Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Msaada wa Kuielewa Biblia
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Julai 1
    • Msaada wa Kuielewa Biblia

      BIBLIA ni kitabu cha pekee. Waandishi wake hudai kwamba walipuliziwa na Mungu, na yaliyomo hutoa uthibitisho wa kutosha kwamba dai hilo ni kweli. (2 Timotheo 3:16) Biblia hueleza tulitoka wapi, kwa nini tupo hapa, na tunaelekea wapi. Bila shaka, Biblia ni kitabu ambacho kinastahili kuchunguzwa!

      Labda umejaribu kuisoma Biblia lakini ukaona kwamba ni vigumu kuielewa. Labda hujui jinsi ya kupata majibu ya maswali yako. Ikiwa ndivyo, kuna wengine walio kama wewe. Hali yako ni kama ya yule mtu aliyeishi katika karne ya kwanza. Alikuwa anasafiri kwenye gari la kukokotwa na farasi kutoka Yerusalemu kwenda Ethiopia, nchi ya kwao. Ofisa huyo Mwethiopia alikuwa akisoma kwa sauti kubwa kitabu cha Biblia cha Isaya, kilichokuwa kimeandikwa zaidi ya miaka 700 awali.

      Kwa ghafula akasalimiwa na mwanamume fulani aliyekuwa anakimbia kandokando ya gari hilo. Mwanamume huyo alikuwa Filipo, mwanafunzi wa Yesu, naye alimwuliza hivi Mwethiopia huyo: “Je, wewe kwa hakika wajua unayoyasoma?” Huyo Mwethiopia akamjibu: “Kwa kweli, ningewezaje kufanya hivyo, isipokuwa mtu fulani angeniongoza?” Kisha akamwalika Filipo ndani ya gari. Filipo alimweleza maana ya sehemu hiyo aliyokuwa anasoma na kumwambia “habari njema juu ya Yesu.”—Matendo 8:30-35.

      Kama vile Filipo alivyomsaidia Mwethiopia huyo kulielewa Neno la Mungu hapo zamani, Mashahidi wa Yehova huwasaidia watu kuielewa Biblia leo. Watafurahia kukusaidia pia. Kwa kawaida, ni vizuri kujifunza Biblia kwa utaratibu, ukianza na mafundisho ya msingi ya Kimaandiko. (Waebrania 6:1) Unapofanya maendeleo, utaweza kula kile Paulo alichokiita “chakula kigumu”—yaani, kweli zenye kina. (Waebrania 5:14) Ingawa Biblia ndiyo unayojifunza, kuna vichapo vingine vinavyoweza kukusaidia kupata na kuelewa maandiko ya Biblia kuhusu habari mbalimbali.

      Kwa kawaida funzo linaweza kupangwa wakati na mahali panapokufaa. Wengine hata hujifunza kupitia simu. Funzo hilo sio kama mafunzo ya darasani; ni mpango wa kibinafsi unaorekebishwa ufaane na hali zako, kutia ndani malezi na elimu yako. Huhitaji kulipia funzo hilo la Biblia. (Mathayo 10:8) Hakuna mitihani, na hutaaibishwa. Maswali yako yatajibiwa, na utajifunza namna ya kumkaribia Mungu. Basi, kwa nini ujifunze Biblia? Chunguza sababu kadhaa zinazoonyesha kwamba funzo la Biblia linaweza kukuongezea shangwe maishani.

  • Kwa Nini Ujifunze Biblia?
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Julai 1
    • Kwa Nini Ujifunze Biblia?

      BILL alikuwa kijana mwenye nguvu, mwenye elimu, na tajiri. Lakini hakuwa ameridhika. Alisumbuka sana kwa kuwa maisha yake hayakuwa na kusudi. Alichunguza dini mbalimbali akijaribu kupata kusudi la maisha, lakini hakufanikiwa. Katika mwaka wa 1991 alikutana na mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyemwachia kitabu kinachozungumzia maoni ya Biblia kuhusu kusudi la maisha. Walipanga kujifunza Biblia ili Bill apate kujua kusudi la maisha na mambo mengineyo.

      Bill anakumbuka: “Tulipojifunza mara ya kwanza tulirejezea Biblia mara nyingi sana hivi kwamba nilijua nimepata nilichokuwa nikitafuta. Majibu ya Biblia yalikuwa yenye kusisimua sana. Baada ya funzo hilo, niliendesha gari langu hadi milimani, nikashuka, na kupaza sauti kwa furaha. Nilisisimuka sana kwamba mwishowe nilikuwa ninapata majibu ya maswali yangu.”

      Bila shaka, si kila mtu anayepata kweli ya Biblia hupaza sauti kwa furaha. Hata hivyo, kujua majibu ya maswali muhimu maishani ni jambo linalofurahisha wengi. Wanahisi kama yule mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu ambaye aligundua hazina fulani iliyokuwa imefichwa katika shamba. Yesu alisema: “Kwa sababu ya shangwe aliyo nayo yeye aenda na kuuza vitu alivyo navyo na kununua shamba hilo.”—Mathayo 13:44.

      Jinsi ya Kuwa na Maisha Yenye Kusudi

      Bill alikuwa ametafakari juu ya swali la msingi, Kusudi la maisha ni nini? Wanafalsafa, wanatheolojia, na wanasayansi wamejitahidi kupata jibu la swali hilo kwa maelfu ya miaka. Vitabu vingi sana vimeandikwa na watu wanaojaribu kujibu swali hilo. Jitihada zao zimeambulia patupu na wengi wamefikia mkataa kwamba swali hilo haliwezi kujibiwa. Hata hivyo, kuna jibu. Jibu hilo ni zito lakini halitatanishi. Linaelezwa katika Biblia. Ni lazima tuwe na uhusiano ufaao pamoja na Yehova, Muumba na Baba yetu wa mbinguni ili tupate furaha na kuelewa kusudi la maisha. Tunawezaje kuwa na uhusiano kama huo?

      Kuna mambo mawili yanayoonekana kana kwamba yanapingana ambayo yanahusika katika kumkaribia Mungu. Wale ambao wanamkaribia Mungu humhofu na kumpenda. Acheni tuchunguze maandiko mawili yanayounga mkono jambo hilo. Zamani za kale, Solomoni, Mfalme mwenye hekima, aliwachunguza wanadamu kwa makini na kuandika matokeo ya uchunguzi wake katika kitabu cha Biblia cha Mhubiri. Akimalizia maelezo yake alisema: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche [“mhofu,” NW] Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.” (Mhubiri 12:13, italiki ni zetu.) Karne kadhaa baadaye, Yesu alipoulizwa ni ipi iliyo amri kuu zaidi katika Sheria iliyopewa Musa, Yesu alijibu: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Je, unaliona kuwa jambo lisilo la kawaida kumhofu Mungu na wakati uleule kumpenda? Acheni tuchunguze umuhimu wa hofu na upendo na jinsi sifa hizo mbili kwa pamoja zinavyoweza kutokeza uhusiano mzuri pamoja na Mungu.

      Kumhofu Mungu Kwamaanisha Nini?

      Hofu yenye staha ni muhimu iwapo tutamwabudu Mungu kwa njia inayokubalika. Biblia inasema: “Kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA ndio mwanzo wa hekima.” (Zaburi 111:10) Mtume Paulo aliandika: “Acheni sisi tuendelee kuwa na fadhili isiyostahiliwa, ambayo kupitia hiyo twaweza kumtolea Mungu katika njia ya kukubalika utumishi mtakatifu kwa hofu ya kimungu na kicho.” (Waebrania 12:28) Vivyo hivyo, malaika fulani aliyekuwa katikati ya mbingu, ambaye alionekana katika njozi na mtume Yohana, alianza kutangaza habari njema kwa maneno haya: “Hofuni Mungu na kumpa utukufu.”—Ufunuo 14:6, 7.

      Kumhofu Mungu ambako ni muhimu sana ili kuwa na maisha yenye kusudi, ni tofauti na kuwa na woga usiofaa. Tunaweza kuogopa tukitishwa na mhalifu hatari na mkatili. Lakini kumhofu Mungu—au hofu ya kimungu—ni kuwa na kicho na staha nyingi kwa Muumba. Hiyo yatia ndani hofu ifaayo ya kutompendeza Mungu kwa sababu yeye ndiye Hakimu Mkuu Zaidi na Mweza Yote, naye ana uwezo na mamlaka ya kuadhibu wale wasiotii.

      Hofu na Upendo Zinahusiana

      Hata hivyo, Yehova hataki watu wamtumikie kwa sababu tu wanamwogopa. Yehova ni Mungu mwenye upendo sana. Mtume Yohana alichochewa kuandika: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Yehova Mungu ameshughulika na wanadamu kwa upendo mwingi sana, naye anataka watu waitikie kwa kumpenda. Lakini upendo huo wapatanaje na hofu ya kimungu? Sifa hizo mbili zinahusiana. Mtunga-zaburi aliandika: “Siri ya BWANA iko kwao wamchao [“wanaomhofu,” NW].”—Zaburi 25:14.

      Hebu wazia staha na hofu ambayo mtoto huwa nayo kwa baba mwenye nguvu na hekima na wakati huohuo mtoto huyo huitikia upendo wa baba huyo. Mtoto huyo anamtumaini baba na kumtazamia amwongoze, akiwa na uhakika kwamba uongozi huo utaleta manufaa. Vivyo hivyo, ikiwa tunampenda na kumhofu Yehova, tutatii mwongozo wake na kunufaika. Ona yale ambayo Yehova alisema kuhusu Waisraeli: “Laiti wangekuwa na moyo kama huu ndani yao sikuzote, wa kunicha [“kunihofu,” NW] na kushika amri zangu zote sikuzote, wapate kufanikiwa wao na watoto wao milele!”—Kumbukumbu la Torati 5:29.

      Naam, hofu ya kimungu huleta uhuru wala si utumwa, shangwe wala si huzuni. Isaya alitabiri hivi kuhusu Yesu: “Na furaha yake itakuwa katika kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA.” (Isaya 11:3) Naye mtunga-zaburi akaandika: “Heri mtu yule amchaye [“amhofuye,” NW] BWANA, apendezwaye sana na maagizo yake.”—Zaburi 112:1.

      Ni wazi kwamba hatuwezi kumhofu Mungu wala kumpenda ikiwa hatumjui. Hiyo ndiyo sababu funzo la Biblia ni muhimu sana. Funzo kama hilo hutusaidia kuelewa utu wa Mungu na kutambua hekima ya kufuata mwongozo wake. Tunapomkaribia Mungu, tunataka kufanya mapenzi yake na tunachochewa kushika amri zake, tukijua kwamba zitatunufaisha.—1 Yohana 5:3.

      Ni furaha kujua kwamba unaishi maisha yafaayo. Bill aliyetajwa awali anajua hivyo. Hivi majuzi yeye alisema: “Katika miaka sita ambayo imepita tangu nijifunze Biblia mara ya kwanza, uhusiano wangu na Yehova umekua. Ile furaha niliyokuwa nayo awali imekuwa njia ya maisha yenye shangwe kwelikweli. Sikuzote ninatazamia mema maishani, na badala ya kutafuta raha tu bila kusudi, nina mambo mengi yenye maana ya kufanya maishani. Yehova amekuwa mtu halisi kwangu, na ninajua kwamba ananijali kwelikweli.”

      Katika makala ifuatayo, tutachunguza zaidi jinsi kumjua Yehova huleta furaha na manufaa kwa wale wanaoutumia maishani mwao.

      [Blabu katika ukurasa wa 5]

      Kumkaribia mungu humaanisha kumpenda na kumhofu pia

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Yesu alipata furaha katika kumhofu Yehova

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki