Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • 1. Mwombe Mtungaji wa Biblia Akusaidie
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Julai 1
    • Jinsi Unavyoweza Kuielewa Biblia

      1. Mwombe Mtungaji wa Biblia Akusaidie

      “Kuna wakati ambapo nilikuwa nikisoma Biblia usiku kabla ya kulala,” anasema Ninfa, anayeishi huko Italia. “Nilifanya hivyo kwa kuwa nilitambua kwamba ni Neno la Mungu, na hata ingawa sikufurahia kuisoma, nilitaka kujua mambo ambayo Mungu aliandika katika Biblia. Nilitaka kuisoma Biblia nzima. Mwanzoni niliona ni jambo rahisi, lakini nilipofika kwenye sehemu ngumu, nikaacha kuisoma.”

      JE, WEWE pia una maoni kama ya Ninfa? Watu wengi wana maoni kama hayo. Ingawa hivyo, kama tulivyoona katika habari iliyotangulia, Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu, anataka ulielewe Neno lake. Lakini, unaweza kupata uelewaji huo jinsi gani? Hatua ya kwanza ni kumwomba Mtungaji wa Biblia akusaidie.

      Mitume wa Yesu walionwa kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu” kwa sababu hawakuwa wamehudhuria shule za kirabi ili wapate elimu ya kidini. (Matendo 4:13) Hata hivyo, Yesu aliwahakikishia kwamba wangeweza kuelewa Neno la Mungu. Jinsi gani? Yesu alieleza hivi: “Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba atatuma katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote.” (Yohana 14:26) Mungu alitumia roho hiyo takatifu, au nguvu za utendaji, kuumba dunia na uhai wote uliomo. (Mwanzo 1:2) Pia, aliitumia kuwaongoza waandikaji 40 hivi ili waandike mawazo yake katika Biblia. (2 Petro 1:20, 21) Roho hiyohiyo inaweza kuwasaidia watu wanaotaka kuielewa Biblia.

      Unaweza kuipokea roho takatifu ya Mungu jinsi gani? Ni lazima uombe kwa imani ili Mungu akupe roho takatifu. Kwa kweli, huenda ukahitaji kuendelea kuomba ili upewe roho hiyo. “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa,” akasema Yesu. “Ikiwa ninyi . . . mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:9, 13) Yehova yuko tayari kuwapa kwa ukarimu roho takatifu wale wanaomwomba kwa unyoofu. Nguvu hizo za utendaji zinaweza kukusaidia kuelewa maneno yaliyoongozwa kwa roho ambayo yaliandikwa katika Biblia maelfu ya miaka iliyopita. Pia, roho ya Mungu inaweza kukupa hekima inayohitajika ili uishi kupatana na ujumbe wenye nguvu ulio katika Biblia.—Waebrania 4:12; Yakobo 1:5, 6.

      Hivyo basi, kila mara kabla hujaanza kusoma Biblia, sali kwa Mungu na umwombe akupe roho takatifu ili ikusaidie kulielewa Neno lake.

  • 2. Soma Ukiwa na Maoni Mazuri
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Julai 1
    • Jinsi Unavyoweza Kuielewa Biblia

      2. Soma Ukiwa na Maoni Mazuri

      Je, rafiki yako amewahi kukuambia mambo mabaya kumhusu mtu fulani ambaye hujawahi kukutana naye? Baadaye ulipokutana na mtu huyo, je, mambo ambayo ulikuwa umeambiwa na rafiki yako kumhusu yalikufanya usione vipawa na sifa zake nzuri? Inaweza kuwa hivyo pia kuhusu Biblia.

      MTUME Paulo alitoa onyo kuhusu jambo linaloweza kutukia ikiwa tutasoma Biblia tukiwa na maoni yasiyofaa. Paulo aliandika hivi kuhusu Wayahudi fulani wa nyakati zake: “Nawatolea ushahidi kwamba wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.”—Waroma 10:2.

      Wayahudi hao wa karne ya kwanza hawakuwa tayari kukubali ukweli fulani ambao ulifunuliwa waziwazi na Maandiko ya Kiebrania, yaani, utambulisho wa Masihi. Yesu wa Nazareti alitimiza kila takwa la Kimaandiko na alitimiza kila unabii uliomhusu Masihi. Hata hivyo, maoni yasiyofaa ambayo Wayahudi walikuwa wameshikilia yaliwazuia wengi wao wasielewe Neno la Mungu.

      Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi hilo la Biblia? Ni jambo la maana kuisoma Biblia tukiwa na maoni mazuri. Maoni yasiyofaa yanaweza kumzuia msomaji asielewe ukweli ulio katika Biblia.

      Kwa mfano, profesa wa mambo ya kidini huko North Carolina, Marekani, anafafanua Biblia kuwa “kitabu ambacho kimejaa mawazo ya wanadamu na mengi ya mawazo hayo yanapingana na hayawezi kutupa mwongozo wenye kutegemeka maishani.” Ikiwa mtu angesoma Biblia akiwa na maoni ya kwamba ni “kitabu ambacho kimejaa mawazo ya wanadamu,” je, hatakuwa na mwelekeo wa kupuuza mwongozo au kanuni ambazo hapendi?

      Kinyume cha hilo, Biblia inatutia moyo tuisome kwa bidii. Maandiko yanasema hivi kuhusu Waberoya ambao waliishi katika siku za Paulo: “Walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:11) Kama wasomaji hao Waberoya, huenda ukahitaji kusoma Biblia ukiwa na maoni mazuri, na kuepuka maoni yoyote yasiyofaa ambayo yanaweza kukuzuia usiielewe. Soma Neno la Mungu ukiwa na maoni mazuri, na pia ukiwa na hamu ya kuelewa ujumbe wenye kusisimua kutoka kwa Mtungaji wake.

  • 3. Kubali Kusaidiwa na Wengine
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Julai 1
    • Jinsi Unavyoweza Kuielewa Biblia

      3. Kubali Kusaidiwa na Wengine

      Wakati mvumbuzi Edward John Eyre alipovuka kwa miguu Uwanda wa Nullarbor wenye ukame, wenyeji wa asili wa Australia walimfundisha Eyre jinsi ya kuteka maji kutoka kwenye marundo makubwa ya mchanga na miti ya mikalitusi. Kwa kuwa alikubali msaada kutoka kwa wale walioelewa nchi hiyo, baadaye aliokoa uhai wake.

      KAMA mfano huo unavyoonyesha, ili mtu afanikiwe katika kutimiza kazi fulani ngumu, kwa kawaida anahitaji kusaidiwa na mtu mwenye uzoefu. Ndivyo unavyopaswa kufanya pia unapoanza kuisoma Biblia.

      Yesu hakutazamia wafuasi wake waelewe Biblia bila kusaidiwa na wengine. Pindi moja, ‘alifungua akili zao ili wafahamu maana ya Maandiko.’ (Luka 24:45) Yesu alitambua kwamba wasomaji wa Biblia wanahitaji kusaidiwa ili waelewe mafundisho ya Maandiko.

      Ni Nani Atakayekusaidia?

      Yesu aliwaagiza wafuasi wake wa kweli wawasaidie watu. Kabla hajapanda kwenda mbinguni, Yesu aliwaamuru hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kazi kuu ya Wakristo inatia ndani kufundisha, jambo ambalo linahusisha kueleza jinsi ambavyo kanuni za Biblia zinaweza kufuatwa kila siku maishani. Wakristo wa kweli wanawasaidia wengine waelewe Biblia.

      Muda mfupi baada ya Yesu kuwapa wafuasi wake daraka hilo, jambo lenye kusisimua lilitokea. Biblia inamtaja ofisa wa makao ya kifalme kutoka Ethiopia ambaye alikuwa akisoma sehemu ya unabii wa Isaya. Alisoma kifungu ambacho hakuelewa hata kidogo. Kulingana na Biblia, kifungu kilichomtatanisha ni hiki: “Kama kondoo aliletwa machinjioni, na kama mwana-kondoo asiye na sauti mbele ya mwenye kumnyoa, ndivyo huyo asivyofungua kinywa chake. Wakati wa kufedheheshwa kwake hukumu iliondolewa mbali naye. Ni nani atakayeeleza kirefu habari za kizazi chake? Kwa sababu uhai wake unaondolewa kutoka duniani.”—Matendo 8:32, 33; Isaya 53:7, 8.

      Ofisa huyo alimuuliza hivi Filipo, Mkristo mwenye uzoefu ambaye alielewa Maandiko vizuri: “Nabii anasema hivyo juu ya nani? Juu yake mwenyewe au juu ya mtu mwingine?” (Matendo 8:34) Mwethiopia huyo mnyoofu alikuwa ametoka Yerusalemu kuabudu, na inaelekea kwamba alikuwa amesali ili apate mwongozo. Inaonekana kwamba alikuwa akisoma kwa hamu akiwa na mtazamo wa unyenyekevu. Ingawa hivyo, bado ofisa huyo hakuelewa kifungu hicho. Kwa unyenyekevu, alimwomba Filipo amsaidie. Baada ya Filipo kueleza kifungu hicho vizuri, mwanamume huyo alifurahi sana hivi kwamba akachochewa kuwa Mkristo.—Matendo 8:35-39.

      Mashahidi wa Yehova wanaendeleza kazi iliyokuwa ikifanywa na Filipo na Wakristo wengine wa kale. Katika nchi zaidi ya 235, Mashahidi wanajitolea kuwasaidia wengine waelewe mambo ambayo Biblia inafundisha hasa. Wanafanya hivyo kwa kujifunza na watu habari mbalimbali kutoka katika Maandiko. Njia hii ya kujifunza Biblia hatua kwa hatua inahusisha kuchanganua yale ambayo Biblia inasema kuhusu habari au kichwa fulani kikuu.a—Ona sanduku “Majibu Yanayoridhisha ya Maswali ya Biblia.”

      “Maswali Yangu Yote Yalijibiwa”

      Steven, Valvanera, na Jo-Anne, ambao walitajwa mwanzoni, walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. “Nilishangaa sana kuona kwamba kwa kulinganisha kanuni au masimulizi mbalimbali ya Kimaandiko, kwa kawaida nilipata katika Biblia majibu ya maswali yangu,” anasema Steven. “Kabla sijaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, hakuna mtu aliyenisaidia kupata majibu. Nilitiwa moyo nilipojua kwamba Biblia si kitabu cha mabishano yasiyo na mwisho wala kitabu chenye mawazo yanayopingana.”

      Valvanera anakubali hivi: “Kila jambo ambalo nilijifunza na Mashahidi lilieleweka wazi na lilipatana na akili.” Anaendelea kusema hivi: “Sikuamini mambo niliyojifunza kwa sababu tu ‘Dini’ iliyafundisha, lakini niliamini kwa kuwa kila jambo lilifafanuliwa kwa njia yenye kusadikisha.” Jo-Anne anaeleza hivi: “Kwa kuwa maswali yangu yote yalijibiwa kwa kutumia Biblia, jambo hilo lilinichochea kumheshimu sana Mtungaji wa Biblia kwa kuwa alijua kimbele kwamba wanadamu wangekuwa na maswali mengi yenye kutatanisha na hivyo akaweka majibu katika Biblia.”

      Je, unamfahamu Shahidi yeyote wa Yehova? Tafadhali mwombe akuonyeshe jinsi funzo la Biblia linavyofanywa. Ikiwa humfahamu kibinafsi Shahidi yeyote wa Yehova, tafadhali tuandikie ukitumia moja ya anwani zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 4 wa gazeti hili. Unaweza kuielewa Biblia ikiwa utakubali msaada wa roho takatifu ya Mungu, ikiwa utakuwa na maoni yanayofaa, na ikiwa utakubali kujifunza pamoja na mwalimu wa Biblia anayestahili. Ndiyo, unaweza kuielewa Biblia!

      [Maelezo ya chini]

      a Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kinachochapishwa na Mashahidi wa Yehova kimewasaidia wengi kujifunza habari mbalimbali za Maandiko.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

      Majibu Yanayoridhisha ya Maswali ya Biblia

      Zifuatazo ni kati ya habari ambazo Mashahidi wa Yehova wanazungumzia wanapojifunza na watu Biblia:

      • Mungu ana kusudi gani kwa dunia?

      • Wafu wako wapi?

      • Je, tunaishi katika “siku za mwisho”?

      • Kwa nini Mungu anawaacha watu wateseke?

      • Ninaweza kufanya nini ili maisha ya familia yangu yawe yenye furaha?

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Ili kuelewa Biblia . . . sali ili upate roho takatifu ya Mungu, isome ukiwa na maoni mazuri, kubali kusaidiwa na wengine

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki