Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Daima Kaza Uangalifu kwa Kufundisha Kwako
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Machi 15
    • Upendo na Staha kwa Wale Wanaofundishwa

      12. Mtazamo wa Yesu kuelekea wanafunzi wake ulikuwa nini?

      12 Sifa nyingine muhimu ni mtazamo unaofaa kuelekea wale unaofundisha. Mafarisayo waliwadharau wale waliomsikiliza Yesu. “Umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa,” wakasema. (Yohana 7:49) Lakini Yesu alikuwa na upendo wenye kina kirefu na pia staha kwa wanafunzi wake. Yeye alisema: “Siwaiti nyinyi tena watumwa, kwa sababu mtumwa hayajui yale afanyayo bwana-mkubwa wake. Lakini nimewaita nyinyi marafiki, kwa sababu mambo yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu nimewajulisha nyinyi.” (Yohana 15:15) Hilo lilionyesha namna ambavyo wanafunzi wa Yesu wanapaswa kuendesha utendaji wao wa kufundisha.

      13. Paulo alihisije juu ya wale aliofundisha?

      13 Kwa mfano, Paulo hakudumisha uhusiano usio wa kirafiki, ulio kama wa kikazi, baina yake na wanafunzi wake. Aliwaambia Wakorintho hivi: “Ingawa huenda mkawa mna wafunzi elfu kumi katika Kristo, hakika si baba wengi mlio nao; kwa maana katika Kristo Yesu mimi nimekuwa baba yenu kupitia habari njema.” (1 Wakorintho 4:15) Nyakati nyingine, Paulo alitoa machozi huku akiwaonya kwa upole wale aliofundisha! (Matendo 20:31) Alionyesha pia saburi na fadhili isiyo ya kawaida. Kwa hiyo angeweza kuwaambia Wathesalonike hivi: “Tulipata kuwa waanana katikati yenu, kama wakati mama mwenye kunyonyesha atunzavyo sana watoto wake mwenyewe.”—1 Wathesalonike 2:7.

      14. Kwa nini ni jambo muhimu sana kupendezwa kibinafsi na wanafunzi wetu? Toa kielezi.

      14 Je, wewe unawaiga Yesu na Paulo? Upendo wa kweli kwa wanafunzi wetu unaweza kujazia upungufu wowote katika uwezo mbalimbali wa kiasili ambao huenda tukawa nao. Je, wanafunzi wetu wa Biblia wanahisi kwamba kweli tunapendezwa nao kibinafsi? Je, tunatumia wakati ili tupate kuwajua? Mwanamke mmoja Mkristo alipokuwa na tatizo la kumsaidia mwanafunzi afanye maendeleo ya kiroho, aliuliza kwa fadhili hivi: “Je, kuna jambo fulani linalokuhangaisha?” Huyo mwanamke akaanza kufunua yaliyokuwa moyoni mwake, akasimulia mahangaiko yake mengi sana. Mazungumzo hayo yenye upendo yakawa mwanzo wa mabadiliko makubwa kwa huyo mwanamke. Katika visa kama hivyo, mawazo na maneno ya Kimaandiko yenye kufariji na kutia moyo yafaa. (Waroma 15:4) Ingawa hivyo, kuna neno la tahadhari: Huenda mwanafunzi wa Biblia anafanya maendeleo ya haraka lakini huenda bado anahitaji kushinda mazoea fulani yasiyo ya Kikristo. Kwa hiyo huenda lisiwe jambo la hekima kuwa na uhusiano wa karibu sana na mtu huyo. Mipaka ya Kikristo inayofaa yapasa kudumishwa.—1 Wakorintho 15:33.

      15. Twaweza kuonyeshaje staha kwa wanafunzi wetu wa Biblia?

      15 Staha kwa wanafunzi wetu yahusisha kuepuka kujaribu kudhibiti maisha yao ya kibinafsi. (1 Wathesalonike 4:11) Kwa mfano, twaweza kuwa tunajifunza na mwanamke ambaye anaishi na mwanamume ambaye hajafunga ndoa naye. Labda wamezaa watoto pamoja. Mwanamke huyo ataka kurekebisha mambo ili ajipatanishe na viwango vya Yehova kwa kuwa amepata ujuzi sahihi juu ya Mungu. (Waebrania 13:4) Je, apaswa kuolewa na mwanamume huyo au kutengana naye? Labda twahisi kwa dhati kwamba kuolewa na mwanamume ambaye hapendezwi sana na mambo ya kiroho kungezuia maendeleo yake ya baadaye. Kwa upande mwingine, huenda tukahofia hali njema ya watoto wake na kufikiria kwamba ingekuwa afadhali aolewe na huyo mwanamume. Kwa vyovyote vile, itakuwa kukosa kuonyesha staha na upendo kuingilia maisha ya mwanafunzi na kujaribu kumlazimisha akubali maoni yetu katika mambo kama hayo. Kwani, ni huyo mwanamke ambaye ni lazima aishi na matokeo ya uamuzi wake. Basi, je, haingekuwa bora kumzoeza mwanafunzi wa aina hiyo kutumia ‘nguvu zake mwenyewe za ufahamu’ na kujiamulia yale anayopaswa kufanya?—Waebrania 5:14.

  • Daima Kaza Uangalifu kwa Kufundisha Kwako
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Machi 15
    • Kuitikia Mahitaji Yao

      18, 19. (a) Twapaswa kuitikiaje mahitaji ya wanafunzi wa Biblia walio na upungufu mbalimbali? (b) Huenda tukawasaidiaje wanafunzi walio na tatizo la mambo hususa?

      18 Mwalimu mwenye matokeo huwa tayari kubadilikana ili afae uwezo na upungufu mbalimbali wa wanafunzi wake. (Linganisha Yohana 16:12.) Katika kielezi cha Yesu kuhusu talanta, bwana-mkubwa alimpa mapendeleo “kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe.” (Mathayo 25:15) Twaweza kufuata kiolezo kama hicho tunapoongoza mafunzo ya Biblia. Kwa kawaida, ni vizuri kumaliza kichapo kinachotegemea Biblia kwa muda mfupi ifaavyo. Hata hivyo, ni lazima ikubaliwe kwamba si wote walio na stadi nzuri za kusoma au uwezo wa kuelewa mawazo mapya haraka. Kwa hiyo, ufahamu wahitajika ili kuamua ni wakati gani tunapopaswa kusonga kutoka kwenye hoja moja hadi nyingine kwenye funzo ikiwa watu mmoja-mmoja wanaoitikia vizuri wanakabili tatizo la kufanya maendeleo haraka. Jambo muhimu zaidi ni kuwasaidia wanafunzi wapate maana ya yale wanayojifunza kuliko tu kumaliza habari kwa mwendo uliowekwa.—Mathayo 13:51.

      19 Jambo hilohilo laweza kusemwa kuhusu wanafunzi wa Biblia ambao wana tatizo la mambo hususa, kama vile Utatu au sikukuu za kidini. Ingawa kwa kawaida si lazima kutia ndani habari za utafiti unaotegemea Biblia tunapokuwa kwenye mafunzo yetu, twaweza kufanya hivyo mara kwa mara ikiwa hilo litakuwa na manufaa iliyo wazi. Uamuzi mzuri wapasa kutumiwa ili tusipunguze maendeleo ya mwanafunzi isivyo lazima.

      Uwe na Shauku!

      20. Paulo aliwekaje kielelezo katika kuonyesha shauku na usadikisho katika kufundisha kwake?

      20 “Iweni wenye kuwaka roho,” asema Paulo. (Waroma 12:11) Ndiyo, iwe tunaongoza funzo la Biblia nyumbani au tunashiriki sehemu fulani katika mikutano ya kutaniko, twapaswa kufanya hivyo kwa bidii na kwa shauku. Paulo aliwaambia Wathesalonike hivi: “Habari njema tuhubiriyo haikutokea miongoni mwenu kwa usemi pekee bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu na usadikisho wenye nguvu.” (1 Wathesalonike 1:5) Kwa njia hiyo Paulo na waandamani wake waliwapa “si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi [zao] wenyewe.”—1 Wathesalonike 2:8.

      21. Twaweza kudumishaje mtazamo wenye shauku kuelekea migawo yetu ya kufundisha?

      21 Shauku ya kweli hutokana na usadikisho imara kwamba wanafunzi wetu wa Biblia wahitaji kusikia yale tunayotaka kusema. Acheni tusiuone kamwe mgawo wowote wa kufundisha kana kwamba ni jambo la kawaida tu. Kwa hakika mwandishi Ezra alikaza uangalifu kwa kufundisha kwake kuhusiana na hili. Yeye ‘aliuelekeza [“aliutayarisha,” NW] moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda, na kufundisha . . . katika Israeli.’ (Ezra 7:10) Twapaswa kufanya vivyo hivyo kwa kutayarisha kikamili na kutafakari juu ya umuhimu wa habari hizo. Acheni tusali kwa Yehova atujaze imani na usadikisho. (Luka 17:5) Shauku yetu yaweza kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia kusitawisha upendo halisi kwa ile kweli. Bila shaka, kukaza uangalifu kwa kufundisha kwetu kwaweza kutia ndani pia kutumia mbinu hususa za kufundisha. Makala yetu inayofuata itazungumzia baadhi ya mbinu hizo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki