-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kupanua Ofisi ya Tawi
Katika miaka ya 1930, Llewelyn Phillips na wafanyakazi wenzake waliendesha kazi katika jengo lililokodiwa lenye vyumba viwili huko Lusaka. Ni watu wachache sana waliofikiri kwamba Betheli iliyo na makao kwa ajili ya zaidi ya watumishi 250 wa kujitolea ingejengwa kwenye uwanja wa ekari 270. Ndugu na dada hao wenye kujitolea wanawategemeza kiroho wahubiri na mapainia zaidi ya 125,000. Hebu tuchunguze kifupi jinsi ongezeko hilo lilivyotokea.
Kama tulivyoona mwanzoni, kufikia 1936 wakuu wa serikali walikuwa wametulia sana hivi kwamba walitupa kibali cha kufungua depo huko Lusaka. Muda si muda, ikawa lazima kuhamia kwenye jengo kubwa kwa sababu ya ongezeko. Nyumba fulani ilinunuliwa karibu na kituo cha polisi katikati ya jiji. Jonas Manjoni anasema: “Ilikuwa na vyumba viwili vya kulala. Idara ya Utumishi ilikuwa katika chumba cha kulia chakula nayo Idara ya Upakizi na Usafirishaji ilikuwa varandani.” Katika 1951, Jonas alichukua likizo ya majuma mawili na kuenda kufanya kazi Betheli, na baadaye akahamia huko. Anasema: “Kulikuwa na utaratibu na furaha. Nilitumika katika Idara ya Upakizi na Usafirishaji pamoja na Ndugu Phillips. Tulishughulikia maandikisho na pia tuliweka stampu kwenye vifurushi vya magazeti. Tulifurahi sana kuwatumikia ndugu.” Baadaye Harry Arnott alijiunga na Llewelyn Phillips nao wakafanya kazi pamoja na ndugu wenyeji kama vile Job Sichela, Andrew John Mulabaka, John Mutale, Potipher Kachepa, na Morton Chisulo.
Katika eneo la shaba la Zambia, biashara ya shaba ilipanuka, nayo mifumo muhimu kama vile barabara, simu, na umeme ikasitawishwa haraka. Hivyo, watu wengi sana walihamia kwenye eneo hilo na ndugu walilizingatia zaidi kuliko jiji la Lusaka. Ian Fergusson alipendekeza jengo linunuliwe katika mji fulani kwenye eneo la migodi, na katika 1954, ofisi ya tawi ikafunguliwa kwenye Barabara ya King George, Luanshya. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, jengo hilo likawa dogo lisiweze kutumiwa kusimamia kazi katika eneo lililokuwa likipanuka haraka, ambalo wakati huo lilitia ndani sehemu kubwa ya Afrika Mashariki. Nathan Knorr, kutoka makao makuu alipokuja kwa ajili ya Kusanyiko la Wilaya la “Wahudumu Wanaokesha” la 1959, alikagua maeneo kadhaa yaliyopendekezwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi mpya, kisha akaidhinisha ujenzi huo. Geoffrey Wheeler anasema: “Mimi, Frank Lewis, na Eugene Kinaschuk, tuliandamana pamoja na mtaalamu fulani wa ujenzi kwenda kwenye uwanja huo mpya huko Kitwe ili kuweka alama mahali hasa ambapo Betheli mpya ingejengwa.” Mnamo Februari 3, 1962, ofisi mpya ya tawi, iliyokuwa na makao, chumba cha uchapaji, na Jumba la Ufalme, iliwekwa wakfu kwa Yehova. Akimalizia programu ya wakfu, Harry Arnott, ambaye wakati huo alikuwa mtumishi wa ofisi ya tawi, alikazia kwamba ujenzi wa kiroho ndio muhimu zaidi, nasi tunapaswa kuushiriki kwa bidii kwa kutumia vifaa vya ujenzi kama vile imani, tumaini, na upendo.
Katika miaka kumi iliyofuata, idadi ya wahubiri iliongezeka kutoka 30,129 hadi 57,000 hivi. Hivyo, upesi ofisi hiyo ya tawi ikawa ndogo sana isiweze kufaa kwa uhitaji uliokuwapo. Ian Fergusson alisema: “Ndugu Knorr alituhimiza tupanue kiwanda chetu cha uchapaji. Nilitembelea ofisi ya tawi ya Elandsfontein, Afrika Kusini, ili kushauriana na akina ndugu. Muda mfupi baadaye, mashine ya kuchapa ikasafirishwa kwa ndege hadi Kitwe.”
Huduma Yetu ya Ufalme ya kila mwezi na pia magazeti na vichapo vingine kwa ajili ya Kenya na nchi nyingine za Afrika Mashariki, vilikuwa vikichapwa huko Kitwe. Punde baadaye, kiwanda chetu cha uchapaji kikawa kidogo sana na ikatubidi kujenga kiwanda kipya. Baraza la mji lilipotuzuia tusijenge kiwanda hicho katika kiwanja fulani kilichokuwa kimepatikana, ndugu mmoja alitupa kiwanja. Ujenzi ulikamilika katika 1984. Kwa miaka 30, mji wa Kitwe ulikuwa kitovu cha kiroho cha kazi ya kuhubiri nchini Zambia.
Katika ile miaka ya hali ngumu baada ya wamishonari kufukuzwa nchini, idadi ya wafanyakazi katika ofisi ya tawi iliongezeka hivi kwamba Wanabetheli 14 walilazimika kuishi nje ya Betheli pamoja na familia zao. Marekebisho yalihitajiwa ili kazi ishughulikiwe vizuri. Baadaye, nyumba mbili zilinunuliwa, na nyingine ikakodiwa, na hivyo ikawezekana kuwa na Wanabetheli zaidi. Hata hivyo, ilikuwa wazi kwamba majengo mapya yalihitajiwa. Inapendeza kwamba hali ziliboreka muda mfupi baadaye. Katika 1986, ndugu katika maeneo muhimu waliombwa watafute kiwanja kwa ajili ya ofisi mpya. Kiwanja cha ekari 270 kilipatikana umbali wa kilometa 15 magharibi ya jiji kuu. Kilifaa sana kwa sababu eneo hilo lina maji mengi ardhini. Dayrell Sharp alisema hivi: “Naamini kwamba Yehova alituelekeza mahali hapa penye kupendeza.”
Ongezeko na Kuweka Wakfu Majengo Mapya
Jumamosi, Aprili 24, 1993, mamia ya wahudumu wa muda mrefu wa Yehova walikusanyika kwa ajili ya kuwekwa wakfu kwa majengo mapya. Mbali na ndugu na dada 4,000 ambao ni wenyeji, wageni wa kimataifa zaidi ya 160 walikuwapo, kutia ndani wamishonari waliokuwa wamefukuzwa Zambia miaka 20 hivi mapema. Theodore Jaracz, mmoja wa washiriki wawili wa Baraza Linaloongoza ambao walikuwapo, alitoa hotuba yenye kichwa, “Kujipendekeza Wenyewe Kuwa Wahudumu wa Mungu.” Aliwaambia wale waliotumika kwa uaminifu kwa miaka mingi kwamba uhitaji wa kujenga haungalikuwako ikiwa hawangalivumilia. Akirejelea maneno ya Paulo kwa Wakorintho, alikazia kwamba mhudumu wa kweli husitawisha matunda ya roho, ambayo humwezesha kuvumilia hali ngumu, majaribu, na mateso. Alisema: “Mmejipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu. Tumejenga ofisi hii mpya ya tawi kwa sababu kuna ongezeko.”
Katika 2004, ujenzi wa jengo jipya la makazi lenye orofa nne zenye vyumba 32 ulikamilika. Eneo lenye ukubwa wa meta 1,000 hivi za mraba katika kiwanda cha uchapaji limerekebishwa. Eneo hilo sasa lina ofisi 47 za tafsiri, sehemu ya kuhifadhi faili, vyumba vya mikutano, na maktaba.
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 251]
Wafanya kazi wenye shangwe wakijenga ofisi ya tawi ya sasa huko Lusaka
[Picha katika ukurasa wa 252, 253]
(1, 2) Majumba ya Ufalme yaliyojengwa hivi karibuni
(3, 4) Ofisi ya tawi ya Zambia, Lusaka
(5) Stephen Lett wakati wa kuwekwa wakfu kwa majengo mapya ya ofisi ya tawi mnamo Desemba 2004
-