Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Utumishi wa Shambani na Tengenezo Yawa Masuala

      Kuanzia toleo lalo la kwanza, na kwa mkazo wenye kuongezeka baada ya hapo, Zion’s Watch Tower lilihimiza kila Mkristo wa kweli ashiriki kweli na wengine. Baada ya hapo, wasomaji wa Watch Tower walitiwa moyo mara kwa mara kuthamini pendeleo na daraka lao la kupiga mbiu ya habari njema kwa wengine. Wengi walishiriki katika njia ndogo, lakini wachache kwa kadiri fulani walikuwa katika mstari wa mbele katika kazi, wakihubiri nyumba hadi nyumba ili kumpa kila mtu fursa ya kusikia ujumbe wa Ufalme.

      Hata hivyo, kuanzia mwaka 1919, ushiriki katika utumishi wa shambani ulikaziwa kwa nguvu zaidi. Ndugu Rutherford alikazia jambo hilo kwa dhati katika hotuba jijini Cedar Point, Ohio, mwaka huo. Katika kila kutaniko lililoomba Sosaiti kulipanga kitengenezo kwa ajili ya utumishi, mipango ilifanywa ili mwelekezi wa utumishi, aliyeteuliwa na Sosaiti, ashughulikie kazi hiyo. Alipaswa achukue uongozi yeye mwenyewe na kuona kwamba kutaniko lilikuwa na ugavi uliohitajiwa.

      Katika 1922, The Watch Tower lilitangaza makala yenye kichwa “Utumishi Ni wa Lazima.” Ilielekeza kwenye uhitaji mkubwa wa watu kusikia habari njema za Ufalme, ikaelekeza fikira kwenye amri ya kiunabii ya Yesu kwenye Mathayo 24:14, na kuwaambia wazee makutanikoni: “Mtu yeyote asifikiri kwamba kwa sababu yeye ni mzee darasani utumishi wake wapaswa uwe wa kuhubiri tu kwa mdomo. Ikiwa fursa zamruhusu kwenda miongoni mwa watu na kuwakabidhi ujumbe uliochapwa, hilo ni pendeleo kubwa na ni kuhubiri gospeli, mara nyingi kwa matokeo zaidi ya njia nyingineyo ya kuihubiri.” Kisha makala hiyo ikauliza: “Je, yeyote ambaye amejitakasa ka­bi­sa­kabisa kwa Bwana aweza kujitetea mwenyewe kwa kuwa mzembe wakati huu?”

      Wengine walijizuia. Walizusha visababu vya aina zote. Hawakufikiri kuwa yafaa “kuuza vitabu,” ingawa kazi hiyo haikuwa inafanywa ili kufaidika kifedha na ingawa ni kupitia vichapo hivyohivyo kwamba walikuwa wamejifunza kweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Wakati kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba kwa kutumia vitabu siku ya Jumapili kulipotiwa moyo, kuanzia mwaka 1926, wengine walipinga hilo, ingawa Jumapili ilikuwa siku ambayo watu wengi waliweka kando kidesturi kwa ajili ya ibada. Tatizo la msingi ni kwamba walijiona wenyewe kuwa wa maana zaidi kuweza kuhubiri nyumba hadi nyumba. Na bado, Biblia husema wazi kwamba Yesu alituma wanafunzi wake kwenye nyumba za watu ili kuhubiri, na mtume Paulo alihubiri ‘hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.’—Mdo. 20:20; Mt. 10:5-14, NW.

      Mkazo juu ya utumishi wa shambani uliongezeka, na wale ambao mioyo yao haikuwasukuma kumwiga Yesu na mitume wake wakiwa mashahidi waliacha tengenezo hatua kwa hatua. Kutaniko la Skive katika Denmark, pamoja na wengine, lilipungua kufikia nusu hivi. Kati ya watu mia hivi walioshirikiana na Kutaniko la Dublin katika Ireland, ni wanne tu waliobaki. Kulikuwa na kutahiniwa na kupepetwa kwa aina hiyohiyo katika Marekani, Kanada, Norway, na nchi nyinginezo. Hilo lilitakasa makutaniko.

      Wale ambao kwa kweli walitaka kumwiga Mwana wa Mungu waliitikia ifaavyo kitia-moyo kutoka kwa Maandiko. Hata hivyo, utayari wao haukufanya iwe rahisi kwao kuanza kwenda nyumba hadi nyumba. Wengine walikuwa na wakati mgumu kuanza. Lakini mipango ya kutoa ushahidi wa kikundi na makusanyiko ya utumishi wa pekee yalikuwa kitia-moyo. Dada wawili kutoka Jut­land kaskazini, katika Denmark, walikumbuka kwa muda mrefu siku yao ya kwanza ya utumishi wa shambani. Walikutana na kikundi, wakasikia maagizo, wakaanza kwenda kwenye eneo lao, lakini kisha wakaanza kulia. Ndugu wawili waliona yale yaliyokuwa yakitukia na wakawaalika dada wafanye kazi pamoja nao. Upesi wakaanza kuchangamka tena. Baada ya kuonja utumishi wa shambani, wengi walijawa na shangwe na walikuwa na msisimko wa kufanya zaidi.

      Kisha, katika 1932, The Watch Tower likawa na makala yenye sehemu mbili yenye kichwa “Tengenezo la Yehova.” (Matoleo ya Agosti 15 na Septemba 1) Hiyo ilionyesha kwamba uchaguzi wa uzee katika makutaniko haukuwa wa kimaandiko. Makutaniko yalihimizwa kutumia katika vyeo vya madaraka wanaume wale tu waliokuwa watendaji katika utumishi wa shambani, wanaume walioishi kulingana na madaraka yaliyomaanishwa na jina Mashahidi wa Yehova. Hao wangefanya kazi wakiwa halmashauri ya utumishi. Mmoja wao, akiteuliwa na kutaniko, angewekwa rasmi na Sosaiti kuwa mwelekezi wa utumishi. Katika Belfast, Ireland, hilo lilipepeta nje wengine zaidi ambao tamaa yao ilikuwa ni umashuhuri wa kibinafsi badala ya utumishi wa unyenyekevu.

      Kufikia miaka ya mapema ya 1930, wengi wa wale waliokuwa Ujerumani waliokuwa wakijaribu kupinga utumishi wa shambani walikuwa wameacha kushirikiana na makutaniko. Wengine wao waliacha kwa woga kazi ilipopigwa marufuku katika 1933 katika majimbo mengi ya Ujerumani. Lakini maelfu walivumilia kutahiniwa huko kwa imani na wakawa na hiari ya kuhubiri kujapokuwa na hatari zilizohusika.

      Kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme iliongeza mwendo duniani pote. Utumishi wa shambani ukawa sehemu ya maana ya maisha ya Mashahidi wa Yehova wote. Kwa kielelezo, kutaniko katika Oslo, Norway, lilikodisha mabasi kwenye miisho-juma ili kusafirisha wahubiri hadi majiji ya karibu. Walikutana mapema asubuhi, wakawa katika eneo lao kufikia saa tatu au nne, wakafanya kazi kwa bidii katika utumishi wa shambani kwa muda wa saa saba au nane, na kisha wakajiunga na kikundi cha basi kwa ajili ya safari ya kurudi nyumbani. Wengine walisafiri kwenye maeneo ya mashambani kwa baiskeli, mikoba ya vitabu na katoni zikiwa zimepakiwa ugavi wa ziada. Mashahidi wa Yehova walikuwa wenye furaha, bidii, na umoja katika kufanya mapenzi ya Mungu.

      Katika 1938, wakati fikira zilipoelekezwa tena kwenye kuwekwa rasmi kwa wanaume wenye madaraka makutanikoni,j kuondolewa kwa uchaguzi wote wa watumishi wa mahali kulikaribishwa kwa ujumla. Makutaniko yalipitisha maazimio kwa furaha yakionyesha uthamini kwa tengenezo la kitheokrasi na kuomba “Sosaiti” (waliyoelewa kuwa yamaanisha mabaki watiwa-mafuta, au mtumwa mwaminifu na mwenye busara) kupanga kutaniko kitengenezo kwa ajili ya utumishi na kuweka watumishi wote. Baadaye, Baraza Linaloongoza linaloonekana liliweka rasmi wale waliohitajiwa na kupanga makutaniko kitheokrasi kwa ajili ya utendaji wenye umoja na matokeo. Ni vikundi vichache tu vilivyojizuia na kuacha tengenezo wakati huo.

  • Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Picha katika ukurasa wa 639]

      Mkazo ulipoongezwa juu ya utumishi wa shambani, wengi waliacha kushiriki; wengine walionyesha bidii zaidi

      “Watch Tower,” Aprili 1, 1928

      “Watch Tower,” Juni 15, 1927

      “Watch Tower,” Agosti 15, 1922

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki