka 3:1; Matendo 18:12) Ezra 5:6 inamtaja Tatenai, gavana wa mkoa wa Uajemi “ng’ambo ya Mto,” yaani, Mto Efrati. Sarafu iliyotengenezwa katika karne ya nne K.W.K. ina maelezo kama hayo, ikimtambulisha gavana Mwajemi Mazeasi kuwa mtawala wa mkoa “Ng’ambo ya Mto.”
Usahihi hata katika mambo madogo haupaswi kupuuzwa. Ikiwa tunaweza kuwaamini waandikaji wa Biblia hata katika mambo madogo, je, hilo halipaswi kuongeza uhakika wetu katika mambo mengine ambayo waliandika?
[Picha katika ukurasa wa 5]
1: Photograph © Israel Museum, Jerusalem; courtesy of Israel Antiquities Authority; 2: HUC, Tel Dan Excavations; photo: Zeev Radovan
-
-
2. Iliandikwa Bila Kupendelea na kwa UnyoofuAmkeni!—2007 | Novemba
-
-
Sababu za Kuitegemea Biblia
2. Iliandikwa Bila Kupendelea na kwa Unyoofu
Unyoofu huweka msingi wa kumwamini mtu. Unaweza kumwamini mtu anayejulikana kuwa mnyoofu, lakini akikudanganya hata mara moja tu, huenda ukaacha kumwamini kabisa.
WANAUME walioandika Biblia walikuwa wanyoofu na waliandika bila kupendelea. Unyoofu wao unathibitisha kwamba maandishi yao ni ya kweli.
Makosa na udhaifu.
Waandikaji wa Biblia hawakuficha makosa na udhaifu wao. Musa alisimulia kosa ambalo lilimletea madhara makubwa. (Hesabu 20:7-13) Asafu alielezea jinsi ambavyo kwa muda fulani alionea wivu maisha yenye ufanisi ya waovu. (Zaburi 73:1-14) Yona alieleza namna alivyokosa kutii na mwelekeo mbaya aliokuwa nao mwanzoni Mungu alipowaonyesha rehema watenda-dhambi waliotubu. (Yona 1:1-3; 3:10; 4:1-3) Mathayo alieleza bila kuficha jinsi alivyomwacha Yesu usiku ule ambao Yesu alikamatwa.—Mathayo 26:56.
Waandikaji wa Maandiko ya Kiebrania walieleza waziwazi malalamiko ya kila mara na uasi wa watu wa taifa lao wenyewe. (2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16) Waandikaji hawakuficha makosa ya mtu yeyote, hata ya watawala wa mataifa yao. (Ezekieli 34:1-10) Wakiwa na unyoofu huohuo, mitume waliandika barua zilizozungumzia matatizo mazito ya Wakristo fulani kutia ndani ya wale wenye madaraka, na pia ya makutaniko fulani katika karne ya kwanza W.K.—1 Wakorintho 1:10-13; 2 Timotheo 2:16-18; 4:10.
Waandikaji wa Biblia kama vile Yona, waliandika makosa yao wenyewe
Kusema kweli bila kurairai.
Waandikaji wa Biblia hawakujaribu kufunika-funika kweli ambazo zingeweza kuonwa kuwa zinaaibisha. Wakristo wa karne ya kwanza walieleza waziwazi kwamba hawakupendwa na ulimwengu uliowazunguka na walionwa kuwa wapumbavu na wenye kudharauliwa. (1 Wakorintho 1:26-29) Waandikaji hao walisema kwamba mitume wa Yesu walionwa kuwa “wasio na elimu na wa kawaida tu.”—Matendo 4:13.
Waandikaji wa Injili hawakusema uwongo ili Yesu aonekane kuwa mtu mwenye kuvutia zaidi. Badala yake waliripoti kwa unyoofu kwamba alizaliwa katika familia ya hali ya chini, kwamba hakusoma katika shule za hali ya juu za wakati huo, na kwamba wasikilizaji wake wengi walikataa ujumbe wake.—Mathayo 27:25; Luka 2:4-7; Yohana 7:15.
Kwa kweli, Biblia inatoa uthibitisho wa kutosha kwamba iliandikwa na watu wanyoofu. Je, unyoofu wao haukufanyi uitumaini Biblia?
-
-
3.UpatanoAmkeni!—2007 | Novemba
-
-
Sababu za Kuitegemea Biblia
3.Upatano
Hebu wazia ukiwaomba watu 40 kutoka malezi tofauti waandike sehemu tofauti-tofauti za kitabu kimoja. Waandikaji hao wanaishi nchi mbalimbali na si wote wanaojuana. Wengine hawajui wenzao wameandika nini. Je, ungetarajia kitabu kama hicho kipatane?
BIBLIA imeandikwa kwa njia hiyo.a Upatano wake ni wenye kustaajabisha kwani Biblia iliandikwa katika hali zisizo za kawaida kuliko zile zilizotajwa hapo juu.
Hali za pekee. Biblia iliandikwa kwa kipindi cha miaka 1,600, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. hadi mwaka wa 98 W.K. hivi. Wengi kati ya hao waandikaji 40 hivi waliishi katika karne tofauti. Walifanya kazi tofauti-tofauti. Wengine walikuwa wavuvi, wengine walikuwa wafugaji au wafalme, na mmoja alikuwa tabibu.
Ujumbe unaopatana. Waandikaji wa Biblia waliandika kuhusu kichwa kikuu cha Biblia: kutetewa kwa haki ya Mungu ya kutawala wanadamu na utimizo wa kusudi lake kupitia Ufalme wake wa kimbingu, yaani, serikali itakayotawala ulimwengu. Kichwa hicho kinaonekana kwa mara ya kwanza katika kitabu cha Mwanzo, kisha kinafafanuliwa katika vitabu vinavyofuata na mwishowe kinafikia tamati katika kitabu cha Ufunuo.—Ona sehemu yenye kichwa “Biblia Inazungumzia Nini?” katika ukurasa wa 19.
Upatano hata katika mambo madogo. Waandikaji wa Biblia walipatana hata katika mambo madogo-madogo, lakini mara nyingi upatano huo haukukusudiwa. Fikiria mfano mmoja. Mwandikaji wa Biblia Yohana anatuambia kwamba wakati umati mkubwa ulipokuja kumsikiliza Yesu, Yesu alimwuliza Filipo mahali ambapo wangeweza kununua mikate ya kuwalisha watu. (Yohana 6:1-5) Katika simulizi linalolingana na hilo, Luka anasema kwamba tukio hilo lilitukia karibu na jiji la Bethsaida. Mwanzoni mwa kitabu chake, Yohana alikuwa ametaja kwamba Filipo anatoka Bethsaida. (Luka 9:10; Yohana 1:44) Hivyo, haishangazi kwamba Yesu alimwuliza mwanafunzi aliyewahi kuishi karibu na mahali hapo. Mambo hayo madogo yanapatana hata ingawa waandikaji hawakukusudia jambo hilo.b
Tofauti ndogondogo. Kuna tofauti ndogondogo kati ya masimulizi mbalimbali, lakini je, hatupaswi kutarajia hilo? Kwa mfano, tuseme kikundi cha watu kimeshuhudia uhalifu. Ikiwa kila mmoja wao angesimulia mambo yaleyale kwa kutumia maneno yaleyale, je, hungeshuku wanadanganya? Ungetazamia maelezo yao yatofautiane kwa njia fulani ikitegemea mahali ambapo kila mmoja wao alisimama aliposhuhudia jambo hilo. Waandikaji wa Biblia waliandika mambo kwa njia hiyohiyo.
Fikiria mfano huu. Je, Yesu alivaa vazi la rangi ya zambarau siku alipokufa, kama vile Marko na Yohana wanavyoripoti? (Marko 15:17; Yohana 19:2) Au je, joho hilo lilikuwa jekundu kama Mathayo anavyosema? (Mathayo 27:28) Huenda maelezo yote yakawa sahihi. Rangi nyekundu hutumiwa katika mchanganyiko ambao mwishowe hutokeza rangi ya zambarau. Ikitegemea mahali ambapo mtu amesimama, mwangaza wa jua na mandhari ya nyuma ingeweza kuficha rangi fulani na hivyo kufanya kila mmoja wao aone vazi hilo kuwa lina rangi tofauti.c
Upatano wa waandikaji wa Biblia, kutia ndani kupatana kusikokusudiwa, kunathibitisha zaidi kwamba mambo waliyoandika yanategemeka.
[Maelezo ya Chini]
a Biblia ina vitabu 66, kuanzia Mwanzo hadi Ufunuo.
b Ukitaka habari zaidi kuhusu kupatana huko, ona ukurasa wa 16-17 katika broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
c Kwa habari zaidi, ona sura ya 7 ya kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? yenye kichwa “Je, Biblia Hujipinga Yenyewe?” kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Je, vazi la Yesu lilikuwa la zambarau au jekundu?
-
-
4. Ni Sahihi KisayansiAmkeni!—2007 | Novemba
-
-
Sababu za Kuitegemea Biblia
4. Ni Sahihi Kisayansi
Sayansi imepiga hatua kubwa katika nyakati za karibuni. Kwa sababu hiyo, nadharia za kisasa zimechukua mahali pa zile za kale. Kile ambacho wakati mmoja kilionekana kuwa kweli sasa huonekana kuwa hadithi tu. Mara nyingi vitabu vya kufundishia sayansi huhitaji kurekebishwa.
BIBLIA si kitabu cha kufundishia sayansi. Hata hivyo, kuhusiana na mambo ya kisayansi, Biblia haitambuliwi tu kwa mambo inayosema bali pia kwa yale isiyosema.
U.S. Fish & Wildlife Service, Washington, D.C./NASA
Haina maoni yasiyo ya kisayansi.
Nadharia nyingi zisizo za kweli zilikubaliwa na watu wengi zamani. Kuna wale waliosema kuwa dunia ni tambarare na wengine wakasema kuwa inashikiliwa na vitu fulani. Muda mrefu kabla ya wanasayansi kugundua jinsi ambavyo magonjwa huambukizwa na jinsi ya kuyazuia, madaktari walitumia mbinu ambazo hazingefanya kazi au hata zilizowaua watu. Lakini katika sura zake zaidi ya 1,100, Biblia haijapendekeza hata mara moja maoni yoyote yasiyo ya kisayansi au mazoea yanayodhuru.
Maneno yanayopatana na sayansi.
Miaka 3,500 iliyopita, Biblia ilisema kwamba dunia inaning’inia “pasipo na kitu.” (Ayubu 26:7) Katika karne ya nane K.W.K., Isaya alisema kwa njia ya wazi kuhusu “mviringo wa [au, duara ya] dunia.” (Isaya 40:22) Je, kusema kwamba dunia ni ya mviringo na inaning’inia pasipo kitu si wazo linalopatana na sayansi ya kisasa?
Sheria ya Musa, iliyoandikwa mnamo 1500 K.W.K. (inayopatikana katika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia) ilitoa sheria zinazofaa kuhusu kuwatenga wagonjwa, kushughulika na miili iliyokufa, na kushughulikia uchafu.—Mambo ya Walawi 13:1-5; Hesabu 19:1-13; Kumbukumbu la Torati 23:13, 14.
Kwa sababu ya kutumia darubini zenye nguvu kuangalia mbingu, wanasayansi walisema kwamba ulimwengu ulitokea ghafula. Si wanasayansi wote wanaopenda maelezo hayo. Profesa mmoja alisema: “Ulimwengu uliotokea unaonyesha kuwa lazima uwe ulitokezwa na kitu fulani; ni nani anayeweza kuwazia matokeo yanayoonekana bila mwanzilishi?” Hata hivyo, muda mrefu kabla ya darubini kubuniwa, andiko la kwanza la Biblia lilisema wazi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”—Mwanzo 1:1.
Zamani sana, Biblia ilisema kwa usahihi kwamba dunia ni duara na inaning’inia “pasipo na kitu”
Ingawa Biblia ni kitabu cha zamani kinachozungumzia mambo mengi, hakina kasoro zozote za kisayansi. Je, kitabu kama hicho hakistahili kuchunguzwa?a
a Ili upate mifano zaidi inayoonyesha kwamba Biblia ni sahihi kisayansi, ona ukurasa wa 18-21 katika broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
5. Unabii UliotimizwaAmkeni!—2007 | Novemba
-
-
Sababu za Kuitegemea Biblia
5. Unabii Uliotimizwa
Hebu wazia mtabiri wa hali ya hewa ambaye ana rekodi ya muda mrefu ya kuwa sahihi nyakati zote. Ikiwa angetabiri kwamba mvua itanyesha, je, ungebeba mwavuli?
BIBLIA imejaa utabiri, au unabii.a Rekodi yake katika historia ni wazi. Unabii wa Biblia ni sahihi nyakati zote.
Mambo ya pekee.
Mara nyingi unabii wa Biblia hutaja mambo hususa nayo yametimizwa hata katika mambo madogo-madogo. Kwa kawaida, unabii huo huhusisha mambo muhimu na hutabiri mambo tofauti na matarajio ya wale wanaoishi wakati unabii huo unapoandikwa.
Mfano wenye kutokeza.
Jiji la kale la Babiloni lililojengwa likiwa limezungukwa na Mto Efrati, liliitwa “kitovu cha kisiasa, kidini, na utamaduni cha nchi za kale za Mashariki.” Mnamo 732 K.W.K., nabii Isaya aliandika unabii wa maangamizi. Alisema kwamba Babiloni litaanguka. Isaya alitaja mambo hususa: Kiongozi anayeitwa “Koreshi” ndiye angekuwa mshindi, maji ya Mto Efrati ‘yatakaushwa’ na malango ya jiji ‘hayatafungwa.’ (Isaya 44:27–45:3) Miaka 200 hivi baadaye, Oktoba 5, 539 K.W.K. (5/10/539), kila sehemu ya unabii huo ilitimizwa. Mwanahistoria Mgiriki Herodotus (wa karne ya tano K.W.K.) alithibitisha jinsi Babiloni lilivyoanguka.b
Sehemu ya unabii yenye kushangaza.
Isaya alitoa utabiri mwingine wenye kushangaza kuhusu Babiloni: “Hatakaliwa kamwe.” (Isaya 13:19, 20) Lilikuwa jambo la ujasiri kutabiri kwamba jiji lenye utendaji mwingi na lililojengwa mahali panapofaa sana lingefanywa ukiwa kabisa. Kwa kawaida, ingetarajiwa kwamba jiji kama hilo lingejengwa tena ikiwa lingeharibiwa. Ingawa Babiloni liliendelea kwa muda fulani baada ya kushindwa, mwishowe maneno ya Isaya yalithibitika kuwa ya kweli. Gazeti Smithsonian linaripoti kuwa leo eneo la Babiloni la kale “ni tambarare, lenye joto, halina mtu na lina vumbi jingi.”
Inapendeza kufikiria umuhimu wa unabii wa Isaya. Kile alichotabiri kinalingana na mtu kutabiri njia hususa ambayo jiji la kisasa, kama vile New York au London, litaharibiwa miaka 200 kutoka sasa, kisha kusema kwa mkazo kwamba jiji hilo halitakaliwa tena. Bila shaka, jambo lenye kupendeza zaidi ni kwamba unabii wa Isaya ulitimia!c
Biblia ilitabiri kwa usahihi kwamba kiongozi anayeitwa Koreshi angeshinda Babiloni lenye nguvu
Katika makala hizi, tumechunguza uthibitisho mbalimbali ambao umewasadikisha mamilioni ya watu kwamba Biblia inategemeka. Kwa sababu hiyo, wao huiona kuwa mwongozo unaotegemeka wa kuongoza hatua zao. Kwa nini usijifunze mengi kuhusu Biblia ili ujiamulie ikiwa wewe pia unaweza kuitegemea?
a Utabiri wa hali ya hewa unaonyesha mambo ambayo huenda yakatukia. Unabii wa Biblia umeongozwa na Mungu, ambaye anaweza kubadilisha mambo akiamua kufanya hivyo.
b Kwa habari zaidi kuhusu kutimizwa kwa unabii wa Isaya, ona ukurasa wa 27-29 wa broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
c Ili kupata mifano zaidi ya unabii wa Biblia na mambo hakika ya kihistoria yanayothibitisha unabii huo, ona ukurasa wa 117-133 wa kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Ni Nani Aliyeitunga Biblia?Amkeni!—2007 | Novemba
-
-
Maoni ya Biblia
Ni Nani Aliyeitunga Biblia?
BIBLIA inaeleza wazi ni nani waliotumiwa kuiandika. Sehemu mbalimbali za kitabu hicho zinaanza kwa maneno kama vile, “maneno ya Nehemia,” “maono ya Isaya,” na “neno la Yehova lililomjia Yoeli.” (Nehemia 1:1; Isaya 1:1; Yoeli 1:1) Masimulizi fulani huelezwa kuwa yaliandikwa na Gadi, Nathani, au Samweli. (1 Mambo ya Nyakati 29:29) Maneno ya utangulizi ya zaburi nyingi yanaonyesha watungaji wa zaburi hizo ni nani.—Zaburi 79, 88, 89, 90, 103, na 127.
Kwa kuwa wanadamu walitumiwa kuandika Biblia, wachambuzi wanasema kwamba Biblia ni matokeo ya hekima ya wanadamu, kama ilivyo kwa vitabu vingine. Je, maoni hayo yana msingi?
Waandikaji 40, Mtungaji Mmoja
Waandikaji wengi wa Biblia walikiri kwamba waliandika kwa jina la Yehova, Mungu wa pekee wa kweli, na kwamba waliongozwa naye au na malaika. (Zekaria 1:7, 9) Zaidi ya mara 300, manabii walioandika Maandiko ya Kiebrania walitangaza hivi: “Yehova amesema hivi.” (Amosi 1:3; Mika 2:3; Nahumu 1:12) Mara nyingi walianza kwa maneno kama vile “neno la Yehova lililomjia Hosea.” (Hosea 1:1; Yona 1:1) Kuhusu manabii wa Mungu, mtume Petro alieleza hivi: “Wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 Petro 1:21.
Hivyo, ijapokuwa Biblia ina vitabu vingi vidogo-vidogo vilivyoandikwa na watu wengi, ina upatano, na waandikaji wake walitambua kwamba Mungu ndiye aliyekuwa akiwaongoza. Kwa maneno mengine, Mungu alitumia wanadamu waandike mawazo yake. Alifanyaje hivyo?
“Limeongozwa na Roho”
Mtume Paulo alifafanua hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kuongozwa na roho ya Mungu” linamaanisha “lililotiwa pumzi ya Mungu.” Inamaanisha kwamba Mungu alitumia nguvu yake isiyoonekana kuongoza akili za waandikaji, na hivyo kupitisha ujumbe wake. Lakini kuhusu zile Amri Kumi, Yehova mwenyewe aliziandika kwenye yale mabamba ya mawe. (Kutoka 31:18) Nyakati nyingine, Mungu alitoa ujumbe moja kwa moja kwa watumishi wake. Andiko la Kutoka 34:27 linasema hivi: “Yehova akaendelea kumwambia Musa: ‘Jiandikie maneno haya . . . ’”
Katika pindi nyingine, Mungu aliwawezesha wanadamu kuona maono ya kile alichotaka wakiandike. Hivyo Ezekieli alisema: “Nami nikaanza kuona maono ya Mungu.” (Ezekieli 1:1) Vivyo hivyo, “Danieli aliona ndoto na maono ya kichwa chake kitandani mwake. Ndipo akaandika ndoto hiyo.” (Danieli 7:1) Kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, kilitolewa kwa mtume Yohana kwa njia kama hiyo. Yohana aliandika: “Kwa uongozi wa roho nilikuja kuwa katika siku ya Bwana, nami nikasikia nyuma yangu sauti yenye nguvu kama ile ya tarumbeta, ikisema: ‘Yale unayoona yaandike katika kitabu cha kukunjwa.’”—Ufunuo 1:10, 11.
Hisia za Waandikaji
Kuongozwa na roho ya Mungu hakukumaanisha kwamba waandikaji hawangewasilisha hisia zao. Kwa kweli, waandikaji walihitaji kufanya jitihada fulani ili kuandika ujumbe wa Mungu. Kwa mfano, mwandikaji wa Biblia wa kitabu cha Mhubiri aliandika kwamba “alijitahidi kutafuta maneno yenye kupendeza na kuandika maneno sahihi ya kweli.” (Mhubiri 12:10) Ili kuandika rekodi zake za kihistoria, Ezra alilazimika kuchunguza angalau vyanzo 14, kama vile “hesabu ya mambo ya siku za Mfalme Daudi,” na “Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli.” (1 Mambo ya Nyakati 27:24; 2 Mambo ya Nyakati 16:11) Mwandikaji wa Injili, Luka, ‘alifuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi, ili kuyaandika hayo kwa utaratibu wenye kufuatana.’—Luka 1:3.
Vitabu fulani vya Biblia vinafunua mambo mbalimbali kuhusu utu wa waandikaji wake. Kwa mfano, Mathayo Lawi, ambaye kabla ya kuwa mwanafunzi wa Yesu alikuwa mkusanya kodi, alikazia uangalifu namba hususa. Mathayo ndiye mwandikaji pekee wa Injili aliyeandika kwamba Yesu alisalitiwa kwa “vipande 30 vya fedha.” (Mathayo 27:3; Marko 2:14) Luka, ambaye alikuwa tabibu, alieleza kwa undani mambo ya kitiba. Kwa mfano, alipokuwa akielezea hali ya wale ambao Yesu aliwaponya, alitumia maneno kama vile “homa kali” na “kujaa ukoma.” (Luka 4:38; 5:12; Wakolosai 4:14) Hivyo, Yehova aliwaruhusu waandikaji wajieleze kwa maneno na kwa mtindo wao wenyewe; wakati uleule, aliongoza akili zao ili kwamba maneno hayo yawe sahihi na yafikishe ujumbe wake.—Methali 16:9.
Biblia Kamili
Je, haishangazi kwamba watu 40, wakiandika wakiwa katika nchi kadhaa kwa zaidi ya miaka 1,600, waliweza kuandika kitabu chenye upatano na chenye kichwa kimoja kikuu? (Ona sanduku “Biblia Inazungumzia Nini?” katika ukurasa wa 19.) Hilo lisingewezekana ikiwa wote hawakuongozwa na Mtungaji mmoja.
Je, ilikuwa ni lazima Yehova atumie watu kuandika Neno lake? Jibu ni hapana. Lakini kufanya hivyo kulikuwa ni wonyesho wa hekima yake. Kwa kweli, kinachofanya Biblia ipendwe ulimwenguni pote ni kwamba waandikaji wake hueleza kwa wazi hisia ambazo wanadamu huwa nazo, kwa mfano, kisa cha Mfalme Daudi kinaonyesha mtenda-dhambi anayetubu ambaye aliomba aonyeshwe rehema na Mungu.—Zaburi 51:2-4, 13, 17, maneno ya utangulizi.
Ingawa Yehova alitumia wanadamu kuandika, tuna hakika na walichoandika kama vile Wakristo wa mapema ambao waliyakubali Maandiko Matakatifu “si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.
JE, UMEJIULIZA HIVI?
◼ Mtungaji wa “Andiko lote” ni nani?—2 Timotheo 3:16.
◼ Yehova alitumia njia zipi kufikisha mawazo yake?—Kutoka 31:18; 34:27; Ezekieli 1:1; Danieli 7:1.
◼ Utu na mapendezi ya waandikaji walioongozwa na roho yanaonyeshwaje katika uandikaji wao? —Mathayo 27:3; Luka 4:38.
-
-
Jinsi Biblia IlivyotufikiaAmkeni!—2007 | Novemba
-
-
Jinsi Biblia Ilivyotufikia
Ni muujiza mkubwa kwamba Biblia imetufikia leo bila kuharibiwa. Ilikamilishwa zaidi ya miaka 1,900 iliyopita kwenye karatasi zilizotengenezwa kwa mafunjo na ngozi, na ni watu wachache leo wanaoweza kuzungumza lugha za awali zilizotumiwa kuiandika. Pia watu wenye mamlaka kutia ndani maliki na viongozi wa kidini walijaribu juu chini kuiharibu Biblia.
KITABU hiki chenye kustaajabisha kiliokokaje na kuwa kitabu kinachojulikana zaidi? Tutachunguza mambo mawili tu.
Kunakili Kulihifadhi Maandishi
Waisraeli ambao ndio watunzaji wa maandishi ya Biblia ya mapema, walihifadhi kwa uangalifu vitabu vya kukunja vya awali na wakatoa nakala nyingi sana. Kwa mfano, wafalme wa Israeli waliambiwa waandike “nakala ya sheria hii kutoka katika ile iliyo mkononi mwa makuhani Walawi.”—Kumbukumbu la Torati 17:18.
Waisraeli wengi walipenda kusoma Maandiko na waliyatambua kuwa Neno la Mungu. Hivyo, kunakili maandishi hayo kulifanywa kwa uangalifu mkubwa sana na waandikaji waliokuwa na uzoefu wa hali ya juu. Ezra, mwandikaji ambaye alimwogopa Mungu, anatajwa kuwa “mwandikaji stadi katika sheria ya Musa, ambayo Yehova Mungu wa Israeli alikuwa ametoa.” (Ezra 7:6) Wamasora ambao walinakili Maandiko ya Kiebrania, au “Agano la Kale,” kati ya karne ya sita na ya kumi W.K., walihesabu hata herufi katika maandishi hayo ili wasikosee. Kunakili huko kwa uangalifu kulisaidia kuhakikisha maandishi yalikuwa sahihi na kuokoka kwa Biblia licha ya jitihada kubwa zilizofanywa na maadui ili kuiangamiza.
Kwa mfano, mnamo 168 K.W.K., mfalme Msiria, Antioko wa Nne alijaribu kuharibu nakala zote za Maandiko ya Kiebrania ambazo angezipata huko Palestina. Kitabu cha historia ya Wayahudi kinasema: “Kitabu chochote cha kukunjwa walichopata walikirarua na kukiteketeza.” Kitabu The Jewish Encyclopedia kinasema: “Maofisa waliopewa mgawo wa kutekeleza amri hizo walifanya hivyo kwa ukatili mwingi . . . Mtu aliyekuwa na kitabu kitakatifu . . . alihukumiwa kifo.” Lakini nakala za Maandiko ziliokoka miongoni mwa Wayahudi waliokuwa wakiishi Palestina na wale waliokuwa wakiishi katika nchi nyingine.
Muda mfupi baada ya waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya,” kumaliza kazi yao, nakala za barua zao zilizoongozwa na roho, unabii, na masimulizi ya kihistoria zilienea. Kwa mfano, Yohana aliandika Injili yake huko Efeso au karibu na jiji hilo. Hata hivyo, kipande cha Injili hiyo, ambacho wataalamu wanasema ni sehemu ya nakala iliyoandikwa miaka isiyozidi 50 tangu alipoandika simulizi lake, kilipatikana mamia ya kilomita nchini Misri. Ugunduzi huo ulionyesha kwamba Wakristo katika maeneo ya mbali walikuwa na nakala za maandishi yaliyoongozwa na roho yaliyokuwa yametoka tu kuandikwa.
Kuenezwa sana kwa Neno la Mungu pia kulichangia kuokoka kwake karne nyingi baada ya wakati wa Kristo. Kwa mfano, inasemekana kwamba asubuhi ya Februari 23 mwaka wa 303 W.K. (23/2/303), Maliki Mroma Diokletiani alisimama na kutazama askari wake wakivunja milango ya kanisa na kuteketeza nakala za Maandiko. Diokletiani alifikiri angeweza kuangamiza Ukristo kwa kuharibu maandishi matakatifu. Siku iliyofuata, alitangaza kwamba nakala zote za Biblia ziteketezwe kotekote katika Milki ya Roma. Hata hivyo, nakala ziliokoka na kutokezwa tena. Kwa kweli, sehemu kubwa za nakala mbili za Biblia katika Kigiriki ambazo huenda zilinakiliwa muda mfupi baada ya mnyanyaso wa Diokletiani zimeokoka hadi leo. Nakala moja iko Roma; nyingine iko katika Maktaba ya Uingereza huko London.
Ingawa hakuna hati za Biblia za awali ambazo zimewahi kupatikana, maelfu ya nakala zilizoandikwa kwa mkono za Biblia nzima au sehemu yake zimeokoka hadi leo. Nyingine kati ya hizo ni za zamani sana. Je, ujumbe ulio katika maandishi ya awali ulibadilika uliponakiliwa? Msomi W. H. Green alisema hivi kuhusu Maandiko ya Kiebrania: “Tunaweza kusema kwamba hakuna maandishi mengine ya zamani ambayo yametufikia yakiwa sahihi kadiri hiyo.” Kuhusu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, mmoja wa wataalamu wakuu wa hati za Biblia, Bwana Frederic Kenyon, aliandika hivi: ‘Tofauti kati ya tarehe za maandishi ya kwanza na tarehe ya uthibitisho wa kale zaidi uliopo leo ni ndogo sana hivi kwamba tofauti hiyo haina maana, na kwa hiyo sasa hakuna msingi wa kuwa na shaka kwamba Maandiko hayakutufikia yakiwa jinsi yalivyoandikwa. Uasilia na uaminifu wa ujumla wa vitabu vya Agano Jipya waweza kuonwa kuwa hatimaye umethibitishwa.’ Pia alisema hivi: “Si kusisitiza mno kusema kwamba kwa msingi maandishi ya Biblia ni hakika. . . . Haiwezi kusemwa hivyo kuhusu kitabu kingine chochote cha kale katika ulimwengu.”
Utafsiri wa Biblia
Sababu kubwa ya pili ambayo imefanya Biblia kuwa kitabu kinachojulikana zaidi ni kwamba inapatikana katika lugha nyingi. Jambo hilo linapatana na kusudi la Mungu kwamba watu wa mataifa yote na lugha zote wamjue na kumwabudu “kwa roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24; Mika 4:2.
Tafsiri ya kwanza ya Maandiko ya Kiebrania ilikuwa Septuajinti katika Kigiriki. Ilitayarishwa kwa ajili ya Wayahudi waliozungumza Kigiriki ambao waliishi nje ya Palestina na ilikamilishwa karibu karne mbili kabla ya huduma ya Yesu ya kidunia. Biblia nzima, kutia ndani Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ilitafsiriwa katika lugha nyingi katika muda wa karne chache baada ya uandikaji kukamilishwa. Lakini baadaye, wafalme na makasisi, ambao walipaswa kufanya yote waliyoweza kuhakikisha kwamba watu wanapata Biblia, walifanya kinyume kabisa cha hilo. Walijaribu kufanya makundi yao yakae katika giza la kiroho kwa kuzuia Neno la Mungu lisitafsiriwe katika lugha iliyoeleweka kwa urahisi.
Wanaume wenye ujasiri walihatarisha maisha yao kwa kupingana na Kanisa na Serikali ili watafsiri Biblia katika lugha ambazo watu walizielewa. Kwa mfano, mnamo 1530, Mwingereza William Tyndale, aliyesomea huko Oxford, alitoa toleo la Pentateuki, yaani, vitabu vya kwanza vitano vya Maandiko ya Kiebrania. Licha ya upinzani mwingi, alikuwa mtu wa kwanza kutafsiri Biblia moja kwa moja kutoka Kiebrania hadi Kiingereza. Pia, Tyndale alikuwa mtafsiri wa kwanza wa Kiingereza kutumia jina Yehova. Msomi wa Biblia Mhispania Casiodoro de Reina, kila wakati alikabili hatari ya kifo kutoka kwa wanyanyasaji Wakatoliki alipokuwa akitafsiri Biblia moja ya mapema ya Kihispania. Alipojaribu kumalizia tafsiri yake, alisafiri hadi Ufaransa, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani, na Uswisi.a
Leo, Biblia inaendelea kutafsiriwa katika lugha nyingi zaidi na mamilioni ya nakala zinaendelea kuchapishwa. Kuokoka kwake na kuwa kitabu kinachojulikana zaidi kunathibitisha ukweli wa maneno ya mtume Petro yaliyoongozwa na roho: “Majani hukauka, na ua huanguka, bali neno la Yehova linadumu milele.”—1 Petro 1:24, 25.
[Maelezo ya Chini]
a Tafsiri ya Reina ilichapishwa mnamo 1569 na kurekebishwa na Cipriano de Valera mnamo 1602.
-