-
Mikutano Kwa Ajili ya Ibada, Funzo, na Kitia-moyoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Kutimiza Mahitaji ya Kiroho ya Wanafunzi wa Biblia wa Mapema
Charles Taze Russell na kikundi kidogo cha washirika katika Allegheny, Pennsylvania, walifanyiza darasa kwa ajili ya funzo la Biblia katika 1870. Likiwa tokeo la mikutano yao, walikua hatua kwa hatua katika kumpenda Mungu na Neno lake na kwa kuendelea wakaja kujua yale ambayo Biblia yenyewe hufundisha. Hakukuwa na kusema kimuujiza katika ndimi kwenye mikutano hiyo. Kwa nini? Karama hizo za kimuujiza zilikuwa zimetimiza lengo lazo katika karne ya kwanza, na kama vile Biblia ilivyotabiri, zilikuwa zimekoma. “Hatua iliyofuata ya maendeleo,” Ndugu Russell akaeleza, “ilikuwa udhihirisho wa matunda ya Roho, kama vile Mta. Paulo aonyeshavyo wazi sana.” (1 Kor. 13:4-10) Zaidi ya hilo, kama vile katika karne ya kwanza pia, kulikuwa na kazi muhimu ya kufanya ya kueneza evanjeli, na kwa ajili ya hiyo walihitaji kitia-moyo. (Ebr. 10:24, 25) Kabla ya muda mrefu, wakawa wakifanya mikutano miwili ya ukawaida kila juma.
Ndugu Russell aling’amua kwamba lilikuwa jambo la maana kwa watumishi wa Yehova kuwa watu walioungamanika, si kitu wawe wametawanyika wapi duniani pote. Hivyo, katika 1879, muda mfupi baada ya Watch Tower kuanza kutangazwa, wasomaji walo walialikwa waombe Ndugu Russell au mmoja wa washirika wake awazuru. Takwa lililotaarifiwa wazi lilikuwa “Hakuna kutozwa wala fedha kuchukuliwa.” Baada ya maombi kadhaa kupokewa, Ndugu Russell akaanza safari ya mwezi mzima iliyompeleka mbali sana kufika Lynn, Massachusetts, akifanya mikutano kwa saa nne kufika sita kila siku katika kila kituo. Habari iliyotolewa ilikuwa “Mambo Yahusuyo Ufalme wa Mungu.”
Mapema katika 1881, Ndugu Russell aliwahimiza wasomaji wa Watch Tower ambao walikuwa hawafanyi mikutano kwa ukawaida katika eneo lao: “Anzisha mmoja katika makao yako mwenyewe pamoja na familia yako mwenyewe, au hata wachache ambao huenda wakapendezwa. Someni, jifunzeni, toeni sifa na kuabudu pamoja, na wakutanapo wawili au watatu katika jina Lake, Bwana atakuwa kati yenu—mwalimu wenu. Hiyo ndiyo iliyokuwa hali ya baadhi ya mikutano ya kanisa katika siku za Mitume. (Ona Filemoni, 2).”
Programu ya mikutano ilisitawi hatua kwa hatua. Madokezo yalitolewa, lakini kila kikundi cha mahali kiliachwa kiamue lililofaa zaidi hali zao. Msemaji angetoa hotuba pindi kwa pindi, lakini mkazo zaidi ulitolewa kwa mikutano ambamo kila mtu angeweza kujisikia huru kushiriki. Baadhi ya madarasa ya Wanafunzi wa Biblia mwanzoni hayakutumia sana vichapo vya Sosaiti kwenye mikutano yao, lakini wahudumu wasafirio, wale mapilgrimu, waliwasaidia waone thamani ya kufanya hivyo.
Baada ya baadhi ya yale mabuku ya Millenial Dawn kutangazwa, hayo yakaanza kutumiwa kuwa msingi wa funzo. Katika 1895 vikundi vya funzo vikaja kujulikana kuwa Vikundi vya Mapambazuko kwa Ajili ya Funzo la Biblia.a Wengine katika Norway baadaye walivirejezea kuwa “mikutano ya kusoma na kuzungumza,” wakiongeza: “Vifungu kutoka vitabu vya Ndugu Russell vilisomwa kwa sauti, na watu walipokuwa na maelezo au maswali, waliinua mikono yao.” Ndugu Russell alipendekeza kwamba kwenye mafunzo hayo washiriki watumie tafsiri tofauti-tofauti za Maandiko, marejezo ya pambizoni katika Biblia, na konkodansi za Biblia. Mara nyingi mafunzo yalifanywa pamoja na vikundi vyenye ukubwa wa kiasi, katika makao ya watu binafsi, katika jioni iliyokifaa kikundi. Mikutano hiyo ilikuwa tangulizi za Funzo la Kitabu la Kutaniko la siku hizi.
Ndugu Russell aling’amua kwamba mengi yalihitajiwa zaidi ya kujifunza mambo ya kimafundisho tu. Lazima kuwe pia na wonyesho wa ujitoaji ili mioyo ya watu isukumwe na uthamini wa upendo wa Mungu na tamaa ya kumheshimu na kumtumikia. Madarasa yalihimizwa yapange mkutano wa pekee kwa kusudi hilo mara moja kila juma. Ilirejezewa nyakati nyingine kuwa “Mikutano ya Nyumbani” kwa sababu ilifanywa katika makao ya watu binafsi. Programu ilitia ndani sala, nyimbo za sifa, na shuhuda zilizosimuliwa na wale waliohudhuria.b Shuhuda hizo zilikuwa nyakati nyingine mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo; majaribu, magumu, na matatizo yaliyokabiliwa wakati wa siku za karibuni yalitiwa ndani pia. Katika sehemu fulanifulani mikutano hiyo ilipungukiwa sana katika lengo layo kwa sababu ya kukazia kupita kiasi mambo ya kibinafsi. Madokezo yenye fadhili ya kufanyia maendeleo yalionyeshwa katika The Watch Tower.
Akikumbuka mikutano hiyo, Edith Brenisen, mke wa mmojawapo mapilgrimu wa mapema katika Marekani, alisema hivi: “Ilikuwa jioni ya kutafakari juu ya utunzaji wenye upendo wa Yehova na ya ushirika wa karibu pamoja na ndugu na dada zetu. Tulipokuwa tukisikiliza baadhi ya mambo waliyoona tulizidi kuwajua vema zaidi. Kutazama uaminifu wao, kuona jinsi walivyoshinda magumu yao, mara nyingi kulitusaidia kutatua baadhi ya matatizo yetu wenyewe.” Hata hivyo, baada ya wakati ikawa wazi kwamba mikutano iliyokusudiwa kutayarisha kila mmoja kushiriki katika kazi ya kueneza evanjeli ilikuwa yenye kunufaisha zaidi.
Njia ambayo mikutano ya Jumapili iliendeshwa katika sehemu fulani ilihangaisha akina ndugu. Madarasa fulani yalijaribu kuzungumza Biblia mstari kwa mstari. Lakini nyakati nyingine tofauti za maoni kuhusu maana hazikuwa zenye kujenga hata kidogo. Ili kuleta maendeleo katika hali hiyo, watu fulani katika kutaniko la Los Angeles, California, walitayarisha mihtasari yenye kichwa cha habari kwa ajili ya funzo la Biblia. Mihtasari hiyo ilikuwa na maswali na marejezo ya kuchunguzwa na darasa zima kabla ya kuja kwenye mkutano. Katika 1902 Sosaiti ilitoa Biblia iliyokuwa na “Misaada ya Funzo la Biblia la Kiberoya,” kutia na fahirisi ya vichwa vya habari.c Ili kusahilisha mambo zaidi, kuanzia na Watch Tower la Machi 1, 1905, mihtasari kwa ajili ya mazungumzo ya kutaniko ilitangazwa, ikiwa na maswali pamoja na marejezo kwenye Biblia na vichapo vya Sosaiti kwa ajili ya utafiti. Mihtasari hiyo iliendelea mpaka 1914, kufikia wakati ambapo maswali ya funzo katika mabuku ya Studies in the Scriptures yalitangazwa ili kutumiwa yakiwa msingi kwa ajili ya Mafunzo ya Kiberoya.
Habari ileile ilipatikana kwa madarasa yote, lakini hesabu ya mikutano ya kila juma ilitofautiana kuanzia mmoja kufika minne au zaidi, kulingana na mipango ya mahali. Katika Colombo, Ceylon (sasa ni Sri Lanka), kuanzia 1914, mikutano ilikuwa kwa kweli ikifanywa siku saba kila juma.
Wanafunzi wa Biblia walitiwa moyo wajifunze kufanya utafiti, ili “kuthibitisha mambo yote,” na kueleza mawazo kwa maneno yao wenyewe. (1 The. 5:21, KJ) Ndugu Russell alitia moyo ushiriki kamili na wa hiari wa mazungumzo ya habari ya funzo. Pia alitahadharisha hivi: “Msisahau kamwe kwamba Biblia ndiyo Kiwango chetu na kwamba hata misaada yetu iwe yenye kubarikiwa na Mungu kadiri gani hiyo ni ‘misaada’ na haiwi badala ya Biblia.”
-
-
Mikutano Kwa Ajili ya Ibada, Funzo, na Kitia-moyoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
a Baadaye mikutano hiyo iliitwa Vikundi vya Kiberoya kwa Ajili ya Funzo la Biblia, katika kuiga Waberoya wa karne ya kwanza waliosifiwa kwa ‘kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu.’—Mdo. 17:11, NW.
b Kwa sababu ya yale yaliyoandikwa, mikutano hiyo iliitwa pia Mikutano ya Sala, Sifa na Ushuhuda. Kwa sababu ya umaana wa sala, baada ya wakati ilipendekezwa kwamba mara moja kila miezi mitatu mkutano uwe ibada ya sala tu, kutia na nyimbo lakini bila yaliyoonwa.
c Katika 1907 misaada ya funzo la Kiberoya ilisahihishwa, ikaongezwa sana, na kufanywa kuwa ya karibuni zaidi. Kurasa zaidi zipatazo 300 za habari yenye kusaidia ziliongezwa katika chapa ya 1908.
-