-
Kwa Nini Uichunguze Biblia?Biblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Kwa Nini Uichunguze Biblia?
Je, wewe unaifahamu Biblia? Hakuna kitabu kingine chochote katika historia ambacho kimesambazwa sana kama Biblia. Ujumbe wake umewafariji na kuwapa tumaini watu wa tamaduni zote, nao wamefaidika na mashauri yake maishani. Hata hivyo, watu wengi leo hawaijui Biblia vizuri. Iwe wewe ni mfuasi wa dini fulani au sivyo, huenda kuna mambo fulani ambayo ungependa kujua kuhusu Biblia. Broshua hii imekusudiwa kukusaidia kupata picha ya ujumla kuhusu Biblia.
KABLA ya kuchukua Biblia na kuanza kuisoma, ingefaa kujua mpangilio wake. Biblia, ambayo pia huitwa Maandiko Matakatifu, ni mkusanyo wa vitabu au sehemu 66, kuanzia Mwanzo mpaka Ufunuo.
Biblia ilitungwa na nani? Hilo ni swali ambalo limewasumbua watu wengi. Ukweli ni kwamba Maandiko hayo yaliandikwa na wanaume wapatao 40 katika kipindi cha miaka 1,600 hivi. Hata hivyo, wanaume hao hawakudai kamwe kuwa watungaji wa Biblia. Mmoja wao aliandika: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Mwandikaji mwingine alisema: “Roho ya Yehova ndiyo iliyosema kupitia mimi, na neno lake lilikuwa kwenye ulimi wangu.” (2 Samweli 23:2) Kulingana na waandikaji hao, Yehova Mungu ndiye Mtungaji wa Biblia naye anataka kuwa na uhusiano wa karibu na wanadamu.
Kuna jambo lingine muhimu linalohitajika ili kuielewa Biblia. Biblia ina ujumbe mmoja wa msingi: kutetewa kwa haki ya Mungu ya kuwatawala wanadamu kupitia Ufalme wa mbinguni. Katika broshua hii, utaona jinsi ujumbe huo unavyojitokeza kuanzia kitabu cha Mwanzo mpaka Ufunuo.
Ukiwa na hayo akilini, sasa chunguza ujumbe ulio katika kitabu maarufu zaidi ulimwenguni, Biblia.
-
-
Muumba Ampa Mwanadamu ParadisoBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 1
Muumba Ampa Mwanadamu Paradiso
Mungu aumba ulimwengu na viumbe; aumba mwanamume na mwanamke wakamilifu, awaweka katika bustani nzuri, na kuwapa amri wanazopaswa kutii
“HAPO mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Maneno hayo yamesemwa kuwa maneno maarufu zaidi ya ufunguzi ambayo yamepata kuandikwa. Katika maneno hayo rahisi lakini yenye kujaa maana, Biblia inamtambulisha mhusika mkuu wa Maandiko Matakatifu—Mungu mweza-yote, Yehova. Mstari huo wa kwanza wa Biblia unafunua kwamba Mungu ndiye Muumba wa ulimwengu wote kutia ndani dunia yetu. Mistari inayofuata inaeleza kwamba katika vipindi virefu vya wakati, vinavyoitwa siku, Mungu alitayarisha makao yetu hapa duniani, akitokeza vitu vyote vya ajabu vilivyo katika ulimwengu.
Mwanadamu ndiye kiumbe kikuu zaidi duniani alichoumba Mungu. Aliumbwa katika mfano wa Mungu—akiwa na uwezo wa kuonyesha sifa za Yehova mwenyewe, kama vile upendo na hekima. Mungu alimuumba mwanadamu kutoka katika mavumbi ya dunia, na kumwita Adamu. Kisha, akamweka katika paradiso—bustani ya Edeni. Mungu mwenyewe ndiye aliyetayarisha bustani hiyo na kuweka miti yenye kupendeza ya matunda.
Mungu aliona kwamba mwanamume huyo anahitaji mwenzi. Akitumia ubavu wa Adamu, Mungu alimfanyiza mwanamke na kumleta kwa mwanamume huyo ili awe mke wake. Mwanamke huyo aliitwa Hawa. Akiwa na shangwe kubwa, Adamu akasema kishairi: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu.” Mungu akaeleza: “Ndiyo sababu mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.”—Mwanzo 2:22-24; 3:20.
Mungu aliwapa Adamu na Hawa amri mbili. Kwanza, aliwaagiza walime na kutunza makao yao ya kidunia na hatimaye kuijaza dunia. Pili, aliwaambia wasile tunda la mti mmoja tu katika bustani yote hiyo, “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwanzo 2:17) Ikiwa wangekosa kutii, wangekufa. Kupitia amri hizo, Mungu alimpa mwanamume na mwanamke huyo njia ya kuonyesha kwamba wanamkubali kuwa Mtawala wao. Pia, kutii kwao kungeonyesha upendo na shukrani zao. Hawakuwa na sababu yoyote ya kuukataa utawala wake wenye fadhili. Wanadamu hao wakamilifu hawakuwa na kasoro yoyote. Biblia inatuambia: “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.”—Mwanzo 1:31.
—Inatoka kwenye Mwanzo sura ya 1 na 2.
-
-
Paradiso YapoteaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 2
Paradiso Yapotea
Malaika mwasi amchochea mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, waukatae utawala wa Mungu. Dhambi na kifo zaingia ulimwenguni
MUDA mrefu kabla ya kuwaumba wanadamu, Mungu aliumba viumbe wengi wa kiroho wasioonekana—malaika. Katika bustani ya Edeni, malaika mwasi, ambaye baadaye alikuja kuitwa Shetani Ibilisi, alimshawishi kwa hila Hawa ale tunda la ule mti ambao Mungu alikuwa amewakataza.
Akimtumia nyoka kuzungumza, Shetani alidai kwamba Mungu alikuwa akimnyima mwanamke huyo na mume wake kitu fulani chenye kutamanika. Malaika huyo alimwambia Hawa kwamba yeye na mume wake wakila tunda hilo hawatakufa. Hivyo, Shetani alidai kwamba Mungu aliwadanganya watoto wake wa kibinadamu. Mdanganyi huyo alifanya ionekane kana kwamba kumwasi Mungu ni jambo lenye kupendeza ambalo lingewapa ujuzi na uhuru mwingi zaidi. Huo ulikuwa uwongo, uwongo wa kwanza duniani. Suala kuu lilikuwa enzi au utawala wa Mungu—iwapo Mungu ana haki ya kutawala na ikiwa anaitumia ifaavyo.
Hawa alimwamini Shetani. Akaanza kutamani tunda hilo, kisha akala sehemu yake. Baadaye akampa mume wake, naye pia akala. Hivyo wakawa watenda-dhambi. Tendo hilo lililoonekana kuwa dogo lilikuwa uasi. Kwa kukataa kimakusudi kutii amri ya Mungu, Adamu na Hawa waliukataa utawala wa Muumba aliyekuwa amewapa kila kitu, kutia ndani uhai mkamilifu.
“Atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.”—Mwanzo 3:15
Mungu aliwahukumu waasi hao. Alitabiri Uzao au Mkombozi aliyeahidiwa ambaye angemharibu Shetani, anayewakilishwa na nyoka. Kwa kutotekeleza hukumu ya kifo papo hapo, Mungu aliwaonyesha rehema wazao wa Adamu na Hawa ambao hawakuwa wamezaliwa. Watoto hao wangekuwa na tumaini kwa kuwa Yule ambaye Mungu angemtuma, angeondolea mbali madhara ya uasi huo katika Edeni. Hatua kwa hatua, kadiri Biblia ilivyoendelea kuandikwa, ilijulikana wazi Mwokozi huyo ni nani, na jinsi atakavyotimiza kusudi la Mungu.
Mungu alimfukuza Adamu na Hawa kutoka katika Paradiso. Walilazimika kutoa jasho na kuchoka ili kujiruzuku nje ya bustani ya Edeni. Kisha Hawa akawa mja-mzito na kumzaa Kaini, mtoto wa kwanza wa Adamu na Hawa. Wazazi hao wa kwanza walipata wana na mabinti wengine, kutia ndani Abeli na Sethi, babu ya Noa.
—Inatoka kwenye Mwanzo sura ya 3 mpaka 5; Ufunuo 12:9.
-
-
Wanadamu Waokoka GharikaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 3
Wanadamu Waokoka Gharika
Mungu auharibu ulimwengu mwovu; amwokoa Noa na familia yake
WANADAMU walipozidi kuongezeka, dhambi na uovu zilizidi duniani. Enoko, nabii aliyekuwa peke yake, alionya kwamba siku moja Mungu atawaharibu waovu. Hata hivyo, uovu ulizidi. Malaika fulani walimwasi Yehova kwa kuacha makao yao mbinguni, wakajivika miili ya kibinadamu, wakaja duniani na kujitwalia wanawake kuwa wake zao. Mahusiano hayo yasiyo ya kawaida yalitokeza Wanefili, majitu yenye kukandamiza yaliyozidisha jeuri na umwagaji damu duniani. Mungu alihuzunika sana kuona uumbaji wake ukiharibiwa.
Baada ya kifo cha Enoko, kuna mtu mmoja aliyekuwa tofauti kabisa na ulimwengu mwovu uliomzunguka. Aliitwa Noa. Yeye na familia yake walijitahidi kufanya yaliyo sawa machoni pa Mungu. Mungu aliamua kuwaharibu waovu. Hata hivyo, hakutaka kumwangamiza Noa na wanyama pamoja nao. Kwa hiyo Mungu akamwambia ajenge safina—chombo kikubwa chenye umbo la sanduku. Humo, Noa na familia yake wangehifadhiwa wakiwa hai, pamoja na wanyama wa aina mbalimbali, na kuokoka gharika ya dunia nzima. Noa alimtii Mungu. Kwa makumi ya miaka ambayo Noa alijenga safina hiyo, alikuwa pia “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Aliwaonya watu kuhusu Gharika iliyokuwa ikikaribia, lakini wakampuuza. Wakati ulipofika, Noa na familia yake wakaingia katika safina pamoja na wanyama. Mungu akaufunga mlango wa safina. Mvua ikanyesha.
Mvua ikamwagika bila kukoma kwa siku 40, mchana na usiku, mpaka dunia yote ikafunikwa. Waovu wote wakaangamia. Miezi kadhaa baadaye, maji yalipopungua, safina ikatua juu ya mlima. Kufikia wakati ambapo Noa na familia yake pamoja na wanyama wangeweza kutoka nje ya safina, mwaka mzima ulikuwa umepita. Noa alionyesha shukrani zake kwa kumtolea Yehova toleo. Mungu alikubali toleo hilo na kumhakikishia Noa na familia yake kwamba hataleta tena gharika ili kuondolea mbali kila kitu chenye uhai kutoka katika uso wa dunia. Yehova aliandaa upinde wa mvua uwe ishara ya kuwakumbusha ahadi hiyo yenye kufariji.
Baada ya Gharika, Mungu aliwapa wanadamu amri kadhaa mpya. Aliwaruhusu kula nyama za wanyama. Hata hivyo aliwakataza wasile damu. Pia aliwaamuru wazao wa Noa waijaze dunia, lakini baadhi yao wakaasi. Watu walijiunga na Nimrodi katika uasi nao wakaanza kujenga mnara mkubwa katika jiji la Babeli, ambalo baadaye lilikuja kuitwa Babiloni. Lengo lao lilikuwa kukaidi amri ya Mungu ya kuijaza dunia. Hata hivyo, Mungu alivunja mipango ya waasi hao kwa kuvuruga lugha yao moja na kuwafanya wazungumze lugha mbalimbali. Kwa kuwa hawakuweza kuwasiliana, waliuacha mradi huo na kutawanyika.
—Inatoka kwenye Mwanzo sura ya 6 hadi 11; Yuda 14, 15.
-
-
Mungu Afanya Agano na AbrahamuBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 4
Mungu Afanya Agano na Abrahamu
Abrahamu aonyesha imani kwa kumtii Mungu; Yehova aahidi kumbariki na kuzidisha uzao wake
MIAKA 350 baada ya Gharika ya siku za Noa, Abrahamu alikuwa akiishi katika jiji lenye ufanisi la Uru, eneo ambalo leo linaitwa Iraki. Abrahamu alikuwa mtu mwenye imani ya pekee. Hata hivyo imani yake ilijaribiwa.
Yehova alimwambia Abrahamu aondoke katika nchi alimozaliwa na kwenda nchi asiyoijua, nchi ya Kanaani. Abrahamu alitii bila kusita. Alikusanya watu wa nyumba yake, kutia ndani mke wake, Sara, na mpwa wake Loti, akafunga safari ndefu na kwenda kuishi katika mahema huko Kanaani. Katika agano alilofanya pamoja na Abrahamu, Yehova alimwahidi kwamba atamfanya kuwa taifa kubwa, na kwamba familia zote za dunia zitajibariki kupitia kwake, nao uzao wake utaimiliki nchi ya Kanaani.
Abrahamu na Loti walipata ufanisi, wakajikusanyia kondoo na ng’ombe wengi. Abrahamu alimtanguliza Loti kwa kumpa nafasi achague eneo analotaka. Loti alichagua mkoa wenye rutuba wa Mto Yordani na kwenda kukaa karibu na jiji la Sodoma. Lakini, watu wa Sodoma walikuwa wapotovu kiadili—watenda-dhambi nzito mbele za Yehova.
Yehova Mungu alimhakikishia Abrahamu baadaye kwamba uzao wake ungeongezeka na kuwa kama nyota za mbinguni. Abrahamu aliamini ahadi hiyo. Hata hivyo, Sara, mke wake mpendwa hakuwa na mtoto. Kisha, Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 99, naye Sara akikaribia umri wa miaka 90, Mungu alimwambia Abrahamu kwamba Sara atapata mtoto. Maneno ya Mungu yalitimia. Sara akamzaa Isaka. Abrahamu alikuwa na watoto wengine, hata hivyo, yule Mkombozi aliyeahidiwa katika Edeni angetokana na ukoo wa Isaka.
Wakati huohuo, Loti na familia yake walikuwa wakiishi Sodoma, lakini Loti hakuwa kama wakaaji wa jiji hilo waliokuwa na maadili mapotovu. Yehova alipoamua kutekeleza hukumu juu ya Sodoma, aliwatuma malaika wawili wakamwonye Loti kuhusu uharibifu uliokuwa ukikaribia. Malaika hao walimhimiza Loti na familia yake wakimbie kutoka Sodoma na wasitazame nyuma. Kisha Mungu akanyesha mvua ya moto na kiberiti juu ya Sodoma na jiji jirani la Gomora lililojaa uovu. Wakaaji wote wa majiji hayo wakaangamia. Loti na binti zake wawili waliokoka. Mke wa Loti alitazama nyuma, huenda akitamani vitu alivyokuwa ameviacha. Kutotii huko kulimfanya apoteze uhai wake.
—Inatoka kwenye Mwanzo 11:10–19:38.
-
-
Mungu Ambariki Abrahamu na Familia YakeBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 5
Mungu Ambariki Abrahamu na Familia Yake
Wazao wa Abrahamu wapata ufanisi. Mungu amlinda Yosefu nchini Misri
YEHOVA alijua kwamba kuna wakati ambapo mwana wake mpendwa atateseka na kufa. Unabii uliorekodiwa katika Mwanzo 3:15 ulidokeza hilo. Je, Mungu angeweza kuwasaidia wanadamu waelewe jinsi kifo cha mwana wake kingemhuzunisha? Biblia ina mfano halisi uliotokea. Mungu alimwagiza Abrahamu amtoe dhabihu Isaka mwana wake mpendwa.
Abrahamu alikuwa na imani kubwa. Kumbuka kwamba Mungu alikuwa ameahidi kwamba Mkombozi, au Uzao ulioahidiwa, angetokea katika ukoo wa Isaka. Akiwa na imani kwamba Mungu atamfufua Isaka ikihitajika, Abrahamu alikuwa tayari kutii na kumtoa mwana wake mwenyewe awe dhabihu. Lakini malaika wa Mungu akamzuia Abrahamu dakika ya mwisho. Akimsifu Abrahamu kwa nia yake ya kumtolea Mungu kitu kilichokuwa na thamani zaidi kwake, Mungu alirudia ahadi Yake aliyokuwa amemtolea.
Baadaye, Isaka alipata wana wawili, Esau na Yakobo. Tofauti na Esau, Yakobo alithamini mambo ya kiroho naye akathawabishwa. Mungu alibadili jina la Yakobo likawa Israeli, na wana 12 wa Israeli wakawa vichwa vya makabila ya Israeli. Lakini familia hiyo ilipataje kuwa taifa kubwa?
Mambo yalianza wakati ambapo wengi kati ya wana hao walianza kumwonea kijicho Yosefu, ndugu yao mdogo. Walimuuza utumwani, naye akapelekwa Misri. Hata hivyo Mungu alimbariki kijana huyo mwenye ujasiri. Ijapokuwa alikabili hali ngumu, Yosefu aliteuliwa na Farao, mtawala wa Misri, na kupewa mamlaka kubwa. Hilo lilitokea wakati barabara, kwa kuwa njaa kali ilimfanya Yakobo awatume baadhi ya wana wake waende Misri kununua vyakula—naye Yosefu ndiye aliyekuwa akisimamia ugawanyaji wa chakula! Baada ya kuungana tena na ndugu zake wenye toba, Yosefu aliwasamehe na kupanga familia nzima ihamie Misri. Walipewa eneo zuri sana, ambapo wangeweza kukaa na kupata ufanisi. Yosefu alielewa kwamba Mungu alikuwa ameelekeza mambo hivyo ili atimize ahadi Zake.
Yakobo alimalizia maisha yake huko Misri, akiwa na familia yake iliyokuwa ikizidi kuongezeka. Alipokuwa akikaribia kufa, alitabiri kwamba Mkombozi, au Uzao ulioahidiwa, angekuwa Mtawala mwenye nguvu ambaye angezaliwa katika ukoo wa mwana wake Yuda. Kabla hajafa miaka kadhaa baadaye, Yosefu alitabiri kwamba siku moja, Mungu angeitoa familia ya Yakobo nchini Misri.
—Inatoka kwenye Mwanzo sura ya 20 hadi 50; Waebrania 11:17-22.
-
-
Ayubu Adumisha UtimilifuBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 6
Ayubu Adumisha Utimilifu
Shetani atilia shaka utimilifu wa Ayubu mbele za Mungu, lakini Ayubu abaki mwaminifu kwa Yehova
JE, MWANADAMU yeyote angeweza kuendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu ikiwa angejaribiwa vya kutosha na iwapo ingeonekana kana kwamba kuendelea kwake kumtii Mungu hakuna faida yoyote? Swali hilo lilitokezwa—na kujibiwa—katika kisa cha mtu anayeitwa Ayubu.
Waisraeli walipokuwa wangali Misri, Ayubu, mtu wa jamaa ya Abrahamu, alikuwa akiishi katika eneo ambalo leo ni Uarabuni. Wakati huohuo, malaika mbinguni walikusanyika mbele za Mungu, na yule mwasi, Shetani, alikuwa katikati yao. Katika mkutano huo huko mbinguni, Yehova alimsifu mtumishi wake mwaminifu Ayubu. Alisema kwamba hakuna mwanadamu mwingine yeyote aliye na utimilifu kama wa Ayubu. Lakini Shetani alisisitiza kwamba Ayubu anamtumikia Mungu kwa sababu Mungu anambariki na kumlinda. Shetani alidai kwamba ikiwa Ayubu angenyang’anywa kila kitu alichokuwa nacho, angemlaani Mungu.
Kwanza, Mungu alimruhusu Shetani amnyang’anye Ayubu mali yake na watoto wake, kisha aingilie afya yake. Kwa kuwa Ayubu hakujua Shetani anahusika, hakuelewa ni kwa nini Mungu anaruhusu apatwe na mambo yote hayo. Hata hivyo, Ayubu hakumkana Mungu kamwe.
Marafiki watatu bandia walimjia Ayubu. Walisema mengi wakijaribu kumsadikisha eti Mungu anamhukumu kwa sababu ya dhambi alizofanya kisiri. Hata walidai kwamba Mungu hapendezwi na watumishi wake wala hana imani nao. Ayubu alikataa maoni yao yenye kosa. Akiwa na uhakika, Ayubu alitangaza kwamba atadumisha utimilifu wake mpaka kifo!
Hata hivyo, Ayubu alikosea kwa kutaka sana kuonyesha kwamba hana kosa lolote. Kijana anayeitwa Elihu, ambaye alikuwa akisikiliza mjadala wote huo, akaanza kuzungumza. Elihu alimkaripia Ayubu kwa kutotambua kwamba kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova Mungu ni muhimu kuliko kutetewa kwa mwanadamu yeyote. Pia aliwakaripia vikali rafiki watatu bandia wa Ayubu.
Kisha Yehova Mungu akazungumza na Ayubu, akirekebisha maoni yake. Akitaja uumbaji mbalimbali wa ajabu, Yehova alimsaidia Ayubu kuona jinsi mwanadamu alivyo duni kwa kulinganishwa na ukuu wa Mungu. Ayubu alikubali nidhamu hiyo kutoka kwa Mungu. Kwa kuwa Yehova ni “mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema,” alimponya Ayubu, akampa maradufu mali aliyokuwa nayo, na kumbariki kwa wana wengine kumi. (Yakobo 5:11) Kwa kudumisha utimilifu wake kwa Yehova chini ya jaribu kali, Ayubu alitoa jibu tosha kwa dai la Shetani kwamba wanadamu hawawezi kuwa waaminifu kwa Mungu wakijaribiwa.
—Inatoka kwenye Kitabu cha Ayubu.
-
-
Mungu Awakomboa Wana wa IsraeliBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 7
Mungu Awakomboa Wana wa Israeli
Yehova aleta mapigo juu ya Misri, na Musa awaongoza wana wa Israeli kutoka katika nchi hiyo. Mungu awapa Waisraeli Sheria kupitia Musa
WANA wa Israeli waliishi Misri kwa miaka mingi, wakizidi kuongezeka na kupata ufanisi. Hata hivyo, Farao mpya alitokea. Mtawala huyo hakumjua Yosefu. Mtawala huyo mkatili aliyehofu idadi inayozidi kuongezeka ya Waisraeli, aliwafanya kuwa watumwa na kuagiza wazaliwa wote wa kwanza wa kiume wauawe kwa kutupwa katika Mto Nile. Lakini mama mmoja mwenye ujasiri alimhifadhi mwana wake mchanga, akamweka katika kikapu na kumficha katikati ya matete. Binti ya Farao alimpata mtoto huyo, akamwita Musa, na kumlea katika nyumba ya kifalme ya Misri.
Musa alipokuwa na umri wa miaka 40, alijikuta taabani alipompiga Mmisri aliyekuwa akimpiga mtumwa Mwisraeli. Musa alikimbilia nchi ya mbali, alikoishi uhamishoni. Musa alipokuwa na umri wa miaka 80, Yehova alimtuma arudi Misri, asimame mbele ya Farao na kudai watu wa Mungu waachiliwe.
Farao alikataa katakata. Kwa hiyo Mungu akaleta mapigo kumi juu ya Misri. Kila mara Musa aliposimama mbele ya Farao na kumpa nafasi ya kuepuka pigo linalofuata, Farao alikuwa mkaidi, na kumwonyesha Musa na Mungu wake, Yehova, dharau. Mwishowe, pigo la kumi lilitokeza kifo cha wazaliwa wote wa kwanza nchini—isipokuwa wale wa familia zilizomtii Yehova kwa kutia alama miimo ya milango yao kwa damu ya mwana-kondoo aliyetolewa dhabihu. Malaika wa Mungu aliyetumwa kuwaangamiza wazaliwa wote wa kwanza alipita nyumba zilizokuwa na alama. Baadaye Waisraeli walifanya maadhimisho ya kila mwaka yanayoitwa Pasaka ili kukumbuka ukombozi huo wa pekee.
Baada ya kumpoteza mwana wake mwenyewe mzaliwa wa kwanza, Farao aliagiza Musa na Waisraeli wengine wote waondoke Misri. Mara moja wakapanga umati huo mkubwa uondoke Misri. Lakini Farao akabadili nia. Akawafuata akiwa na askari wengi na magari ya vita. Ilionekana kana kwamba Waisraeli hawana pa kwenda kwa kuwa walikuwa katika ufuo wa Bahari Nyekundu. Yehova alitenganisha maji ya Bahari Nyekundu, na hivyo Waisraeli wakapita katika sakafu kavu ya bahari, katikati ya kuta za maji! Wamisri walipoingia wakiwafuata, Mungu aliyaachilia yale maji, yakarudi kwa kishindo na kumfunika Farao pamoja na jeshi lake.
Baadaye, Waisraeli walipopiga kambi katika Mlima Sinai, Yehova alifanya agano pamoja nao. Akimtumia Musa kuwa mpatanishi, Mungu aliwapa Waisraeli sheria za kuwaongoza na kuwalinda katika nyanja zote maishani. Maadamu Waisraeli wangeukubali kabisa utawala wa Mungu, Yehova angekuwa pamoja nao na kulifanya taifa hilo kuwa baraka kwa wengine.
Hata hivyo, inasikitisha kwamba Waisraeli wengi hawakumwamini Mungu. Kwa hiyo, Yehova akafanya kizazi hicho kitange-tange nyikani kwa miaka 40. Kisha, Musa akamteua Yoshua, aliyekuwa mtu mnyoofu, achukue mahali pake. Hatimaye, taifa la Israeli likakaribia kuingia nchi ambayo Mungu alimwahidi Abrahamu.
—Inatoka kwenye Kutoka; Mambo ya Walawi; Hesabu; Kumbukumbu la Torati; Zaburi 136:10-15; Matendo 7:17-36.
-
-
Waisraeli Waingia KanaaniBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 8
Waisraeli Waingia Kanaani
Waisraeli waitwaa nchi ya Kanaani wakiongozwa na Yoshua. Yehova atumia waamuzi kuwakomboa watu wake kutoka mikononi mwa adui zao
KARNE nyingi kabla ya Waisraeli kuingia Kanaani, Yehova alikuwa ameahidi kwamba wazao wa Abrahamu wangeimiliki nchi hiyo. Wakiongozwa na Yoshua, sasa Waisraeli wako tayari kuimiliki Nchi ya Ahadi.
Mungu aliamua Wakanaani wanastahili kuangamizwa. Walikuwa wameijaza nchi mazoea machafu ya ngono na umwagaji wa damu kimakusudi. Hivyo, majiji ya Kanaani yaliyokuwa yametwaliwa na Waisraeli yalipaswa kuharibiwa kabisa.
Hata hivyo, kabla ya kuingia nchi hiyo, Yoshua aliwatuma wapelelezi wawili. Wapelelezi hao walikaa katika nyumba ya Rahabu jijini Yeriko. Rahabu aliwapokea na kuwalinda, ingawa alijua ni Waisraeli. Rahabu alimwamini Mungu wa Waisraeli kwa sababu alikuwa amesikia jinsi Yehova alivyokuwa ametenda ili kuwakomboa watu wake. Aliwaambia wapelelezi hao wamwapie kwamba yeye na watu wa nyumba yake hawataangamizwa.
Baadaye, Waisraeli walipoingia Kanaani na kulizunguka Yeriko, Yehova aliangusha kuta za Yeriko kimuujiza. Vikosi vya Yoshua vikaingia ndani na kuliharibu jiji hilo, hata hivyo, Rahabu na familia yake hawakuangamizwa. Kisha, kwa miaka sita tu, Yoshua akatwaa sehemu kubwa ya Nchi ya Ahadi. Baadaye, makabila ya Israeli yakagawiwa nchi hiyo.
Akikaribia mwisho wa utumishi wake wa muda mrefu kwa Mungu, Yoshua aliwakusanya watu pamoja. Akawaambia jinsi Yehova alivyoshughulika na babu zao, kisha akawatia moyo wamtumikie Yehova. Hata hivyo, baada ya Yoshua na wanaume wazee kufa, Waisraeli walimwacha Yehova, wakaanza kutumikia miungu ya uwongo. Kwa miaka 300 hivi, taifa hilo halikushikamana kabisa na sheria za Yehova. Wakati huo, Yehova aliruhusu Waisraeli wakandamizwe na adui zao, kama vile Wafilisti. Lakini Waisraeli walipomwomba Yehova msaada, aliweka rasmi jumla ya waamuzi 12 wawakomboe.
Kipindi cha Waamuzi wanaotajwa katika kitabu cha Waamuzi kilianza siku za Othnieli mpaka siku za Samsoni, mwanadamu mwenye nguvu zaidi aliyepata kuishi. Ukweli wa msingi unaothibitishwa tena na tena katika masimulizi yenye kusisimua ya kitabu cha Biblia cha Waamuzi ni: Kumtii Yehova huleta baraka, kutotii huleta msiba.
—Inatoka kwenye Yoshua; Waamuzi; Mambo ya Walawi 18:24, 25.
-
-
Waisraeli Wataka MfalmeBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 9
Waisraeli Wataka Mfalme
Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli, akosa kutii. Daudi, ambaye Mungu afanya pamoja naye agano la ufalme wa kudumu, atawala baada yake
BAADA ya siku za Samsoni, Samweli alikuwa nabii na mwamuzi katika taifa la Israeli. Waisraeli walikuwa wakimwambia kwamba wanataka kuwa kama mataifa mengine, na kuwa na mfalme wa kibinadamu. Ijapokuwa ombi hilo halikumpendeza Yehova, alimwagiza Samweli alitekeleze. Mungu alimchagua mwanamume mnyenyekevu anayeitwa Sauli awe mfalme. Hata hivyo, baada ya muda, Mfalme Sauli alibadilika na kuwa mwenye kiburi na mkaidi. Yehova alimkataa na kumwambia Samweli amteue mwingine—kijana anayeitwa Daudi. Hata hivyo, miaka kadhaa ilipita kabla ya Daudi kuanza kutawala.
Yamkini akiwa katika miaka ya utineja, Daudi aliwatembelea ndugu zake waliokuwa katika jeshi la Sauli. Jeshi zima lilikuwa limebabaishwa na askari mmoja adui, jitu linaloitwa Goliathi, lililokuwa likimdhihaki Mungu wao. Akiwa na ghadhabu, Daudi alijitolea kupigana na jitu hilo. Akiwa na kombeo na mawe matano, kijana huyo alikwenda kukutana na mpinzani wake, aliyekuwa na urefu wa karibu mita tatu. Goliathi alipomdhihaki, Daudi alijibu kwamba amejihami kuliko jitu hilo kwa kuwa anapigana kwa jina la Yehova Mungu! Daudi alilipiga na kuliangusha jitu hilo kwa jiwe moja tu kisha akauchukua upanga wa jitu hilo na kulikata kichwa. Jeshi la Wafilisti likakimbia kwa hofu.
Mwanzoni, Sauli alipendezwa sana na ujasiri wa Daudi na kumweka aongoze jeshi lake. Hata hivyo, mafanikio ya Daudi yalimfanya Sauli awe na wivu mbaya. Daudi alilazimika kukimbia aokoe uhai wake. Aliishi akiwa mkimbizi kwa miaka mingi. Hata hivyo, Daudi alibaki mshikamanifu kwa Sauli aliyekuwa akijaribu kumuua, akijua kwamba Mfalme Sauli aliwekwa na Yehova Mungu. Hatimaye, Sauli akafa vitani. Muda mfupi baadaye, Daudi akatawazwa, kama vile Yehova alivyokuwa ameahidi.
“Nitakifanya imara kiti cha ufalme wake mpaka wakati usio na kipimo.”—2 Samweli 7:13
Akiwa mfalme, Daudi alitamani sana kumjengea Yehova hekalu. Lakini Yehova akamwambia Daudi kwamba mmoja wa wazao wake ndiye atakayefanya hivyo. Mzao aliyepata pendeleo hilo ni Sulemani, mwana wa Daudi. Hata hivyo, Mungu alimthawabisha Daudi kwa kufanya pamoja naye agano lenye kusisimua: Familia yake ingetokeza ukoo wa kifalme usio na kifani. Hatimaye, Mkombozi, au Uzao ulioahidiwa katika shamba la Edeni ungetokea kupitia ukoo huo. Mkombozi huyo angekuwa Masihi, yaani, “Mtiwa Mafuta,” aliyewekwa rasmi na Mungu. Yehova aliahidi kwamba Masihi huyo angekuwa Mtawala wa Ufalme au serikali ambayo ingedumu milele.
Akiwa na shukrani nyingi, Daudi alikusanya vifaa vingi sana vya ujenzi na madini ya thamani kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa hekalu. Pia, aliongozwa na roho kuandika zaburi nyingi. Alipokuwa akikaribia kufa, Daudi alikiri hivi: “Roho ya Yehova ndiyo iliyosema kupitia mimi, na neno lake lilikuwa kwenye ulimi wangu.”—2 Samweli 23:2.
—Inatoka kwenye 1 Samweli; 2 Samweli; 1 Nyakati; Isaya 9:7; Mathayo 21:9; Luka 1:32; Yohana 7:42.
-
-
Sulemani Atawala kwa HekimaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
SEHEMU YA 10
Sulemani Atawala kwa Hekima
Yehova ampa Mfalme Sulemani moyo wa hekima; wakati wa utawala wa Sulemani, Waisraeli waishi kwa amani na ufanisi usio na kifani
MAISHA yangekuwaje ikiwa taifa zima na mtawala wake wangemtambua Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu na kutii sheria Zake? Ndivyo ilivyokuwa wakati wa utawala wa miaka 40 ya Mfalme Sulemani.
Kabla ya Daudi kufa, alimteua Sulemani atawale baada yake. Katika ndoto, Mungu alimwambia Sulemani aombe anachotaka. Sulemani aliomba hekima na ujuzi wa kuwahukumu watu kwa haki na busara. Yehova alipendezwa na jibu lake naye akampa Sulemani moyo wenye hekima na uelewaji. Pia, Yehova alimwahidi utajiri, utukufu, na maisha marefu maadamu angeendelea kuwa mtiifu.
Sulemani alipata umaarufu kwa sababu ya hekima yake katika kuhukumu. Katika kisa kimoja, wanawake wawili walikuwa wakibishania mtoto mvulana, kila mmoja akidai kuwa mama yake. Sulemani aliagiza mtoto huyo akatwe vipande viwili na kila mwanamke apewe nusu ya mtoto huyo. Mwanamke wa kwanza akakubali, lakini mara moja mama halisi ya mtoto huyo akaanza kusihi mtoto huyo akabidhiwe mwanamke yule mwingine. Sulemani akaona wazi kwamba mwanamke mwenye huruma ndiye mama ya mtoto huyo, akamkabidhi. Muda si muda taifa zima la Israeli likasikia kuhusu uamuzi huo wa kihukumu, na watu wakatambua kwamba Sulemani ana hekima kutoka kwa Mungu.
Mojawapo ya mafanikio makuu ya Sulemani ni ujenzi wa hekalu la Yehova—jengo lenye fahari jijini Yerusalemu ambalo lingekuwa kituo cha ibada katika taifa la Israeli. Wakati wa kuzinduliwa kwa hekalu hilo, Sulemani alisali hivi: “Tazama! Mbingu, ndiyo, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha; jinsi gani basi, nyumba hii ambayo nimeijenga!”—1 Wafalme 8:27.
Sifa za Sulemani zilifika katika nchi za mbali, hata kufikia Sheba, Uarabuni. Malkia wa Sheba alisafiri kwenda kuuona utukufu na utajiri wa Sulemani, na kupima hekima yake. Malkia huyo alivutiwa sana na hekima ya Sulemani na ufanisi wa taifa la Israeli hivi kwamba akamsifu Yehova kwa kumtawaza mfalme mwenye hekima hivyo. Kwa kweli, Yehova aliubariki utawala wa Sulemani, nao ukawa utawala wenye ufanisi na amani zaidi katika historia yote ya taifa la kale la Israeli.
Kwa kusikitisha, Sulemani hakuendelea kutenda kulingana na hekima ya Yehova. Alipuuza amri ya Mungu, akaoa mamia ya wanawake, kutia ndani wengi waliokuwa wakiabudu miungu ya kigeni. Pole kwa pole wake zake wakaugeuza moyo wake kutoka kwa Yehova, akaanza kuabudu sanamu. Yehova akamwambia Sulemani kwamba atanyang’anywa sehemu ya ufalme. Sehemu ndogo tu ndiyo ingebaki katika familia yake, kwa sababu ya ahadi ambayo Mungu alimtolea Daudi, baba ya Sulemani. Licha ya kutotii kwa Sulemani, Yehova aliendelea kuwa mshikamanifu kwa agano la Ufalme alilofanya na Daudi.
—Inatoka kwenye 1 Wafalme, sura ya 1 hadi 11; 2 Nyakati, sura ya 1 hadi 9; Kumbukumbu la Torati 17:17.
-
-
Nyimbo Zilizoongozwa na Roho Ambazo Zinafariji na KufundishaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 11
Nyimbo Zilizoongozwa na Roho Ambazo Zinafariji na Kufundisha
Daudi na wengine watunga nyimbo kwa ajili ya ibada. Kitabu cha Zaburi kina nyimbo 150
KITABU kikubwa zaidi katika Biblia ni mkusanyo wa nyimbo takatifu. Kitabu hicho kilichukua miaka 1,000 hivi kuandikwa. Kitabu cha Zaburi kina maneno yenye kupendeza na yenye kuchochea sana ya imani kuliko kitabu kingine chochote. Nyimbo hizo za sifa zinafunua hisia mbalimbali za wanadamu, kama vile, shangwe, shukrani, huzuni, sikitiko, na toba. Ni wazi kwamba mtunga-zaburi alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu naye alimtumaini. Fikiria baadhi ya mambo yaliyo katika nyimbo hizo.
Yehova ana haki ya kutawala, kuabudiwa na kusifiwa. Katika Zaburi 83:18 tunasoma: “Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Zaburi nyingi zinamsifu Yehova kwa kazi zake za uumbaji, kama vile mbingu zenye nyota, viumbe vya ajabu duniani, na jinsi mwanadamu alivyoumbwa kwa njia ya ajabu. (Zaburi 8, 19, 139, 148) Zaburi nyingine humtukuza Yehova kuwa Mungu ambaye huwawaokoa na kuwalinda washikamanifu wake. (Zaburi 18, 97, 138) Na katika zaburi nyingine anatajwa kuwa Mungu mwenye haki, anayewafariji walioonewa na kuwaadhibu waovu. —Zaburi 11, 68, 146.
Yehova huwasaidia na kuwafariji wanaompenda. Huenda zaburi inayojulikana sana ni ya 23. Katika zaburi hiyo, Daudi anamtaja Yehova kuwa Mchungaji mwenye upendo anayewaongoza, kuwalinda, na kuwajali kondoo wake. Zaburi 65:2 inawakumbusha waabudu wa Mungu kwamba Yehova ni “msikiaji wa sala.” Wengi ambao wametenda dhambi nzito wamefarijiwa sana na Zaburi ya 39 na ya 51. Katika zaburi hizo, Daudi anatubu kwa unyoofu dhambi nzito alizofanya nayo maneno yake yanaonyesha wazi anaamini kwamba Yehova husamehe. Zaburi 55:22 inatuhimiza tumtegemee Yehova na kumtupia mizigo yetu yote.
Yehova ataubadili ulimwengu kupitia Ufalme wa Masihi. Sehemu mbalimbali za kitabu cha Zaburi zinamhusu moja kwa moja Masihi, Mfalme aliyeahidiwa. Zaburi ya 2 inatabiri kwamba Mtawala huyo ataharibu mataifa maovu yanayompinga. Zaburi ya 72 inaonyesha kwamba Mfalme huyo ataondoa njaa, ukosefu wa haki, na uonevu. Kulingana na Zaburi 46:9, Mungu atakomesha vita na kuharibu silaha zote za vita kupitia Ufalme wa Kimasihi. Katika Zaburi ya 37, tunasoma kwamba waovu wataharibiwa, lakini waadilifu wataishi milele duniani, wakifurahia amani na upatano.
—Inatoka kwenye Kitabu cha Zaburi.
-
-
Hekima Kutoka kwa Mungu Inayotuongoza MaishaniBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 12
Hekima Kutoka kwa Mungu Inayotuongoza Maishani
Kitabu cha Methali ni hazina ya mashauri kutoka kwa Mungu yanayotupa mwongozo maishani. Nyingi za methali hizo ziliandikwa na Sulemani
JE, Yehova ni Mtawala mwenye hekima? Njia moja yenye kuridhisha ya kujibu swali hilo ni kuchunguza mashauri anayotoa. Je, yanafanya kazi? Je, kuyatumia kunafanya maisha yawe mazuri zaidi na yenye kusudi? Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika mamia ya methali. Methali hizo zinazungumzia nyanja zote za maisha. Fikiria mifano kadhaa.
Kumtegemea Mungu. Ili kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, lazima tumtegemee. Sulemani aliandika: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” (Methali 3:5, 6) Kumtegemea Mungu kwa kufuata mwongozo wake na kumtii hufanya maisha yawe na kusudi. Mtu anayefanya hivyo huufurahisha moyo wa Mungu na kumpa Yehova jibu la masuala yaliyozushwa na mpinzani Wake, Shetani.—Methali 27:11.
Kushughulika na watu wengine kwa hekima. Leo, kuliko wakati mwingine wowote, tunafaidika na shauri la Mungu kwa waume, wake, na watoto. “Ushangilie pamoja na mke wa ujana wako,” Mungu awashauri waume, akiwaagiza wawe waaminifu kwa wake zao. (Methali 5:18-20) Wanawake walioolewa wanaweza kufaidika na ufafanuzi wenye kupendeza ulio katika kitabu cha Methali kuhusu mke mwenye uwezo anayejipatia sifa kutoka kwa mumewe na watoto wake. (Methali, sura ya 31) Nao watoto wanaagizwa wawatii wazazi wao. (Methali 6:20) Kitabu hicho kinaonyesha kwamba urafiki ni muhimu, kwa kuwa kujitenga hutokeza ubinafsi. (Methali 18:1) Marafiki wanaweza kuwa na uvutano mzuri au mbaya, kwa hiyo tunapaswa kuwachagua kwa uangalifu.—Methali 13:20; 17:17.
Kujitunza kwa hekima. Kitabu cha Methali kina mashauri mazuri kuhusu kuepuka matumizi yasiyofaa ya vileo, kusitawisha hisia zinazofaa na kuondolea mbali zisizofaa, na kuwa mfanyakazi mwenye bidii. (Methali 6:6; 14:30; 20:1) Kitabu hicho kinaonya kwamba kutegemea akili ya mwanadamu na kupuuza shauri la Mungu hutokeza msiba. (Methali 14:12) Kinatuhimiza tumlinde yule mtu wa ndani, moyo wetu, dhidi ya uvutano mbalimbali usiofaa, na kutukumbusha kwamba katika moyo “ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.”—Methali 4:23.
Mamilioni ya watu ulimwenguni wamejionea kwamba kuishi kupatana na mashauri hayo hufanya maisha yawe mazuri zaidi. Kwa sababu hiyo, wana sababu nzuri ya kumkubali Yehova kuwa Mtawala wao.
—Inatoka kwenye Kitabu cha Methali.
-
-
Wafalme Wazuri na Wafalme WabayaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 13
Wafalme Wazuri na Wafalme Wabaya
Taifa la Israeli limegawanyika. Wafalme wengi watawala taifa hilo, na wengi wao si waaminifu. Yerusalemu laharibiwa na Wababiloni
KAMA Yehova alivyotabiri, kwa sababu Sulemani aliiacha ibada safi, taifa la Israeli liligawanyika. Mwana wake aliyetawala baada yake, Rehoboamu, alikuwa mkali. Kwa hiyo, makabila kumi ya Israeli yakaasi na kufanyiza ufalme wa kaskazini wa Israeli. Makabila mawili yakaendelea kuwa chini ya mtawala aliyeketi katika kiti cha ufalme cha Daudi jijini Yerusalemu, yakifanyiza ufalme wa kusini wa Yuda.
Falme zote mbili zilikuwa na misukosuko, hasa kwa sababu ya wafalme wake ambao hawakuwa watiifu. Hali ya Israeli ilikuwa mbaya kuliko ya Yuda, kwa kuwa wafalme wake waliunga mkono ibada ya uwongo tangu mwanzo. Licha ya kazi zenye nguvu za manabii kama vile Eliya na Elisha—ambao hata waliwafufua wafu—taifa la Israeli lilirudia njia mbaya tena na tena. Mwishowe, Mungu akawaruhusu Waashuru wauharibu ufalme wa kaskazini.
Ufalme wa Yuda ulidumu miaka mia moja hivi baada ya ufalme wa Israeli kuangamizwa, lakini huo pia ulihukumiwa na Mungu. Ni wafalme wachache wa Yuda waliotii maonyo ya manabii wa Mungu na kujaribu kuliongoza taifa limrudie Yehova. Kwa mfano, Mfalme Yosia alianza kusafisha Yuda, akiondolea mbali ibada ya uwongo na kurekebisha hekalu la Yehova. Nakala ya awali ya Sheria ya Mungu iliyotolewa kupitia Musa ilipopatikana, Yosia alichochewa sana naye akazidisha kampeni yake ya kufanya mabadiliko.
Hata hivyo, inasikitisha kwamba wafalme waliotawala baada ya Yosia hawakufuata mfano wake mzuri. Kwa hiyo, Yehova akaruhusu taifa la Babiloni lishinde Yuda, na kuharibu Yerusalemu pamoja na hekalu lake. Waliookoka walipelekwa uhamishoni Babiloni. Mungu alitabiri kwamba wangekaa uhamishoni kwa miaka 70. Wakati wote huo Yuda palikuwa magofu—hadi, kama ilivyotabiriwa, taifa hilo liliporuhusiwa kurudi katika nchi yao.
Hata hivyo, hakuna wafalme wowote wa ukoo wa Daudi wangetawala hadi utawala wa yule Mkombozi aliyeahidiwa, Masihi aliyetabiriwa. Utawala wa wengi kati ya wafalme walioketi katika kiti cha ufalme cha Daudi jijini Yerusalemu ulionyesha wazi kwamba wanadamu wasio wakamilifu hawastahili kutawala. Masihi tu ndiye angestahili kikweli. Hivyo, Yehova akamwambia mfalme wa mwisho katika ukoo huo wa Daudi: ‘Livue taji. Hakika hili halitakuwa la mtu yeyote mpaka atakapokuja yule aliye na haki ya kisheria, nami nitampa yeye.’—Ezekieli 21:26, 27.
—Inatoka kwenye 1 Wafalme; 2 Wafalme; 2 Nyakati, sura ya 10 hadi 36; Yeremia 25:8-11.
-
-
Mungu Asema Kupitia Manabii WakeBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 14
Mungu Asema Kupitia Manabii Wake
Manabii wawekwa na Yehova watangaze ujumbe kuhusu hukumu, ibada safi, na tumaini la Kimasihi
WAKATI wa wafalme wa Israeli na Yuda, kulikuwa na kikundi fulani cha wanaume wa pekee—manabii. Walikuwa na imani ya pekee na ujasiri wa kutangaza ujumbe mbalimbali wa Mungu. Fikiria mambo manne makuu yaliyozungumziwa na manabii hao wa Mungu.
1. Kuharibiwa kwa Yerusalemu. Mapema sana, manabii wa Mungu—Isaya na Yeremia hasa—walianza kuonya kwamba Yerusalemu lingeharibiwa na kuachwa ukiwa. Walitangaza waziwazi ni kwa nini jiji hilo lilistahili hasira ya Mungu. Mazoea yake ya dini za uongo, ufisadi, na jeuri yalithibitisha dai lake la kumwakilisha Yehova kuwa la uwongo.—2 Wafalme 21:10-15; Isaya 3:1-8, 16-26; Yeremia 2:1–3:13.
2. Kurudishwa kwa ibada ya kweli. Baada ya miaka 70 ya uhamisho, watu wa Mungu waliachiliwa kutoka Babiloni. Walirudi katika makao yao yaliyokuwa ukiwa na kujenga upya hekalu la Yehova jijini Yerusalemu. (Yeremia 46:27; Amosi 9:13-15) Miaka 200 hivi mapema, Isaya alitabiri jina la mshindi—Koreshi—ambaye angeshinda Babiloni na kuwaruhusu watu wa Mungu warudishe tena ibada safi. Isaya hata alieleza waziwazi jinsi ambavyo Koreshi angefanya hivyo.—Isaya 44:24–45:3.
3. Kufika kwa Masihi na mambo yaliyompata. Masihi angezaliwa katika mji wa Bethlehemu. (Mika 5:2) Angekuwa mnyenyekevu, angeingia Yerusalemu akiwa amepanda punda. (Zekaria 9:9) Ijapokuwa alikuwa mpole na mwenye fadhili, hangependwa na wengi, badala yake wengi wangemkataa. (Isaya 42:1-3; 53:1, 3) Angeuawa kikatili. Je, huo ndio ungekuwa mwisho wake? Hapana, kwa kuwa dhabihu yake ingewezesha msamaha wa dhambi za watu wengi. (Isaya 53:4, 5, 9-12) Ufufuo wake tu ndio ungewezesha hilo.
4. Utawala wa Masihi juu ya dunia. Wanadamu wasio wakamilifu hawawezi kujitawala wenyewe kwa amani, lakini Mfalme wa Kimasihi angeitwa Mkuu wa Amani. (Isaya 9:6, 7; Yeremia 10:23) Chini ya utawala wake, kungekuwa na amani kati ya wanadamu wote na pia wanyama. (Isaya 11:3-7) Magonjwa hayatakuwako. (Isaya 33:24) Hata kifo kitamezwa milele. (Isaya 25:8) Wakati wa utawala wa Masihi, wafu watafufuliwa waishi duniani.—Danieli 12:13.
—Inatoka kwenye Isaya, Yeremia, Danieli, Amosi, Mika, na Zekaria.
-
-
Nabii Aliye Uhamishoni Apata Maono ya Wakati UjaoBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 15
Nabii Aliye Uhamishoni Apata Maono ya Wakati Ujao
Danieli atabiri kuhusu Ufalme wa Mungu na Masihi atakayekuja. Ufalme wa Babiloni waanguka
DANIELI, kijana mwenye utimilifu wa pekee, alipelekwa uhamishoni Babiloni kabla ya Yerusalemu kuharibiwa. Yeye na Wayahudi wengine—waliohamishwa kutoka katika ufalme ulioshindwa wa Yuda—walipewa kiasi fulani cha uhuru na wale waliowateka. Kwa muda mrefu aliokuwa Babiloni, Danieli alibarikiwa sana na Mungu, hata akaponyoka kifo katika shimo la simba na kupokea maono yaliyomwezesha kuona wakati ujao ulio mbali. Unabii muhimu zaidi wa Danieli ulikazia Masihi na utawala Wake.
Danieli apata kujua Masihi atafika wakati gani. Danieli aliambiwa wakati ambapo watu wa Mungu wangeweza kutazamia “Masihi Kiongozi” afike—Majuma 69 ya miaka baada ya amri ya kujengwa upya kuta za Yerusalemu kutolewa. Juma la kawaida lina siku saba; juma la miaka ni miaka saba. Amri hiyo ilitolewa muda mrefu baada ya wakati wa Danieli, yaani, mwaka wa 455 K.W.K. “Majuma” hayo 69 yalianza wakati huo na kuendelea kwa muda wa miaka 483, hadi mwaka wa 29 W.K. Katika sehemu inayofuata ya broshua hii, tutaona kilichotokea mwaka huo. Danieli aliona kimbele kwamba Masihi “angekatiliwa mbali,” au kuuawa, ili kufanya upatanisho wa dhambi.—Danieli 9:24-26.
Masihi angekuwa Mfalme mbinguni. Katika maono yasiyo ya kawaida ya mbingu zenyewe, Danieli alimwona Masihi, akirejelewa kuwa “mtu fulani kama mwana wa binadamu,” akikaribia kiti cha ufalme cha Yehova mwenyewe. Yehova alimkabidhi “utawala na heshima na ufalme.” Ufalme huo ungedumu milele. Danieli alipata kujua jambo lingine lenye kusisimua kuhusu Ufalme wa Kimasihi—Mfalme huyo angetawala pamoja na wengine, kikundi kinachoitwa “watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi.”—Danieli 7:13, 14, 27.
Ufalme utaharibu serikali za ulimwengu huu. Mungu alimpa Danieli uwezo wa kufasiri ndoto ambayo ilimkanganya Nebukadneza, mfalme wa Babiloni. Mfalme huyo aliona sanamu kubwa yenye kichwa cha dhahabu, kifua na mikono ya fedha, tumbo na mapaja ya shaba, miguu ya chuma, na nyayo za mchanganyiko wa chuma na udongo. Jiwe lililokatwa kutoka katika mlima lilipiga nyayo dhaifu za sanamu hiyo na kuivunjavunja. Danieli alieleza kwamba sehemu mbalimbali za sanamu hiyo ziliwakilisha mfuatano wa serikali mbalimbali za ulimwengu, kuanzia Babiloni iliyowakilishwa na kile kichwa cha dhahabu. Danieli aliona kimbele kwamba wakati wa utawala wa serikali ya mwisho ya ulimwengu huu mwovu, Ufalme wa Mungu ungechukua hatua. Ungezivunja-vunja serikali zote za ulimwengu huu. Kisha utawale milele.—Danieli, sura ya 2.
Akiwa mzee sana, Danieli alijionea kuanguka kwa Babiloni. Mfalme Koreshi alilipindua jiji hilo kama manabii walivyotabiri. Punde baadaye, Wayahudi wakaachiliwa huru kutoka uhamishoni—wakati barabara ulioahidiwa, baada ya ile miaka 70 ya ukiwa wa nchi yao. Wakiongozwa na magavana, makuhani, na manabii waaminifu, Wayahudi walijenga upya Yerusalemu na kulirekebisha hekalu la Yehova. Hata hivyo, ni nini ambacho kingetokea baada ya ile miaka 483 kumalizika?
—Inatoka kwenye Kitabu cha Danieli.
-
-
Masihi AfikaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 16
Masihi Afika
Yehova amtambulisha Yesu wa Nazareti kuwa Masihi aliyeahidiwa
JE, Yehova angewasaidia watu wake kumtambua Masihi? Ndiyo. Fikiria aliyofanya. Karne nne baada ya Maandiko ya Kiebrania kumalizika, katika jiji linaloitwa Nazareti, eneo la kaskazini la Galilaya, mwanamke kijana anayeitwa Maria alitembelewa na mgeni asiye wa kawaida. Malaika anayeitwa Gabrieli alimtokea na kumwambia kwamba ijapokuwa yeye ni bikira, Mungu angetumia nguvu zake za utendaji, roho takatifu, kumfanya azae mwana. Mwana huyo ndiye Mfalme aliyeahidiwa zamani, yule ambaye angetawala milele! Mtoto huyo angekuwa Mwana wa Mungu mwenyewe. Mungu angeuhamisha uhai wake kutoka mbinguni na kuutia katika tumbo la uzazi la Maria.
Maria alikubali kwa unyenyekevu mgawo huo wa pekee. Mchumba wake, seremala anayeitwa Yosefu, alimwoa baada ya Mungu kumtuma malaika amhakikishie chanzo cha uja-uzito wa Maria. Hata hivyo, unabii uliosema kwamba Masihi angezaliwa Bethlehemu ungetimizwa jinsi gani? (Mika 5:2) Jiji hilo dogo lilikuwa umbali wa kilomita 140 hivi kutoka Nazareti!
Mtawala Mroma aliagiza watu wahesabiwe. Watu walipaswa kujiandikisha katika miji ya nyumbani kwao. Inaonekana kwamba Bethlehemu kulikuwa nyumbani kwa Yosefu na Maria, kwa hiyo Yosefu na mke wake wakasafiri hadi huko. (Luka 2:3) Maria alizalia zizini, na kumlaza mtoto wake katika hori. Kisha Mungu akatuma malaika wengi wakawaambie wachungaji waliokuwa mlimani kwamba mtoto ambaye amezaliwa ndiye Masihi, au Kristo, aliyeahidiwa.
Baadaye, wengine pia walishuhudia kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. Nabii Isaya alitabiri kwamba mtu fulani angetokea na kutayarisha njia kwa ajili ya kazi muhimu ya Masihi. (Isaya 40:3) Mtu huyo ni Yohana Mbatizaji. Alipomwona Yesu, alipaaza sauti: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” Baadhi ya wanafunzi wa Yohana wakamfuata Yesu mara moja. Mmoja wao akasema: “Tumempata Masihi.”—Yohana 1:29, 36, 41.
Kulikuwa na ushuhuda zaidi. Yohana alipombatiza Yesu, Yehova mwenyewe alisema kutoka mbinguni. Akitumia roho takatifu, alimweka rasmi Yesu kuwa Masihi na kusema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:16, 17) Masihi aliyeahidiwa akawa amefika!
Hilo lililotokea wakati gani? Mwaka wa 29 W.K., wakati ambapo ile miaka 483 iliyotabiriwa na Danieli ilipokamilika. Ndiyo, utimizo huo ni mojawapo ya ushuhuda wenye kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi, au Kristo. Hata hivyo, alitangaza ujumbe gani alipokuwa duniani?
—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 1 hadi 3; Marko, sura ya 1; Luka, sura ya 2; Yohana, sura ya 1.
-
-
Yesu Afundisha Kuhusu Ufalme wa MunguBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 17
Yesu Afundisha Kuhusu Ufalme wa Mungu
Yesu awafundisha wanafunzi wake mambo mengi, hata hivyo akazia jambo moja kuu—Ufalme wa Mungu
KWA nini Yesu alikuja duniani? Yeye mwenyewe alisema: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Fikiria mambo manne ambayo Yesu alifundisha kuhusu Ufalme, jambo kuu katika mahubiri yake.
1. Yesu aliteuliwa kuwa Mfalme. Yesu alisema waziwazi kwamba yeye ndiye Masihi aliyeahidiwa. (Yohana 4:25, 26) Pia, alionyesha kwamba ndiye Mfalme ambaye nabii Danieli aliona katika maono. Yesu aliwaambia mitume wake kwamba siku moja ataketi juu ya ‘kiti cha ufalme chenye utukufu’ na kwamba wao pia wataketi juu ya viti vya ufalme. (Mathayo 19:28) Alikiita kikundi hicho cha watawala “kundi dogo,” naye alisema kwamba ana “kondoo wengine,” ambao si sehemu ya kikundi hicho.—Luka 12:32; Yohana 10:16.
2. Ufalme wa Mungu utaleta haki ya kweli. Yesu alionyesha kwamba Ufalme utaondolea mbali ukosefu mkubwa zaidi wa haki kwa kulitakasa, au kulifanya kuwa takatifu, jina la Yehova Mungu na kuliondolea masuto yote ambayo Shetani amelimbikiza juu ya jina hilo tangu uasi wa Edeni. (Mathayo 6:9, 10) Pia, Yesu alionyesha kila siku kwamba hana ubaguzi, kwa kuwahubiria wanaume kwa wanawake, matajiri kwa maskini. Ijapokuwa alipaswa kuwafundisha Waisraeli hasa, alikuwa tayari kuwasaidia Wasamaria na Watu wa Mataifa au wasio Wayahudi. Tofauti na viongozi wa dini wa siku zake, hakuonyesha upendeleo hata kidogo.
3. Ufalme wa Mungu si sehemu ya ulimwengu huu. Yesu aliishi wakati ambapo kulikuwa na misukosuko mingi. Nchi ya kwao ilikuwa ikitawaliwa na serikali ya nchi nyingine. Hata hivyo, watu walipojaribu kumhusisha katika masuala ya kisiasa ya siku zake, alijiondoa. (Yohana 6:14, 15) Alimwambia mwanasiasa mmoja: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Nao wafuasi wake, aliwaambia: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Hakuwaruhusu kutumia silaha za vita, hata kwa kusudi la kumlinda yeye mwenyewe.—Mathayo 26:51, 52.
“Akaanza kusafiri . . . kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Luka 8:1
4. Kristo atatawala kwa upendo. Yesu aliahidi kwamba atawaburudisha watu, na kuwapumzisha mizigo yao. (Mathayo 11:28-30) Ndivyo alivyofanya. Alitoa mashauri yenye upendo na yenye kutumika kuhusu kukabiliana na mahangaiko ya maisha, kuboresha mahusiano, kuepuka kufuatia vitu vya kimwili, na kupata furaha. (Mathayo, sura ya 5-7) Kwa sababu alionyesha upendo watu wa tabaka zote walipenda kuwa pamoja naye. Hata watu wa hali ya chini walimiminika kwake, wakiwa na hakika kwamba atawatendea kwa fadhili na heshima. Kwa kweli Yesu atakuwa Mtawala asiye na kifani!
Kuna njia nyingine yenye matokeo sana ambayo Yesu alitumia kuwafundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu. Alifanya miujiza mingi. Kwa nini? Tutaona.
-
-
Yesu Afanya MiujizaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 18
Yesu Afanya Miujiza
Yesu, kupitia miujiza aliyofanya, alionyesha jinsi atakavyotumia nguvu zake akiwa Mfalme
MUNGU alimwezesha Yesu kufanya mambo ambayo wanadamu wengine hawangeweza kufanya. Yesu alifanya miujiza mingi—mara nyingi mbele ya watazamaji wengi. Miujiza hiyo ilionyesha kwamba Yesu ana nguvu kuliko adui zake na pia kuliko vizuizi vingine ambavyo wanadamu wasio wakamilifu hawangeweza kamwe kushinda kwa mafanikio. Fikiria mifano kadhaa.
Njaa. Muujiza wa kwanza wa Yesu ulikuwa kubadili maji yawe divai. Katika pindi nyingine mbili, alilisha maelfu ya watu kwa mikate na samaki wachache. Pindi zote hizo kulikuwa na chakula cha kumtosha kila mtu na hata kubaki.
Ugonjwa. Yesu aliwaponya watu “kila namna ya ugonjwa na kila namna ya udhaifu.” (Mathayo 4:23) Aliwaponya vipofu, viziwi, wenye ukoma, wenye kifafa, vilema, viwete, na wasiojiweza. Hakuna ugonjwa uliomshinda.
Dhoruba kali. Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakisafiri katika Bahari ya Galilaya, dhoruba kali ilizuka. Wanafunzi waliogopa sana. Yesu aliitazama dhoruba hiyo na kusema: “Nyamaza, utulie!” Nayo dhoruba hiyo ikatulia. (Marko 4:37-39) Pindi nyingine, alitembea juu ya maji kulipokuwa na dhoruba yenye kuogopesha.—Mathayo 14:24-33.
Roho waovu. Roho waovu wana nguvu kuliko wanadamu. Watu wengi wameshindwa kujitoa katika mtego wa adui hao hatari wa Mungu. Hata hivyo, tena na tena, Yesu alipowaamuru watoke watu, roho hao hawangeweza tena kuendelea kuwasumbua. Hakuwaogopa. Badala yake, walitambua mamlaka yake nao walimwogopa.
Kifo. Kifo ni adui ambaye hakuna mwanadamu anaweza kumshinda. Ndiyo sababu kinaitwa “adui wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:26) Hata hivyo, Yesu aliwafufua wafu. Alimfufua kijana wa mjane na binti ya wazazi waliokuwa na huzuni. Katika kisa cha pekee, Yesu alimfufua rafiki yake mpendwa, Lazaro, mbele ya umati wa waombolezaji, ijapokuwa alikuwa mfu kwa karibu siku nne! Hata adui za Yesu walikiri kwamba alifanya muujiza huo.—Yohana 11:38-48; 12:9-11.
Kwa kuwa wote waliosaidiwa na Yesu hatimaye walikufa, kwa nini alifanya miujiza yote hiyo? Miujiza ya Yesu ilitimiza mambo mazuri yenye kudumu. Ilithibitisha kwamba unabii wote wenye kupendeza kuhusu utawala wa Mfalme wa Kimasihi una msingi. Hakuna haja ya kuwa na shaka kwamba Mfalme aliyewekwa na Mungu hawezi kuondolea mbali njaa, magonjwa, hali hatari ya hewa, roho waovu, au kifo chenyewe. Tayari amethibitisha kwamba Mungu amemkabidhi nguvu za kufanya hivyo.
-
-
Yesu Atabiri Matukio ya Wakati Ujao Yatakayoikumba Dunia NzimaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 19
Yesu Atabiri Matukio ya Wakati Ujao Yatakayoikumba Dunia Nzima
Yesu ataja mambo yatakayotia alama kuwapo kwake katika mamlaka ya kifalme na ya umalizio wa mfumo wa mambo
KATIKA Mlima wa Mizeituni, ambapo jiji la Yerusalemu na hekalu lake lilikuwa likionekana vizuri, mitume wanne wa Yesu walimuuliza faraghani kuhusu mambo fulani aliyokuwa amezungumzia. Yesu alikuwa ametoka kusema kwamba hekalu lililo Yerusalemu litaharibiwa. Na mapema, alikuwa amewaambia kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 13:40, 49) Sasa mitume wakamuuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—Mathayo 24:3.
Akiwajibu, Yesu aliwaambia mambo ambayo yangetokea kabla ya Yerusalemu kuharibiwa. Lakini maneno yake yalikuwa na utimizo zaidi. Unabii wake ungetimizwa kwa kiwango kikubwa zaidi ulimwenguni pote. Yesu alitabiri matukio na hali za ulimwengu ambazo zingekuwa ishara. Ishara hiyo ingewaonyesha walio duniani kwamba kuwapo kwa Yesu akiwa Mfalme mbinguni kumeanza. Yaani, ishara hiyo ingeonyesha kwamba Yehova Mungu amemfanya Yesu kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi ulioahidiwa zamani za kale. Ishara hiyo ingemaanisha kwamba karibuni Ufalme huo utaondolea mbali uovu na kuwaletea wanadamu amani. Mambo ambayo Yesu alitabiri yangetia alama siku za mwisho za mfumo huu wa kale wa mambo—mifumo ya dini, siasa, na kijamii iliyopo leo—na kuashiria mwanzo wa mfumo mpya.
Akieleza mambo ambayo yangetokea duniani wakati wa kuwapo kwake akiwa Mfalme mbinguni, Yesu alisema kwamba kungekuwa na vita kati ya mataifa, upungufu wa chakula, matetemeko makuu ya ardhi, na magonjwa yenye kuenea. Uvunjaji wa sheria ungeongezeka. Wanafunzi wa kweli wa Yesu wangehubiri habari njema za Ufalme wa Mungu katika dunia yote. Yote hayo yangeishia katika “dhiki kuu” ambayo haijapata kutokea tena.—Mathayo 24:21.
Wafuasi wa Yesu wangejua jinsi gani kwamba dhiki hiyo iko karibu? Yesu aliwaambia: “Jifunzeni jambo hili kutokana na mtini.” (Mathayo 24:32) Majani ya mtini yanapotokea kwenye matawi ni ishara ya kwamba msimu wa kiangazi unakaribia. Vivyo hivyo, kutokea kwa ishara zote hizo alizotabiri Yesu katika kipindi kimoja cha wakati kungekuwa ishara ya kwamba mwisho uko karibu. Hakuna yeyote ila Baba aliyejua siku na saa barabara ambayo dhiki kuu ingeanza. Kwa hiyo, Yesu aliwahimiza hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni gani.”—Marko 13:33.
—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 24 na 25; Marko, sura ya 13; Luka, sura ya 21.
-
-
Yesu Kristo AuawaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 20
Yesu Kristo Auawa
Yesu aanzisha maadhimisho mapya; asalitiwa na kutundikwa mtini
BAADA ya Yesu kuhubiri na kufundisha kwa miaka mitatu na nusu, alijua kwamba anakaribia mwisho wa maisha yake duniani. Viongozi wa dini Wayahudi walikuwa wakipanga njama ya kumuua, lakini wakawaogopa watu walioamini kwamba yeye ni nabii. Wakati huohuo, Shetani alimshawishi mmoja wa mitume 12 wa Yesu—Yuda Iskariote—akawa msaliti. Viongozi wa dini walimpa Yuda vipande 30 vya fedha ili amsaliti Yesu.
Usiku wake wa mwisho, Yesu aliwakusanya mitume wake kuadhimisha Pasaka. Baada ya Yuda kuondoka, Yesu alianzisha maadhimisho mapya, Mlo wa Jioni wa Bwana. Akachukua mkate, akashukuru, akawapa wale mitume 11 waliobaki. Akasema: “Huu unamaanisha mwili wangu ambao utatolewa kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” Alifanya vivyo hivyo kuhusiana na kikombe na kusema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu.”—Luka 22:19, 20.
Yesu alikuwa na mengi ya kuwaambia mitume wake usiku huo. Aliwapa amri mpya—kwamba wapendane bila ubinafsi. Aliwaambia: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Aliwahimiza wasiruhusu mioyo yao itaabike kwa sababu ya mambo yenye kuhuzunisha yaliyokuwa karibu kutokea. Yesu alisali sana kwa ajili yao. Wakaimba nyimbo za sifa na kuondoka.
Wakiwa katika bustani ya Gethsemane, Yesu akapiga magoti na kumimina moyo wake katika sala. Punde si punde askari-jeshi wenye silaha, makuhani, na watu wengine wakaja kumkamata. Yuda akakaribia na kumtambulisha Yesu kwao kwa kumbusu. Askari-jeshi hao walipomkamata Yesu, mitume wakatoroka.
Yesu akiwa mbele ya mahakama kuu ya Wayahudi, alijitambulisha kuwa Mwana wa Mungu. Mahakama hiyo ilimhukumu kuwa na hatia ya kukufuru na anastahili kifo. Baada ya hapo Yesu akapelekwa kwa Gavana Mroma, Pontio Pilato. Ingawa hakumpata Yesu kuwa na hatia, alimkabidhi Yesu kwa umati uliotaka auawe.
Kisha Yesu akapelekwa Golgotha, ambapo askari-jeshi Waroma walimtundika mtini. Kimuujiza, giza likaingia katikati ya mchana. Baadaye, alasiri hiyohiyo, Yesu akafa na kukawa na tetemeko kubwa la nchi. Mwili wake ukalazwa katika kaburi lililokuwa limechongwa katika mwamba. Siku iliyofuata, makuhani wakalifunika kaburi na kuweka mlinzi katika mwingilio wake. Je, Yesu angeendelea kuwa kaburini? Hapana. Muujiza mkubwa kuliko yote ulikuwa karibu kutokea.
—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 26 na 27; Marko sura, ya 14 na 15; Luka, sura ya 22 na 23; Yohana, sura ya 12 hadi 19.
-
-
Yesu Yuko Hai!Biblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 21
Yesu Yuko Hai!
Yesu awatokea wafuasi wake ili kuwapa maagizo na kuwatia moyo
SIKU ya tatu baada ya kifo cha Yesu, wanawake fulani waliokuwa wanafunzi wake waligundua kwamba jiwe lililokuwa kwenye mwingilio wa kaburi limeondolewa. Isitoshe, kaburi lilikuwa tupu!
Malaika wawili wakatokea. Mmoja wao akasema: “Mnamtafuta Yesu Mnazareti. . . . Alifufuliwa.” (Marko 16:6) Bila kukawia, wanawake hao wakakimbia kwenda kuwaambia mitume. Wakiwa njiani, wakakutana na Yesu. Akawaambia: “Msiogope! Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu, ili wapate kwenda zao Galilaya; na huko wataniona.”—Mathayo 28:10.
Baadaye siku hiyo, wanafunzi wawili walikuwa wakitembea kutoka Yerusalemu kuelekea kijiji cha Emau. Mtu wasiyemjua alijiunga nao na kuwauliza wanazungumzia nini. Mtu huyo alikuwa Yesu aliyefufuliwa, aliyewatokea katika umbo ambalo hawakutambua mwanzoni. Wakiwa na nyuso zenye huzuni wakamjibu kwamba wanaongea kuhusu Yesu. Kisha mtu huyo akaanza kuwaeleza mambo kuhusu Masihi katika Maandiko yote. Kwa kweli, Yesu alikuwa ametimiza mambo yote yaliyotabiriwa kuhusu Masihi.a Wanafunzi hao walipotambua kwamba ni Yesu aliyefufuliwa akiwa na mwili wa roho, akatoweka.
Wanafunzi hao wawili wakarudi Yerusalemu mara moja. Wakawakuta mitume wamekusanyika katika chumba kilichokuwa kimefungwa. Walipokuwa wakisimulia mambo waliyokuwa wamejionea, Yesu akatokea. Wafuasi wake walioduwaa hawakuamini macho yao! Yesu akawauliza: “Kwa nini shaka zinatokea mioyoni mwenu?” Kisha akawaambia: “Imeandikwa kwamba Kristo angeteseka na kufufuliwa kutoka kati ya wafu siku ya tatu.”—Luka 24:38, 46.
Kwa siku 40 baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea wanafunzi wake katika pindi tofauti-tofauti. Katika pindi moja, aliwatokea wanafunzi zaidi ya 500! Pengine katika pindi hiyo ndiyo alipowapa mgawo huu mzito: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 28:19, 20.
Alipokutana kwa mara ya mwisho pamoja na mitume wake 11 waliokuwa waaminifu, Yesu aliwaahidi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Kisha Yesu akapanda juu na mawingu yakamfunika.
—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 28; Marko, sura ya 16; Luka, sura ya 24; Yohana, sura ya 20 na 21; 1 Wakorintho 15:5, 6.
a Unabii mbalimbali wa Kimasihi ambao Yesu alitimiza unazungumziwa katika broshua hii Sehemu ya 14, Sehemu ya 15 na Sehemu ya 16 pia nyongeza yenye kichwa “Yesu Kristo—Masihi Aliyeahidiwa” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
Mitume Wahubiri kwa UjasiriBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 22
Mitume Wahubiri kwa Ujasiri
Kutaniko la Kikristo laongezeka licha ya mateso
SIKU kumi baada ya Yesu kurudi mbinguni, wanafunzi wake 120 hivi walikusanyika katika nyumba fulani jijini Yerusalemu wakati wa Sikukuu ya Kiyahudi ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K. Ghafula, katika nyumba hiyo kukawa na kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma. Wanafunzi wakaanza kuzungumza lugha ambazo hawakuwa wanazijua. Iliwezekanaje? Mungu alikuwa amewapa wanafunzi roho takatifu.
Nje, kulikuwa na umati kwa sababu watu walikuwa wametoka sehemu mbalimbali ili kusherehekea sikukuu hiyo. Walishangaa kuwasikia wanafunzi wa Yesu wakizungumza kwa ufasaha lugha zao wenyewe. Akieleza yaliyotokea, Petro alirejelea unabii wa Yoeli kwamba Mungu ‘angemimina’ roho yake, ambayo ingewawezesha wenye kuipokea kufanya miujiza. (Yoeli 2:28, 29) Uthibitisho huo wenye nguvu wa roho takatifu ulionyesha wazi kwamba badiliko kubwa limetokea: Mungu ameacha kushughulika na taifa la Israeli na kuanza kushughulika na kutaniko jipya la Kikristo lililokuwa limeanzishwa. Sasa, wote waliotaka kumtumikia Mungu walipaswa kuwa wafuasi wa Kristo.
Wakati huohuo upinzani uliongezeka, nao adui wakawatupa wanafunzi gerezani. Hata hivyo, wakati wa usiku, malaika wa Yehova alifungua milango ya gereza na kuwaambia wanafunzi waendelee kuhubiri. Ilipofika asubuhi wakaendelea kuhubiri. Wakaingia hekaluni na kuanza kufundisha habari njema kumhusu Yesu. Wapinzani wao wa kidini walikuwa na hasira nao wakawaagiza waache kuhubiri. Mitume wakajibu kwa ujasiri: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:28, 29.
Mateso yakaongezeka. Wayahudi fulani walimshtaki mwanafunzi Stefano wakidai kwamba amekufuru, nao wakamuua kwa kumpiga kwa mawe. Kijana, anayeitwa Sauli wa Tarso, alikuwa akitazama na kukubaliana na mauaji hayo. Kisha akaenda Damasko kumkamata mfuasi yeyote wa Kristo. Sauli akiwa njiani, nuru kutoka mbinguni ilimulika kumzunguka na akasikia sauti: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” Akiwa amepofushwa na nuru hiyo, Sauli akauliza: “Wewe ni nani?” Sauti hiyo ikasema: “Mimi ni Yesu.”—Matendo 9:3-5.
Siku tatu baadaye, Yesu alimtuma mwanafunzi anayeitwa Anania ili kumponya Sauli. Sauli akabatizwa na kuanza kuhubiri kwa ujasiri kumhusu Yesu. Baadaye, Sauli akaitwa mtume Paulo naye akawa Mkristo mwenye bidii wa kutaniko la Kikristo.
Wanafunzi wa Yesu walikuwa wakiwatangazia habari njema za Ufalme wa Mungu Wayahudi na Wasamaria pekee. Sasa malaika amtokea Kornelio, ofisa-jeshi Mroma, anayemwogopa Mungu na kumwambia awatume watu wakamwite mtume Petro. Akiwa pamoja na wengine, Petro akamhubiria Kornelio na watu wa nyumbani mwake. Petro alipokuwa akizungumza, roho takatifu ikaja juu ya waamini hao kutoka kwa Mataifa, naye akaagiza wabatizwe katika jina la Yesu. Tangu wakati huo na kuendelea, watu wa mataifa yote wangeweza kupata uzima wa milele. Kutaniko lilikuwa tayari kuhubiri habari njema kwa mapana na marefu.
—Inatoka kwenye Matendo 1:1–11:21.
-
-
Habari Njema YaeneaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 23
Habari Njema Yaenea
Paulo asafiri nchi kavu na baharini akihubiri
BAADA ya kuwa Mkristo, Paulo alitangaza kwa bidii habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Mtu huyo aliyekuwa mpinzani alikumbana na upinzani mkali mara nyingi. Mtume huyo mwenye bidii alisafiri sehemu mbalimbali akihubiri habari njema ya Ufalme ambao utatimiza kusudi la awali la Mungu kwa wanadamu.
Katika safari yake ya kwanza ya kuhubiri huko Listra, Paulo alimponya mwanamume aliyekuwa kilema tangu kuzaliwa. Umati ulianza kupaaza sauti kwamba Paulo na Barnaba, msafiri mwenzake ni miungu. Wanaume hao wawili walijaribu sana kuwazuia watu wasiwatolee dhabihu. Hata hivyo, baadaye umati huohuo ulichochewa na adui za Paulo, ukampiga kwa mawe na kumwacha akiwa mahututi. Paulo hakufa na baadaye alirudi katika jiji hilohilo kuwaimarisha wanafunzi kwa maneno ya kutia moyo.
Wakristo fulani Wayahudi walidai kwamba waamini wasio Wayahudi wanapaswa kutimiza matakwa fulani ya Sheria ya Musa. Paulo alikwenda Yerusalemu kwa mitume na wanaume wazee ili kuwasilisha tatizo hilo. Baada ya kuyachunguza Maandiko kwa makini na kwa mwongozo wa roho takatifu ya Mungu, wanaume hao waliyaandikia makutaniko na kuyashauri yajiepushe na ibada ya sanamu, kula damu na nyama zenye damu, na kuepuka uasherati. Amri hizo zilikuwa za “lazima,” hata hivyo, haikumaanisha kwamba walipaswa kufuata Sheria ya Musa.—Mdo. 15:28, 29.
Katika safari yake ya pili ya kuhubiri, Paulo alienda Beroya, eneo ambalo leo liko Ugiriki. Wayahudi waliokuwa wakiishi huko walilipokea neno kwa hamu, wakiyachunguza Maandiko kila siku ili kuyathibitisha mafundisho yake. Kwa mara nyingine tena, upinzani ukamfanya aondoke na kwenda Athene. Akiwa mbele ya Waathene wenye elimu, Paulo alitoa hotuba yenye kuchochea kwelikweli. Leo tunaweza kumwiga Paulo kwa kusema kwa busara, utambuzi, na ufasaha tunapohubiri.
Baada ya safari yake ya tatu ya kuhubiri, Paulo alienda Yerusalemu. Alipoenda hekaluni, Wayahudi fulani walizusha ghasia, wakitaka kumuua. Askari-jeshi Waroma wakaingilia kati na kumhoji Paulo. Kwa kuwa alikuwa raia wa Roma, baadaye alijitetea mbele ya Feliksi, gavana Mroma. Wayahudi hawakuwa na uthibitisho wowote kuhusu mashtaka yao dhidi ya Paulo. Ili kumzuia Festo, aliyekuwa pia gavana Mroma, asimtie mikononi mwa Wayahudi, Paulo alisema: “Ninakata rufani kwa Kaisari!” Festo akajibu: “Utaenda kwa Kaisari.”—Mdo. 25:11, 12
Kisha Paulo akasafirishwa kwa meli hadi Italia ili akahukumiwe. Baada ya meli yao kuvunjika, alilazimika kukaa katika kisiwa cha Malta wakati wa majira ya baridi kali. Mwishowe alipofika Roma, alikaa katika nyumba ya kukodi kwa miaka miwili. Hata ingawa alikuwa akilindwa na askari, mtume huyo mwenye bidii aliendelea kuwahubiria wote waliomtembelea kuhusu Ufalme wa Mungu.
—Inatoka kwenye Matendo 11:22–28:31.
-
-
Paulo Ayaandikia MakutanikoBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 24
Paulo Ayaandikia Makutaniko
Barua za Paulo zaliimarisha kutaniko la Kikristo
KUTANIKO changa la Kikristo lilikuwa na kazi kubwa mbele yake. Lingetimiza sehemu muhimu katika kusudi la Yehova. Hata hivyo, baada ya muda usio mrefu Wakristo hao wa karne ya kwanza walishambuliwa. Je, wangedumisha utimilifu wao kwa Mungu wajapokabili mateso na hali nyingine zenye kuhatarisha uaminifu wao kutoka nje na ndani ya kutaniko? Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yana barua 21 zenye kutia moyo na zenye shauri lililohitajiwa.
Barua 14, Waroma mpaka Waebrania, ziliandikwa na mtume Paulo. Barua hizo zina majina ya wale walioandikiwa—iwe ni mtu binafsi au kutaniko fulani. Fikiria baadhi ya mambo ambayo Paulo anazungumzia katika barua zake.
Mashauri kuhusu maadili na mwenendo. Waasherati, wazinzi, na wanaotenda dhambi nyingine nzito “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Wagalatia 5:19-21; 1 Wakorintho 6:9-11) Waabudu wa Mungu kutoka mataifa yote wanapaswa kuwa na umoja. (Waroma 2:11; Waefeso 4:1-6) Wanapaswa kuwasaidia kwa hiari waamini wenzao walio na uhitaji. (2 Wakorintho 9:7) Paulo anasema: “Salini bila kuacha.” Kwa kweli, waabudu wanatiwa moyo kummiminia Yehova mioyo yao katika sala. (1 Wathesalonike 5:17; 2 Wathesalonike 3:1; Wafilipi 4:6, 7) Ili sala zinazotolewa zisikiwe na Mungu, lazima zitolewe kwa imani.—Waebrania 11:6.
Ni nini kinachoweza kusaidia familia ziwe na furaha? Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Wake wanapaswa kuwaheshimu sana waume zao. Watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao, kwa kuwa hilo linampendeza Mungu. Wazazi wanapaswa kuwaongoza na kuwafundisha watoto wao kwa upendo, wakitumia kanuni za Mungu.—Waefeso 5:22–6:4; Wakolosai 3:18-21.
Wakristo wasaidiwa kuelewa kusudi la Mungu. Sheria ya Musa ilikusudiwa hasa kuwalinda na kuwaongoza Waisraeli mpaka wakati ambapo Kristo angefika. (Wagalatia 3:24) Hata hivyo, Wakristo hawahitaji kushika Sheria hiyo ili ibada yao kwa Mungu ikubaliwe. Alipokuwa akiwaandikia Waebrania, Wakristo waliokuwa na asili ya Kiyahudi, Paulo alieleza maana ya Sheria na jinsi kusudi la Mungu linavyotimizwa katika Kristo. Paulo alieleza kwamba sehemu mbalimbali za Sheria hiyo zilikuwa za kinabii. Kwa mfano, dhabihu ya Yesu ilikusudiwa kuleta msamaha wa dhambi, nayo iliwakilishwa na dhabihu za wanyama. (Waebrania 10:1-4) Kupitia kifo cha Yesu, Mungu alifuta agano la Sheria, kwa kuwa halikuwa na kazi tena.—Wakolosai 2:13-17; Waebrania 8:13.
Maagizo kuhusu utaratibu wa kutaniko. Wanaume wanaotaka kufikia mapendeleo kutanikoni wanapaswa kuwa na mwenendo mzuri na kutimiza sifa za kiroho. (1 Timotheo 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Waabudu wa Yehova Mungu wanapaswa kukusanyika kwa ukawaida pamoja na waamini wenzao ili kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Mikutano ya ibada inapaswa kuwa yenye kujenga na kuelimisha.—1 Wakorintho 14:26, 31.
Kufikia wakati ambapo alimwandikia Timotheo barua ya pili, Paulo alikuwa amerudi Roma; alikuwa gerezani akisubiri hukumu. Ni watu wachache tu waliojasiria kumtembelea. Paulo alijua kwamba ana wakati mfupi. Alisema: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.” (2 Timotheo 4:7) Yaelekea kwamba muda mfupi baadaye, Paulo aliuawa kwa sababu ya imani yake. Hata hivyo, barua za mtume huyo zina mwongozo ambao waabudu wa kweli wa Mungu wanafuata mpaka leo.
—Inatoka kwenye Waroma; 1 Wakorintho; 2 Wakorintho; Wagalatia; Waefeso; Wafilipi; Wakolosai; 1 Wathesalonike; 2 Wathesalonike; 1 Timotheo; 2 Timotheo; Tito; Filemoni; Waebrania.
-
-
Mashauri Kuhusu Imani, Mwenendo, na UpendoBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 25
Mashauri Kuhusu Imani, Mwenendo, na Upendo
Yakobo, Petro, Yohana, na Yuda, waandika barua za kuwatia moyo waamini wenzao
YAKOBO na Yuda walikuwa ndugu wa kambo wa Yesu. Petro na Yohana walikuwa mitume wa Yesu. Wanaume hao wanne waliandika jumla ya barua saba katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kila moja ya barua hizo ina jina la mwandikaji. Mashauri yaliyoongozwa na roho yaliyo katika barua hizo yalikusudiwa kuwasaidia Wakristo kudumisha utimilifu kwa Yehova na kuendelea kuutazamia Ufalme wake.
Wakristo wanapaswa kuwa na imani. Haitoshi tu kudai kwamba mtu ana imani. Imani ya kweli huambatana na matendo. Yakobo aliandika: “Imani bila matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Mtu anapotenda kwa imani akiwa katika majaribu, anasitawisha sifa ya uvumilivu. Ili kufanikiwa, Mkristo anahitaji kumwomba Mungu ampe hekima, akiwa na imani kwamba Mungu atampa. Uvumilivu humfanya mtu akubaliwe na Mungu. (Yakobo 1:2-6, 12) Mwabudu wa Mungu akidumisha utimilifu kwa imani, Yehova Mungu atajibu sala yake. Yakobo asema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.
Mkristo anapaswa kuwa na imani yenye nguvu inayoweza kumsaidia kushinda vishawishi na kuepuka upotovu wa maadili. Kwa sababu ya upotovu wa maadili uliokuwa umeenea, Yuda aliwahimiza waamini wenzake ‘wafanye pigano kali kwa ajili ya imani.’—Yuda 3.
Dumisha mwenendo safi. Yehova hutaka waabudu wake wawe watakatifu au safi katika kila njia. Petro aandika: “Ninyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Muwe watakatifu, kwa sababu mimi [Yehova] ni mtakatifu.’” (1 Petro 1:15, 16) Wakristo wamewekewa mfano wa kuiga. Petro asema: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Ijapokuwa huenda Wakristo wakateseka kwa sababu wanaishi kulingana na viwango vya Mungu, wanadumisha “dhamiri njema.” (1 Petro 3:16, 17) Petro anawahimiza Wakristo wawe na mwenendo na matendo matakatifu ya ujitoaji-kimungu huku wakiingojea siku ya hukumu ya Mungu na dunia mpya iliyoahidiwa ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:11-13.
“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8
Wakristo wanapaswa kuwa na upendo. Yohana aliandika: “Mungu ni upendo.” Mtume huyo anasema kwamba Mungu alionyesha upendo wake mkuu kwa kumtuma Yesu awe ‘dhabihu kwa ajili ya dhambi zetu.’ Kwa hiyo basi, Wakristo wanapaswa kufanya nini? Yohana anajibu: “Wapendwa, ikiwa Mungu alitupenda hivi, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu wa kupendana.” (1 Yohana 4:8-11) Njia moja ya kuonyesha upendo kama huo ni kwa kuwaonyesha ukarimu waamini wenzetu.—3 Yohana 5-8.
Hata hivyo, waabudu wa Yehova wanaweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanampenda? Yohana anajibu: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3; 2 Yohana 6) Wale wanaomtii Mungu kwa njia hiyo wanahakikishiwa kwamba Mungu ataendelea kuwapenda huku ‘wakitazamia uzima wa milele.’—Yuda 21.
—Inatoka kwenye Yakobo; 1 Petro; 2 Petro; 1 Yohana; 2 Yohana; 3 Yohana; Yuda.
-
-
Paradiso Yarudishwa!Biblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 26
Paradiso Yarudishwa!
Kupitia Ufalme wa Kristo, Yehova alitakasa jina Lake, atetea enzi Yake kuu, na kuondolea mbali uovu
KITABU cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, kinawapa wanadamu wote tumaini. Kitabu hicho kilichoandikwa na mtume Yohana, kina maono mbalimbali ambayo upeo wake ni kutimizwa kwa kusudi la Yehova.
Katika maono ya kwanza, Yesu aliyefufuliwa anapongeza na kurekebisha makutaniko kadhaa. Katika maono yanayofuata tunaona kiti cha Ufalme cha Mungu, ambapo viumbe wa roho wanamsifu.
Huku kusudi la Mungu likizidi kutimizwa, Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, apokea kitabu cha kukunjwa chenye mihuri saba. Anapofungua mihuri ya kwanza minne, wapanda-farasi wa mfano watokea. Mpanda-farasi wa kwanza ni Yesu akiwa juu ya farasi mweupe naye amevishwa taji la kifalme. Kisha wapanda-farasi juu ya farasi wenye rangi mbalimbali, wanaowakilisha vita, njaa, na tauni, mambo ambayo yanatendeka katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Muhuri wa saba unapofunguliwa, tarumbeta saba za mfano zinapulizwa zikiashiria kutangazwa kwa hukumu za Mungu. Kisha yafuata mapigo saba ya mfano, yanayowakilisha hasira ya Mungu.
Ufalme wa Mungu, unaofananishwa na mwana wa kiume aliyetoka kuzaliwa, wasimamishwa mbinguni. Vita vyatokea mbinguni, Shetani na malaika wake waovu watupwa duniani. Sauti kubwa inasema: “Ole wa dunia.” Ibilisi ana hasira kali, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.—Ufunuo 12:12.
Yohana amwona mwana-kondoo, Yesu, pamoja na wale 144,000 ambao wamechaguliwa kati ya wanadamu, ‘watakaotawala wakiwa wafalme pamoja’ na Yesu. Hivyo, kitabu cha Ufunuo kinafunua kwamba sehemu ya pili ya ule uzao inafanyizwa na jumla ya watu 144,000.—Ufunuo 14:1; 20:6.
Watawala wa dunia wanakusanyika pamoja kwa ajili ya Har–Magedoni, “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Wanapigana vita na yule anayeketi juu ya farasi mweupe—Yesu, anayeyaongoza majeshi ya mbinguni. Watawala wote wa ulimwengu huu wanaharibiwa. Shetani anafungwa, naye Yesu na wale 144,000 wanatawala juu ya dunia kwa “miaka elfu.” Mwishoni mwa ile miaka elfu, Shetani aharibiwa.—Ufunuo 16:14; 20:4.
Utawala huo wa Kristo na watawala wenzake utawatimizia nini wanadamu watiifu? Yohana anaandika: “[Yehova] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Kisha, dunia inakuwa paradiso!
Hivyo, kitabu cha Ufunuo kinakamilisha ujumbe wa Biblia. Ufalme wa Kimasihi, utalitakasa jina la Yehova na kuitetea enzi yake kuu milele!
—Inatoka kwenye Kitabu cha Ufunuo.
-
-
Ujumbe wa BibliaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Ujumbe wa Biblia
Yehova awaumba Adamu na Hawa wakiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso. Shetani amchongea Mungu na kutilia shaka haki Yake ya kutawala. Adamu na Hawa wajiunga na Shetani katika uasi, wajiletea dhambi na kifo wao wenyewe na wazao wao
Yehova awahukumu waasi hao na kuahidi Mkombozi, au Uzao, ambao utamponda Shetani, na kubatilisha matokeo yote ya uasi na dhambi
Yehova awaahidi Abrahamu na Daudi kwamba watakuwa babu za Uzao, au Masihi, ambaye atatawala akiwa Mfalme milele
Yehova awaongoza kwa roho manabii kutabiri kwamba Masihi ataondoa dhambi na kifo. Pamoja na watawala wenzake, atatawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, ambao utamaliza vita, magonjwa, hata kifo
Yehova amtuma Mwana wake duniani na kumtambulisha kuwa Masihi. Yesu ahubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na kutoa uhai wake kuwa dhabihu. Kisha Yehova amfufua akiwa kiumbe wa roho
Yehova amtawaza Mwana wake kuwa Mfalme mbinguni, hatua hiyo ikitia alama mwanzo wa siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Yesu awaongoza wafuasi wake duniani wanapohubiri Ufalme wa Mungu duniani pote
Yehova amwagiza Mwana wake aanze kuitawala dunia. Ufalme huo wazivunja-vunja serikali zote mbovu, waleta Paradiso, na kuwasaidia wanadamu waaminifu kufikia ukamilifu. Haki ya Yehova ya kutawala yatetewa, na jina lake latukuzwa milele
-
-
Mfululizo wa MatukioBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Mfululizo wa Matukio
“Hapo mwanzo . . . ”
4026 K.W.K. Kuumbwa kwa Adamu
3096 K.W.K. Kifo cha Adamu
2370 K.W.K. Gharika yaanza
2018 K.W.K. Abrahamu azaliwa
1943 K.W.K. Agano la Kiabrahamu
1750 K.W.K. Yosefu auzwa utumwani
kabla ya 1613 K.W.K. Ayubu ajaribiwa
1513 K.W.K. Kutoka Misri
1473 K.W.K. Taifa la Israeli laingia Kanaani likiongozwa na Yoshua
1467 K.W.K. Ushindi dhidi ya Kanaani wakamilika
1117 K.W.K. Sauli atiwa mafuta awe mfalme
1070 K.W.K. Mungu amwahidi Daudi Ufalme
1037 K.W.K. Sulemani awa mfalme
1027 K.W.K. Hekalu la Yerusalemu lakamilika
mnamo 1020 K.W.K. Wimbo wa Sulemani wakamilika
997 K.W.K. Taifa la Israeli lagawanyika na kuwa falme mbili
mnamo 717 K.W.K. Kuandikwa kwa Methali kwakamilika
607 K.W.K. Jiji la Yerusalemu laharibiwa; uhamisho wa Babiloni waanza
539 K.W.K. Koreshi aangusha Babiloni
537 K.W.K. Wayahudi warudi Yerusalemu
455 K.W.K. Kuta za Yerusalemu zajengwa upya; Majuma 69 ya miaka yaanza
Baada ya 443 K.W.K. Malaki akamilisha kitabu chake cha kinabii
mnamo 2 K.W.K. Kuzaliwa kwa Yesu
29 W.K. Yesu abatizwa Yesu aanza kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu
31 W.K. Yesu achagua mitume 12; Mahubiri ya Mlimani
32 W.K. Yesu amfufua Lazaro
Nisani 14, 33 W.K. Yesu atundikwa (Sehemu ya mwezi wa 3 na sehemu ya mwezi wa 4 katika kalenda ya leo)
Nisani 16, 33 W.K. Yesu afufuliwa
Sivani 6, 33 W.K. Pentekoste; roho takatifu yamiminwa (Sehemu ya mwezi wa 5 na sehemu ya mwezi wa 6 katika kalenda ya leo)
36 W.K. Kornelio awa Mkristo
mnamo 47-48 W.K. Safari ya kwanza ya Paulo ya kuhubiri
mnamo 49-52 W.K. Safari ya pili ya Paulo ya kuhubiri
mnamo 52-56 W.K. Safari ya tatu ya Paulo ya kuhubiri
mnamo 60-61 W.K. Paulo aandika barua akiwa gerezani Roma
kabla ya 62 W.K. Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, aandika barua yake
66 W.K. Wayahudi waasi dhidi ya Roma
70 W.K. Waroma waharibu Yerusalemu pamoja na hekalu lake
mnamo 96 W.K. Yohana aandika Ufunuo
mnamo 100 W.K. Kifo cha Yohana, mtume wa mwisho
-