Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Unaweza Kufurahia Kuielewa Biblia
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 1
    • Unaweza Kufurahia Kuielewa Biblia

      BIBLIA ina kweli zenye thamani kutoka kwa Mungu. Inatueleza kuhusu kusudi la maisha, kile kinachosababisha mateso ya wanadamu, na wakati ujao wa wanadamu. Inatufundisha jinsi ya kupata furaha, jinsi ya kupata marafiki, na jinsi ya kusuluhisha matatizo. Zaidi ya hayo, tunajifunza kuhusu Muumba wetu ambaye ni Baba yetu wa mbinguni, Yehova. Ujuzi huo hutuletea furaha na hutupa kusudi maishani.

      Biblia inalinganisha kupata ujuzi kumhusu Mungu na kula. Yesu alisema hivi: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4; Waebrania 5:12-14) Kama vile ni muhimu kwetu kula chakula kinachojenga mwili kila siku ili tuendelee kuishi, ndivyo ilivyo muhimu kulisoma Neno la Mungu kwa ukawaida ili tufaidike na ahadi ya Mungu ya uzima wa milele.

      Tunafurahia kula kwa sababu ya jinsi tulivyoumbwa na kwa sababu kula hutosheleza uhitaji wa msingi. Hata hivyo, tuna uhitaji mwingine wa msingi ambao tunapaswa kuutosheleza pia ikiwa tunataka kuwa wenye furaha. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Inawezekana kupata furaha kwa sababu uhitaji wetu wa kiroho unaweza kutoshelezwa kwa kulielewa Neno la Mungu.

      Ni kweli kwamba watu wengine huona ni vigumu kuielewa Biblia. Kwa mfano, huenda ukahitaji msaada kuyaelewa maandiko yanayorejelea desturi usizozijua au yale yanayotumia lugha ya mfano. Pia, kuna unabii mbalimbali ulioandikwa kwa lugha ya mfano ambao unaeleweka tu kwa kuyachunguza maandiko mengine ya Biblia yanayozungumzia habari hiyo. (Danieli 7:1-7; Ufunuo 13:1, 2) Hata hivyo, unaweza kuielewa Biblia. Ni nini kinachoonyesha kwamba inawezekana uielewe?

      Wote Wanaweza Kufurahia

      Biblia ni Neno la Mungu. Ndani yake Mungu anatueleza yale anayotaka tufanye. Je, Mungu angeandaa kitabu ambacho ingekuwa vigumu kukielewa au ambacho kingeeleweka tu na watu wenye elimu ya juu? Hapana, Yehova hangetenda hivyo. Kristo Yesu alisema hivi: “Ni baba gani kati yenu ambaye, ikiwa mwana wake anaomba samaki, labda atampa nyoka badala ya samaki? Au ikiwa pia anaomba yai, atampa nge? Kwa hiyo, ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:11-13) Hivyo, uwe na hakika kwamba unaweza kuielewa Biblia na kwamba ukimwomba Mungu kwa unyoofu, atakupa msaada ambao unahitaji ili ulielewe Neno lake. Ni wazi kwamba hata watoto wanaweza kuyaelewa na kuyathamini mafundisho ya msingi ya Biblia.—2 Timotheo 3:15.

      Ingawa jitihada zinahitajiwa ili kuielewa Biblia, kufanya hivyo kunaweza kutuimarisha na kutuchochea sana. Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea wanafunzi wake wawili na kuzungumza nao kuhusu unabii mbalimbali wa Biblia. Simulizi la Luka linasema hivi: “Akaanzia Musa na Manabii wote, akawafasiria mambo yanayomhusu yeye mwenyewe katika Maandiko yote.” Matokeo yakawaje? Jioni hiyo, walipokuwa wakifikiria mambo waliyojifunza, wanafunzi hao waliambiana hivi: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi barabarani, alipokuwa akitufungulia Maandiko?” (Luka 24:13-32) Walifurahia kulielewa Neno la Mungu kwa sababu liliimarisha imani yao katika ahadi za Mungu nalo likawasaidia kuwa na mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao.

      Badala ya kuwa mzigo, ni jambo lenye kufurahisha na lenye manufaa kulielewa Neno la Mungu, kama vile inavyofurahisha kula chakula kinachojenga mwili. Unahitaji kufanya nini ili upate uelewaji huo? Makala inayofuata inaonyesha jinsi unavyoweza kufurahia “kumjua Mungu.”—Methali 2:1-5.

      [Picha katika ukurasa wa 4]

      Kama baba mwenye upendo, Yehova anatupa roho takatifu ili itusaidie kuielewa Biblia

  • Ni Nini Kitakachokusaidia Kuielewa Biblia?
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 1
    • Ni Nini Kitakachokusaidia Kuielewa Biblia?

      “UMEWAFICHA kwa uangalifu wenye hekima na walio na akili mambo hayo, nawe umeyafunua kwa watoto.” (Luka 10:21) Maneno hayo ambayo Yesu alimwambia Baba yake wa mbinguni yanaonyesha kwamba ili kuielewa Biblia, tunahitaji kuwa na mtazamo unaofaa. Hekima ya Yehova imeonekana wazi katika maana ya kwamba ametokeza kitabu ambacho ni wanyenyekevu tu, watu wanaokubali kufundishwa ndio wanaoweza kukielewa vizuri.

      Wengi wetu huona ni vigumu kuwa wanyenyekevu. Sote tumerithi mwelekeo wa kuwa wenye kiburi. Isitoshe, tunaishi katika “siku za mwisho,” miongoni mwa watu “wenye kujipenda wenyewe, . . . wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi.” (2 Timotheo 3:1-4) Hiyo ni mitazamo inayotuzuia tusilielewe Neno la Mungu. Inasikitisha kwamba, kwa kiasi fulani sote tunaathiriwa na watu tunaoshughulika nao. Hivyo basi, unawezaje kuwa na mtazamo unaohitajiwa ili kuielewa Biblia?

      Kutayarisha Moyo na Akili

      Ezra, kiongozi wa kale wa watu wa Mungu, “alikuwa ameutayarisha moyo wake kutafuta shauri katika sheria ya Yehova.” (Ezra 7:10) Je, kuna namna tunavyoweza kuutayarisha moyo wetu? Ndiyo. Tunaweza kuanza kwa kudumisha mtazamo unaofaa kuhusu Maandiko. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Ingawa watu walitumiwa kuiandika Biblia, mambo waliyoandika yalitoka kwa Yehova. Kutambua ukweli huo muhimu kutatusaidia kukubali mambo tunayosoma.—2 Timotheo 3:16.

      Njia nyingine ya kutayarisha moyo wetu ni kupitia sala. Kwa kuwa Biblia iliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu, roho hiyohiyo inaweza kutusaidia kuelewa ujumbe wake. Hivyo, tunapaswa kusali ili tupate msaada huo. Ona jinsi mtunga-zaburi alivyoandika kuhusiana na hilo: “Unifanye nielewe, ili nipate kuishika sheria yako nami nipate kuishika kwa moyo wote.” (Zaburi 119:34) Tunahitaji kusali si ili tupate uwezo wa akili wa kuelewa mambo yaliyoandikwa tu, bali pia tunahitaji kusali ili tuwe na mwelekeo wa moyo ambao utatuwezesha kukubali yale ambayo Biblia inasema. Ili kuielewa Biblia, tunahitaji kuwa tayari kukubali ukweli.

      Unapotafakari ili kuwa na mtazamo unaofaa, fikiria jinsi kujifunza Biblia kunavyoweza kukusaidia. Tuna sababu nyingi nzuri za kulisoma Neno la Mungu, lakini sababu muhimu hata zaidi ni kwamba Biblia inatusaidia kumkaribia Mungu. (Yakobo 4:8) Tunaposoma jinsi Yehova anavyotenda katika hali mbalimbali, jinsi anavyowathamini wale wanaompenda, na jinsi anavyowatendea wale wanaomwacha, tunatambua yeye ni mtu wa aina gani. Sikuzote kusudi letu kuu la kusoma Biblia linapaswa kuwa kumjua Mungu vizuri zaidi na hivyo kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye.

      Vizuizi vya Kuwa na Mtazamo Unaofaa

      Ni nini kinachoweza kutuzuia tusilielewe Neno la Mungu? Kizuizi kimoja ni kushikilia maoni ya watu ambao tunahisi kwamba tunapaswa kuwa waaminifu kwao. Kwa mfano, huenda ukashikilia imani na maoni ya watu wenye kuheshimika. Hata hivyo, ungefanyaje ikiwa watu hao hawathamini kweli ya Neno la Mungu? Chini ya hali kama hizo, huenda ikawa vigumu kuelewa yale ambayo Biblia hufundisha hasa. Hivyo, Biblia inatutia moyo kuchunguza kwa uangalifu mambo ambayo tumefundishwa.—1 Wathesalonike 5:21.

      Maria, mama ya Yesu, alikabili tatizo hilo. Alilelewa kulingana na mapokeo ya Wayahudi. Alifuata kwa uangalifu Sheria ya Musa na bila shaka alienda kwenye sinagogi. Baadaye, alitambua kwamba namna ya ibada ambayo alifundishwa na wazazi wake haikuwa yenye kukubaliwa tena na Mungu. Hivyo, Maria akakubali mafundisho ya Yesu naye akawa kati ya washiriki wa kwanza wa kutaniko la Kikristo. (Matendo 1:13, 14) Kwa kufanya hivyo hakuwadharau wazazi wake wala desturi zao; badala yake, alionyesha upendo wake kwa Mungu. Ili tufaidike kutokana na Biblia, kama vile Maria, tunapaswa kwanza kuwa waaminifu kwa Mungu kuliko kuwa waaminifu kwa mtu mwingine yeyote.

      Kwa kusikitisha, watu wengi hawaithamini kweli ya Biblia. Baadhi yao wanafurahia kufuata mapokeo ya kidini yanayotegemea uwongo. Wengine wanaidharau kweli kwa maneno na kwa mtindo wao wa maisha. Hivyo, kuikubali kweli ya Biblia kunahitaji kujidhabihu kwa kadiri fulani: Kunaweza kukufanya usielewane na marafiki, majirani, wafanyakazi wenzako, na hata watu wa familia yako. (Yohana 17:14) Hata hivyo, mwanamume mwenye hekima Sulemani aliandika hivi: “Nunua kweli wala usiiuze.” (Methali 23:23) Ukiithamini sana kweli, Yehova atakusaidia uielewe Biblia.

      Hata hivyo, kizuizi kingine cha kuuelewa ujumbe wa Biblia ni kukataa kutumia mambo inayosema. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi mmepewa uwezo wa kuzielewa siri takatifu za ufalme wa mbinguni, lakini wao hawakupewa. Kwa maana moyo wa watu hawa umekuwa mgumu, nao wamesikia kwa masikio yao bila kuitikia.” (Mathayo 13:11, 15) Wengi wa wale ambao Yesu alihubiria hawakutaka kubadilika. Lo! Jinsi walivyokuwa tofauti sana na mwanabiashara msafiri ambaye Yesu alitaja katika mfano wake! Baada ya kupata lulu yenye thamani kubwa, mwanabiashara huyo aliuza haraka vitu vyote alivyokuwa navyo ili kuinunua. Vivyo hivyo, kuielewa kweli ya Biblia kunapaswa kuwa muhimu kwetu.—Mathayo 13:45, 46.

      Ugumu wa Kukubali Kufundishwa

      Tatizo kubwa ambalo huwazuia watu wasiielewe Biblia ni kutotaka kufundishwa. Huenda mtu akaona ni vigumu kukubali mawazo mapya kutoka kwa mtu anayeonekana kuwa wa hali ya chini. Hata hivyo, mitume wa Yesu Kristo walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Matendo 4:13) Akifafanua kwa nini mitume hao walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu,” Paulo aliandika hivi: “Mnaona mwito wake kwenu, akina ndugu, kwamba si wengi wenye hekima katika njia ya kimwili walioitwa, si wengi wenye nguvu, si wengi wa uzawa wa cheo; bali Mungu alivichagua vitu vipumbavu vya ulimwengu, ili awaaibishe watu wenye hekima.” (1 Wakorintho 1:26, 27) Ikiwa unaona kwamba ni vigumu kwako kunyenyekea unapofundishwa na mtu wa hali ya chini, kumbuka kwamba mtu huyo anatumiwa tu na Mungu ili kukufundisha. Je, kuna pendeleo kubwa zaidi kuliko lile la kufundishwa na Yehova, ‘Mfundishaji wetu Mkuu’?—Isaya 30:20; 54:13.

      Naamani, kiongozi wa jeshi la Siria, aliona ni vigumu kukubali maagizo kutoka kwa mtu wa hali ya chini. Alimwendea Elisha nabii wa Yehova ili amponye ukoma. Hata hivyo, Naamani alipewa maagizo ya Mungu kuhusu uponyaji kupitia mtumishi fulani. Ujumbe huo na jinsi ulivyotolewa ulifanya iwe vigumu kwa Naamani kukubali maagizo hayo kwa unyenyekevu, hivi kwamba mwanzoni alikataa kutii neno la nabii wa Mungu. Baadaye, Naamani alibadili mtazamo wake naye akaponywa. (2 Wafalme 5:9-14) Tunakabili tatizo hilohilo tunapojifunza Biblia. Huenda tukajua kwamba ili kuponywa kiroho na kiadili, tunahitaji kufuata njia mpya ya maisha. Je, tutanyenyekea ili kuruhusu mtu fulani atufundishe mambo tunayopaswa kufanya? Ni wale tu walio tayari kufundishwa ndio wanaoweza kuielewa Biblia.

      Mtu mmoja aliyekuwa na mamlaka chini ya Kandake, malkia wa Waethiopia, alionyesha mtazamo unaofaa. Alikuwa akirudi Afrika akiwa ndani ya gari lake la kukokotwa wakati mwanafunzi Filipo alipokimbia kandokando yake na kumkaribia. Filipo alimwuliza mwanamume huyo ikiwa alielewa mambo aliyokuwa akisoma. Ofisa huyo mnyenyekevu alijibu hivi: “Ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” Baada ya kulielewa Neno la Mungu, mtu huyo alibatizwa. Baada ya hapo, “aliendelea kwenda zake akishangilia.”—Matendo 8:27-39.

      Kwa ujumla, Mashahidi wa Yehova ni watu wa kawaida tu. Kila juma wanaongoza mafunzo ya Biblia katika nyumba za watu zaidi ya milioni sita. Kwa kuwa Biblia inafundisha njia bora zaidi ya maisha, inaeleza kuhusu tumaini hakika la pekee kwa wanadamu, na inatuwezesha kumjua Mungu, mamilioni ya watu wametambua kwamba kujifunza Biblia na kuelewa mambo inayosema huleta furaha kubwa. Wewe pia unaweza kupata furaha hiyo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki