-
Sehemu ya 1—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya DuniaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 22
Sehemu ya 1—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
Hiki ni cha kwanza kati ya visehemu vitano katika sura ambayo huripoti jinsi utendaji wa Mashahidi wa Yehova umefika duniani pote. Sehemu ya 1, inayozungumza juu ya enzi ya kutoka miaka ya 1870 hadi 1914, imo katika kurasa 404 hadi 422. Jamii ya kibinadamu haijapata nafuu kutokana na misukosuko iliyosababishwa na Vita ya Ulimwengu 1, iliyoanza katika 1914. Huo ndio mwaka ambao Wanafunzi wa Biblia walikuwa wameutambulisha kwa muda mrefu kuwa waonyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa.
KABLA ya kupaa mbinguni, Yesu Kristo aliwapa mitume wake utume, akisema: “Nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Mdo. 1:8, NW) Pia alikuwa ametabiri kwamba “habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14, NW) Kazi hiyo haikukamilishwa katika karne ya kwanza. Sehemu kubwa yayo imefanywa katika nyakati za kisasa. Na rekodi ya kukamilishwa kwayo tokea miaka ya 1870 hadi sasa ni yenye kusisimua kwelikweli.
Ijapokuwa Charles Taze Russell alipata kujulikana sana kwa sababu ya hotuba zake za Biblia zilizotangazwa sana, kupendezwa kwake hakukuwa tu katika wasikilizaji wengi lakini katika watu. Hivyo, muda mfupi baada ya kuanza kutangaza Watch Tower katika 1879, alianza safari ndefu ili kutembelea vikundi vidogo vya wasomaji wa gazeti hilo na kuzungumza Maandiko pamoja nao.
C. T. Russell alihimiza wale walioamini ahadi zenye thamani za Neno la Mungu wazishiriki pamoja na wengine. Wale ambao mioyo yao ilichochewa sana na yale waliyojifunza walionyesha bidii halisi katika kufanya hilohilo. Ili kusaidia kazi, habari iliyochapwa ilitolewa. Mapema katika 1881, idadi fulani ya trakti zilitokea. Kisha habari kutoka hizo iliunganishwa na habari zaidi ili kufanyiza kijitabu Food for Thinking Christians chenye habari nyingi zaidi, na nakala 1,200,000 zilitayarishwa ili zigawanywe. Lakini kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia (labda 100 wakati ule) kingewezaje kugawanya nakala hizo zote?
Kufikia Waenda-Kanisani
Baadhi yazo zilipewa watu wa ukoo na marafiki. Idadi fulani ya magazeti ya habari yalikubali kupeleka nakala moja kwa kila mmoja wa waandikishaji wayo. (Mkazo wa pekee ulitiwa kwenye magazeti ya kila juma na ya kila mwezi ili kwamba Food for Thinking Christians kiweze kufikia watu wengi walioishi katika maeneo ya mashambani.) Lakini ugawanyaji mwingi ulifanywa katika Jumapili kadhaa mfululizo mbele ya makanisa katika Marekani na Uingereza. Hakukuwa na Wanafunzi wa Biblia wa kutosha kufanya kazi yote wao binafsi, hivyo waliwalipa wengine ili wasaidie.
Ndugu Russell alituma washirika wawili, J. C. Sunderlin na J. J. Bender, Uingereza ili kusimamia kazi ya kugawanya nakala 300,000 huko. Ndugu Sunderlin alienda London, hali Ndugu Bender alisafiri kwenda kaskazini katika Scotland na kisha akafanya kazi akielekea kusini. Majiji makubwa ndiyo yaliyokaziwa fikira zaidi. Kwa njia ya matangazo ya magazeti ya habari, watu wenye uwezo walipatikana, na mikataba ilifanywa pamoja nao wapate wasaidizi wa kutosha kugawanya mafungu yao ya nakala. Wagawanyaji karibu 500 waliajiriwa kazi katika London pekee. Kazi ilifanywa haraka, katika Jumapili mbili mfululizo.
Mwaka huohuo, mipango ilifanywa ili Wanafunzi wa Biblia ambao wangeweza kutumia nusu au zaidi ya wakati wao katika kazi ya Bwana tu, wawe makolpota, wakigawanya fasihi kwa ajili ya funzo la Biblia. Watangulizi hao wa wale wanaojulikana leo kuwa mapainia walifikia ugawanyaji wenye kutokeza kikweli wa habari njema.
Wakati wa mwongo uliofuata, Ndugu Russell alitayarisha trakti mbalimbali ambazo zingeweza kutumiwa kwa urahisi kueneza baadhi ya zile kweli za Biblia zenye kutokeza walizokuwa wamejifunza. Pia aliandika mabuku kadhaa ya Millenial Dawn (baadaye yaliitwa Studies in the Scriptures). Kisha akaanza kusafiri kwenye nchi nyinginezo ili aeneze evanjeli kibinafsi.
Russell Asafiri Ng’ambo
Katika 1891 alizuru Kanada, ambako kupendezwa kwa kutosha kulikuwa kumechochewa tangu 1880 hivi kwamba kusanyiko lililohudhuriwa na 700 lingeweza kufanywa sasa katika Toronto. Pia alisafiri Ulaya katika 1891 ili kuona ni jambo gani lingeweza kufanywa ili kusogeza mbele kuenezwa kwa kweli huko. Safari hiyo ilimpeleka Ireland, Scotland, Uingereza, nyingi za nchi za bara la Ulaya, Urusi (lile eneo liitwalo sasa Moldova), na Mashariki ya Kati.
Alifikia mkataa gani baada ya kuwasiliana na watu katika safari hiyo? “Sisi hatukuona kufunguka au utayari kwa ajili ya kweli katika Urusi . . . Hatukuona jambo lolote la kututia moyo tutumainie vuno lolote katika Italia au Uturuki au Austria au Ujerumani,” akaripoti. “Lakini Norway, Sweden, Denmark, Uswisi, na hasa Uingereza, Ireland, na Scotland, ni mashamba yaliyo tayari na yanangojea kuvunwa. Mashamba hayo yaonekana yakilia, Njooni huku mtusaidie!” Hiyo ilikuwa ile enzi ambayo Kanisa Katoliki lilikuwa lingali likikataza usomaji wa Biblia, wakati Waprotestanti wengi walikuwa wakiacha makanisa yao, na wengi, wakikatishwa tamaa na makanisa, walikuwa wakikataa Biblia kabisa.
Ili kusaidia wale watu waliokuwa na njaa kiroho, baada ya safari ya Ndugu Russell katika 1891, jitihada zilizoongezwa zilifanywa kutafsiri fasihi katika lugha za Ulaya. Pia, mipango ilifanywa ili kuchapa na kuweka akiba ya fasihi katika London ili fasihi hizo ziweze kupatikana kwa urahisi kwa matumizi katika Uingereza. Shamba la Uingereza, lilithibitika kwelikweli kuwa tayari kuvunwa. Kufikia 1900, tayari kulikuwa makutaniko tisa na jumla ya Wanafunzi wa Biblia 138—miongoni mwao makolpota fulani wenye bidii. Wakati Ndugu Russell alipotembelea Uingereza tena katika 1903, watu elfu moja walikusanyika katika Glasgow ili kumsikia akihutubu juu ya “Matumaini na Matarajio ya Mileani,” 800 walihudhuria katika London, na wasikilizaji 500 kufikia 600 katika miji mingine.
Hata hivyo, katika kuthibitisha maoni ya Ndugu Russell, baada ya ziara yake miaka 17 ilipita kabla ya kutaniko la kwanza la Wanafunzi wa Biblia kuundwa katika Italia, katika Pinerolo. Vipi Uturuki? Wakati wa miaka ya mwisho-mwisho ya 1880, Basil Stephanoff alikuwa amehubiri katika Makedonia, katika ile iliyoitwa wakati ule Uturuki ya Ulaya. Ijapokuwa wengine walionekana kuonyesha kupendezwa, wengine kutoka katika wale waliodai kuwa ndugu walitoa ripoti za uwongo, zilizomfanya atiwe gerezani. Haikuwa mpaka 1909 kwamba barua kutoka kwa Mgiriki katika Smirna (sasa Izmir), Uturuki, iliripoti kwamba kikundi huko kilikuwa kikijifunza kwa uthamini vichapo vya Watch Tower. Kwa habari ya Austria, Ndugu Russell mwenyewe alirudi katika 1911 ili kutoa hotuba katika Vienna, ikawa tu kwamba mkutano ulikatizwa na wafanyaghasia. Katika Ujerumani pia, itikio lenye uthamini lilikuja hatua kwa hatua. Lakini Waskandinevia walionyesha kujua zaidi uhitaji wao wa kiroho.
Waskandinevia Washiriki Pamoja na Wengine
Wasweden wengi walikuwa wakiishi katika Amerika. Katika 1883 sampuli ya nakala ya Watch Tower iliyotafsiriwa katika Kisweden ilitolewa ili kugawanywa miongoni mwao. Upesi nakala hizo zikafikia kwa njia ya barua watu wa ukoo na marafiki katika Sweden. Bado hakukuwa na fasihi zilizokuwa zimetolewa katika Kinorway. Hata hivyo, katika 1892, mwaka baada ya safari ya Ndugu Russell kwenda Ulaya, Knud Pederson Hammer, Mnorway aliyekuwa amejifunza kweli katika Amerika, alirudi Norway yeye binafsi ili kutolea watu wake wa ukoo ushahidi.
Halafu, katika 1894, wakati fasihi zilipoanza kutangazwa katika lugha ya mchanganyiko ya Kidenmark na Kinorway, Sophus Winter, Mdenmark-Mwamerika mwenye umri wa miaka 25, alitumwa Denmark akiwa na ugavi wa kugawanya. Kufikia masika yaliyofuata, alikuwa ameangusha mabuku 500 ya Millennial Dawn. Katika muda mfupi, wengine wachache waliosoma vichapo hivyo walishiriki katika kazi pamoja naye. Kwa kuhuzunisha, baadaye aliacha kuona thamani ya pendeleo lake lenye thamani alilokuwa nalo; lakini wengine waliendelea kuacha nuru iangaze.
Hata hivyo, kabla ya kuacha utumishi, Winter alifanya kazi fulani ya kolpota katika Sweden. Muda mfupi baada ya hapo, nyumbani mwa rafiki katika kisiwa cha Sturkö, August Lundborg, kijana kapteni wa Jeshi la Wokovu, aliona mabuku mawili ya Millennial Dawn. Aliyaazima, akayasoma kwa hamu, akaacha kanisa, na kuanza kushiriki pamoja na wengine yale aliyokuwa amejifunza. Macho ya kijana mwingine, P. J. Johansson, yalifunguliwa kama tokeo la kusoma trakti aliyookota juu ya benchi la bustanini.
Kikundi cha Wasweden kilipoanza kukua, baadhi yao walienda Norway ili kugawanya fasihi za Biblia. Hata kabla ya jambo hilo, fasihi zilikuwa zimewasili katika Norway kwa njia ya posta kutoka kwa watu wa ukoo katika Amerika. Ni kwa njia hiyo kwamba Rasmus Blindheim alianza utumishi wa Yehova. Miongoni mwa wengine katika Norway, Theodor Simonsen, mhubiri wa kanisa la Free Mission, alipokea kweli wakati wa miaka hiyo ya mapema. Alianza kukanusha fundisho la moto wa helo katika hotuba zake katika kanisa la Free Mission. Wasikilizaji wake waliinuka juu kwa kusisimuliwa na habari hiyo ya ajabu; lakini ilipojulikana kwamba alikuwa amekuwa akiwasiliana na “Millennial Dawn,” alifukuzwa kutoka kanisa. Hata hivyo, yeye aliendelea tu kuongea juu ya mambo mema aliyokuwa amejifunza. Kijana mwingine aliyepokea baadhi ya fasihi alikuwa Andreas Øiseth. Mara aliposadikishwa kwamba alikuwa amepata kweli, aliondoka kwenye shamba la familia akaanza kazi ya kolpota. Alifanya kazi kwa utaratibu kuelekea kaskazini, kisha kusini kuelekea zile ghuba ndogo, bila kupita kijiji chochote. Wakati wa kipupwe alichukua ugavi wake—chakula, mavazi, na fasihi—katika kigari cha kujisukuma kwa mguu juu ya theluji, nao watu wenye ukaribishaji-wageni walimwandalia mahali pa kulala. Katika safari ya miaka minane, alieneza habari njema katika karibu nchi nzima.
Ebba, mke wa August Lundborg, alitoka Sweden akaenda Finland kufanya kazi ya kolpota katika 1906. Karibu wakati uo huo, watu waliokuwa wakirudi kutoka Marekani walikuja na fasihi za Watch Tower na kuanza kushiriki yale waliyokuwa wakijifunza. Hivyo katika muda wa miaka michache, Emil Österman, aliyekuwa akitafuta kitu bora zaidi ya kilichokuwa kikitolewa na makanisa, alipata The Divine Plan of the Ages. Alikishiriki pamoja na rafiki yake Kaarlo Harteva, aliyekuwa akitafuta pia. Akitambua thamani ya walichokuwa nacho, Harteva alikitafsiri katika Kifinland na, kwa msaada wa kifedha wa Österman, akapanga kitangazwe. Pamoja walianza kukigawanya. Wakionyesha roho ya kweli ya kueneza evanjeli, waliongea na watu hadharani, wakafanya ziara nyumba hadi nyumba, na kutoa hotuba katika majumba makubwa yaliyokuwa yanajaa kabisa. Katika Helsinki, baada ya kufunua mafundisho bandia ya Jumuiya ya Wakristo, Ndugu Harteva aliwaalika wasikilizaji watumie Biblia ili kutetea imani katika nafsi isiyoweza kufa, wakiweza. Macho yote yalielekezwa kwa makasisi waliokuwapo. Hakuna mtu aliyesema; hakuna mtu angeweza kukanusha taarifa iliyo wazi ipatikanayo kwenye Ezekieli 18:4. Baadhi ya wasikilizaji walisema kwamba ilikuwa vigumu kulala usiku huo baada ya yale waliyosikia.
Mtunza-Bustani Mnyenyekevu Awa Mweneza-Evanjeli Katika Ulaya
Wakati huohuo, Adolf Weber, akitiwa moyo na rafiki Mwanabaptisti mwenye umri mkubwa, aliondoka Uswisi kwenda Marekani akatafute uelewevu kamili zaidi wa Maandiko. Huko, ili kujibu tangazo, akawa mtunza-bustani wa Ndugu Russell. Kwa msaada wa The Divine Plan of the Ages (wakati huo kikipatikana kwa Kijerumani) na mikutano iliyoongozwa na Ndugu Russell, Adolf alipata ule ujuzi wa Biblia aliokuwa akitafuta, naye alibatizwa katika 1890. ‘Macho ya moyo wake yalitiwa nuru,’ hivi kwamba alithamini kikweli ile fursa bora sana iliyokuwa imefunguka mbele yake. (Efe. 1:18) Baada ya kutoa ushahidi kwa bidii kwa muda fulani katika Marekani, alirudi katika nchi alimozaliwa akaanze kazi “katika shamba la mizabibu la Bwana” huko. Hivyo, kufikia miaka ya katikati ya 1890, alikuwa amerudi Uswisi akishiriki kweli za Biblia pamoja na wale waliokuwa na mioyo yenye kuitikia.
Adolf alipata riziki yake akiwa mtunza-bustani na mtunza-misitu, lakini lililompendeza zaidi ni kueneza evanjeli. Alitolea ushahidi wale aliofanya kazi nao, pamoja na watu katika miji na vijiji vya karibu vya Uswisi. Yeye alijua lugha kadhaa, naye alitumia ujuzi huo kutafsiri vichapo vya Sosaiti katika Kifaransa. Wakati wa kipupwe alikuwa akipakia fasihi za Biblia katika mfuko wake na kwenda Ufaransa kwa miguu, na nyakati nyingine alisafiri kaskazini-magharibi kwenda Ubelgiji na kusini kwenda Italia.
Ili kufikia watu ambao huenda yeye binafsi asiweze kuonana nao, alitia matangazo katika magazeti na majarida akivuta fikira zao kwenye fasihi zilizopatikana kwa ajili ya funzo la Biblia. Elie Thérond, kutoka katikati mwa Ufaransa, alijibu mojayapo matangazo hayo, akitambua kweli katika jambo alilosoma, upesi alianza kueneza ujumbe huo yeye mwenyewe. Katika Ubelgiji, Jean-Baptiste Tilmant, Sr., aliona pia mojayapo matangazo hayo katika 1901 na kupata mabuku mawili ya Millennial Dawn. Ulikuwa msisimuko kama nini kuona kweli ya Biblia ikiwa imetolewa kwa njia yenye kueleweka jinsi hiyo! Angewezaje kujizuia kuwaambia marafiki wake! Kufikia mwaka uliofuata, kikundi cha funzo kilikuwa kikikutana kwa ukawaida katika kao lake. Upesi baada ya hapo utendaji wa kikundi hicho kidogo ulikuwa ukizaa tunda hata katika kaskazini mwa Ufaransa. Ndugu Weber aliendelea kuwasiliana nao, akitembelea pindi kwa pindi vikundi hivyo mbalimbali vilivyokuwa vimesitawi, akivijenga kiroho na kutoa maagizo juu ya jinsi ya kushiriki habari njema na wengine.
Wakati Habari Njema Zilipofika Ujerumani
Muda mfupi baada ya baadhi ya vichapo hivyo kuanza kutokea katika Kijerumani, katika miaka ya katikati ya 1880, Wajerumani-Waamerika waliovithamini walianza kupeleka nakala kwa watu wao wa ukoo katika nchi walimozaliwa. Mwuguzi mmoja aliyekuwa akifanya kazi katika hospitali moja ya Hamburg alishiriki nakala za Millennial Dawn na wengine katika hospitali. Katika 1896, Adolf Weber, katika Uswisi, alikuwa akitia matangazo katika magazeti ya lugha ya Kijerumani na kupeleka trakti Ujerumani kwa posta. Mwaka uliofuata depo ya fasihi ilifunguliwa katika Ujerumani ili kurahisisha ugawanyaji wa chapa ya Kijerumani ya Watch Tower, lakini matokeo yalikuja hatua kwa hatua. Hata hivyo, katika 1902, Margarethe Demut, aliyekuwa amejifunzia kweli katika Uswisi, alihamia Tailfingen, mashariki mwa Black Forest. Bidii yake ya kutoa ushahidi kibinafsi iliweka msingi wa mojawapo vikundi vya mapema vya Wanafunzi wa Biblia katika Ujerumani. Samuel Lauper, kutoka Uswisi, alihamia Bergisches Land, kaskazini-mashariki mwa Cologne, ili kueneza habari njema katika eneo hilo. Kufikia 1904, mikutano ilikuwa ikifanywa huko katika Wermelskirchen. Miongoni mwa waliokuwapo alikuwa mwanamume mmoja mwenye umri wa miaka 80, Gottlieb Paas, aliyekuwa akitafuta kweli. Akiwa kitandani mwake wakati wa kufa, muda mfupi baada ya mikutano hiyo kuanza, Paas aliinua Watch Tower na kusema: “Hii ndiyo kweli; shikamaneni nayo.”
Idadi ya waliokuwa wakipendezwa katika kweli hizo za Biblia iliongezeka hatua kwa hatua. Ijapokuwa ilikuwa ghali, mipango ilifanywa kutia nakala sampuli za Watch Tower magazetini nchini Ujerumani. Ripoti iliyotangazwa katika 1905 ilisema kwamba zaidi ya nakala 1,500,000 za sampuli hizo za Watch Tower zilikuwa zimegawanywa. Hiyo ilikuwa kazi kubwa iliyotimizwa na kikundi hicho kidogo.
Wanafunzi wa Biblia wote hawakuhisi kwamba kwa kufikia watu karibu na nyumbani walikuwa wamefanya yote yaliyohitajiwa. Mapema sana kama 1907, Ndugu Erler, kutoka Ujerumani, alifunga safari nyingi kwenda Bohemia katika ile iliyokuwa wakati huo Austria na Hungaria (baadaye sehemu ya Chekoslovakia). Aligawanya fasihi zilizoonya juu ya Har–Magedoni na kuwaambia juu ya baraka ambazo zingekuja kwa wanadamu baada yayo. Kufikia 1912 Mwanafunzi wa Biblia mwingine alikuwa amegawanya fasihi za Biblia katika eneo la Memel, katika ile ambayo sasa ni Lithuania. Wengi waliitikia ujumbe huo kwa idili, na upesi vikundi kadhaa vikubwa kidogo vya Wanafunzi wa Biblia vilifanyizwa huko. Hata hivyo, wakati walipojifunza kwamba Wakristo wa kweli lazima pia wawe mashahidi, idadi yao ilianza kupungua. Hata hivyo, wachache walijithibitisha wenyewe kuwa waigaji wa kweli wa Kristo, “shahidi mwaminifu na wa kweli.”—Ufu. 3:14, NW.
Wakati Nikolaus von Tornow, kabaila Mjerumani mwenye mali nyingi katika Urusi, alipokuwa katika Uswisi kama mwaka 1907, alipewa mojayapo trakti za Watch Tower Society. Miaka miwili baadaye alitokea kwenye Kutaniko la Berlin, katika Ujerumani, akiwa amevalia mavazi yake yaliyo bora zaidi huku mtumishi wake wa kibinafsi akiambatana naye. Ilichukua muda ndipo athamini kwa nini Mungu angeaminisha kweli hizo za thamani nyingi sana kwa watu wanyenyekevu, lakini yale aliyosoma kwenye 1 Wakorintho 1:26-29 yalimsaidia: “Mwatazama wito wake kwenu, akina ndugu, kwamba si wengi wenye hekima katika njia ya kimwili walioitwa, si wengi wenye nguvu, si wengi wa uzawa wa kikabaila . . . , ili mwili wowote usipate kujisifu machoni pa Mungu.” Akisadiki kwamba alikuwa amepata kweli, von Tornow aliuza mali zake katika Urusi akajitoa mwenyewe na mali zake kusogeza mbele masilahi ya ibada safi.
Katika 1911, wakati wenzi wawili Wajerumani, akina Herkendell, walipofunga ndoa, bibi-arusi aliomba baba yake, ikiwa mahari, pesa kwa ajili ya fungate isiyo ya kawaida. Yeye na mume wake walifikiria kufunga safari ngumu ambayo ingechukua miezi mingi. Fungate yao ilikuwa safari ya kwenda kuhubiri katika Urusi ili kufikia watu wasemao Kijerumani huko. Hivyo kwa njia nyingi watu wa aina zote walikuwa wakishiriki na wengine yale waliyokuwa wamejifunza juu ya kusudi la Mungu lenye upendo.
Ukuzi Katika Shamba la Uingereza
Baada ya ule ugawanyaji wa bidii wa fasihi katika Uingereza katika 1881, baadhi ya waenda-kanisani waliona uhitaji wa kutenda juu ya yale waliyokuwa wamejifunza. Tom Hart wa Islington, London, alikuwa mmoja wa wale waliovutiwa na shauri la Kimaandiko la Watch Tower, “Tokeni kwake, watu wangu”—yaani, tokeni katika makanisa ya Kibabiloni ya Jumuiya ya Wakristo na kufuata mafundisho ya Biblia. (Ufu. 18:4, NW) Aliacha kanisa katika 1884, akifuatwa na hesabu fulani ya wengine.
Wengi walioshirikiana na vikundi vya funzo walisitawi wakawa waeneza-evanjeli wenye matokeo. Baadhi yao walitoa fasihi za Biblia katika bustani za London na sehemu nyingine ambako watu walikuwa wakistarehe. Wengine walikazia fikira sehemu za biashara. Hata hivyo, ile njia ya kawaida zaidi ilikuwa kufanya ziara za nyumba hadi nyumba.
Sarah Ferrie, mwandikishaji wa Watch Tower, aliandikia ndugu Russell akisema kwamba yeye na marafiki wachache katika Glasgow wangetaka kujitolea kushiriki katika kugawanya trakti. Ulikuwa mshangao kama nini wakati lori lilipowasili mlangoni pake likiwa na trakti 30,000, zote za kugawanywa bila malipo! Wakaanza kutenda mara hiyo. Minnie Greenlees, pamoja na wavulana wake watatu, akiwa na kigari chenye kukokotwa na farasi kikiwa usafiri, alijitahidi kugawanya fasihi za Biblia katika sehemu za mashambani za Scotland. Baadaye, Alfred Greenlees na Alexander MacGillivray, wakisafiri kwa baiskeli, waligawanya trakti katika sehemu iliyo kubwa zaidi ya Scotland. Badala ya kulipa wengine wagawanye fasihi, wenye kujitolea walio wakfu walikuwa sasa wakifanya kazi hiyo wao wenyewe.
Mioyo Yao Iliwasukuma
Katika mmojapo mifano yake, Yesu alikuwa amesema kwamba watu ‘waliosikia neno la Mungu kwa moyo mzuri’ wangezaa tunda. Uthamini wa moyo mweupe wa maandalizi ya Mungu yenye upendo ungewasukuma kushiriki pamoja na wengine habari njema juu ya Ufalme wa Mungu. (Luka 8:8, 11, 15) Bila kujali hali zao, wangepata njia ya kufanya hivyo.
Hivyo ilikuwa ni kutoka kwa baharia Mwitalia kwamba msafiri Mwargentina alipata kisehemu cha ile trakti Food for Thinking Christians. Alipokuwa bandarini katika Peru, msafiri huyo aliandika apate habari zaidi, na akiwa na kupendezwa kulikoongezeka akaandika tena kutoka Argentina katika 1885, kwa mhariri wa Watch Tower aombe fasihi. Mwaka huohuo mshiriki wa Jeshi la Manowari la Uingereza, aliyetumwa pamoja na kikosi chake cha silaha, kwenda Singapore, alichukua Watch Tower. Alifurahia aliyojifunza kutoka kwa gazeti hilo na akalitumia sana kujulisha maoni ya Biblia juu ya habari zilizokuwa mazungumzo ya umma. Katika 1910 meli ambamo wanawake wawili Wakristo walikuwa wakisafiria ilitua kwenye bandari katika Colombo, Ceylon (sasa Sri Lanka). Walichukua fursa hiyo kumtolea ushahidi Bw. Van Twest, ofisa-msimamizi wa bandari. Walisema naye kwa moyo wa bidii juu ya mambo mema waliyokuwa wamejifunza kutoka kitabu The Divine Plan of the Ages. Kama tokeo, Bw. Van Twest akawa Mwanafunzi wa Biblia, na kazi ya kuhubiri habari njema ikaanza katika Sri Lanka.
Hata wale ambao hawangeweza kusafiri walitafuta njia za kushiriki kweli za Biblia zenye kuchangamsha moyo pamoja na watu katika nchi nyinginezo. Kama ilivyofunuliwa na barua ya shukrani iliyochapwa katika 1905, mtu fulani katika Marekani alikuwa amepeleka kitabu The Divine Plan of the Ages kwa mwanamume mmoja katika St. Thomas, katika ile iliyokuwa wakati huo Indies Magharibi ya Denmark. Baada ya kukisoma, mpokeaji alipiga magoti na kueleza tamaa yake ya kutaka kutumiwa na Mungu katika kufanya mapenzi yake. Katika 1911, Bellona Ferguson katika Brazili alitaja kisa chake kuwa “uthibitisho hakika ulio hai kwamba hakuna walio mbali mno wasiweze kufikiwa” na maji ya kweli. Yaonekana alikuwa amekuwa akipokea vichapo vya Sosaiti kwa posta tangu 1899. Wakati fulani kabla ya Vita ya Ulimwengu 1, mhamiaji Mjerumani katika Paraguai alipata mojayapo trakti za Sosaiti katika sanduku lake la posta. Aliagiza fasihi zaidi na upesi akaacha kushirikiana na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Hapakuwa na mwingine nchini wa kuwabatiza, hivyo yeye na shemeji yake wakaamua wabatizane. Kwelikweli, ushahidi ulikuwa ukitolewa katika sehemu za mbali za dunia nao ulikuwa ukizaa tunda.
Bado wengine kati ya Wanafunzi wa Biblia walihisi wakisukumwa wasafiri hadi mahali ambapo wao au wazazi wao walizaliwa ili kuwaambia marafiki na watu wa ukoo juu ya kusudi la ajabu la Yehova na jinsi wao wangelishiriki. Hivyo, katika 1895, Ndugu Oleszynski alirudi Poland akiwa na habari njema juu ya “fidia, kufanywa upya kwa vitu vyote na ule mwito wa juu”; ingawa, kwa kusikitisha, yeye hakuendelea katika utumishi huo. Katika 1898 mmoja aliyekuwa profesa, Mhungaria, aliondoka Kanada ili kueneza ujumbe wa Biblia wenye uharaka katika nchi yake ya kuzaliwa. Katika 1905 mtu aliyekuwa amekuwa Mwanafunzi wa Biblia katika Amerika alirudi Ugiriki ili kutoa ushahidi. Na katika 1913 kijana mmoja alichukua mbegu za kweli ya Biblia kutoka New York hadi mji wa nyumbani mwa familia yao, Ramallah, si mbali na Yerusalemu.
Kufungua Kazi Katika Eneo la Karibea
Wakati idadi ya waeneza-evanjeli ilipokuwa ikikua katika Marekani, Kanada, na Ulaya, kweli ya Biblia ilikuwa inaanza kutia mizizi pia katika Panama, Kosta Rika, Guiana ya Uholanzi (sasa ni Suriname), na Guiana ya Uingereza (sasa ni Guyana). Joseph Brathwaite, aliyekuwa katika Guiana ya Uingereza wakati aliposaidiwa kuelewa kusudi la Mungu, aliondoka kwenda Barbados katika 1905 ili kutumia wakati wake wote katika kufundisha watu huko. Louis Facey na H. P. Clarke, waliosikia habari njema wakati walipokuwa wakifanya kazi katika Kosta Rika, walirudi Jamaika katika 1897 ili kushiriki imani yao mpya waliyoipata miongoni mwa watu wao wenyewe. Wale waliokubali kweli huko walikuwa wafanyakazi wenye bidii. Katika 1906 pekee, kikundi hicho katika Jamaika kiligawanya trakti zipatazo 1,200,000 na vipande vingine vya fasihi. Mfanyakazi mwingine mhamaji, aliyejifunza kweli katika Panama, alipeleka ujumbe wa tumaini katika Grenada.
Mapinduzi katika Mexico katika 1910-1911 yalikuwa jambo jingine lililosaidia katika kuletea watu wenye njaa ya kweli ujumbe wa Ufalme wa Mungu. Watu wengi walikimbilia kaskazini wakaingia Marekani. Huko baadhi yao walionana na Wanafunzi wa Biblia, wakajifunza juu ya kusudi la Mungu la kuletea wanadamu amani ya kudumu, nao wakapeleka fasihi walikotoka Mexico. Hata hivyo, hiyo haikuwa ndiyo mara ya kwanza kwamba Mexico ilipata kufikiwa na ujumbe huo. Mapema sana kama 1893, Watch Tower lilichapisha barua kutoka kwa F. de P. Stephenson, wa Mexico, aliyekuwa amesoma baadhi ya vichapo vya Watch Tower Society naye alitaka zaidi ili avishiriki pamoja na marafiki wake katika Mexico na katika Ulaya pia.
Ili kufungua nchi zaidi za Karibea kwa kazi ya kuhubiri kweli ya Biblia na kupanga mikutano ya ukawaida kwa ajili ya funzo, Ndugu Russell alituma E. J. Coward kwenda Panama katika 1911 na kisha kwenye visiwa. Ndugu Coward alikuwa msemaji mwenye mkazo na mwenye kupendeza, na wasikilizaji ambao mara nyingi walifikia idadi ya mamia walisongamana kusikia hotuba zake zenye kukanusha fundisho la moto wa helo na kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, pia akisimulia juu ya wakati ujao mtukufu kwa ajili ya dunia. Alisonga toka mji mmoja kwenda ufuatao, na toka kisiwa kimoja hadi kingine—St. Lucia, Dominika, St. Kitts, Barbados, Grenada, na Trinidad—akifikia watu wengi iwezekanavyo. Pia alitoa hotuba katika Guiana ya Uingereza. Alipokuwa Panama, alikutana na W. R. Brown, ndugu kijana Mjamaika mwenye bidii sana, ambaye baada ya hapo alitumika pamoja na Ndugu Coward katika visiwa kadhaa vya Karibea. Baadaye Ndugu Brown alisaidia kufungua kazi katika mashamba mengine.
Katika 1913, Ndugu Russell mwenyewe alitoa hotuba katika Panama, Kuba, na Jamaika. Majumba mawili yalijaa pomoni kwa ajili ya hotuba ya watu wote aliyotoa katika Kingston, Jamaika, na bado watu 2,000 hawakuruhusiwa kuingia kwa kutokuwa na nafasi. Vyombo vya habari vilitaja uhakika wa kwamba msemaji hakusema lolote juu ya pesa na michango haikukusanywa.
Nuru ya Kweli Yafika Afrika
Afrika vilevile ilikuwa ikipenywa na nuru ya kweli wakati wa pindi hiyo. Barua moja iliyopelekwa kutoka Liberia katika 1884 ilifunua kwamba msomaji wa Biblia huko alikuwa amepata nakala moja ya Food for Thinking Christians naye alitaka vichapo zaidi ili kushiriki pamoja na wengine. Miaka michache baada ya hapo, iliripotiwa kwamba kasisi mmoja katika Liberia alikuwa ameacha cheo chake cha kasisi ili awe huru kufundisha wengine kweli za Biblia alizokuwa amejifunza kwa msaada wa Watch Tower na kwamba mikutano ya ukawaida ilikuwa ikifanywa huko na kikundi cha Wanafunzi wa Biblia.
Mhudumu wa Dutch Reformed Church kutoka Uholanzi alichukua baadhi ya vichapo vya C. T. Russell akaenda navyo alipotumwa Afrika Kusini katika 1902. Ijapokuwa yeye hakunufaishwa navyo kwa njia yenye kudumu, Frans Ebersohn na Stoffel Fourie, walioziona fasihi hizo katika maktaba yake, walinufaika. Miaka michache baadaye, idadi katika sehemu hiyo ya shamba iliimarishwa wakati Wanafunzi wa Biblia wawili wenye bidii kutoka Scotland walipohamia Durban, Afrika Kusini.
Kwa kuhuzunisha, miongoni mwa wale waliopata fasihi zilizoandikwa na Ndugu Russell na kisha wakatumia baadhi yazo kufundisha wengine, kulikuwa wachache, kama vile Joseph Booth na Elliott Kamwana, waliochanganya mawazo yao wenyewe, yaliyokusudiwa kuchochea mabadiliko ya kijamii. Kwa baadhi ya watazamaji katika Afrika Kusini na Nyasaland (baadaye ikawa Malawi), jambo hilo lilielekea kuvuruga utambulisho wa Wanafunzi wa Biblia wa kweli. Hata hivyo, wengi walikuwa wakisikia na kuthamini ujumbe uliovuta uangalifu kwenye Ufalme wa Mungu ukiwa suluhisho kwa matatizo ya wanadamu.
Hata hivyo, kwa habari ya kazi ya kuhubiri yenye kuenea barani Afrika, hiyo ilikuwa bado ni ya wakati ujao.
Kwenda Nchi za Mashariki na Visiwa vya Pasifiki
Muda mfupi baada ya vichapo vya Biblia vilivyotayarishwa na C. T. Russell kugawanywa mara ya kwanza katika Uingereza, vilifika nchi za Mashariki pia. Katika 1883, Bi. C. B. Downing, mishonari Mpresbiteri katika Chefoo (Yantai), China, alipokea nakala moja ya Watch Tower. Alithamini yale aliyojifunza juu ya kufanywa upya kwa vitu vyote naye alishiriki fasihi hizo na wamishonari wengine, kutia na Horace Randle, aliyeshirikiana na Baraza la Misheni ya Kibaptisti. Baadaye, kupendezwa kwake kulichochewa zaidi na tangazo juu ya Millennial Dawn lililotokea katika gazeti Times la London, nalo lilifuatwa na nakala za vitabu vyenyewe—kimoja kutoka kwa Bi. Downing na kingine kilichopelekwa na mama yake aliyeishi Uingereza. Mwanzoni, alishtushwa na yale aliyosoma. Lakini mara alipopata kusadikishwa kwamba Utatu si fundisho la Biblia, aliacha Kanisa la Baptisti na akaendelea kushiriki na wamishonari wengine yale aliyokuwa amejifunza. Katika 1900 yeye aliripoti kwamba alikuwa amepeleka barua 2,324 na trakti zipatazo 5,000 kwa wamishonari katika China, Japani, Korea, na Siam (Thailand). Wakati ule ushahidi ulikuwa ukitolewa sanasana kwa wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo katika nchi za Mashariki.
Katika pindi iyo hiyo ya wakati, mbegu za kweli zilipandwa pia katika Australia na New Zealand. “Mbegu” za kwanza kati ya hizo zilizowasili katika Australia huenda zikawa zilipelekwa huko katika 1884 au muda mfupi baada ya hapo na mtu aliyefikiwa kwanza na Mwanafunzi wa Biblia katika bustani nchini Uingereza. “Mbegu” nyinginezo zilikuja kwa barua kutoka kwa marafiki na watu wa ukoo kutoka ng’ambo.
Katika muda wa miaka michache baada ya kufanyizwa kwa Jumuiya ya Mikoa ya Australia katika 1901, mamia ya watu huko walikuwa waandikishaji wa Watch Tower. Kama tokeo la utendaji wa wale walioona pendeleo la kushiriki kweli na wengine, maelfu ya trakti zilipelekewa watu ambao majina yao yalikuwa katika orodha ya wenye kujiandikisha kwa ajili ya kupiga kura. Trakti zaidi ziligawanywa kwa watu barabarani, na wafanyakazi na wenye nyumba waliokuwa peke yao katika sehemu za mbali zilizokuwa kandokando ya njia za reli walirushiwa vifurushi vya trakti kutoka katika madirisha ya garimoshi. Watu walikuwa wakijulishwa juu ya mwisho uliokuwa ukikaribia wa Nyakati za Mataifa katika 1914. Arthur Williams, Sr., aliongea juu ya jambo hilo na wateja wote katika duka lake katika Magharibi mwa Australia na akawaalika wenye kupendezwa nyumbani kwake kwa mazungumzo zaidi.
Haijulikani sasa ni nani aliyefika New Zealand kwanza akiwa na kweli ya Biblia. Lakini kufikia 1898, Andrew Anderson, mkazi wa New Zealand, alikuwa amesoma vichapo vya Watch Tower vya kutosha kusukumwa kueneza kweli huko akiwa kolpota. Jitihada zake ziliimarishwa katika 1904 na makolpota wengine waliokuja kutoka Amerika na kutoka ofisi ya tawi ya Sosaiti iliyoanzishwa mwaka huohuo katika Australia. Bi. Thomas Barry, katika Christchurch, alikubali mabuku sita ya Studies in the Scriptures kutoka kwa mmojawapo makolpota. Mwana wake Bill alivisoma katika 1909 wakati wa safari ya majuma sita ya kwenda Uingereza kwa merikebu naye akatambua ukweli wa yaliyokuwamo. Miaka mingi baadaye mwanae Lloyd alipata kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.
Miongoni mwa wafanyakazi wenye bidii katika siku hizo za mapema alikuwa Ed Nelson, ambaye, ijapokuwa hakuwa mwenye busara sana, alitumia wakati wake wote kwa miaka 50 akieneza ujumbe wa Ufalme toka ncha ya kaskazini ya New Zealand hadi kusini. Baada ya miaka michache, Frank Grove ambaye alisitawisha kumbukumbu lake ili kusaidia hali yake ya kutoweza kuona vizuri, na ambaye pia alipainia kwa miaka zaidi ya 50 mpaka kifo chake, alijiunga naye.
Safari ya Ulimwengu ili Kuendeleza Kuhubiriwa kwa Habari Njema
Jitihada nyingine kubwa ilifanywa katika 1911-1912 ili kusaidia watu wa nchi za Mashariki. International Bible Students Association lilituma halmashauri ya wanaume saba, ikiongozwa na C. T. Russell, ili wao binafsi wakadirie hali huko. Kokote walikoenda walisema juu ya kusudi la Mungu la kuletea wanadamu baraka kwa njia ya Ufalme wa Kimesiya. Nyakati nyingine wasikilizaji wao walikuwa wachache, lakini katika Filipino na India, kulikuwa maelfu. Wao hawakuunga mkono kampeni iliyopendwa na wengi wakati huo katika Jumuiya ya Wakristo ya kukusanya pesa kwa ajili ya wongofu wa ulimwengu. Waliona kwamba jitihada iliyo nyingi ya wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo ilitumiwa katika kuendeleza elimu ya kilimwengu. Lakini Ndugu Russell alisadiki kwamba walichohitaji watu kilikuwa “ile Gospeli ya uandalizi wa upendo wa Mungu wa Ufalme ujao wa Mesiya.” Badala ya kutarajia kuongoa ulimwengu, Wanafunzi wa Biblia walielewa kutoka kwa Maandiko kwamba jambo lililopasa kufanywa wakati huo lilikuwa kutoa ushahidi na kwamba hilo lingetumikia kusudi la kukusanya “wachaguliwa wachache kutoka kwa mataifa yote, jamaa, kabila na lugha ili kushiriki katika jamii ya Bibi-arusi wa [Kristo]—ili kukaa pamoja Naye katika kiti Chake cha ufalme wakati wa miaka elfu, wakishirikiana kuinua jamii nzima ya kibinadamu.”a—Ufu. 5:9, 10; 14:1-5.
Baada ya kutumia wakati katika Japani, China, na Filipino, na kwingineko, hao washiriki wa halmashauri hiyo waliongeza kilometa 6,400 zaidi za safari katika India. Watu fulani mmoja-mmoja waliokuwa wakiishi India walikuwa wamesoma fasihi za Sosaiti nao walikuwa wameandika barua kuonyesha uthamini wao kwa ajili yayo mapema sana kama 1887. Kazi ya kutoa ushahidi kwa bidii ilikuwa imefanywa pia miongoni mwa watu wenye kusema lugha ya Tamil tangu 1905 na kijana mmoja mwanamume ambaye, akiwa mwanafunzi katika Amerika, alikuwa amekutana na Ndugu Russell naye akajifunza kweli. Mwanamume huyo kijana alisaidia kuanzisha vikundi vya funzo la Biblia vipatavyo 40 kusini mwa India. Lakini, baada ya kuhubiria wengine, yeye mwenyewe alipata kupoteza kibali kwa kuacha kufuata viwango vya Kikristo.—Linganisha 1 Wakorintho 9:26, 27.
Hata hivyo, karibu na wakati huohuo, A. J. Joseph, wa Travancore (Kerala), katika kujibiwa ulizo alilokuwa amemuuliza kwa barua Mwadventisti mashuhuri, alipelekewa buku la Studies in the Scriptures. Humo alipata majibu ya Kimaandiko yenye kuridhisha kwa maswali yake juu ya Utatu. Upesi yeye na washiriki wa familia yake walitoka kwenda kwenye mashamba ya mpunga na minazi ya kusini mwa India wakishiriki imani zao mpya walizozipata. Baada ya ziara ya Ndugu Russell katika 1912, Ndugu Joseph alianza utumishi wa wakati wote. Kwa njia ya reli, mkokoteni wenye kukokotwa na ng’ombe, mashua, na kwa miguu, alisafiri kugawanya fasihi za Biblia. Alipokuwa akitoa hotuba za watu wote, mara nyingi zilikatizwa na makasisi na wafuasi wao. Katika Kundara, wakati kasisi “Mkristo” alipokuwa akitumia wafuasi wake kukatiza mkutano kama huo na kumtupia Ndugu Joseph kinyesi, mwanamume muungwana mashuhuri Mhindu alikuja kuona kelele zilikuwa za nini. Alimwuliza kasisi huyo hivi: ‘Je, hicho ndicho kielelezo kilichowekwa na Kristo cha kufuatwa na Wakristo, au je, yale unayofanya ni kama mwenendo wa Mafarisayo wa wakati wa Yesu?’ Kasisi huyo akaondoka.
Kabla ya ile safari ya miezi minne ya ulimwengu ya halmashauri ya IBSA haijakamilishwa, Ndugu Russell alikuwa amepangia R. R. Hollister kuwa mwakilishi wa Sosaiti katika nchi za Mashariki na kuhakikisha kwamba kazi inafanywa ya kueneza kwa vikundi vya watu ujumbe wa uandalizi wa upendo wa Mungu wa Ufalme wa Kimesiya. Trakti za pekee zilitayarishwa katika lugha kumi, na mamilioni yazo yalienezwa kotekote katika India, China, Japani, na Korea na waenezaji wenyeji. Kisha vitabu vilitafsiriwa katika lugha nne kati ya hizo ili kuandaa chakula zaidi cha kiroho kwa wale walioonyesha kupendezwa. Hapa palikuwa na shamba kubwa, na mengi bado yalihitaji kufanywa. Hata hivyo, yale yaliyokuwa yametimizwa kufikia hapo yalikuwa yenye kustaajabisha kwelikweli.
Ushahidi Wenye Kutokeza Ulitolewa
Kabla uharibifu wa vita ya kwanza ya ulimwengu haujaanzishwa, ushahidi wa bidii ulikuwa umetolewa ulimwenguni pote. Ndugu Russell alikuwa amesafiri kutoa hotuba katika mamia ya majiji katika Marekani na Kanada, alikuwa amesafiri mara kadhaa kwenda Ulaya, alikuwa ametoa hotuba katika Panama, Jamaika, na Kuba, pamoja na majiji makuu ya nchi za Mashariki. Makumi ya maelfu ya watu walikuwa wamesikia hotuba zake za Biblia zenye kusisimua na walikuwa wameona akijibu hadharani kutoka kwa Maandiko maswali yaliyozushwa na marafiki na maadui pia. Kupendezwa kwingi kulikuwa kumechochewa kwa njia hiyo, na maelfu ya magazeti katika Amerika, Ulaya, Afrika Kusini, na Australia yalikuwa yakichapisha kwa ukawaida mahubiri ya Ndugu Russell. Mamilioni ya vitabu, pamoja na mamia ya mamilioni ya trakti na fasihi nyinginezo katika lugha 35, vilikuwa vimegawanywa na Wanafunzi wa Biblia.
Ingawa fungu lake lilikuwa lenye kutokeza, si Ndugu Russell pekee aliyekuwa akihubiri. Wengine vilevile, waliotawanyika kotekote duniani, walikuwa wakiunganisha sauti zao wakiwa mashahidi wa Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo. Wale walioshiriki hawakuwa wote watoaji wa hotuba za watu wote. Walikuwa watu wa kila aina, nao walitumia kila njia iliyofaa waliyokuwa nayo ili kueneza habari njema.
Katika Januari 1914, mwisho wa Nyakati za Mataifa ukiwa umbali unaopungua mwaka mmoja, ushahidi mwingine wa bidii ulianzishwa. Huo ulikuwa ni ile “Photo-Drama of Creation,” iliyokazia kwa njia mpya kusudi la Mungu kwa dunia. Ilifanya hivyo kwa njia ya slaidi nzuri zenye rangi zilizochorwa kwa mkono na sinema, zilizoambatana na sauti. Vyombo vya habari vya umma katika Marekani viliripoti kwamba kotekote nchini mamia ya maelfu ya watazamaji walikuwa wakizitazama kila juma. Kufikia mwisho wa mwaka wa kwanza, jumla ya hudhurio katika Marekani na Kanada ilikuwa imefika karibu milioni nane. Katika London, Uingereza, kulikuwa umati uliojaa na ukazidi kwenye majumba Opera House na Royal Albert Hall ili kuona wonyesho huo wa picha uliokuwa wa sehemu nne za saa 2 kila moja. Katika muda wa nusu mwaka, zaidi ya watu 1,226,000 walikuwa wamehudhuria katika majiji 98 katika Visiwa Uingereza. Vikundi vya umati katika Ujerumani na Uswisi vilijaza kabisa majumba yaliyokuwa yanapatikana. Pia ilionwa na watazamaji wengi katika nchi za Skandinevia na visiwa vya Pasifiki Kusini.
Lo! ulikuwa ushahidi wa bidii wenye kutokeza kama nini wa duniani pote uliotolewa katika miongo hiyo ya mapema ya historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova! Lakini, kwa kweli, kazi ilikuwa ndiyo tu inaanza.
Ni mamia wachache tu waliokuwa wameshiriki kwa bidii katika kueneza kweli ya Biblia wakati wa miaka ya mapema ya 1880. Kufikia 1914, kulingana na ripoti zipatikanazo, kulikuwa kama 5,100 walioshiriki katika kazi. Wengine huenda wakawa waligawanya trakti pindi kwa pindi. Wafanyakazi walikuwa wachache.
Kikosi hiki kidogo cha waeneza-evanjeli kilikuwa, kwa njia mbalimbali, tayari kimeeneza kazi yao ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kuingia katika nchi 68 kufikia nusu ya pili ya 1914. Na kazi yao wakiwa wahubiri na walimu wa Neno la Mungu ilikuwa imeimarishwa kwa msingi uliokuwa imara vya kutosha katika nchi 30 kati ya hizo.
Mamilioni ya vitabu na mamia ya mamilioni ya trakti yalikuwa yamegawanywa kabla ya mwisho wa Nyakati za Mataifa. Kwa kuongezea hayo, kufikia 1913 magazeti ya habari mengi kama 2,000 yalikuwa yakitangaza kwa ukawaida mahubiri yaliyotayarishwa na C. T. Russell, na katika mwaka 1914 wasikilizaji wanaojumlika kuwa zaidi ya 9,000,000 katika mabara matatu waliona ile “Photo-Drama of Creation.”
Kwelikweli, ushahidi wenye kushangaza ulikuwa umetolewa! Lakini mengi zaidi yangekuja.
[Maelezo ya Chini]
a Ripoti kamili juu ya safari hiyo ya ulimwengu huonekana katika The Watch Tower la Aprili 15, 1912.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 405]
C. T. Russell binafsi alitoa hotuba za Biblia katika majiji zaidi ya 300 (katika maeneo yanayoonyeshwa kwa alama) katika Amerika Kaskazini na Karibea—katika mengi yayo mara 10 au 15
[Ramani]
(See publication)
[Ramani katika ukurasa wa 407]
(See publication)
Safari za Russell za kwenda kuhubiri Ulaya, kwa kawaida kupitia Uingereza
1891
1903
1908
1909
1910 (mara mbili)
1911 (mara mbili)
1912 (mara mbili)
1913
1914
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 408]
Aliposadiki kwamba alikuwa amepata kweli, Andreas Øiseth aligawanya kwa bidii fasihi za Biblia katika karibu kila sehemu ya Norway
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
NORWAY
Mzingo Aktiki
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 409]
Adolf Weber, mtunza-bustani mnyenyekevu, alieneza habari njema kutoka Uswisi hadi kwenye nchi nyinginezo katika Ulaya
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
UBELGIJI
UJERUMANI
USWISI
ITALIA
UFARANSA
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 413]
Bellona Ferguson, katika Brazili—“hakuna walio mbali mno wasiweze kufikiwa”
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
BRAZILI
[Ramani katika ukurasa wa 415]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
ALASKA
KANADA
GREENLAND
ST. PIERRE NA MIQUELON
MAREKANI
BERMUDA
BAHAMAS
VISIWA VYA TURKS NA CAICOS
KUBA
MEXICO
BELIZE
JAMAIKA
HAITI
JAMHURI YA DOMINIKA
PUERTO RIKO
VISIWA VYA CAYMAN
GUATEMALA
EL SALVADOR
HONDURAS
NIKARAGUA
KOSTA RIKA
PANAMA
VENEZUELA
GUYANA
SURINAME
GUIANA YA UFARANSA
KOLOMBIA
EKUADO
PERU
BRAZILI
BOLIVIA
PARAGUAI
CHILE
ARGENTINA
URUGUAI
VISIWA VYA FALKLAND
VISIWA VYA VIRGIN (MAREKANI)
VISIWA VYA VIRGIN (UINGEREZA)
ANGUILLA
ST. MAARTEN
SABA
ST. EUSTATIUS
ST. KITTS
NEVIS
ANTIGUA
MONTSERRAT
GUADELOUPE
DOMINIKA
MARTINIQUE
ST. LUCIA
ST. VINCENT
BARBADOS
GRENADA
TRINIDAD
ARUBA
BONAIRE
KURASAO
BAHARI YA ATLANTIKI
BAHARI YA KARIBEA
BAHARI YA PASIFIKI
[Ramani katika ukurasaw wa 416, 417]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
GREENLAND
SWEDEN
ICELAND
NORWAY
VISIWA VYA FAEROE
FINLAND
URUSI
ESTONIA
LATVIA
LITHUANIA
BELARUS
UKRAINIA
MOLDOVA
GEORGIA
ARMENIA
AZERBAIJAN
TURKMENISTAN
UZBEKISTAN
KAZAKHSTAN
TAJIKISTAN
KYRGYZSTAN
POLAND
UJERUMANI
UHOLANZI
DENMARK
UINGEREZA
IRELAND
UBELGIJI
LUXEMBOURG
LIECHTENSTEIN
USWISI
CHEKOSLOVAKIA
AUSTRIA
HUNGARIA
RUMANIA
YUGOSLAVIA
SLOVENIA
KROATIA
BOSNIA NA HERZEGOVINA
BULGARIA
ALBANIA
ITALIA
GIBRALTAR
HISPANIA
URENO
MADEIRA
MOROKO
SAHARA MAGHARIBI
SENEGAL
ALGERIA
LIBYA
MISRI
LEBANONI
ISRAELI
SAIPRASI
SIRIA
UTURUKI
IRAKI
IRAN
BAHRAIN
KUWAIT
YORDANI
SAUDI ARABIA
KATAR
MUUNGANO WA FALME ZA KIARABU
OMANI
YEMENI
JIBUTI
SOMALIA
ETHIOPIA
SUDAN
CHAD
NIGER
MALI
MAURITANIA
GAMBIA
GUINEA-BISSAU
SIERRA LEONE
LIBERIA
CÔTE D’IVOIRE
GHANA
TOGO
BENIN
GUINEA YA IKWETA
ST. HELENA
GUINEA
BURKINA FASO
NIGERIA
JAMHURI YA AFRIKA YA KATI
KAMERUN
SÃO TOMÉ
KONGO
GABON
ZAIRE
ANGOLA
ZAMBIA
NAMIBIA
BOTSWANA
AFRIKA KUSINI
LESOTHO
SWAZILAND
MSUMBIJI
MADAGASKA
RÉUNION
MAURITIUS
RODRIGUES
ZIMBABWE
MAYOTTE
KOMORO
SHELISHELI
MALAWI
TANZANIA
BURUNDI
RWANDA
UGANDA
UFARANSA
PAKISTAN
AFGHANISTAN
NEPAL
BHUTAN
MYANMAR
BANGLADESH
INDIA
SRI LANKA
UGIRIKI
MALTA
TUNISIA
KENYA
BAHARI YA ATLANTIKI
BAHARI YA HINDI
ALASKA
MONGOLIA
JAMHURI YA KIDEMOKRASI YA WATU WA KOREA
JAPANI
JAMHURI YA KOREA
CHINA
MACAO
TAIWAN
HONG KONG
LAOS
THAILAND
VIETNAM
KAMBODIA
FILIPINO
BRUNEI
MALASIA
SINGAPORE
INDONESIA
SAIPAN
ROTA
GUAM
YAP
BELAU
CHUUK
POHNPEI
KOSRAE
VISIWA VYA MARSHALL
NAURU
PAPUA NEW GUINEA
AUSTRALIA
NEW ZEALAND
KISIWA CHA NORFOLK
NEW CALEDONIA
VISIWA VYA WALLIS NA FUTUNA
VANUATU
TUVALU
FIJI
KIRIBATI
TOKELAU
HAWAII
SAMOA MAGHARIBI
SAMOA YA MAREKANI
NIUE
TONGA
VISIWA VYA COOK
TAHITI
VISIWA VYA SOLOMON
BAHARI YA PASIFIKI
BAHARI YA HINDI
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 421]
A. J. Joseph, wa India, pamoja na binti yake Gracie, aliyetumikia akiwa mishonari aliyezoezwa Gileadi
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
INDIA
[Picha katika ukurasa wa 411]
Hermann Herkendell, pamoja na bibi-arusi wake, walifunga safari ya miezi mingi wakati wa fungate yao wakahubirie wasemao Kijerumani katika Urusi
[Picha katika ukurasa wa 412]
Makolpota katika Uingereza na Scotland walijitahidi kumpa kila mtu fursa ya kupokea ushahidi; hata watoto wao walisaidia kugawanya trakti
[Picha katika ukurasa wa 414]
E. J. Coward alieneza kwa bidii kweli ya Biblia katika eneo la Karibea
[Picha katika ukurasa wa 418]
Frank Grove (kushoto) na Ed Nelson (waonekanao hapa wakiwa na wake zao) kila mmoja alitumia zaidi ya miaka 50 kueneza ujumbe wa Ufalme wakati wote kotekote katika New Zealand
[Picha katika ukurasa wa 420]
C. T. Russell na washirika sita walifunga safari ya ulimwenguni pote katika 1911-1912 ili kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema
-
-
Sehemu ya 2—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya DuniaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 22
Sehemu ya 2—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
Kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme tokea 1914 hadi 1935 inazungumziwa katika kurasa 423 hadi 443. Mashahidi wa Yehova huonyesha mwaka 1914 kuwa wakati ambapo Yesu Kristo alitawazwa akiwa Mfalme wa kimbingu akiwa na mamlaka juu ya mataifa. Alipokuwa duniani, Yesu alitabiri kwamba kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme duniani pote kujapokuwa mnyanyaso mkali ingekuwa sehemu ya ishara ya kuwapo kwake katika uweza wa Ufalme. Ni jambo gani hasa lililotukia wakati wa miaka iliyofuata 1914?
VITA ya kwanza ya ulimwengu iligharikisha Ulaya haraka katika 1914. Kisha ikafikilia na kuhusisha ndani nchi zenye asilimia iliyokadiriwa kuwa 90 ya idadi ya watu wa ulimwengu. Matukio yaliyoshirikishwa na vita hiyo yaliathirije utendaji wa kuhubiri wa watumishi wa Yehova?
Ile Miaka Yenye Msiba ya Vita ya Ulimwengu 1
Wakati wa ile miaka ya mapema ya vita, hakukuwa na kizuizi hata kidogo isipokuwa Ujerumani na Ufaransa. Trakti ziligawanywa bila kizuizi katika mahali pengi, na “Photo-Drama” iliendelea kutumiwa, ingawa kwa kadiri ndogo zaidi baada ya 1914. Kadiri harara ya vita ilivyoongezeka, makasisi katika Indies Magharibi ya Uingereza walitoa uvumi kwamba E. J. Coward, aliyewakilisha Watch Tower Society, alikuwa jasusi wa Ujerumani, hivyo aliamriwa aondoke. Wakati ugawanyaji wa kitabu The Finished Mystery ulipoanza katika 1917, upinzani ukawa wenye kuenea.
Umma ulikuwa na hamu ya kupata kitabu hicho. Ilikuwa lazima kuongeza agizo la kwanza la Sosaiti kwa wachapaji kwa zaidi ya mara kumi katika muda wa miezi michache. Lakini makasisi wa Jumuiya ya Wakristo walikasirika sana kwa kufunuliwa kwa mafundisho yao bandia. Walitumia harara ya wakati wa vita ili kushutumu Wanafunzi wa Biblia mbele ya maofisa wa serikali. Kotekote Marekani, wanaume na wanawake walioshirikishwa na ugawanyaji wa fasihi za Wanafunzi wa Biblia walishambuliwa na wafanyaghasia, na pia wakapakwa lami na kutiwa manyoya. Katika Kanada, makao yalipekuliwa, na watu waliopatikana na vichapo fulani vya Shirika la Kimataifa la Wanafunzi wa Biblia walitozwa faini kubwa au wakatiwa gerezani. Hata hivyo, Thomas J. Sullivan, ambaye wakati huo alikuwa katika Port Arthur, Ontario, aliripoti kwamba katika pindi moja, wakati alipotiwa jela kwa usiku mmoja, polisi katika jiji hilo walichukua nakala za fasihi zilizopigwa marufuku wakaenda nazo nyumbani kwa ajili yao wenyewe na marafiki wao, hivyo wakagawanya akiba yote iliyopatikana—nakala kama 500 au 600.
Makao makuu ya Watch Tower Society yenyewe yalishambuliwa, na washiriki wa wafanyakazi wasimamizi walihukumiwa vifungo virefu gerezani. Ilionekana kwa maadui wao kwamba Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamepigwa pigo la kifo. Kazi yao ya kutoa ushahidi kwa njia iliyovuta uangalifu mwingi wa umma kwa kweli ilikoma.
Ingawa hivyo, hata Wanafunzi wa Biblia waliofungwa gerezani walipata fursa za kuongea na wafungwa wenzao juu ya kusudi la Mungu. Wakati maofisa wa Sosaiti na washirika wao wa karibu walipowasili gerezani katika Atlanta, Georgia, kwanza walikatazwa kuhubiri. Lakini walizungumza Biblia miongoni mwao wenyewe, na wengine walivutwa kwao na tabia yao, njia yao ya maisha. Baada ya miezi michache, makamu wa mkuu wa gereza aliwapa mgawo wa kutoa maagizo ya kidini kwa wafungwa wengine. Idadi iliongezeka hadi kufikia 90 wakawa wakihudhuria darasa.
Wakristo wengine waaminifu-washikamanifu walipata pia njia za kutoa ushahidi wakati wa miaka hiyo ya vita. Nyakati nyingine hiyo ilitokeza kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme katika nchi ambako habari njema hazikuwa zimehubiriwa. Hivyo, katika 1915 Mwanafunzi wa Biblia katika New York, Mkolombia, alipeleka kwa posta chapa ya Kihispania ya The Divine Plan of the Ages kwa mwanamume mmoja katika Bogotá, Kolombia. Baada ya miezi sita hivi, jibu likawasili kutoka kwa Ramón Salgar. Alikuwa amejifunza kitabu hicho kwa uangalifu, kikampendeza, naye alitaka nakala 200 azigawanye kwa wengine. Ndugu J. L. Mayer, kutoka Brooklyn, New York, pia alipeleka kwa posta nakala za Kihispania za Bible Students Monthly. Idadi kubwa yazo ilienda Hispania. Na wakati Alfred Joseph, aliyekuwa katika Barbados wakati ule, alipochukua kazi ya mkataba katika Sierra Leone, Afrika Magharibi, alitumia kwa faida fursa za kutoa ushahidi juu ya kweli za Biblia alizokuwa amejifunza karibuni.
Kwa makolpota, ambao huduma yao ilihusu kutembelea makao na mahali pa biashara, mara nyingi ilikuwa vigumu zaidi. Lakini idadi kadhaa waliokwenda El Salvador, Honduras, na Guatemala walikuwa na shughuli nyingi huko katika 1916 wakishiriki pamoja na watu kweli zenye kutoa uhai. Wakati wa pindi hiyo, Fanny Mackenzie, kolpota mmoja Mwingereza, alisafiri mara mbili kwenda nchi za Mashariki kwa meli, akitua katika China, Japani, na Korea ili kugawanya fasihi za Biblia, na kisha akafuatia kupendezwa kwa kuandika barua.
Hata hivyo, kulingana na rekodi zipatikanazo, idadi ya Wanafunzi wa Biblia walioripotiwa kuwa walikuwa na ushiriki fulani katika kazi ya kuhubiri habari njema kwa wengine wakati wa 1918 ilipungua kwa asilimia 20 ulimwenguni pote ilinganishwapo na ripoti ya 1914. Baada ya kutendewa vikali wakati wa miaka hiyo ya vita, je, wangeendelea na huduma yao?
Watiwa Uhai Mpya
Katika Machi 26, 1919, msimamizi wa Watch Tower Society na washirika wenzake waliachiliwa kutoka kifungo chao kisicho cha haki. Mipango ilifanywa haraka ili kusonga mbele na kazi ya kupiga mbiu ya habari njema ya Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote.
Kwenye mkusanyiko mkuu katika Cedar Point, Ohio, katika Septemba wa mwaka huo, J. F. Rutherford, wakati huo akiwa msimamizi wa Sosaiti, alitoa hotuba iliyokazia kwamba kazi ya kutangaza kuja kwenye utukufu kwa Ufalme wa Mungu wa Kimesiya ndiyo kazi ya maana kwelikweli kwa watumishi wa Yehova.
Hata hivyo, idadi hasa ya waliokuwa wakishiriki katika kazi hiyo wakati huo ilikuwa ndogo. Wengine waliokuwa wamejizuia kutoa ushahidi kwa ajili ya woga wakati wa 1918 wakawa watendaji tena, na wachache zaidi wakajiunga na idadi zao. Lakini rekodi zipatikanazo huonyesha kwamba katika 1919 walikuwako kama 5,700 tu waliokuwa wakitoa ushahidi kwa bidii katika nchi 43. Hata hivyo Yesu alikuwa ametabiri: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14, NW) Hiyo ingetimizwaje? Hawakujua, wala hawakujua kazi ya kutoa ushahidi ingeendelea kwa muda mrefu kadiri gani. Hata hivyo, wale waliokuwa watumishi wa Mungu waaminifu-washikamanifu walikuwa na nia na hamu ya kuendelea na kazi. Walikuwa na uhakika kwamba Yehova angeelekeza mambo kupatana na mapenzi yake.
Wakitiwa bidii na yale waliyoona yameonyeshwa waziwazi katika Neno la Mungu, walianza kufanya kazi. Katika muda wa miaka mitatu idadi iliyokuwa ikishiriki sehemu katika kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu ikakaribia kuwa mara tatu, kulingana na ripoti zipatikanazo, na wakati wa 1922 walikuwa na shughuli wakihubiri katika nchi 15 zaidi ya ilivyokuwa katika 1919.
Habari Yenye Kuvutia
Lo! ni ujumbe wenye kusisimua kama nini walioutangaza—“Mamilioni wanaoishi sasa hawatakufa kamwe!” Ndugu Rutherford alikuwa ametoa hotuba juu ya habari hiyo katika 1918. Ilikuwa pia kichwa cha kijitabu cha kurasa 128 kilichotangazwa katika 1920. Tokea 1920 hadi 1925, habari hiyohiyo ilitolewa tena na tena ulimwenguni pote katika mikutano ya hadhara katika maeneo yote ambako wasemaji walipatikana na kwa lugha zaidi ya 30. Badala ya kusema, kama isemavyo Jumuiya ya Wakristo, kwamba watu wote wema wangeenda mbinguni, hotuba hiyo ilikazia fikira tumaini lenye msingi wa Biblia la uhai wa milele katika dunia iliyo paradiso kwa wanadamu watiifu. (Isa. 45:18; Ufu. 21:1-5) Na ilionyesha usadikisho wa kwamba wakati wa utimizo wa tumaini hilo ulikuwa karibu sana.
Taarifa katika magazeti ya habari na karatasi zilizoangikwa kwenye mbao zilitumiwa kutangaza mihadhara hiyo. Habari hiyo ilikuwa yenye kuvutia sana. Katika Februari 26, 1922, watu zaidi ya 70,000 walihudhuria katika mahali mbalimbali 121 katika Ujerumani pekee. Ilikuwa kawaida idadi ya kikao kimoja cha wasikilizaji kufikia maelfu. Kwa kielelezo, katika Cape Town, Afrika Kusini, 2,000 walikuwapo wakati mhadhara huo ulipotolewa katika Opera House. Kwenye jumba la chuo kikuu katika jiji kuu la Norway, si kwamba tu viti vyote vilijazwa bali pia wengi sana walizuiwa kuingia kwa kukosa nafasi hivi kwamba ilikuwa lazima kurudia programu hiyo saa moja na nusu baadaye—katika jumba lililojaa tena.
Katika Klagenfurt, Austria, Richard Heide alimwambia baba yake hivi: “Mimi nitaenda kusikia hotuba hiyo hata yeyote aseme nini. Mimi nataka kujua kama huu ni udanganyifu tu au kama mna ukweli wowote!” Alichochewa sana na yale aliyosikia, na upesi yeye na dada yake, pamoja na wazazi wao, walikuwa wakiisimulia wengine.
Lakini ujumbe huo wa Biblia haukuwa tu wa watu ambao wangehudhuria mhadhara wa watu wote. Wengine vilevile walihitaji kujulishwa. Si umma tu kwa ujumla bali pia viongozi wa kisiasa na wa kidini walihitaji kuusikia. Hilo lingetimizwaje?
Ugawanyaji wa Majulisho Yenye Nguvu
Habari iliyochapwa ilitumiwa ili kufikia mamilioni ya watu ambao kwa wakati uliopita walikuwa wamesikia tu ujumbe ambao Wanafunzi wa Biblia walitangaza. Tokea 1922 hadi 1928, ushahidi wenye mafanikio ulitolewa kwa njia ya majulisho saba yenye nguvu, maazimio yaliyokubaliwa kwenye mikusanyiko ya kila mwaka ya Wanafunzi wa Biblia. Hesabu ya nakala zilizochapwa za mengi ya maazimio hayo moja moja yaliyogawanywa kufuatia mikusanyiko hiyo ilijumlika kuwa milioni 45 hadi 50—utimizo wenye kustaajabisha kwelikweli kwa kikosi hicho kidogo cha wapiga-mbiu wa Ufalme kilichokuwa kikitumikia wakati huo!
Azimio la 1922 lilikuwa na kichwa “Mwito kwa Viongozi wa Ulimwengu”—naam, wito wathibitishe dai lao la kwamba wangeweza kuleta amani, ufanisi, na furaha kwa ajili ya wanadamu au, wakishindwa, wakiri kwamba ni Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Mesiya wake uwezao kutimiza mambo hayo. Katika Ujerumani, azimio hilo lilipelekwa kwa posta kwa maliki Mjerumani aliyekuwa uhamishoni, kwa rais, na kwa washiriki wote wa Bunge la Ujerumani; na nakala milioni nne unusu hivi zikapelekewa umma. Katika Afrika Kusini, Edwin Scott, akibeba mgongoni fasihi zilizokuwa katika mfuko na bakora ikiwa mkononi mwake ili kufukuza mbwa wakali, alitembelea miji 64, akigawanya binafsi nakala 50,000. Baadaye, wakati makasisi Waholanzi katika Afrika Kusini walipotembelea makao ya washiriki wa parishi wao ili kukusanya michango, wengi wao walitikisa azimio hilo usoni pa makasisi na kusema: “Yawapasa msome hili nanyi hamngekuja tena kupata pesa kutoka kwetu.”
Katika 1924 azimio lenye kichwa “Makasisi Washtakiwa” lilifunua mafundisho na mazoea ya makasisi yasiyo ya Kimaandiko, likafunua fungu lao wakati wa vita ya ulimwengu, na likahimiza watu wajifunze Biblia ili wapate kujua binafsi juu ya maandalizi ya ajabu aliyofanya Mungu kwa ajili ya kubariki wanadamu. Katika Italia wakati huo, wachapaji walitakwa kuandika jina lao katika kila kitu walichochapa, na pia walionwa kuwa na daraka juu ya yaliyomo. Mwanafunzi wa Biblia aliyesimamia kazi katika Italia alipeleka nakala ya azimio hilo kwa maofisa wa serikali walioichunguza na kwa urahisi wakatoa ruhusa ichapwe na kugawanywa. Wachapaji pia walikubali kuichapa. Akina ndugu katika Italia waligawanya nakala 100,000. Hasa walihakikisha kwamba papa na maofisa wengine wa vyeo vya juu wa Vatikani walipokea nakala moja kila mmoja wao.
Katika Ufaransa, ugawanyaji wa azimio hilo ulitokeza itikio kali na mara nyingi lenye jeuri kutoka kwa makasisi. Kwa kukata tamaa kasisi mmoja katika Pomerania, Ujerumani, alishtaki Sosaiti na meneja wayo mahakamani, lakini kasisi huyo alishindwa kesi wakati mahakama iliposikia yaliyokuwamo katika azimio hilo lote. Ili kazi yao isisumbuliwe na wale wasiotaka watu wajue kweli, Wanafunzi wa Biblia katika mkoa wa Quebec, katika Kanada, waliacha maazimio hayo katika makao ya watu wakati wa saa za alfajiri, kuanzia saa 9:00 za usiku. Hizo zilikuwa nyakati zenye kusisimua!
Kuonyesha Shukrani kwa Majibu Yenye Kuridhisha
Wakati wa Vita ya Ulimwengu 1, Waarmenia wengi walifukuzwa bila huruma kutoka makao na nchi yao walimozaliwa. Miongo miwili tu mapema kidogo, mamia ya maelfu ya Waarmenia walikuwa wamechinjwa, na wengine walikuwa wamekimbia ili kuokoa uhai wao. Wachache kati ya watu hao walikuwa wamesoma vichapo vya Watch Tower Society katika nchi yao. Lakini walio wengi kati yao walipewa ushahidi katika nchi ambako walisafiri wakiwa wakimbizi.
Baada ya ukatili waliokuwa wamevumilia, wengi walikuwa na maswali mazito kuhusu kwa nini Mungu aliruhusu uovu. Ungeendelea kwa muda mrefu kadiri gani? Ungekoma wakati gani? Baadhi yao walishukuru kujifunza majibu yenye kuridhisha yapatikanayo katika Biblia. Vikundi vya Wanafunzi wa Biblia Waarmenia vikasitawi haraka katika majiji mbalimbali ya Mashariki ya Kati. Bidii yao kwa ajili ya kweli ya Biblia ilikuwa na matokeo katika maisha za wengine. Katika Ethiopia, Argentina, na Marekani, Waarmenia wenzao walikubali habari njema na wakakubali kwa furaha daraka la kuzishiriki pamoja na wengine. Mmoja wao alikuwa Krikor Hatzakortzian, ambaye akiwa painia peke yake alieneza ujumbe wa Ufalme katika Ethiopia katika miaka ya katikati ya 1930. Katika pindi moja, aliposhtakiwa kwa uwongo na wapinzani, hata alikuwa na fursa ya kutoa ushahidi kwa maliki, Haile Selassie.
Kupeleka Kweli Zenye Thamani Kwenye Nchi za Kwao
Tamaa yenye kuwaka ya kushiriki kweli muhimu za Biblia ilihimiza watu wengi warudi kwenye nchi zao walimozaliwa ili kushiriki katika kazi ya kueneza evanjeli. Itikio lao lilikuwa kama lile la watu wa kutoka nchi nyingi waliokuwa katika Yerusalemu katika 33 W.K. na ambao walipata kuwa waamini wakati roho takatifu iliposukuma mitume na washiriki wao waseme kwa lugha nyingi, kuhusu “mambo yenye fahari ya Mungu.” (Mdo. 2:1-11, NW) Kama vile tu waamini hao wa karne ya kwanza walivyopeleka kweli kwenye nchi zao, ndivyo na hawa wanafunzi wa kisasa.
Wanaume kwa wanawake waliokuwa wamejifunza kweli ng’ambo walirudi Italia. Walitoka Amerika, Ubelgiji, na Ufaransa wakatangaza kwa bidii ujumbe wa Ufalme mahali walipokaa. Makolpota kutoka mkoa wa Tisino wa Uswisi wenye kusema Kiitalia walihamia Italia pia waendelee na kazi yao. Ingawa idadi yao ilikuwa ndogo, kama tokeo la utendaji wao wa umoja, upesi walifikia karibu kila jiji kuu na vingi vya vijiji vya Italia. Wao hawakuwa wakihesabu saa walizotumia katika kazi hiyo. Wakisadiki kwamba walikuwa wakihubiri kweli ambazo Mungu alitaka watu wazijue, mara nyingi walifanya kazi tokea asubuhi hadi usiku ili kufikia watu wengi iwezekanavyo.
Wagiriki waliokuwa wamekuwa Wanafunzi wa Biblia katika Albania ya karibu na mbali kama vile Amerika pia walielekeza fikira kwenye nchi ya kwao. Walisisimuka kujifunza kwamba ibada ya sanamu si ya Kimaandiko (Kut. 20:4, 5; 1 Yoh. 5:21), kwamba watenda dhambi hawachomwi katika moto wa helo (Mhu. 9:5, 10; Eze. 18:4; Ufu. 21:8), na kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la kweli kwa wanadamu (Dan. 2:44; Mt. 6:9, 10). Walikuwa na hamu ya kushiriki kweli hizo pamoja na wananchi wenzao—kibinafsi au kwa barua. Kama tokeo, vikundi vya Mashahidi wa Yehova vikaanza kusitawi katika Ugiriki na visiwa vya Ugiriki.
Kufuatia Vita ya Ulimwengu 1, maelfu ya watu kutoka Poland walihamia Ufaransa ili kufanya kazi ya kuchimba makaa-mawe. Makutaniko ya Kifaransa hayakuwapuuza kwa sababu walisema lugha tofauti. Walipata njia za kushiriki kweli za Biblia pamoja na wachimbaji hao na familia zao, na idadi ya walioitikia vizuri ikazidi upesi ile ya Mashahidi Wafaransa. Wakati serikali ilipotoa amri ya kuwarudisha kwao, 280 walilazimika kurudi Poland katika 1935, hiyo ilitumika tu kuimarisha kazi ya kueneza ujumbe wa Ufalme huko. Hivyo, katika 1935, kulikuwa wapiga-mbiu wa Ufalme 1,090 walioshiriki kutoa ushahidi nchini Poland.
Wengine waliitikia mialiko ya kuondoka nchi za kwao wakachukue utumishi katika mashamba ya kigeni.
Waeneza-Evanjeli Wenye Bidii wa Ulaya Wasaidia Katika Mashamba ya Kigeni
Kwa ushirikiano wa kimataifa, Nchi za Baltiki (Estonia, Latvia, na Lithuania) zilisikia ile kweli yenye kuchangamsha moyo juu ya Ufalme wa Mungu. Wakati wa miaka ya 1920 na ya 1930, ndugu na dada wenye bidii kutoka Denmark, Uingereza, Finland, na Ujerumani walifanya kazi nyingi ya kutoa ushahidi katika eneo hilo. Fasihi nyingi ziliangushwa, nao maelfu wakasikia hotuba za Biblia zilizotolewa. Kutoka Estonia programu za Biblia zilizotangazwa kwa redio kwa ukawaida kwa lugha kadhaa zilifikia hata ile iliyokuwa wakati huo Muungano wa Sovieti.
Kutoka Ujerumani wafanyakazi wenye moyo wa kupenda wakati wa miaka ya 1920 na ya 1930 walichukua migawo katika sehemu nyingi kama vile Austria, Ubelgiji, Bulgaria, Chekoslovakia, Ufaransa, Luxembourg, Uholanzi, Hispania, na Yugoslavia. Willy Unglaube alikuwa miongoni mwao. Baada ya kutumikia kwa wakati katika Betheli ya Magdeburg, katika Ujerumani, alisonga mbele akashughulikie migawo akiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote katika Ufaransa, Algeria, Hispania, Singapore, Malasia, na Thailand.
Wakati mwito ulipotolewa kutoka Ufaransa wa kupata msaada wakati wa miaka ya 1930, makolpota kutoka Uingereza walitoa ithibati kwamba walikuwa wanajua kwamba utume wa Kikristo wa kuhubiri ulitaka kueneza evanjeli si katika nchi yao tu bali pia katika sehemu nyingine za dunia. (Mk. 13:10) John Cooke alikuwa mmojawapo wa wafanyakazi wenye bidii aliyeitikia mwito wa Kimakedonia. (Linganisha Matendo 16:9, 10.) Wakati wa miongo sita iliyofuata, yeye alishughulikia migawo ya utumishi katika Ufaransa, Hispania, Ireland, Ureno, Angola, Msumbiji, na Afrika Kusini. Kaka yake Eric aliacha kazi kwenye Benki ya Barclay akajiunga na John katika huduma ya wakati wote Ufaransa; baadaye, yeye vilevile alitumikia katika Hispania na Ireland na akashiriki katika kazi ya mishonari katika Rhodesia Kusini (sasa ni Zimbabwe) na Afrika Kusini.
Katika Mei 1926, George Wright na Edwin Skinner, wakiwa Uingereza, walikubali mwaliko wakasaidie kupanua kazi ya Ufalme katika India. Mgawo wao ulikuwa mkubwa sana! Ulitia ndani sehemu za Afghanistan, Burma (sasa ni Myanmar), Ceylon (sasa ni Sri Lanka), India, na Persia (sasa ni Iran). Walipowasili Bombay, walilakiwa na mvua ya majira. Hata hivyo, kwa kuwa hawakuhangaikia kupita kiasi starehe au raha ya kibinafsi, upesi walikuwa wakisafiri kwenda sehemu za mbali za nchi ili kuwatafuta Wanafunzi wa Biblia waliojulikana ili kuwatia moyo. Pia waliangusha kiasi kikubwa cha fasihi ili kuchochea kupendezwa miongoni mwa wengine. Kazi ilifanywa kwa bidii. Hivyo wakati wa 1928 wale wapiga-mbiu wa Ufalme 54 katika Travancore (Kerala), katika kusini mwa India, walipanga mikutano ya watu wote 550 iliyohudhuriwa na watu 40,000 hivi. Katika 1929 mapainia wanne zaidi kutoka shamba la Uingereza walihamia India kusaidia kazi. Na katika 1931 wengine watatu kutoka Uingereza waliwasili Bombay. Walijitahidi tena na tena kufikia sehemu mbalimbali za nchi hiyo kubwa, wakigawanya fasihi si katika Kiingereza tu bali pia katika lugha za Kihindi.
Wakati huohuo, kulikuwa kukitukia nini katika Ulaya Mashariki?
Vuno la Kiroho
Kabla ya vita ya ulimwengu ya kwanza, mbegu za kweli ya Biblia zilikuwa zimetawanywa katika Ulaya Mashariki, na baadhi yazo zilikuwa zimetia mizizi. Katika 1908 Andrásné Benedek, mwanamke Mhungaria mnyenyekevu, alikuwa amerudi Austria na Hungaria, ili kushiriki pamoja na wengine mambo mema aliyokuwa amejifunza. Miaka miwili baadaye, Károly Szabó na József Kiss walikuwa wamerudi pia kwenye nchi hiyo na walikuwa wakieneza kweli ya Biblia hasa katika maeneo ambayo baadaye yalikuja kujulikana kuwa Rumania na Chekoslovakia. Ujapokuwa upinzani wenye jeuri kutoka kwa makasisi wenye hasira, vikundi vya funzo vilifanyizwa, na kazi kubwa ya kutoa ushahidi ikafanywa. Wengine walijiunga nao katika kujulisha hadharani imani yao, na kufikia 1935 idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika Hungaria ilikuwa imekua kufikia 348.
Rumania ilikaribia kuwa na ukubwa maradufu wakati ramani ya Ulaya iliporekebishwa na washindi kufuatia Vita ya Ulimwengu 1. Iliripotiwa kwamba katika nchi hiyo iliyoongezewa ukubwa, katika 1920, kulikuwa vikundi 150 hivi vya Wanafunzi wa Biblia, ambavyo watu 1,700 walishirikiana navyo. Mwaka uliofuata, kwenye mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana, karibu 2,000 walishiriki mifano ya Ukumbusho, kuonyesha kwamba walidai kuwa ndugu za Kristo watiwa-mafuta kwa roho. Hesabu hiyo iliongezeka kwa njia yenye kutokeza wakati wa miaka minne iliyofuata. Katika 1925, kulikuwa 4,185 katika hudhurio la Ukumbusho, na kama ilivyokuwa desturi wakati huo, walio wengi wao bila shaka walishiriki mifano. Hata hivyo, imani ya hao wote ingetahiniwa. Je, wangethibitika kuwa “ngano” halisi, au mwigo tu? (Mt. 13:24-30, 36-43) Je, kweli wangefanya kazi ya kutoa ushahidi ambayo Yesu alikuwa amegawia wafuasi wake? Je, wangestahimili katika kazi hiyo wakabiliwapo na upinzani mkali? Je, wangekuwa waaminifu hata wakati wengine waonyeshapo roho kama ile ya Yuda Iskariote?
Ripoti ya 1935 huonyesha kwamba si wote waliokuwa na imani ya aina iliyowawezesha kuvumilia. Katika mwaka huo, walikuwa 1,188 tu waliokuwa na ushiriki fulani katika kazi ya kutoa ushahidi katika Rumania, ingawa hesabu iliyo zaidi ya mara mbili yayo walikuwa wakishiriki mifano ya Ukumbusho katika wakati huo. Hata hivyo, wale waaminifu waliendelea kujishughulisha na utumishi wa Bwana-Mkubwa. Walishiriki na watu wengine wanyenyekevu kweli za Biblia zilizowaletea shangwe katika mioyo yao wenyewe. Njia moja yenye kutokeza waliyotumia kufanya hivyo ni kugawanya fasihi. Kati ya 1924 na 1935, walikuwa tayari wameangushia wenye kupendezwa vitabu na vijitabu zaidi ya 800,000, kuongezea trakti.
Vipi Chekoslovakia, iliyokuwa imekuwa taifa katika 1918 baada ya kuanguka kwa Milki ya Austria na Hungaria? Huko kazi ya kutoa ushahidi kwa bidii hata zaidi ilikuwa ikichangia vuno la kiroho. Kazi ya kuhubiri ya mapema zaidi ilikuwa imefanywa katika Kihungaria, Kirusi, Kirumania, na Kijerumani. Halafu, katika 1922, Wanafunzi wa Biblia kadhaa walirudi kutoka Amerika ili kuelekeza fikira zao kwenye idadi ya watu wasemao Kislovaki, na mwaka uliofuata wenzi wa ndoa kutoka Ujerumani walianza kukazia fikira eneo la Wacheki. Makusanyiko ya ukawaida, ingawa madogo, yalisaidia kuwatia moyo na kuwaunganisha akina ndugu. Baada ya makutaniko kupangwa kitengenezo vizuri zaidi kwa ajili ya kazi ya kueneza evanjeli nyumba hadi nyumba katika 1927, ukuzi ulipata kuwa wazi zaidi. Katika 1932 kichocheo chenye nguvu kwa kazi kilitolewa na mkusanyiko wa kimataifa katika Prague, uliohudhuriwa na watu 1,500 hivi kutoka Chekoslovakia na nchi jirani. Kuongezea hayo, vikundi vikubwa vya umati viliona namna ya “Photo-Drama of Creation” ya saa nne iliyoonyeshwa toka upande mmoja wa nchi hadi ule mwingine. Katika pindi ya mwongo mmoja tu, fasihi mbalimbali za Biblia zaidi ya 2,700,000 ziligawanywa kwa vile vikundi mbalimbali vya lugha katika nchi hiyo. Kazi yote hiyo ya kupanda, kupalilia, na kumwagilia maji ilichangia vuno ambalo kwalo wapiga-mbiu wa Ufalme 1,198 walishiriki katika mwaka 1935.
Yugoslavia (iliyojulikana awali kuwa Ufalme wa Waserbia, Wakroati, na Waslovenia) ilikuwa imetokea kama tokeo la kurekebishwa kwa ramani ya Ulaya kufuatia vita ya ulimwengu ya kwanza. Mapema sana kama 1923, iliripotiwa kwamba kikundi cha Wanafunzi wa Biblia kilikuwa kikitoa ushahidi katika Belgrade. Baadaye ile “Photo-Drama of Creation” ilionyeshwa kwa vikundi vikubwa vya watu kotekote nchini. Wakati Mashahidi wa Yehova walipokuja chini ya mnyanyaso mkali katika Ujerumani, idadi katika Yugoslavia iliimarishwa na mapainia Wajerumani. Bila kuhangaikia raha ya kibinafsi, walijitahidi kufikia sehemu za mbali za nchi hii yenye milima ili kuhubiri. Wengine kati ya mapainia hao walienda Bulgaria. Jitihada zilikuwa zikifanywa pia kuhubiri habari njema katika Albania. Katika sehemu hizo zote, mbegu za kweli ya Ufalme zilipandwa. Baadhi ya mbegu hizo zilizaa tunda. Lakini ingekuwa baada ya miaka mingi kwamba kungekuwa vuno kubwa zaidi katika sehemu hizi.
Kusini zaidi, katika bara la Afrika, habari njema zilikuwa zikienezwa pia na wale waliothamini sana pendeleo la kuwa mashahidi wa Aliye Juu Zaidi.
Nuru ya Kiroho Yaangaza Katika Afrika Magharibi
Miaka saba hivi baada ya Mwanafunzi wa Biblia kutoka Barbados kwenda kwanza katika Afrika Magharibi kwa ajili ya mkataba wa kazi, aliandikia ofisi ya Watch Tower Society katika New York kuwaarifu kwamba watu wengi kiasi walikuwa wakionyesha kupendezwa na Biblia. Miezi michache baadaye, katika Aprili 14, 1923, kwa mwaliko wa Ndugu Rutherford, W. R. Brown, aliyekuwa akitumikia katika Trinidad, aliwasili Freetown, Sierra Leone, pamoja na familia yake.
Mipango ilifanywa mara hiyo ili Ndugu Brown atoe hotuba katika Jumba la Ukumbusho la Wilberforce. Katika Aprili 19, kulikuwa hudhurio la watu 500 hivi, kutia na walio wengi wa makasisi wa Freetown. Jumapili iliyofuata alitoa hotuba tena. Habari yake ilikuwa ile ambayo C. T. Russell alikuwa ametumia mara nyingi—“Kwenda Helo na Kurudi. Nani Walio Humo?” Hotuba za Ndugu Brown zilitia ndani kwa ukawaida manukuu ya Maandiko yaliyoangaziwa kwa slaidi za taa ili wasikilizaji waweze kuyaona. Alipokuwa akihutubu, alikuwa akisema hivi kwa kurudiarudia: “Si Brown anayesema, bali Biblia yasema.” Kwa sababu ya hilo, yeye akaja kuitwa “Bible Brown.” Na kama tokeo la utoaji wake wa Kimaandiko, wenye kupatana na akili, baadhi ya washiriki mashuhuri wa kanisa waliondoka kanisani na kuanza utumishi wa Yehova.
Alisafiri sana ili kuanzisha kazi ya Ufalme katika maeneo zaidi. Kwa kusudi hilo, alitoa mihadhara mingi ya Biblia, na kugawanya kiasi kikubwa cha fasihi, naye aliwatia moyo wengine wafanye vivyo hivyo. Kazi yake ya kueneza evanjeli ilimpeleka katika Gold Coast (sasa ni Ghana), Liberia, Gambia, na Nigeria. Kutoka Nigeria wengine walipeleka ujumbe wa Ufalme katika Benin (wakati huo ikijulikana kuwa Dahomey) na Kamerun. Ndugu Brown alijua kwamba umma hawakuwa na staha kwa ile waliyoiita “dini ya mzungu,” hivyo katika Jumba la Ukumbusho la Glover katika Lagos, alitoa hotuba juu ya kushindwa kwa dini ya Jumuiya ya Wakristo. Baada ya mkutano wasikilizaji hao wenye kuchangamka walipata vitabu 3,900 wavisome na kuvishiriki na wengine.
Wakati Ndugu Brown alipokwenda Afrika Magharibi kwa mara ya kwanza, ni watu wachache tu waliokuwa wamesikia ujumbe wa Ufalme. Wakati alipoondoka miaka 27 baadaye, walikuwa Mashahidi wa Yehova watendaji zaidi ya 11,000 katika eneo hilo. Uwongo wa kidini ulikuwa ukifunuliwa wazi; ibada ya kweli ilikuwa imeanzishwa na ilikuwa ikienea haraka.
Kuelekea Juu Kwenye Pwani ya Afrika Mashariki
Mapema sana katika karne ya 20, baadhi ya vichapo vya C. T. Russell vilikuwa vimeenezwa katika sehemu ya kusini-mashariki mwa Afrika na watu mmoja-mmoja waliokuwa wamekubali mawazo machache ya vitabu hivyo lakini walikuwa wameyachanganya na falsafa zao wenyewe. Matokeo yakawa zile zilizoitwa eti harakati za Watchtower ambazo hazikuwa na uhusiano wowote na Mashahidi wa Yehova. Baadhi yazo zilikuwa na maelekeo ya kisiasa, zikichochea msukosuko miongoni mwa Waafrika wenyeji. Kwa miaka mingi ile sifa mbaya ya vikundi hivyo ilitokeza vizuizi kwa kazi ya Mashahidi wa Yehova.
Hata hivyo, hesabu fulani ya Waafrika walitambua kati ya kweli na uwongo. Wafanyakazi wenye kusafirisafiri walipeleka habari njema za Ufalme wa Mungu kwenye nchi jirani na kuzishiriki pamoja na watu waliosema lugha za Kiafrika. Idadi ya watu wasemao Kiingereza katika kusini-mashariki mwa Afrika sanasana ilipokea ujumbe, kwa njia ya mawasiliano na Afrika Kusini. Hata hivyo, katika nchi nyinginezo, upinzani mkali wa maofisa wa serikali, ukichochewa na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo, ulizuia kazi ya kuhubiri kwa upande wa Mashahidi Wazungu miongoni mwa vikundi vyenye kusema lugha za Kiafrika. Hata hivyo, kweli ilienea, ingawa watu wengi walioonyesha kupendezwa katika ujumbe wa Biblia walihitaji msaada zaidi ili wafanye utumizi sahihi wenye mafaa wa yale waliyokuwa wakijifunza.
Baadhi ya wakuu wa serikali wasiopendelea upande wowote hawakukubali bila kuuliza maswali yale mashtaka ya kikatili yaliyofanywa na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo dhidi ya Mashahidi. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya kamishna wa polisi katika Nyasaland (sasa ni Malawi) aliyejifanya asiweze kutambulika akaenda kwenye mikutano ya Mashahidi wenyeji ili apate kujionea mwenyewe walikuwa watu wa aina gani. Alivutiwa vizuri. Wakati kibali kilipotolewa na serikali ili kuwa na mwakilishi Mzungu mkazi, Bert McLuckie na baadaye ndugu yake Bill walitumwa huko katika miaka ya katikati ya 1930. Waliendelea kuwasiliana na polisi na makamishna wa wilaya ili maofisa hao waweze kuwa na uelewevu ulio wazi wa utendaji wao na ili wasichanganyikiwe kati ya Mashahidi wa Yehova na yoyote ya zile harakati ziitwazo Watchtower kibandia. Wakati huohuo, walifanya kazi kwa saburi, pamoja na Gresham Kwazizirah, Shahidi mwenyeji aliyekomaa, ili wasaidie mamia ya wale waliotaka kushirikiana na makutaniko watambue kwamba ukosefu wa adili kingono, matumizi mabaya ya vileo, na ushirikina ni mambo yasiyofaa maishani mwa Mashahidi wa Yehova.—1 Kor. 5:9-13; 2 Kor. 7:1; Ufu. 22:15.
Katika 1930, kulikuwa Mashahidi wa Yehova kama mia moja tu katika sehemu yote ya kusini mwa Afrika. Hata hivyo, walikuwa na mgawo uliotia ndani karibu Afrika yote kusini mwa ikweta na baadhi ya maeneo yaliyoenea kaskazini mwa ikweta. Kueneza eneo lenye mweneo mkubwa sana kadiri hiyo kwa ujumbe wa Ufalme kulitaka mapainia halisi. Frank na Gray Smith walikuwa wa aina hiyo.
Walisafiri kwa meli kilometa 4,800 mashariki na kaskazini kutoka Cape Town na kisha wakaendelea kwa gari muda wa siku nne katika barabara mbovumbovu ili wafike Nairobi, Kenya (katika Afrika Mashariki ya Uingereza). Katika muda uliopungua mwezi mmoja, waliangusha vibweta 40 vya fasihi ya Biblia. Lakini, kwa kusikitisha, wakiwa katika safari yao ya kurudi, Frank akafa kwa maleria. Ijapokuwa hivyo, muda mfupi baadaye, Robert Nisbet na David Norman walifunga safari tena—wakati huu wakiwa na vibweta 200 vya fasihi—wakahubiri katika Kenya na Uganda, pia Tanganyika na Zanzibar (zote mbili sasa ni Tanzania), wakifikia watu wengi kwa ujumbe wa Ufalme kadiri ilivyowezekana. Safari nyingine kama hizo zilieneza ujumbe wa Ufalme kwenye visiwa vya Mauritius na Madagaska katika Bahari ya Hindi na St. Helena katika Bahari Atlantiki. Mbegu za kweli zilipandwa, lakini hazikumea na kukua mara hiyo kila mahali.
Kutoka Afrika Kusini kazi ya kuhubiri habari njema ilienea pia katika Basutoland (sasa ni Lesotho), Bechuanaland (sasa ni Botswana), na Swaziland, mapema sana kama 1925. Kama miaka minane baadaye, wakati mapainia walipokuwa wakihubiri tena katika Swaziland, Mfalme Sobhuza 2 aliwakaribisha kifalme. Alikusanya walinzi wake wa kibinafsi, mashujaa-wa-vita mia moja, akasikiliza ushahidi kamili, na kisha akapata vichapo vyote vya Sosaiti ambavyo ndugu walikuwa navyo.
Hatua kwa hatua hesabu ya Mashahidi wa Yehova ilikua katika sehemu hii ya shamba la ulimwengu. Wengine walijiunga na wale wachache walioanzisha kazi barani Afrika mapema katika karne hii ya 20, na kufikia 1935 walikuwa 1,407 katika bara la Afrika walioripoti kuwa walishiriki katika kazi ya kutoa ushahidi juu ya Ufalme wa Mungu. Hesabu kubwa zao zilikuwa katika Afrika Kusini na Nigeria. Vikundi vingine vikubwa vilivyojitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova vilikuwa katika Nyasaland (sasa ni Malawi), Rhodesia Kaskazini (sasa ni Zambia), na Rhodesia Kusini (sasa ni Zimbabwe).
Wakati wa pindi hiyohiyo, fikira zilikuwa zikielekezwa pia kwenye nchi zenye kusema Kihispania na Kireno.
Kupalilia Mashamba ya Hispania na Ureno
Vita ya Ulimwengu 1 ilipokuwa ingali inaendelea, Watch Tower lilichapwa kwa mara ya kwanza katika Kihispania. Lilikuwa na anwani ya ofisi katika Los Angeles, California, iliyokuwa imefunguliwa ili kutoa uangalifu wa pekee kwa shamba la wasemao Kihispania. Akina ndugu kutoka ofisi hiyo walitoa msaada mwingi wa kibinafsi kwa wenye kupendezwa katika Marekani na pia katika nchi zilizokuwa kusini.
Juan Muñiz, aliyekuwa amekuwa mmoja wa watumishi wa Yehova katika 1917, alitiwa moyo na Ndugu Rutherford katika 1920 aondoke Marekani arudi Hispania, nchi ya kwao, ili akapange kitengenezo kazi ya kuhubiri Ufalme huko. Hata hivyo, matokeo yalikuwa madogo, si kwa sababu ya ukosefu wa bidii kwa upande wake, bali kwa sababu ya kufuatwafuatwa daima na polisi; kwa hiyo baada ya miaka michache, alihamishwa akatumwa Argentina.
Katika Brazili waabudu wachache wa Yehova walikuwa tayari wanahubiri. Mabaharia wanane wanyenyekevu walikuwa wamejifunza kweli walipokuwa likizoni kutoka meli zao katika New York. Waliporudi Brazili mapema katika 1920, walikuwa na shughuli wakishiriki ujumbe wa Biblia pamoja na wengine.
George Young, Mkanada, alitumwa Brazili katika 1923. Hakika alisaidia kuchochea kazi. Akitoa mihadhara mingi kupitia wakalimani, alionyesha yale Biblia inayosema kuhusu hali ya wafu, akafunua uwasiliano na roho kuwa ibada ya mashetani, na kueleza kusudi la Mungu kwa ajili ya kubariki familia zote za dunia. Mihadhara yake ilikuwa yenye kushawishi zaidi kwa sababu nyakati nyingine alionyesha maandiko ya Biblia yaliyozungumzwa kwenye kiwambo ili kwamba wasikilizaji wake waweze kuyaona katika lugha yao wenyewe. Alipokuwa katika Brazili, Bellona Ferguson, wa São Paulo, aliweza kubatizwa hatimaye, pamoja na wanne kati ya watoto wake. Alikuwa amengojea fursa hiyo kwa miaka 25. Miongoni mwa wale waliokubali kweli, baadhi yao walijitolea wakati huo kusaidia katika kazi ya kutafsiri fasihi katika Kireno. Upesi kukawa na ugavi mwingi wa vichapo katika lugha hiyo.
Kutoka Brazili, Ndugu Young alisonga mbele hadi Argentina katika 1924 na kupanga ugawanyaji wa bila malipo wa fasihi 300,000 katika Kihispania katika 25 kati ya ile miji na majiji makubwa. Mwaka huohuo yeye binafsi alisafiri pia kwenda Chile, Peru, na Bolivia ili kugawanya trakti.
Upesi George Young akasafiri tena ili kushughulikia mgawo mpya. Wakati huu ilikuwa Hispania na Ureno. Baada ya kujulishwa kwa maofisa wa serikali nchini na balozi wa Uingereza, aliweza kupangia Ndugu Rutherford ahutubie wasikilizaji katika Barcelona na Madrid, pamoja na jiji kuu la Ureno. Kufuatia hotuba hizo, jumla ya watu 2,350 walitoa majina na anwani zao wakiomba wapate habari zaidi. Baada ya hapo, hotuba hiyo ilitangazwa katika mojawapo magazeti ya habari ya Hispania makubwa, na kwa namna ya trakti ilipelekewa watu kwa posta kotekote nchini. Ilitokea pia katika magazeti ya Ureno.
Kwa njia hiyo ujumbe ulifika mbali kupita mipaka ya Hispania na Ureno. Kufikia mwisho wa 1925, habari njema zilikuwa zimepenya kuingia Visiwa Cape Verde (sasa ni Jamhuri ya Cape Verde), Visiwa Madeira, Afrika Mashariki ya Ureno (sasa Msumbiji), Afrika Magharibi ya Ureno (sasa Angola), na visiwa katika Bahari ya Hindi.
Mwaka uliofuata mipango ilifanywa ya kuchapa lile azimio lenye nguvu “Ushuhuda kwa Watawala wa Ulimwengu” kwenye gazeti la Kihispania La Libertad. Matangazo ya redio na ugawanyaji wa vitabu, vijitabu, na trakti, pamoja na kuonyeshwa kwa “Photo-Drama of Creation,” kulisaidia kuzidisha ushahidi. Katika 1932 mapainia kadhaa Waingereza waliitikia mwaliko wa kusaidia katika shamba hili, nao walieneza kwa utaratibu sehemu kubwakubwa za nchi kwa fasihi za Biblia mpaka Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe ya Hispania ilipowalazimisha kuondoka.
Wakati huohuo, alipowasili katika Argentina, Ndugu Muñiz alikuwa ameanza kuhubiri upesi, huku akijiruzuku kwa kurekebisha saa. Kuongezea kazi yake katika Argentina, alitoa uangalifu kwa Chile, Paraguai, na Uruguai. Kwa ombi lake baadhi ya ndugu walitoka Ulaya ili kutoa ushahidi kwa idadi ya watu wasemao Kijerumani. Miaka mingi baadaye Carlos Ott alisimulia kwamba walianza utumishi wao wa siku saa 10:00 za usiku kwa kuacha trakti chini ya kila mlango katika eneo. Baadaye mchana, walikuwa wakizuru kutoa ushahidi zaidi na kutoa fasihi zaidi ya Biblia kwa wenye nyumba wenye kupendezwa. Kutoka Buenos Aires wale walioshiriki katika huduma ya wakati wote walitawanyika kotekote nchini, kwanza kwa kufuata njia za reli zilizoanzia kwenye jiji kuu na kugawanyika kama vidole vya kiganja chako kwenda umbali wa mamia ya kilometa, kisha kwa kutumia kila njia nyingine ya usafiri ambayo wangeweza kupata. Walikuwa na vitu vichache sana vya kimwili na walivumilia magumu mengi, lakini walikuwa tajiri kiroho.
Mmojawapo wafanyakazi hao wenye bidii katika Argentina alikuwa Nicolás Argyrós, Mgiriki. Mapema katika 1930, alipopata baadhi ya fasihi zilizotangazwa na Watch Tower Society, alivutiwa hasa na kijitabu chenye kichwa Hell, kikiwa na vichwa vidogo vilivyouliza “Hiyo Ni Nini? Nani Walio Humo? Je, Waweza Kutoka?” Alishangaa kuona kwamba kijitabu hicho hakikuwaonyesha watenda dhambi kuwa wakichomwa katika kichoma-nyama. Ulikuwa mshangao kama nini alipojua kwamba moto wa helo ni uwongo wa kidini uliobuniwa kuogopesha watu, kama vile ulivyokuwa umemwogopesha yeye! Mara hiyo alianza kushiriki kweli hiyo—kwanza na Wagiriki; kisha, pamoja na wengine, kadiri Kihispania chake kilivyokua. Kila mwezi alitumia kati ya saa 200 na 300 kushiriki habari njema pamoja na wengine. Kwa kutembea na kwa kutumia njia nyingine yoyote iliyopatikana ya kusafiri, alieneza kweli za Biblia katika mikoa 14 kati ya ile 22 ya Argentina. Alipokuwa akitoka mahali pamoja hadi pengine, alilala vitandani wakati watu wenye ukaribishaji-wageni walipomwandalia kitanda, mara nyingi alilala nje, na hata katika zizi huku kilio cha punda kikimwamsha asubuhi!
Mwingine aliyekuwa na roho ya painia halisi alikuwa Richard Traub, aliyekuwa amejifunza kweli katika Buenos Aires. Alikuwa na hamu ya kushiriki habari njema pamoja na watu kwenye ile ng’ambo nyingine ya Andes, katika Chile. Katika 1930, miaka mitano baada ya kubatizwa, aliwasili katika Chile—Shahidi pekee katika nchi ya watu 4,000,000. Mwanzoni, alikuwa na Biblia tu ya kutumia kufanya kazi, lakini alianza kutembelea watu nyumba hadi nyumba. Hakukuwa na mikutano ya kutaniko ambayo angeweza kuhudhuria, hivyo, Jumapili, katika ule wakati wa kawaida wa mikutano, alikuwa akitembea kwenda kwenye Mlima San Cristóbal, na kuketi chini ya kivuli cha mti na kujizamisha katika funzo la kibinafsi na sala. Baada ya kukodi nyumba, alianza kualika watu kwenye mkutano humo. Yule mtu pekee aliyekuja kwa ajili ya mkutano wa kwanza alikuwa Juan Flores, aliyeuliza hivi: “Na wale wengine, watakuja lini?” Ndugu Traub alijibu tu: “Watakuja.” Nao walikuja. Katika muda uliopungua mwaka mmoja, 13 wakawa watumishi wa Yehova waliobatizwa.
Miaka minne baadaye, Mashahidi wawili ambao hawakuwa wamekutana tena waliungana ili kuhubiri habari njema katika Kolombia. Baada ya mwaka wenye matokeo huko, Hilma Sjoberg alilazimika kurudi Marekani. Lakini Kathe Palm aliabiri kwa meli hadi Chile, akitumia zile siku 17 baharini kutolea ushahidi wafanyakazi na abiria pia. Wakati wa mwongo uliofuata, alifanya kazi kutoka bandari ya Arica ya juu kaskazini, hadi chini kusini, katika Tierra del Fuego. Alizuru sehemu za biashara na akatolea ushahidi maofisa wa serikali. Alifikia kambi za wachimba migodi na malisho ya kondoo ya mbali sana, huku akichukua fasihi zake kwa mfuko alioweka mabegani, alimotia ndani mahitaji yake kama vile blanketi ya kulalia. Hayo yalikuwa maisha ya painia halisi. Na kulikuwa wengine waliokuwa na roho hiyohiyo—wengine wakiwa waseja, wengine wakiwa wamefunga ndoa, vijana kwa wazee.
Wakati wa mwaka 1932, jitihada ya pekee ilifanywa kueneza ujumbe wa Ufalme katika nchi za Amerika ya Latini ambako kazi kidogo sana ya kuhubiri ilikuwa imefanywa. Katika mwaka huo kile kijitabu The Kingdom, the Hope of the World kiligawanywa kwa njia yenye kutokeza sana. Kijitabu hicho kilikuwa na hotuba iliyokuwa tayari imesikiwa katika matangazo ya redio ya kimataifa. Sasa nakala zipatazo 40,000 za hotuba hiyo kwa namna ya chapa ziligawanywa katika Chile, nakala 25,000 katika Bolivia, nakala 25,000 katika Peru, nakala 15,000 katika Ekuado, nakala 20,000 katika Kolombia, nakala 10,000 katika Santo Domingo (sasa ni Jamhuri ya Dominika), na nakala nyingine 10,000 katika Puerto Riko. Kwelikweli, ujumbe wa Ufalme ulikuwa ukipigiwa mbiu, na kwa bidii nyingi.
Kufikia 1935, kulikuwa katika Amerika Kusini yenyewe watu 247 tu waliokuwa wameunga sauti zao katika kupiga mbiu kwamba Ufalme wa Mungu tu ndio utaletea wanadamu furaha ya kudumu. Lakini lo, ni ushahidi mkubwa kama nini waliokuwa wakitoa!
Kufikia Watu Katika Maeneo ya Mbali Hata Zaidi
Mashahidi wa Yehova hawakuwa wakichukua hata kidogo maoni ya kwamba daraka lao mbele za Mungu lilikuwa limetimizwa ikiwa waliongea tu na wachache waliokuwa majirani wao. Walijitahidi kufikia kila mtu kwa habari njema.
Watu walioishi katika sehemu ambazo Mashahidi hawangeweza kusafiri wao binafsi wakati ule wangeweza kufikiwa kwa njia nyinginezo. Hivyo, katika miaka ya mwishomwisho ya 1920, Mashahidi katika Cape Town, Afrika Kusini, walipeleka kwa posta vijitabu 50,000 kwa wakulima, watunzaji wa minara yenye taa, watunza misitu wote, na wengineo walioishi katika sehemu zilizo ngumu kufikia. Kitabu cha anwani cha posta kwa ajili ya sehemu yote ya nchi ya Kusini-Magharibi mwa Afrika (sasa yajulikana kuwa Namibia), chenye habari za karibuni zaidi kilipatikana pia, na nakala ya kile kijitabu The Peoples Friend ilipelekwa kwa posta kwa kila mtu ambaye jina lake lilionekana katika kitabu hicho cha anwani.
Katika 1929, F. J. Franske aliwekwa asimamie mashua ya Watch Tower Society iitwayo Morton na akapewa mgawo, pamoja na Jimmy James, afikie watu katika Labrador na vijiji vyote vya uvuvi vya Newfoundland. Katika majira ya kipupwe mara nyingi Ndugu Franske alisafiri pwani hiyo kwa kutumia kigari kilichokokotwa na kundi la mbwa. Ili kugharimia fasihi za Biblia alizowaachia, Waeskimo na wakazi wa Newfoundland walimpa vitu kama vile bidhaa za ngozi na samaki. Miaka michache baadaye, alijitahidi kuwatembelea wachimba madini, wakataji miti, wategaji wanyama, wafugaji, na Wahindi-Waamerika walioishi katika nchi yenye milimamilima ya Cariboo ya British Columbia. Alipokuwa akisafiri, aliwinda wanyama ili kupata nyama, akachuma beri za mwituni, na kuoka mkate kwa kikaangio juu ya moto wa kambi usiokingwa. Halafu, katika wakati mwingine, yeye na mwenzake walitumia mashua ya kuvua samaki-salmoni ikiwa njia yao ya usafiri walipokuwa wakipeleka ujumbe wa Ufalme kwenye kila kisiwa, ghuba ndogo, kambi za wakataji miti, minara yenye taa, na vijiji vilivyokuwa kandokando ya pwani ya magharibi ya Kanada. Yeye alikuwa mmoja tu wa wengi waliokuwa wakitia jitihada ya pekee kufikia watu walioishi katika sehemu za mbali za dunia.
Kuanzia mwishoni-mwishoni mwa 1920, Frank Day alisafiri kaskazini kupitia vijiji vya Alaska, akihubiri, akiangusha fasihi, na kuuza miwani ili kujitimizia mahitaji yake ya kimwili. Ingawa alikuwa akichechemea kwa mguu bandia, alieneza eneo lililotapakaa kuanzia Ketchikan hadi Nome, umbali wa kilometa kama 1,900. Mapema sana kama 1897, mchimba dhahabu mmoja alikuwa amepata nakala za Millennial Dawn na Watch Tower alipokuwa katika California naye alikuwa akifanya mipango ya kurudi nazo Alaska. Na katika 1910, Captain Beams, wa mashua ya kuwinda nyangumi, alikuwa ameangusha fasihi kwenye bandari za Alaska alipotua. Lakini utendaji wa kuhubiri ulianza kupanuka wakati Ndugu Day alipofunga safari zake za wakati wa kiangazi kuingia katika Alaska tena na tena kwa muda wa miaka zaidi ya 12.
Mashahidi wengine wawili, wakitumia motaboti ya urefu wa meta 12 iliyoitwa Esther, walifanya kazi kuelekea kaskazini mwa pwani ya Norway hadi ndani sana ya Aktiki. Walitoa ushahidi kwenye visiwa, minara yenye taa, katika vijiji vya pwani, na sehemu zilizo peke yazo nyuma sana kwenye milima. Watu wengi waliwakaribisha, na katika muda wa mwaka mmoja, waliweza kuangusha vitabu na vijitabu 10,000 hadi 15,000 vyenye kuelezea kusudi la Mungu kwa wanadamu.
Visiwa Vyasikia Sifa za Yehova
Si visiwa vile tu vilivyokuwa karibu na fuo za bara ambavyo vilipewa ushahidi. Huko mbali katikati ya Bahari Pasifiki, katika miaka ya mapema ya 1930, Sydney Shepherd alitumia miaka miwili akisafiri kwa mashua kuhubiri katika Visiwa vya Cook na Tahiti. Mbali zaidi magharibi, George Winton alikuwa akitembelea New Hebrides (sasa ni Vanuatu) akiwa na habari njema.
Karibu na wakati huohuo, Joseph Dos Santos, Mreno-Mwamerika, alisafiri pia akafikie eneo lisiloguswa. Kwanza alitoa ushahidi katika visiwa vya njenje vya Hawaii; kisha akaanza safari ya kuhubiri ya duniani pote. Hata hivyo, alipofika Filipino, alipokea barua kutoka kwa Ndugu Rutherford ikimwomba akae huko na kujenga na kupanga kitengenezo utendaji wa kuhubiri Ufalme. Alifanya hivyo, kwa miaka 15.
Katika wakati huo, tawi la Sosaiti katika Australia lilikuwa likielekeza fikira kwenye kazi katika Pasifiki Kusini. Mapainia wawili waliotumwa kutoka huko walitoa ushahidi mwingi katika Fiji katika 1930-1931. Samoa ilipokea ushahidi katika 1931. New Caledonia ilifikiwa katika 1932. Wenzi wa ndoa mapainia kutoka Australia hata walichukua utumishi katika China katika 1933 nao walitoa ushahidi katika 13 kati ya majiji yayo makubwa wakati wa miaka michache iliyofuata.
Akina ndugu katika Australia walitambua kwamba mengi zaidi yangeweza kutimizwa ikiwa wangekuwa na mashua ya kutumia. Baada ya wakati waliunda mashua ya urefu wa meta 16 iliyoitwa Lightbearer, na kuanzia mapema katika 1935, wakaitumia kuwa kituo cha utendaji kwa miaka kadhaa kwa ajili ya kikundi cha ndugu wenye bidii walipokuwa wakitoa ushahidi katika Indies Mashariki ya Uholanzi (sasa ni Indonesia), Singapore, na Maleya. Kuwasili kwa mashua hiyo sikuzote kulivuta uangalifu mwingi, na jambo hilo mara nyingi lilifungua njia kwa akina ndugu ya kuhubiri na kuangusha fasihi nyingi.
Wakati huohuo, kwenye ule upande mwingine wa dunia, dada wawili mapainia kutoka Denmark waliamua kufunga safari ya kwenda likizo kwenye Visiwa vya Faeroe katika Bahari ya Atlantiki Kaskazini katika 1935. Lakini walikusudia zaidi ya safari ya kutazama mandhari tu. Walikwenda wakiwa na maelfu ya fasihi mbalimbali, nao waliitumia vizuri. Bila kujali upepo na mvua na uhasama wa makasisi, walieneza sehemu kubwa ya visiwa vilivyokaliwa kadiri walivyoweza wakati wa kukaa kwao.
Mbali zaidi magharibi, Georg Lindal, wa kutoka Iceland-Kanada, alianza mgawo uliochukua muda mrefu zaidi. Kwa dokezo la Ndugu Rutherford, alihamia Iceland katika 1929 ili kupainia. Alionyesha uvumilivu kama nini! Kwa sehemu iliyo kubwa ya miaka 18 iliyofuata, alitumikia humo peke yake. Alitembelea miji na vijiji tena na tena. Fasihi mbalimbali makumi ya maelfu iliangushwa, lakini wakati huo hakuna watu wa Iceland waliojiunga naye katika utumishi wa Yehova. Isipokuwa katika mwaka mmoja tu, hakukuwa na Mashahidi ambao angeweza kushirikiana nao katika Iceland mpaka 1947, wakati wamishonari wawili waliozoezwa Gileadi walipowasili.
Wanadamu Wanapokataza Aliyoamuru Mungu
Walipokuwa wakishiriki katika huduma yao ya hadharani, lilikuwa jambo la kawaida, hasa kuanzia miaka ya 1920 hadi miaka ya 1940, kwa Mashahidi kupata upinzani, kwa kawaida ukichochewa na makasisi wenyeji na nyakati nyingine na maofisa wa serikali.
Katika maeneo ya mashambani kaskazini mwa Vienna, Austria, Mashahidi walijipata wamekabiliwa na umati wa wanavijiji wenye uhasama wakiwa wamechochewa na padri mwenyeji, aliyekuwa anaungwa mkono na polisi. Mapadri walikuwa wameazimia kwamba Mashahidi wa Yehova hawangehubiri katika vijiji vyao. Lakini Mashahidi, wakiwa wameazimia kutimiza mgawo wao waliopewa na Mungu, walichukua njia tofauti na kurudi siku nyingine, wakiingia vijijini kwa vijia vya kandokando.
Bila kujali vitisho na madai ya wanadamu, Mashahidi wa Yehova walijua kwamba walikuwa na wajibu kwa Mungu wa kupiga mbiu ya Ufalme wake. Walichagua kumtii Mungu akiwa mtawala kuliko wanadamu. (Mdo. 5:29) Mahali ambako maofisa wenyeji walijaribu kuwanyima Mashahidi wa Yehova uhuru wa kidini, Mashahidi walileta tu Mashahidi zaidi ili kuongezea nguvu wale waliopo.
Baada ya kukamatwa mara nyingi katika sehemu moja ya Bavaria, katika Ujerumani, katika 1929, walikodi magarimoshi mawili ya pekee—moja lianzie Berlin na jingine Dresden. Yaliunganishwa pamoja katika Reichenbach, na kama saa 8:00 za usiku garimoshi moja liliingia eneo la Regensburg likiwa na abiria 1,200 waliokuwa na hamu ya kushiriki katika kutoa ushahidi. Usafiri ulikuwa ghali, na kila mmoja alikuwa amelipa nauli yake mwenyewe. Kwenye kila kituo cha reli, baadhi yao walishuka. Hesabu fulani yao walikuwa wamekuja na baiskeli ili waweze kufikia sehemu za ndani zaidi za mashambani. Wilaya yote ilienezwa katika siku moja. Walipoona matokeo ya jitihada yao ya umoja, walikumbuka ahadi ya Mungu kwa watumishi wake: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa.”—Isa. 54:17.
Mashahidi katika Ujerumani walikuwa wenye bidii sana hivi kwamba kati ya 1919 na 1933, inakadiriwa kwamba waligawanya angalau vitabu, vijitabu, na magazeti 125,000,000, pamoja na mamilioni ya trakti. Hata hivyo, kulikuwa familia kama 15,000,000 tu katika Ujerumani wakati huo. Wakati wa pindi hiyo Ujerumani ilipata ushahidi kamili kama ule wa nchi nyingine yoyote duniani. Katika sehemu hiyo ya dunia ilipatikana idadi kubwa zaidi ya watu waliodai kuwa wafuasi watiwa-mafuta kwa roho wa Kristo. Lakini wakati wa miaka iliyofuata, walipatwa pia na mitihani ya uaminifu-maadili iliyo migumu zaidi.—Ufu. 14:12.
Katika mwaka 1933, upinzani wa kiserikali kwa kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani uliongezeka sana. Makao ya Mashahidi na ofisi ya tawi ya Sosaiti vilipekuliwa na Gestapo mara nyingi. Utendaji wa Mashahidi ulipigwa marufuku katika mikoa mingi ya Ujerumani, na baadhi yao walikamatwa. Tani nyingi za Biblia zao na fasihi za Biblia zilichomwa hadharani. Katika Aprili 1, 1935, sheria ya kitaifa ilipitishwa kupiga marufuku Ernste Bibelforscher (International Association of Earnest Bible Students, au Mashahidi wa Yehova), na jitihada za utaratibu zilifanywa za kuwanyang’anya riziki yao. Mashahidi kwa upande wao, walifanya mikutano yao katika vikundi vidogovidogo, wakapanga kutokeza tena habari yao ya funzo la Biblia kuwa katika namna ambayo Gestapo hawangeitambua kwa urahisi, na wakaanza kutumia njia za kuhubiri zisizotambuliwa kwa urahisi.
Hata kabla ya hilo, tangu 1925, akina ndugu katika Italia walikuwa wamekuwa wakiishi chini ya udikteta wa Kifashisti, na katika 1929 mwafaka ulikuwa umetiwa sahihi kati ya Kanisa Katoliki na Serikali ya Kifashisti. Wakristo wa kweli waliwindwa bila huruma. Baadhi yao walikutana katika mazizi na vibanda vya chakula cha mifugo ili kuepuka kukamatwa. Katika wakati huo Mashahidi wa Yehova katika Italia walikuwa wachache sana katika hesabu; hata hivyo, jitihada zao za kueneza ujumbe wa Ufalme ziliongezewa nguvu katika 1932 wakati Mashahidi 20 kutoka Uswisi walipovuka mpaka na kuingia Italia, na kugawanya kwa haraka sana nakala 300,000 za kijitabu The Kingdom, the Hope of the World.
Katika Mashariki ya Mbali pia, mkazo ulikuwa ukiongezeka. Mashahidi wa Yehova walikuwa wakikamatwa katika Japani. Kiasi kikubwa cha fasihi zao za Biblia kiliharibiwa na maofisa katika Seoul (katika ile ambayo sasa ni Jamhuri ya Korea) na Pyongyang (katika ile ambayo sasa ni Jamhuri ya Kidemokrasi ya Watu wa Korea).
Katikati ya mkazo huo uliokuwa ukiongezeka, katika 1935, Mashahidi wa Yehova walipata uelewevu ulio wazi kutoka katika Biblia wa utambulisho wa ile “halaiki kubwa,” au “umati mkubwa,” wa Ufunuo 7:9-17. (KJ, NW) Uelewevu huo uliwawezesha kupata kujua juu ya kazi ya haraka na isiyotazamiwa. (Isa. 55:5) Hawakuwa tena na maoni ya kwamba wote ambao si wa “kundi dogo” la warithi wa Ufalme wa kimbingu wangepata fursa wakati fulani ujao ya kupatanisha maisha zao na matakwa ya Yehova. (Luka 12:32) Walitambua kwamba wakati ulikuwa umefika wa kufanya wanafunzi wa watu hao sasa ili wapate kuokolewa kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu. Hawakujua kukusanywa kwa huo umati mkubwa kutoka mataifa yote kungeendelea kwa muda mrefu kadiri gani, ingawa walihisi kwamba mwisho wa mfumo mwovu wa mambo lazima uwe ulikuwa karibu sana. Hawakuwa na hakika kazi hiyo ingetimizwaje kwa sababu ya kuelekeana na mnyanyaso uliokuwa ukienea na kuzidi kuwa wenye ukatili. Hata hivyo, walikuwa na uhakika kwamba—kwa kuwa ‘mkono wa Yehova si mfupi mno,’ yeye angewafungulia njia ili watimize mapenzi yake.—Isa. 59:1.
Katika mwaka 1935, Mashahidi wa Yehova walikuwa kidogo wachache—56,153 tu ulimwenguni pote.
Walikuwa wakihubiri katika nchi 115 wakati wa mwaka huo; lakini katika karibu nusu ya nchi hizo, kulikuwa Mashahidi wanaopungua kumi. Ni nchi mbili tu zilizokuwa na Mashahidi wa Yehova watendaji 10,000 au zaidi (Marekani, ikiwa na 23,808; Ujerumani, ikiwa na waliokadiriwa kuwa 10,000 kati ya wale 19,268 waliokuwa wameweza kuripoti miaka miwili mapema). Nchi nyingine saba (Australia, Chekoslovakia, Kanada, Poland, Rumania, Ufaransa, na Uingereza) kila moja iliripoti Mashahidi zaidi ya 1,000 lakini wasiozidi 6,000. Rekodi ya utendaji katika nchi nyinginezo 21 huonyesha Mashahidi kati ya 100 na 1,000 kila moja. Hata hivyo, wakati wa mwaka huo mmoja, kikosi hicho cha Mashahidi wenye bidii kilitumia saa 8,161,424 ulimwenguni pote kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee kwa wanadamu.
Kuongezea zile nchi ambazo katika hizo walikuwa wakihubiri kwa bidii wakati wa 1935, tayari walikuwa wameeneza habari njema kwenye sehemu nyinginezo, hivi kwamba nchi 149 na vikundi vya visiwa vilikuwa vimefikiwa na ujumbe wa Ufalme kufikia wakati huo.
[Blabu katika ukurasa wa 424]
Ingawa walifungwa gerezani, walipata fursa za kuhubiri
[Blabu katika ukurasa wa 425]
Wenye nia na hamu ya kuendelea na kazi!
[Blabu katika ukurasa wa 441]
Hawakujali upepo, mvua, na uhasama wa makasisi
[Blabu katika ukurasa wa 442]
Ushahidi mwingi ajabu ulitolewa katika Ujerumani kabla ya “Ernste Bibelforscher” kupigwa marufuku humo
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 423]
Ulimwengu ulipokuwa ukijizamisha katika vita, R. R. Hollister na Fanny Mackenzie walikuwa wakipeleka ujumbe wa amani kwa watu wa China, Japani, na Korea
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
KOREA
JAPANI
CHINA
BAHARI YA PASIFIKI
[Ramani katika ukurasa wa 428]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Wakati wahamaji kutoka nchi zilizotajwa katika ramani hii walipojifunza juu ya kusudi la ajabu la Mungu la kubariki wanadamu, walihisi wakilazimika kurudi wapeleke habari hiyo katika nchi za kwao
MABARA YA AMERIKA
↓ ↓
AUSTRIA
BULGARIA
SAIPRASI
CHEKO-SLOVAKIA
DENMARK
FINLAND
UJERUMANI
UGIRIKI
HUNGARIA
ITALIA
UHOLANZI
NORWAY
POLAND
URENO
RUMANIA
HISPANIA
SWEDEN
USWISI
UTURUKI
YUGOSLAVIA
[Ramani katika ukurasa wa 432]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Wakati wa miaka ya 1920 na ya 1930, waeneza-evanjeli walitoka Ujerumani wakaenda nchi nyingi ili kutoa ushahidi
UJERUMANI
↓ ↓
AMERIKA KUSINI
AFRIKA KASKAZINI
ASIA
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 435]
Mapainia wenye bidii kama vile Frank Smith na ndugu yake Gray (anayeonyeshwa katika picha iliyo upande wa juu) walieneza habari njema katika pwani ya mashariki ya Afrika
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
UGANDA
KENYA
TANZANIA
AFRIKA KUSINI
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 439]
Kotekote katika Kusini-Magharibi mwa Afrika (sasa ni Namibia) watu walipokea kijitabu hiki kwa posta katika 1928
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
NAMIBIA
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 440]
Wakiwa ndani ya “Lightbearer,” mapainia wenye bidii walieneza ujumbe wa Ufalme katika Kusini-Mashariki mwa Asia
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
MALEYA
BORNEO
CELEBES
SUMATRA
JAVA
TIMOR
NEW GUINEA
AUSTRALIA
BAHARI YA PASIFIKI
[Picha katika ukurasa wa 426]
Katika nchi nyingi mhadhara “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe” ulivutia idadi kubwa ya wasikilizaji
[Picha katika ukurasa wa 427]
Edwin Scott, katika Afrika Kusini, aligawanya yeye binafsi nakala 50,000 za “Mwito kwa Viongozi wa Ulimwengu”
[Picha katika ukurasa wa 429]
Akiitikia wito wa waeneza-evanjeli, Willy Unglaube alitumikia katika Ulaya, Afrika, na nchi za Mashariki
[Picha katika ukurasa wa 430]
Kufikia 1992, Eric Cooke na ndugu yake John (aketiye) kila mmoja alikuwa amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 60, wakifurahia mambo yaliyoonwa yenye kusisimua katika Ulaya na Afrika
[Picha katika ukurasa wa 431]
Alipokwenda India katika 1926, Edwin Skinner alikuwa na mgawo uliotia ndani nchi tano; aliendelea kuhubiri huko kwa uaminifu kwa miaka 64
[Picha katika ukurasa wa 433]
Alfred na Frieda Tuček, wakiwa wamejitayarisha kwa mahitaji ya maisha na fasihi ili kutoa ushahidi, walitumikia wakiwa mapainia katika Yugoslavia ya Kale
[Picha katika ukurasa wa 434]
Kotekote katika Afrika Magharibi, “Bible Brown” alishiriki kwa juhudi katika kufunua ibada bandia
[Picha katika ukurasa wa 436]
George Young alishiriki kueneza sana upigaji mbiu ya Ufalme wa Mungu katika Amerika Kusini, Hispania, na Ureno
[Picha katika ukurasa wa 437]
Juan Muñiz (kushoto), aliyekuwa amekuwa akihubiri katika Amerika Kusini tangu 1924, alikuwapo kumkaribisha N. H. Knorr wakati alipotembelea Argentina kwa mara ya kwanza miaka 20 baadaye
[Picha katika ukurasa wa 438]
Nicolás Argyrós alieneza kweli ya Biblia yenye kuleta uhuru katika mikoa 14 ya Argentina
[Picha katika ukurasa wa 439]
F. J. Franske, akisafiri kupitia nchi kavu na kwa mashua, alijitahidi kufikia vijiji vya mbali kuvipelekea kweli ya Biblia
-