-
Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la MunguAmkeni!—2011 | Desemba
-
-
Kuzuia Biblia Isitafsiriwe
Mwishowe, Kanisa Katoliki likaanza kuona Kilatini kuwa lugha takatifu. Kwa sababu hiyo, katika mwaka wa 1079 Vratislaus, dyuki wa Bohemia, alipoandika barua akiomba ruhusa ya kutumia Kislavonia katika ibada kanisani, Papa Gregory wa Saba alimjibu hivi: “Hatuwezi kwa njia yoyote kukubali ombi hili.” Kwa nini?
“Kwa wale wanaochunguza jambo hili kwa uangalifu,” akasema Gregory, “ni wazi kwamba ilimpendeza Mungu kufanya sehemu fulani ya Maandiko Matakatifu isieleweke kabisa kwa sababu, ikiwa kila mtu angeelewa kila kitu, basi [Maandiko] yangefanywa kuwa ya kawaida tu na kuvunjiwa heshima au watu wasio na akili nyingi wangeyaelewa vibaya na hivyo waasi.”
Watu wa kawaida hawangeweza kupata Biblia kwa urahisi, na ilipaswa kuwa hivyo. Msimamo huo uliwafanya makasisi waendelee kuwa na mamlaka juu ya watu wa kawaida. Hawakutaka watu wa kawaida wachunguze mambo ambayo waliona kuwa ni ya makasisi tu.
Mnamo 1199, Papa Innocent wa Tatu aliandika kuhusu watu walioonwa kuwa wazushi ambao walitafsiri Biblia katika Kifaransa na wakaamua kuwa na mazungumzo kati yao kuihusu. Innocent alitumia maneno haya ya Yesu kuwahusu: “Msiwape mbwa kitu kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe.” (Mathayo 7:6) Kwa nini alikuwa na maoni hayo? “Ili mtu wa kawaida na ambaye hana elimu asiwe na kimbelembele cha kujifunza Maandiko matakatifu yaliyotukuka, au kuwahubiria watu kuyahusu.” Mara nyingi, wale waliopinga amri ya papa walipelekwa kwa watesaji ambao waliwalazimisha waungame kwamba wao ni wazushi. Wale waliokataa kukana msimamo wao waliteketezwa wakiwa hai.
Wakati wa kile kipindi kirefu cha kuwazuia watu wasiipate na kuisoma Biblia, barua ya Papa Innocent ilitumiwa mara nyingi ili kutetea wazo la kwamba Biblia haipaswi kutumiwa wala kutafsiriwa katika lugha nyingine. Punde tu baada ya amri yake kutolewa, Biblia katika lugha nyingine zikaanza kuteketezwa, na pia watu fulani waliomiliki Biblia waliteketezwa. Katika karne zilizofuata, maaskofu na watawala wa nchi za Ulaya zilizokuwa chini ya udhibiti wa Kanisa Katoliki walitumia njia yoyote waliyoweza ili kuhakikisha kwamba marufuku yaliyowekwa na Papa Innocent wa Tatu yalifuatwa.
Viongozi wa Kanisa Katoliki walijua kwamba mafundisho mengi ya dini hiyo hayakutegemea Biblia bali yalitegemea mapokeo ya kanisa. Bila shaka, hiyo ilikuwa sababu moja iliyowafanya wawazuie waumini wao wasiipate Biblia. Iwapo wangeisoma basi wangetambua kwamba mafundisho ya kanisa yalipingana na Maandiko.
-
-
Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la MunguAmkeni!—2011 | Desemba
-
-
Tafsiri ya Luther ya Kijerumani na usambazaji wake ulivuta fikira za Kanisa Katoliki, ambalo liliona kwamba umaarufu wa Biblia ya Luther ulipaswa kufunikwa kwa kutokeza Biblia nyingine iliyokubaliwa na kanisa. Tafsiri mbili za aina hiyo katika Kijerumani zilitokezwa upesi baada ya hapo. Lakini, mnamo 1546, baada ya miaka isiyozidi 25, Baraza la Trent la Kanisa Katoliki, liliamua kwamba kuchapishwa kwa vichapo vyovyote, kutia ndani tafsiri za Biblia, hakupaswi kufanywa bila idhini ya kanisa.
Baraza la Trent liliagiza kwamba “kuanzia sasa Maandiko matakatifu . . . yatachapishwa kwa njia sahihi iwezekanayo; na kwamba itakuwa kinyume cha sheria kwa yeyote kuchapisha, au kumlipa mtu achapishe, vitabu vyovyote kuhusu mambo matakatifu bila jina la mwandishi kuonyeshwa; au kuviuza wakati ujao, au kuvimiliki, isipokuwa kwanza viwe vimechunguzwa na kuidhinishwa [na askofu wa eneo hilo].”
Mnamo 1559, Papa Paul wa Nne alichapisha orodha ya kwanza ya vitabu vilivyopigwa marufuku na Kanisa Katoliki. Orodha hiyo ilikataza mtu kuwa na tafsiri za Biblia za Kifaransa, Kihispania, Kiholanzi, Kiingereza, Kiitaliano, na Kijerumani, kutia ndani tafsiri fulani za Kilatini. Watu wowote waliotaka kusoma Biblia waliambiwa wapate idhini iliyoandikwa kutoka kwa maaskofu au watesaji—jambo ambalo hakuna mtu angetaka kufanya kwani angeshukiwa kuwa mzushi.
Watu waliojaribu kumiliki au kugawa Biblia katika lugha za kawaida katika eneo lao walilazimika kukabiliana na hasira ya Kanisa Katoliki. Wengi walikamatwa, wakateketezwa kwenye mti ulio wima au juu ya mti uliolazwa, wakahukumiwa kifungo cha maisha, au wakapelekwa kwenye meli wakafanye kazi ngumu ya kupiga makasia. Biblia zilizokusanywa ziliteketezwa. Makasisi Wakatoliki waliendelea kukusanya na kuteketeza Biblia hadi kufikia karne ya 20.
-