-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Kielelezo Kifaacho kwa Kundi
Ndugu Rutherford alijua kwamba ili kazi iendelee kusonga mbele kwa njia ya utaratibu na ya umoja, hata wakati uwe mfupi kadiri gani, kielelezo kifaacho kwa kundi ni cha muhimu. Yesu alikuwa amewaeleza wafuasi wake kuwa kama kondoo, na kondoo hufuata mchungaji wao. Bila shaka, Yesu mwenyewe ndiye Mchungaji Mwema, lakini yeye hutumia pia wanaume wazee, au wazee, wakiwa wachungaji wadogo wa watu wake. (1 Pet. 5:1-3) Wazee hao lazima wawe wanaume ambao wao wenyewe hushiriki katika kazi ambayo Yesu aliwagawia na ambao huwatia wengine moyo wafanye hivyo. Ni lazima wawe kikweli na roho ya kueneza evanjeli. Hata hivyo, wakati wa ugawanyaji wa The Finished Mystery, baadhi ya wazee walikuwa wamekataa; wengine hata walisema waziwazi sana wakiwavunja wengine moyo wasishiriki.
Hatua ya maana sana kuelekea kusahihishwa kwa hali hiyo ilichukuliwa katika 1919 gazeti The Golden Age lilipoanza kutangazwa. Hilo lingekuwa kifaa chenye nguvu cha kutangaza Ufalme wa Mungu kuwa utatuzi pekee wenye kudumu kwa matatizo ya wanadamu. Kila kutaniko ambalo lilitaka kushiriki katika utendaji huo lilialikwa liombe kwamba lisajiliwe na Sosaiti kuwa “tengenezo la utumishi.” Halafu mwelekezi, au mwelekezi wa utumishi kama alivyokuja kujulikana, ambaye hakulazimika kuchaguliwa kila mwaka, aliwekwa na Sosaiti.f Akiwa ndiye mwakilishi wa Sosaiti mwenyeji, alipaswa kupanga kazi, kutoa migawo ya eneo, na kutia kutaniko moyo lishiriki katika utumishi wa shambani. Hivyo, sambamba na wazee na mashemasi waliochaguliwa kidemokrasi, mpango wa kitengenezo wa aina nyingine ulianza kufanya kazi, ambao ulitambua mamlaka yenye kuweka rasmi yaliyo nje ya kutaniko la mahali na ambao ulitia mkazo mwingi zaidi katika kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu.g
-
-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Miongoni mwa Mashahidi hao wenye bidii, walikuwamo watumishi wa Yehova wengi wanyenyekevu na waliojitoa, ambao walikuwa wazee katika makutaniko. Hata hivyo, katika sehemu nyingine, wakati wa miaka ya 1920 na mapema katika miaka ya 1930, kulikuwako pia ukinzani mwingi kwa wazo la kila mtu kushiriki katika utumishi wa shambani. Wazee waliochaguliwa kidemokrasi mara nyingi walisema waziwazi wakipinga yale ambayo The Watch Tower lilisema juu ya daraka la kuhubiria watu walio nje ya kutaniko. Kukataa kusikiliza yale ambayo roho ya Mungu ilihitaji kuliambia kutaniko juu ya jambo hilo kwa njia ya Maandiko Matakatifu, kulizuia umiminikaji wa roho ya Mungu katika vikundi hivyo.—Ufu. 2:5, 7.
Hatua zilichukuliwa katika 1932 kusahihisha hali hiyo. Jambo la kuhangaikiwa zaidi halikuwa kama baadhi ya wazee mashuhuri wangeudhiwa au kama baadhi ya wale walioshirikiana na makutaniko wangeondoka. Bali, tamaa ya akina ndugu ilikuwa kumpendeza Yehova na kufanya mapenzi yake. Kwa kusudi hilo, matoleo ya Agosti 15 na Septemba 1 ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) mwaka huo yalizungumzia habari “Tengenezo la Yehova.”
-