Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Usemi Unaoeleweka
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • Tumia kanuni hizo hata unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani. Usijaribu kuelezea kila jambo dogo. Msaidie mwanafunzi aelewe vizuri mawazo makuu. Baadaye, anaweza kujazia mambo mengine katika funzo la kibinafsi na mikutano ya kutaniko.

  • Usemi Unaoeleweka
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • Fafanua Maneno Yasiyoeleweka. Nyakati nyingine tunahitaji kueleza maana ya maneno ambayo wasikilizaji hawaelewi. Usidhani wasikilizaji wanajua mambo mengi sana, wala usidhani hawajui jambo lolote. Kwa sababu ya kujifunza Biblia, huenda ukatumia maneno ambayo watu wengine hawaelewi vizuri. Wale ambao hawashirikiani na Mashahidi wa Yehova hawawezi kuelewa kwamba maneno kama “mabaki,” “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” “kondoo wengine,” na “umati mkubwa” yanarejelea vikundi fulani vya watu usipoyafafanua. (Rom. 11:5; Mt. 24:45; Yn. 10:16; Ufu. 7:9) Hali kadhalika, mtu asiyejua tengenezo la Mashahidi wa Yehova huenda asielewe maneno kama “mhubiri,” “painia,” “mwangalizi wa mzunguko,” na “Ukumbusho.”

      Huenda ikafaa kufafanua maneno mengine ya Biblia ambayo pia hutumiwa sana na hata watu ambao si Mashahidi. Watu wengi wanafikiri “Har-magedoni” inamaanisha maafa ya nyuklia. Wanaweza kufikiri “Ufalme wa Mungu” ni hali fulani iliyo ndani ya mtu au wafikiri unahusiana na mbingu wala si serikali. Wengine wakisikia neno “nafsi,” wanaweza kufikiria sehemu fulani ya kiroho ya binadamu ambayo huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Mamilioni ya watu wamefundishwa kwamba “roho takatifu” ni mtu, sehemu ya Utatu. Na kwa sababu watu wengi sana hawafuati kanuni za Biblia, wanaweza kuhitaji kusaidiwa kuelewa Biblia inamaanisha nini inaposema: “Ukimbieni uasherati.”—1 Kor. 6:18.

      Watu ambao hawasomi Biblia kwa kawaida huenda wasikuelewe unaposema, “Paulo aliandika . . . ” au “Luka alisema . . . ” Labda rafiki zao au majirani wao wanaitwa hivyo. Inaweza kufaa kufafanua kidogo kwamba huyo ni mtume Mkristo au ni mwandishi wa Biblia.

      Mara nyingi watu wa siku zetu wanahitaji kusaidiwa kuelewa maandiko yanayotaja vipimo au desturi za nyakati za kale. Kwa mfano, huenda wasielewe maneno yanayosema kwamba safina ya Noa ilikuwa urefu wa mikono 300, upana wa mikono 50, na kwenda juu mikono 30. (Mwa. 6:15) Lakini ukifafanua vipimo hivyo kwa njia zilizo rahisi kueleweka kwenu, wasikilizaji wataelewa mara moja ukubwa wa safina.

      Eleza Mambo Magumu. Kufafanua tu jambo hakutoshi kuwafanya wasikilizaji walielewe vizuri. Katika siku za Ezra kule Yerusalemu, Sheria ilisomwa na kufafanuliwa. Ili watu waelewe maana ya Sheria, Walawi waliifafanua na kuonyesha jinsi ilivyohusu hali za watu wakati huo. (Neh. 8:8, 12) Vivyo hivyo, eleza maandiko unayosoma na kuonyesha jinsi yanavyotumika maishani.

      Baada ya kufa na kufufuliwa, Yesu aliwaeleza wanafunzi wake kwamba tukio hilo lilitimiza Maandiko. Pia alikazia daraka lao wakiwa mashahidi wa mambo hayo. (Luka 24:44-48) Ukiwasaidia watu waone jinsi mambo ambayo wamefundishwa yanahusu maisha yao, watayaelewa kwa urahisi zaidi.

      Jinsi Moyo Unavyohusika. Hata kama unafafanua mambo kwa njia ya wazi, kuna mambo mengine yanayomfanya mtu akuelewe au asikuelewe. Mtu mwenye moyo mgumu hawezi kupata maana ya mambo yanayosemwa. (Mt. 13:13-15) Watu ambao wameshikilia sana maoni ya kimwili huona mambo ya kiroho kuwa upumbavu tu. (1 Kor. 2:14) Mtu akiwa na roho kama hiyo, huenda likawa jambo la hekima kumaliza mazungumzo hayo angalau kwa wakati huo.

      Lakini mioyo ya wengine huwa migumu kwa sababu ya magumu ya maisha. Na moyo wa mtu kama huyo unaweza kukubali mambo akisikia kweli ya Biblia kwa kipindi fulani. Yesu alipowaambia mitume wake kwamba angechapwa na kuuawa, hawakuelewa. Kwa nini? Hawakutarajia mambo hayo wala hawakutaka yatukie! (Luka 18:31-34) Lakini baada ya muda, wale mitume 11 walionyesha kwamba wamemwelewa Yesu kwa kufuata mambo aliyowafundisha.

      Matokeo ya Mfano Mzuri Tunaoweka. Mbali na kuwasaidia watu kuelewa mambo kupitia maneno yetu, matendo yetu vilevile yanasaidia. Watu wengi husema kwamba walipohudhuria Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza jambo wanalokumbuka zaidi ni upendo walioona wala si mambo waliyosikia. Hali kadhalika, furaha yetu imesaidia watu wengi kukubali kweli ya Biblia. Wengi wamekata kauli ya kwamba dini ya Mashahidi ndiyo ya kweli kwa sababu waliona upendo wenye fadhili ambao watu wa Yehova wameonyeshana na jinsi ambavyo wamewajali wale ambao wamepata misiba. Basi, unapojitahidi kuwasaidia watu waelewe kweli ya Biblia, fikiria jinsi unavyoifafanua na mfano ambao wewe mwenyewe unaweka.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki