-
Kuna Faida za Kuwa MnyoofuAmkeni!—2012 | Januari
-
-
Kuna Faida za Kuwa Mnyoofu
“Mkate unaopatikana kwa udanganyifu humpendeza mtu, lakini baadaye kinywa chake kitajaa changarawe.”—Methali 20:17.
JE, NI lazima mtu awe mdanganyifu ili biashara yake ifanikiwe? Jibu ni la. Mara nyingi kukosa kuwa mnyoofu huleta hasara. Kwa nini? Kwa sababu unyoofu hufanya mtu aaminiwe, na hilo ni muhimu ili mtu aendelee kufanikiwa.
Faida za Kuaminika
Unyoofu wako huathiri mafanikio yako—iwe unajua au hujui. Kisa cha Franz, aliyetajwa katika makala iliyotangulia, kinaonyesha jambo hilo. “Nilipoajiriwa,” anasema, “waajiri wangu walijaribu unyoofu na uaminifu wangu mara kadhaa bila mimi kujua. Nilikuja kujua baadaye kwamba nilipita mtihani huo. Kwa sababu hiyo, nimepewa madaraka zaidi na uhuru zaidi na waajiri wangu wamenithawabisha kwa sababu ya kuwa mnyoofu. Ninajua kwamba kuna watu wanaoweza kufanya kazi yangu kwa njia bora zaidi na walio na akili kuliko mimi. Hata hivyo, nadhani sijafutwa kazi kwa muda wote huu kwa sababu waajiri wangu wananiamini.”
Epuka Kujasiria Mambo
David, mfanyabiashara aliyenukuliwa katika makala iliyotangulia anasema hivi: “Ninapowaona watu wakivunja sheria ili wapate faida ya muda mfupi tu, mimi hujiambia, ‘Mtu atavuna anachopanda, hata kama si mara hiyohiyo.’ Yaani hatimaye, kukosa kuwa mnyoofu kutakuletea matatizo kwa njia moja au nyingine. Tulikataa biashara nyingi zenye kutiliwa shaka. Kampuni nyingi ambazo zilijihusisha katika biashara hizo zilitoweka baadaye, na watu fulani wakashtakiwa. Kampuni yetu iliepuka matatizo hayo yote.”
Alipokuwa akianzisha shamba la kufuga ng’ombe huko kusini-mashariki mwa Afrika, Ken angeweza kushawishiwa awape rushwa maofisa fulani ili aweze kuuza haraka bidhaa zake nje ya nchi na wamsaidie kuepuka kulipa ushuru. Anasema hivi: “Wafugaji wengine wengi walijihusisha katika zoea hilo. Kwa kuwa tulifanya mambo kwa unyoofu, ilichukua miaka kumi ili tupate kila kitu tulichohitaji katika shamba letu. Je, tulifaidika kwa kuwa wanyoofu? Ndiyo! Wale waliotoa rushwa walisumbuliwa kila mara na maofisa wafisadi ambao walitaka rushwa zaidi.”
Kukabiliana na Matatizo ya Kiuchumi
Biashara inapokabili hatari ya kuanguka, watu hushinikizwa waache kuwa wanyoofu. Hata hivyo, hali hizo zinaweza kuonyesha faida ya kuwa mnyoofu.
Fikiria mfano wa Bill, ambaye biashara yake ya ujenzi ilianguka wakati biashara ya nyumba nchini Marekani ilikumbwa na matatizo. Anasema hivi: “Wengi wa wateja wetu wakubwa walifilisika na kwenda na deni letu la maelfu ya dola. Nilipoona kwamba hakuna tumaini, nilimfikia mtu aliyekuwa akifanya biashara kama yangu na kumwomba aniajiri pamoja na wafanyakazi wangu. Saa 48 hivi baada ya mkutano huo, waliniajiri mimi pamoja na wengi wa wafanyakazi wangu. Niliambiwa kwamba nilikuwa na sifa ya kutoa huduma nzuri na kuwa mnyoofu.”
Visa vyote vilivyotajwa hapa ni vya watu ambao ni Mashahidi wa Yehova. Viwango wanavyofuata katika biashara, sawa na viwango wanavyofuata maishani vinategemea Biblia. Kama vile makala hii imeonyesha, badala ya unyoofu wao kuwazuia wafanikiwe katika biashara, umewasaidia kupata faida.
-
-
Unyoofu Huleta Mafanikio ya KweliAmkeni!—2012 | Januari
-
-
Unyoofu Huleta Mafanikio ya Kweli
“Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—Luka 12:15.
KUTAFUTA riziki ni sehemu muhimu ya maisha. Tuna wajibu mbele za Mungu wa kuandaa mahitaji yetu na ya familia zetu.—1 Timotheo 5:8.
Lakini namna gani ikiwa badala ya kutafuta riziki tu unaanza kukazia fikira kutafuta pesa na vitu unavyoweza kununua? Vipi ikiwa hilo ndilo kusudi lako kuu maishani? Wale ambao lengo lao kuu ni kutajirika huona kuwa ni rahisi kutumia njia zisizo za unyoofu kupata pesa. Huenda wasitambue kwamba kukosa unyoofu kunawafanya wasifanikiwe kikweli mpaka inapokuwa kuchelewa mno. Isitoshe, kama vile Biblia inavyosema, kupenda pesa husababisha maumivu mengi.—1 Timotheo 6:9, 10.
Fikiria mifano minne ifuatayo ya watu ambao wanasema kwamba kufanikiwa hakumaanishi kujirundikia mali.
Kujiheshimu
“Miaka kadhaa iliyopita, nilimhoji mteja aliyetaka kununua bima ya maisha ambayo ingemgharimu dola milioni moja. Ningelipwa maelfu ya dola kwa kukamilisha mkataba huo. Aliniambia kwamba ili awe mteja wangu, ingebidi nimpe nusu ya pesa nilizopata. Ombi lake lilikuwa kinyume cha maadili na pia tungekuwa tukivunja sheria, nami nilimwambia hivyo waziwazi.
“Nilijaribu kuzungumza naye na kumwuliza ikiwa angetaka mtu asiye mnyoofu ajue habari zake za kibinafsi na za kifedha ambazo ni siri. Nilimweleza tena msimamo wangu na kumwambia awasiliane nami ikiwa bado angetaka nimwakilishe. Hakuwahi kuwasiliana nami tena.
“Kama ningekubali ombi lake, ningeacha kuwa mwaminifu na ningeacha kujiheshimu kama Mkristo. Ningekuwa mtumwa wa mwanadamu ambaye alitaka kunishinikiza nijiunge naye katika ukosefu wa unyoofu.”—Don, Marekani.
Amani ya Akili
Kama ilivyotajwa katika makala ya kwanza ya mfululizo huu, mmiliki wa kiwanda fulani alitaka kumpa Danny rushwa kubwa ili adanganye kwamba kiwanda hicho kinaweza kutokeza bidhaa zinazofaa. Danny alifanya nini?
“Nilimshukuru meneja huyo kwa kunikaribisha kwenye mlo kisha nikamrudishia bahasha hiyo iliyokuwa na pesa. Alinishinikiza kwa kusema kwamba ikiwa kiwanda chake kingepita ukaguzi wetu, angeniongezea pesa zaidi. Nilikataa.
“Kama ningekubali rushwa hiyo, ningekuwa na wasiwasi daima kwamba nitagunduliwa. Baadaye, mwajiri wangu alipata habari kuhusu kisa hicho. Nilifurahi sana kwamba sikuwa nimefanya jambo lolote lenye ukosefu wa unyoofu. Nilikumbuka andiko la Methali 15:27: ‘Mtu anayepata faida isiyo ya haki anailetea nyumba yake mwenyewe taabu, lakini anayechukia zawadi [au rushwa] ndiye atakayeendelea kuishi.’”—Danny, Hong Kong.
Furaha ya Familia
“Nina biashara yangu ya ujenzi. Mimi hupata fursa nyingi za kuwadanganya wateja wangu au kukwepa kulipa kodi. Lakini mimi na familia yangu tumefaidika kutokana na jitihada zangu za kuendelea kuwa mnyoofu.
“Mtu anapaswa kuwa mnyoofu katika kila sehemu ya maisha yake, si kazini au katika biashara tu. Kujua kwamba mume au mke wako hatavunja kanuni za Mungu za unyoofu kunafanya washiriki wa familia waaminiane. Mwenzi wako anajihisi akiwa salama kwa sababu anajua kwamba unyoofu wako si kama vazi unalovaa na kuvua inapohitajika.
“Unaweza kuwa mmiliki wa kampuni kubwa zaidi ulimwenguni lakini huwezi kununua suluhisho la matatizo ya familia yako. Nikiwa Shahidi wa Yehova, nimegundua kwamba kufuata kanuni za Biblia hufanya niwe na usawaziko. Nina wakati wa kuwa pamoja na familia yangu bila kufuata tu ulimwengu huu unaoongozwa na pupa na pesa.”—Durwin, Marekani.
Uhusiano Mzuri na Mungu
“Kazi yangu inahusisha kununua bidhaa kwa ajili ya kampuni yetu. Nyakati nyingine wauzaji huniambia kwamba badala ya kuipunguzia kampuni bei, watanipa kiasi fulani cha faida wanayopata kutoka kwa kampuni yetu. Lakini kufanya hivyo kungekuwa kuiba pesa za kampuni.
“Mimi hupata mshahara wa chini, na pesa hizo za ziada zingenisaidia sana. Lakini hakuna kitu kinachoweza kulinganishwa na dhamiri safi na kupata kibali machoni pa Yehova Mungu. Kwa hiyo, ninaponunua bidhaa yoyote, mimi hufuata kanuni ya Biblia kwenye Waebrania 13:18: ‘Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.’”—Raquel, Filipino.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
Kanuni Kuhusu Kufanya Biashara kwa Unyoofu
Kanuni za maadili za biashara hutofautiana katika sehemu mbalimbali. Hata hivyo, kanuni za Biblia zinaweza kutumiwa kuwa msingi wa kufanya maamuzi yanayopatana na maadili. Zifuatazo ni kanuni sita za kufanya biashara kwa unyoofu:
Kusema Kweli
Kanuni: “Msiwe mkiambiana uwongo.”—Wakolosai 3:9.
Kutegemeka
Kanuni: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.”—Mathayo 5:37.
Kuaminika
Kanuni: “Usifunue mazungumzo ya siri ya mwingine.”—Methali 25:9.
Unyoofu
Kanuni: “Usikubali rushwa, kwa maana rushwa hupofusha watu wanaoona.”—Kutoka 23:8.
Tenda kwa Haki
Kanuni: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.
Fuata Sheria
Kanuni: “Wapeni wote haki zao, yeye anayetaka kodi, kodi.”—Waroma 13:7.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
Jinsi ya Kuwa Mnyoofu Katika Biashara
● Amua Mambo Utakayotanguliza. Kwa mfano, ni jambo gani lililo muhimu zaidi kwako—kupata utajiri au kudumisha msimamo mzuri mbele za Mungu?
● Amua Mapema. Fikiria hali ambazo zinaweza kufanya iwe vigumu kuwa mnyoofu, na uamue jinsi utakavyokabiliana nazo.
● Tangaza Msimamo Wako Waziwazi. Unapoanza kufanya biashara na wengine, waeleze kwa busara kuhusu viwango vyako.
● Waombe Wengine Mashauri. Unapokabili kishawishi, mwombe mashauri mtu ambaye anafuata viwango kama vyako.
-