Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Biblia Ni Neno la Mungu?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Machi 1
    • Je, Biblia Ni Neno la Mungu?

      “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 TIMOTHEO 3:16, 17.

      MTUME Paulo alisema maneno yenye nguvu kama nini kuhusu thamani kubwa ya Biblia! Bila shaka, alikuwa akizungumzia hasa sehemu ya Biblia ambayo alikuwa nayo wakati huo, yaani, maandishi ambayo nyakati nyingine wengine wanayaita Agano la Kale. Lakini maneno yake yanahusu pia vitabu vyote 66 vya Biblia, kutia ndani vile vilivyoandikwa na wanafunzi waaminifu wa Yesu katika karne ya kwanza W.K.

      Je, unaiheshimu sana Biblia kama Paulo alivyoiheshimu? Je, unafikiri kwamba kwa kweli waandikaji wa Biblia waliongozwa na roho ya Mungu? Wakristo wa karne ya kwanza waliamini hivyo. Sikuzote Wakristo wa kweli wameamini hivyo. Kwa mfano, kasisi Mwingereza wa karne ya 14, John Wycliffe, aliiona Biblia kuwa “sheria isiyokosea ya kweli.” Kikieleza kuhusu maneno ya Paulo yaliyo hapo juu, kitabu kimoja (The New Bible Dictionary) kinasema kwamba ‘kwa kuwa Biblia imeongozwa na roho ya Mungu basi ni hakika kwamba mambo yote ambayo inasema ni ya kweli.’

      Mitazamo ya Watu Kuelekea Biblia Yabadilika

      Hata hivyo, katika nyakati za hivi karibuni, watu wengi wameacha kuitegemea Biblia. Kitabu kimoja (The World’s Religions) kinasema hivi: “Wakristo wote [bado] wanakubali kwa maneno tu kwamba Biblia inategemeka katika kuongoza matendo yao na kujenga imani yao.” Hata hivyo, kwa matendo, mambo yamebadilika kabisa. Watu wengi sasa wanaiona Biblia kuwa “mapokeo ya wanadamu ambayo hayategemeki.” Ingawa wanatambua kwamba waandikaji wa Biblia walikuwa watu wenye imani kubwa, wanawaona kuwa watu wasio wakamilifu ambao walijitahidi sana kueleza kweli nzito za kiroho, lakini hawakuwa na ujuzi na elimu tuliyo nayo leo.

      Kwa kweli, ni watu wachache sana leo ambao wanaacha Biblia iongoze mawazo na matendo yao. Kwa mfano, ni mara ngapi unapowasikia watu wakisema kwamba viwango vya Biblia vya maadili vimepitwa na wakati na havitegemeki? Watu wengi wanaona ni sawa kupunguza uzito wa sheria na kanuni za Biblia au hata wanazipuuza kabisa ili kufanya yale wanayotaka. Watu fulani wanaodai kuwa Wakristo wanapuuza kimakusudi yale ambayo Biblia inasema kuhusu uasherati, uzinzi, ukosefu wa unyoofu, na ulevi.—1 Wakorintho 6:9, 10.

      Kwa nini wanatenda hivyo? Mwanzoni mwa karne ya 20, mchunguzi wa vitu vya kale Sir Charles Marston alitaja katika kitabu chake (The Bible Is True) sababu moja inayowafanya watu watende hivyo. Alisema kwamba watu walikuwa tayari sana “kukubali bila kupinga mawazo mengi yasiyo na maana ya waandikaji wa kisasa” ambao walipinga kabisa wazo la kwamba Biblia ni ya kweli. Je, bado wanafanya hivyo leo? Unapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mawazo na mafundisho ya wasomi ambao wanawachochea watu wasiamini Biblia? Ona jinsi habari inayofuata inavyosema kuhusu hilo.

  • Kwa Kweli Biblia Ni Neno la Mungu Lililoongozwa na Roho Yake
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Machi 1
    • Kwa Kweli Biblia Ni Neno la Mungu Lililoongozwa na Roho Yake

      MTUME Paulo alimaanisha nini hasa aliposema kwamba Biblia ‘iliongozwa na roho ya Mungu’? (2 Timotheo 3:16) Akiandika katika lugha ya Kigiriki, Paulo alitumia neno ambalo kihalisi linamaanisha “lenye pumzi ya Mungu.” Paulo aliposema hivyo alimaanisha kwamba Mungu kupitia roho yake takatifu aliwaongoza waandikaji wa Biblia waandike tu mambo ambayo Alitaka waandike.

      Mtume Petro alisema kwamba waandikaji hao wa Biblia “walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Mtume Paulo alisema pia kwamba vitabu vya Biblia ni “maandishi matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.”—2 Timotheo 3:15.

      Watu wengi wanapinga kabisa kwamba Mungu ndiye mtungaji wa Biblia. Wachambuzi wameshambulia vikali usahihi wa Biblia wakiwa na mtazamo wa “kupuuza kwa dharau masimulizi ya Biblia,” kama alivyosema mchunguzi wa vitu vya kale Sir Charles Marston. Wengine wameikataa Biblia na kusema kwamba ni “mkusanyo tu wa hadithi za zamani za uwongo.”

      Chunguza Uthibitisho

      Hivyo basi, je, Biblia inaweza kutegemeka? Ni jambo la maana kwako kufanya uamuzi mzuri kuhusu jambo hilo. Kwa nini? Kwa sababu ikiwa kwa kweli Biblia ina ujumbe kutoka kwa Mungu mwenyewe, ni jambo hatari na la upumbavu kuipuuza. Ukiiona Biblia kuwa maneno ya wanadamu tu badala ya kuiona kuwa Neno la Mungu, haitaongoza matendo yako wala kutia nguvu imani yako.—1 Wathesalonike 2:13.

      Unaweza kuamua jinsi gani ikiwa utaitegemea Biblia? Unaamua jinsi gani ikiwa unaweza kuwaamini watu unaokutana nao? Bila shaka, ni vigumu sana kumwamini mtu ambaye humjui vizuri sana. Ni baada tu ya kuwajua watu vizuri ndipo unaweza kuamua ikiwa kwa kweli ni wanyoofu na wenye kutegemeka. Unaweza kuijua Biblia kwa njia hiyohiyo. Usikubali tu nadharia au mawazo ya ubaguzi ya kukisia-kisia ambayo yanachochea watu wasiiamini Biblia. Tumia wakati kuchunguza uthibitisho ambao unaunga mkono madai ya Biblia ya kwamba ‘imeongozwa na roho ya Mungu.’

      Kushambuliwa na “Marafiki”

      Usidanganywe kwa sababu watu fulani wanaojifanya kuwa marafiki wa Biblia wanaishambulia kwa kusema kwamba si sahihi na haitegemeki. Leo, wafafanuzi wengi wa Biblia, ingawa wanadai kuwa Wakristo, “wanasema kwamba Maandiko yametungwa na wanadamu,” kinasema kitabu kimoja (New Dictionary of Theology).

      Wanatheolojia wengi hawakubali kwamba majina ya wale wanaotajwa katika Biblia ndio walioandika vitabu vya Biblia. Kwa mfano, wengine wanasema kwamba kitabu cha Isaya hakikuandikwa na nabii Isaya. Wanasema kwamba kitabu hicho cha Biblia kiliandikwa miaka mingi baada ya siku za Isaya. Kitabu kimoja (Concise Bible Commentary) kilichoandikwa na Lowther Clarke kinadai kwamba kitabu cha Isaya “kiliandikwa na watu wengi na kwa vizazi vingi.” Lakini madai kama hayo yanapuuza ukweli wa kwamba Yesu Kristo na wanafunzi wake walitaja mara kwa mara kwamba Isaya ndiye aliyeandika kitabu hicho.—Mathayo 3:3; 15:7; Luka 4:17; Yohana 12:38-41; Waroma 9:27, 29.

      Jambo baya hata zaidi ni kwamba wachambuzi wa Biblia, kama vile mfafanuzi wa Biblia J. R. Dummelow, wanasema kwamba unabii mbalimbali ulio katika kitabu cha Danieli “kwa kweli ni matukio yaliyopita ya kihistoria, lakini mwandikaji anayaeleza kana kwamba ni unabii.” Kwa kusema hivyo, wanapuuza kwa mara nyingine tena ushahidi wa Yesu Kristo mwenyewe. Yesu alionya kuhusu kile alichokiita “lile chukizo linalosababisha ukiwa, kama vile lilivyosemwa kupitia nabii Danieli, likiwa limesimama katika mahali patakatifu.” (Mathayo 24:15) Je, ni jambo linalopatana na akili kwa Mkristo kuamini kwamba Yesu Kristo angeshiriki katika kuwadanganya watu, yaani, kuunga mkono mambo yaliyopita ya kihistoria ili yaonekane ni kana kwamba ni unabii? Bila shaka hapana.

      Je, Ni Jambo la Maana?

      “Lakini je, kweli ni jambo la maana kujua ni nani aliyeandika vitabu vya Biblia?” huenda ukauliza. Ndiyo, ni jambo la maana sana kujua hilo. Je, ungeamini hati au maandishi ambayo yanadai kuwa wosia au maneno ya mwisho yaliyoandikwa na rafiki yako ikiwa itajulikana baadaye kwamba kwa kweli si yeye aliyeyaandika? Namna gani ikiwa wataalamu wangekuambia kwamba hati au maandishi hayo ni ya uwongo, na kwamba marafiki wenye nia njema ndio walioandika mambo ambayo waliamini kuwa ni mapendezi ya rafiki yako? Je, si kweli kwamba jambo hilo litapunguza thamani ya hati hiyo? Je, unaweza kuwa na hakika kwamba hati hiyo kwa kweli ina mapendezi ya rafiki yako?

      Ndivyo ilivyo na Biblia. Haishangazi kwamba watu wengi, hata wale ambao wanadai kuwa Wakristo, wanapuuza mambo ambayo Biblia inasema kuhusu unyoofu, maadili ya ngono, na mambo mengine. Ni mara ngapi umewasikia watu wakisema kwa dharau, “Ah, lakini hayo yameandikwa katika Agano la Kale!”—kana kwamba mambo hayo si ya maana sana. Na wanasema hivyo hata ingawa mtume Paulo alisema kwamba ile sehemu wanayoiita Agano la Kale ni “maandishi matakatifu” ambayo ‘yaliongozwa na roho ya Mungu.’

      Huenda ukapinga kwa kusema hivi: “Kwa kweli hatuwezi kupuuza tu uthibitisho wa wataalamu na wasomi wote.” Bila shaka hatuwezi! Kwa mfano, tunawashukuru sana wasomi wanyoofu ambao wametusaidia kutambua maandishi ya kwanza kabisa ya Biblia. Bila shaka, kwa kuwa maandishi ya Biblia yalinakiliwa au kuandikwa kwa mkono tena na tena kwa karne nyingi, makosa madogo yaliingizwa ndani. Hata hivyo, kumbuka jambo hili: Kuna tofauti kubwa kati ya kutambua kwamba makosa madogo yaliingizwa ndani ya nakala za maandishi ya Biblia na kudai kwamba Biblia yote ilitungwa na wanadamu.

      Endelea Kuyaamini “Maandishi Matakatifu”

      Kabla ya kusema kwamba Biblia iliongozwa na Mungu, Paulo alimwambia Timotheo kwa nini maandishi hayo yaliyoongozwa na roho yalikuwa ya maana. Alisema hivi: “Katika siku za mwisho . . . watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.” (2 Timotheo 3:1, 13) Tayari katika siku za Paulo, inaelekea ‘watu wenye hekima na wenye akili’ walikuwa wakitumia “hoja zenye kushawishi” ili kuwadanganya watu na kudhoofisha imani yao katika Yesu Kristo. (1 Wakorintho 1:18, 19; Wakolosai 2:4, 8) Ili kujilinda na uvutano mbaya wa watu hao, mtume Paulo alimhimiza Timotheo ‘aendelee katika mambo aliyojifunza tangu utoto mchanga kupitia maandishi matakatifu’ kutoka kwa Mungu.—2 Timotheo 3:14, 15.

      Ni jambo la maana pia kwako kufanya hivyo katika ‘siku hizi za mwisho.’ Usipuuze hatari ya kudanganywa na “hoja zenye kushawishi” zinazotolewa mara nyingi na watu wajanja sana. Badala yake, kama Wakristo wa karne ya kwanza, jilinde mwenyewe kwa kutegemea kabisa mambo unayojifunza kutoka katika Biblia, ambayo kwa kweli ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake.

      Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujenga imani yako katika Biblia. Kwa mfano, wanaweza kukuonyesha jinsi ambavyo kanuni za Biblia zimethibitika kuwa zenye kutegemeka kabisa katika historia yote; jinsi Biblia inavyopatana na sayansi wakati inapozungumzia mambo ya kisayansi; jinsi inavyopatana kabisa kutoka mwanzo mpaka mwisho; jinsi ambavyo unabii wake mbalimbali umetimia kwa ukamili, na mambo mengine mengi. Ukipenda unaweza kuwaandikia wachapishaji wa gazeti hili ili upate habari ambazo zimesaidia mamilioni ya watu wenye mioyo minyoofu kuona kwamba Biblia kwa kweli ni Neno la Mungu.

      [Blabu katika ukurasa wa 5]

      Unaamua jinsi gani ikiwa unaweza kuwaamini watu unaokutana nao?

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      Tunawashukuru sana wasomi wanyoofu ambao wametusaidia kupata maandishi ya kwanza kabisa ya Biblia

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki