Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Jipe Moyo!”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 24

      “Jipe Moyo!”

      Paulo anusurika kifo na anajitetea mbele ya Feliksi

      Matendo 23:11–24:27

      1, 2. Kwa nini Paulo hashangazwi na mateso anayokabili jijini Yerusalemu?

      BAADA ya kuokolewa kutoka kwenye umati wenye hasira kali jijini Yerusalemu, Paulo awekwa kizuizini tena. Mateso anayokabili katika jiji la Yerusalemu hayamshangazi mtume huyo mwenye bidii. Aliambiwa atazamie ‘kufungwa gerezani na kupatwa na dhiki’ katika jiji hilo. (Mdo. 20:22, 23) Ijapokuwa Paulo hajui kitakachompata, anajua kwamba atateseka kwa ajili ya jina la Yesu.​—Mdo. 9:16.

      2 Hata manabii Wakristo walimwonya Paulo kwamba atafungwa na kutiwa “mikononi mwa watu wa mataifa.” (Mdo. 21:4, 10, 11) Siku chache zilizotangulia, umati wa Wayahudi ulijaribu kumuua, na muda mfupi baadaye, washiriki wa Sanhedrini karibu ‘wangemrarua-rarua’ walipokuwa wakibishana kwa sababu ya mambo aliyosema. Sasa mtume huyo ni mfungwa chini ya ulinzi wa askari jeshi Waroma, akikabili kesi na mashtaka mengi. (Mdo. 21:31; 23:10) Bila shaka, mtume Paulo anahitaji kutiwa moyo!

      3. Sisi hutiwa moyo jinsi gani kuendelea kuhubiri?

      3 Katika siku hizi za mwisho, tunajua kwamba “wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Tim. 3:12) Mara kwa mara, sisi pia tunahitaji kutiwa moyo ili tuendelee katika kazi yetu ya kuhubiri. Tunathamini sana maneno yenye kutia moyo na yenye kufariji tunayopata kwa wakati unaofaa, kupitia machapisho na mikutano inayotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”! (Mt. 24:45) Yehova ametuhakikishia kwamba hakuna adui wa habari njema atakayefanikiwa. Hawawezi kuwaangamiza watumishi wake wakiwa kikundi wala kukomesha kazi yao ya kuhubiri. (Isa. 54:17; Yer. 1:19) Namna gani mtume Paulo? Je, alitiwa moyo kuendelea kutoa ushahidi kamili licha ya upinzani? Ikiwa ndivyo, alitiwa moyo jinsi gani, naye alifanya nini?

      ‘Hila Iliyofungwa kwa Kiapo’ Yazimwa (Mdo. 23:11-34)

      4, 5. Paulo alitiwa moyo jinsi gani, na kwa nini alitiwa moyo kwa wakati unaofaa?

      4 Mtume Paulo alitiwa moyo sana usiku uliofuata, baada ya kuokolewa kutoka kwa Sanhedrini. Masimulizi yaliyoongozwa na roho yanasema: “Bwana akasimama kando yake na kumwambia: ‘Jipe moyo! Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili kunihusu katika Yerusalemu, ndivyo utakavyotoa ushahidi huko Roma pia.’” (Mdo. 23:11) Maneno hayo ya Yesu yanayotia moyo yalimhakikishia Paulo kwamba atakombolewa. Alijua kwamba atafika Roma na kutoa ushahidi kumhusu Yesu.

      Mpwa wa Paulo akiongea na Klaudio Lisia.

      “Wanaume zaidi ya 40 kati yao walio tayari kumvizia.”—Matendo 23:21

      5 Paulo alitiwa moyo kwa wakati unaofaa. Siku iliyofuata, wanaume Wayahudi zaidi ya 40, “wakafanya hila na kujifunga kwa kiapo cha laana, wakisema hawatakula wala kunywa mpaka watakapomuua Paulo.” ‘Hila iliyofungwa kwa kiapo,’ ilionyesha jinsi Wayahudi hao walivyoazimia kabisa kumuua mtume huyo. Waliamini kwamba, ikiwa hawangefanikiwa katika hila yao, basi wangestahili kulaaniwa, au kupatwa na mabaya. (Mdo. 23:12-15) Wakiwa na kibali cha wakuu wa makuhani na wazee, walipanga Paulo arudishwe mbele ya mahakama ya Sanhedrini ili kujibu maswali zaidi, kana kwamba kuna mambo yanayomhusu ambayo wanataka kuhakikisha. Hata hivyo, lengo lao lilikuwa kumvizia Paulo akiwa njiani na kumuua.

      6. Njama ya kumuua Paulo ilifunuliwaje, na vijana wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mpwa wa Paulo?

      6 Hata hivyo, mpwa wa Paulo alipata habari kuhusu njama hiyo, naye akamjulisha Paulo. Kisha, Paulo akamwagiza kijana huyo amwambie Klaudio Lisia, kiongozi wa jeshi la Roma. (Mdo. 23:16-22) Bila shaka, Yehova anawapenda vijana ambao, kama mpwa huyo wa Paulo, hutanguliza kwa ujasiri hali njema ya watu wa Mungu na kufanya kwa uaminifu yote wawezayo ili kuendeleza kazi ya Ufalme.

      7, 8. Klaudio Lisia alifanya nini ili kuhakikisha usalama wa Paulo?

      7 Mara tu baada ya kuambiwa kuhusu njama iliyopangwa dhidi ya Paulo, Klaudio Lisia, aliyekuwa akisimamia askari 1,000, akaamuru kikosi cha askari 470—askari jeshi, wenye mikuki, na wapanda farasi—kiende Yerusalemu usiku huo na kumsindikiza Paulo mpaka Kaisaria. Akiwa huko alipaswa kufikishwa mbele ya Gavana Feliksi.a Jiji la Kaisaria lilikuwa kituo cha serikali ya Roma katika mkoa wa Yudea. Kulikuwa na Wayahudi wengi, lakini wakaaji wengi zaidi walikuwa Watu wa Mataifa. Mkoa huo ulikuwa tofauti kabisa na Yerusalemu, ambako watu wengi walionyesha chuki ya kidini na kusababisha ghasia. Kaisaria lilikuwa pia makao makuu ya majeshi ya Roma katika mkoa wa Yudea.

      8 Kupatana na sheria za Roma, Lisia alimtumia Feliksi barua kumweleza mashtaka yaliyotolewa. Lisia alitaja kwamba alipojua Paulo ni raia wa Roma, alimwokoa ili ‘asiuawe’ na Wayahudi. Lisia alisema kwamba hakumpata Paulo na hatia yoyote ya ‘kustahili kifo au kufungwa gerezani,’ lakini kwa sababu ya hila iliyopangwa dhidi ya Paulo, alimtuma kwa Feliksi ili awasikilize wanaomshtaki na kutoa hukumu.​—Mdo. 23:25-30.

      9. (a) Haki za Paulo akiwa raia wa Roma zilikiukwa jinsi gani? (b) Kwa nini huenda tukahitaji kutumia haki zetu tukiwa raia wa nchi?

      9 Je, mambo yote ambayo Lisia aliandika yalikuwa kweli? Hapana. Inaonekana alikuwa anajitafutia sifa. Ukweli ni kwamba hakumwokoa Paulo kwa kuwa alijua kwamba mtume huyo ni raia wa Roma. Isitoshe, Lisia hakutaja kwamba alikuwa ameamuru Paulo “afungwe kwa minyororo miwili” na baadaye alitoa amri Paulo “ahojiwe huku akipigwa mijeledi.” (Mdo. 21:30-34; 22:24-29) Lisia alikuwa amekiuka haki za Paulo akiwa raia wa Roma. Leo, Shetani hutumia wapinzani wa kidini kuchochea mateso, na huenda uhuru wetu wa ibada ukavurugwa. Hata hivyo, kama Paulo alivyofanya, watu wa Mungu wanaweza kutumia haki zao wakiwa raia wa nchi ili kutafuta ulinzi wa kisheria.

      “Nami Nafurahi Kujitetea Mbele Yako” (Mdo. 23:35–24:21)

      10. Paulo alishtakiwa mambo gani mazito?

      10 Akiwa Kaisaria, Paulo ‘aliwekwa chini ya ulinzi katika jumba la kifalme la Herode’ akingojea waliomshtaki wafike kutoka Yerusalemu. (Mdo. 23:35) Siku tano baadaye, wakafika—Kuhani Mkuu Anania, wakili anayeitwa Tertulo, na kikundi cha wazee. Tertulo alianza kwa kumsifu Feliksi kwa mambo aliyokuwa akiwafanyia Wayahudi, huenda ili apate kibali chake.b Kisha, akianza mashtaka yake, Tertulo alisema kwamba Paulo ni “msumbufu, akichochea uasi miongoni mwa Wayahudi wote katika dunia yote inayokaliwa, naye ni kiongozi wa madhehebu ya Wanazareti. Pia alijaribu kulichafua hekalu, basi tukamkamata.” Wale Wayahudi wengine “wakajiunga katika shambulio hilo, wakisisitiza kwamba mambo hayo ni ya kweli.” (Mdo. 24:5, 6, 9) Kuchochea uasi, kuongoza madhehebu hatari, na kulichafua hekalu—hayo yalikuwa mashtaka mazito ambayo yangeweza kufanya mtu ahukumiwe kifo.

      11, 12. Paulo alikanushaje mashtaka yaliyoletwa dhidi yake?

      11 Kisha, Paulo akaruhusiwa azungumze. Akasema hivi: “Nami nafurahi kujitetea mbele yako.” Kisha, akakanusha mashtaka hayo. Mtume huyo hakuwa amelichafua hekalu, wala kujaribu kuchochea uasi. Alisema kwamba hata hakuwa Yerusalemu kwa “miaka kadhaa” na kwamba alikuwa amefika kuleta “zawadi za rehema”​—michango kwa ajili ya Wakristo ambao walikuwa maskini kwa sababu ya njaa na mateso. Paulo alisisitiza kwamba kabla ya kuingia hekaluni, alikuwa ‘ametakaswa kisherehe’ naye aliazimia “kudumisha dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu.”​—Mdo. 24:10-13, 16-18.

      12 Paulo alikiri kwamba alikuwa akitoa utumishi mtakatifu kwa Mungu wa mababu zake “kulingana na njia wanayoiita madhehebu.” Hata hivyo, alisisitiza kwamba anaamini “mambo yote yaliyo katika Sheria na yaliyoandikwa katika Manabii.” Na kama washtaki wake, alikuwa na tumaini la “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Kisha, Paulo akawataka washtaki wake watoe uthibitisho wa madai yao: “Uwaambie watu walio hapa waseme wenyewe kosa walilopata nilipokuwa nimesimama mbele ya Sanhedrini, isipokuwa jambo hili moja nililosema kwa sauti kubwa nilipokuwa nimesimama kati yao: ‘Mimi ninahukumiwa leo mbele yenu kwa sababu ya ufufuo wa wafu!’”​—Mdo. 24:14, 15, 20, 21.

      13-15. Ni kwa njia gani Paulo alituwekea mfano mzuri wa kutoa ushahidi kwa ujasiri tunaposhtakiwa?

      13 Paulo alituwekea mfano mzuri tunaoweza kufuata ikiwa tutashtakiwa kwa sababu ya ibada yetu na tukishtakiwa kuwa wachochezi, waasi, au washiriki wa “madhehebu hatari.” Paulo hakujaribu kujipendekeza mbele ya gavana, akimsifu kama alivyofanya Tertulo. Paulo alikuwa mtulivu na mwenye heshima. Kwa busara, alitoa ushahidi wenye kusadikisha na wa kweli. Paulo alitaja kwamba “Wayahudi fulani kutoka mkoa wa Asia” waliodai kwamba alichafua hekalu hawako, na kulingana na sheria wanapaswa kuwapo ili wathibitishe mashtaka yao.​—Mdo. 24:18, 19.

      14 Zaidi ya yote, Paulo hakuogopa kutoa ushahidi kuhusu imani yake. Kwa ujasiri mtume alitaja tena na tena imani yake katika ufufuo, suala ambalo lilisababisha vurugu alipokuwa mbele ya Sanhedrini. (Mdo. 23:6-10) Alipokuwa akijitetea, Paulo alikazia tumaini la ufufuo. Kwa nini? Kwa sababu Paulo alikuwa akitoa ushahidi kumhusu Yesu na ufufuo wake—jambo ambalo wapinzani hao hawakukubali. (Mdo. 26:6-8, 22, 23) Vurugu zilizotokea zilitokana na suala la ufufuo, imani katika Yesu na ufufuo wake.

      15 Kama Paulo alivyofanya, tunaweza kutoa ushahidi kwa ujasiri, nasi tunaweza kutiwa moyo na maneno ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu. Lakini yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” Je, tunapaswa kuhangaikia tutakalosema? Hapana, kwa kuwa Yesu alitoa uhakikisho huu: “Watakapokuwa wakiwapeleka kuwashtaki, msihangaike kuhusu jambo mtakalosema; bali semeni jambo mtakalopewa saa hiyo, kwa maana si ninyi mnaosema, bali ni roho takatifu.”​—Marko 13:9-13.

      “Feliksi Akaogopa” (Mdo. 24:22-27)

      16, 17. (a) Feliksi alishughulikia jinsi gani kesi ya Paulo? (b) Huenda ni kwa nini Feliksi aliogopa, hata hivyo ni kwa nini aliendelea kukutana na Paulo?

      16 Hiyo haikuwa mara ya kwanza Gavana Feliksi kusikia kuhusu imani ya Kikristo. Masimulizi hayo yanasema: “Feliksi, akiwa anajua vizuri ukweli kuhusu Njia hii [jina lililotumiwa kufafanua Ukristo wa mapema], akaahirisha kesi yao kwa kusema: ‘Lisia kamanda wa jeshi atakapokuja, nitaamua mambo haya yanayowahusu.’ Naye akamwagiza ofisa wa jeshi kwamba mtu huyo awekwe chini ya kizuizi lakini apewe uhuru fulani, na watu wake waruhusiwe kumhudumia.”​—Mdo. 24:22, 23.

      17 Siku kadhaa baadaye, Feliksi na mke wake Myahudi, Drusila, waliwatuma watu wamwite Paulo ili ‘wamsikilize akizungumza kuhusu imani katika Kristo Yesu.’ (Mdo. 24:24) Hata hivyo, Paulo alipozungumzia “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja, Feliksi akaogopa,” huenda kwa sababu dhamiri yake ilimsumbua kwa kuwa alijua anaishi maisha mapotovu. Kwa hiyo akamruhusu Paulo aondoke na kumwambia: “Kwa sasa unaweza kwenda, lakini nitakapopata nafasi nitakuita tena.” Baada ya hapo Feliksi alikutana na Paulo mara nyingi, si kwa sababu alitaka kujua kweli, lakini kwa sababu alitumaini kwamba Paulo atampa rushwa.​—Mdo. 24:25, 26.

      18. Kwa nini Paulo alizungumza na Feliksi na mke wake kuhusu “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja”?

      18 Kwa nini Paulo alizungumza na Feliksi na mke wake kuhusu “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja”? Kumbuka, walitaka kujua “imani katika Kristo Yesu” inahusisha nini. Kwa kuwa Paulo alijua kwamba walikuwa wakiishi maisha mapotovu, walikuwa wakatili, na wasiotenda haki, aliwaonyesha wazi kinachohitajika ili kuwa wafuasi wa Yesu. Mambo ambayo Paulo alisema yalionyesha tofauti kubwa kati ya viwango vya Mungu vya uadilifu na mwenendo wa Feliksi na mke wake. Hayo yangewasaidia kuona kwamba wanadamu wote wanawajibika mbele ya Mungu kuhusu wanavyofikiri, kusema, na kutenda na kwamba jambo muhimu zaidi kuliko hukumu ambayo Paulo anakabili ni hukumu watakayokabili mbele za Mungu. Ndiyo sababu Feliksi ‘aliogopa’!

      19, 20. (a) Tunapohubiri, tunapaswa kushughulika jinsi gani na watu wanaoonekana kana kwamba wanapendezwa na kweli, lakini wana sababu za kibinafsi? (b) Tunajuaje kwamba Feliksi hakuwa rafiki ya Paulo?

      19 Tunapohubiri, huenda tukawapata watu walio kama Feliksi. Mwanzoni wanaweza kuonekana wanapendezwa na kweli, lakini labda wakawa na sababu za kibinafsi. Tunapaswa kuwa waangalifu tunaposhughulika nao. Hata hivyo, kama Paulo alivyofanya, tunaweza kutumia busara kuwaambia kuhusu viwango vya Mungu vya uadilifu. Huenda kweli ikagusa mioyo yao. Lakini, tukiona wazi kwamba hawana nia ya kuacha njia zao mbaya, tunawaacha na kutafuta wale wanaoitafuta sana kweli.

      20 Nia ya Feliksi inaonekana wazi kutokana na maneno haya: “Miaka miwili ilipokwisha, Porkio Festo alichukua nafasi ya Feliksi; na kwa sababu Feliksi alitamani kukubaliwa na Wayahudi, akamwacha Paulo akiwa amefungwa.” (Mdo. 24:27) Feliksi hakuwa rafiki wa kweli wa Paulo. Feliksi alijua kwamba wafuasi wa “Ile Njia” hawakuwa wachochezi wala wafanya mapinduzi. (Mdo. 19:23) Pia, alijua kwamba Paulo hakuwa amevunja sheria yoyote ya Roma. Hata hivyo, Feliksi alimtia mtume huyo kifungoni ili ‘akubaliwe na Wayahudi.’

      21. Ni nini kilichompata Paulo baada ya Porkio Festo kuwa gavana, na ni nini kilichoendelea kumwimarisha Paulo?

      21 Kama tunavyoona katika mstari wa mwisho wa Matendo sura ya 24, bado Paulo alikuwa gerezani Porkio Festo alipoanza kutawala baada ya Feliksi. Kukawa na mfululizo wa kesi, naye Paulo akapelekwa kutoka kwa ofisa mmoja hadi mwingine. Kwa kweli, mtume huyo mwenye ujasiri ‘alipelekwa mbele ya wafalme na magavana.’ (Luka 21:12) Kama tutakavyoona, baadaye alitoa ushahidi mbele ya mtawala mwenye nguvu zaidi wa siku zake. Wakati wote huo, imani ya Paulo haikuyumba kamwe. Bila shaka, aliendelea kuimarishwa na maneno ya Yesu: “Jipe moyo!”

      FELIKSI—GAVANA WA MKOA WA YUDEA

      Mwaka wa 52 hivi W.K., Klaudio, Maliki Mroma, alimchagua rafiki yake, Antonio Feliksi, kuwa gavana katika mkoa wa Yudea. Kama ndugu yake Pala, Feliksi alikuwa mtumwa wa familia ya maliki, aliyewekwa huru. Halikuwa jambo la kawaida kwa mtu ambaye awali alikuwa mtumwa kuwekwa kuwa gavana, na amiri jeshi.

      Felix.

      Kwa sababu ndugu yake alikuwa na ushawishi mkubwa kwa maliki, Feliksi “aliona kwamba angeweza kufanya uovu wowote bila kuadhibiwa,” asema Tasito, mwanahistoria Mroma. Akiwa gavana, Feliksi “alikuwa mkatili na mwenye tamaa sana, na ingawa alikuwa na mamlaka ya kifalme, alijiendesha kama mtumwa, bila ustaarabu.” Alipokuwa gavana, Feliksi alimwoa Drusila, binti ya Herode Agripa wa Kwanza, baada ya kumshawishi amuache mume wake. Feliksi alimtendea mtume Paulo kwa ufisadi na isivyo halali, akitaka Paulo ampe hongo.

      Utawala wa Feliksi ulikuwa na ufisadi mwingi sana na wenye kukandamiza hivi kwamba Maliki Nero alimuamuru arudi Roma mwaka wa 58 W.K. Kikundi kidogo cha Wayahudi kilimfuata Feliksi kwenda Roma ili kumshtaki kwa sababu ya utawala wake mbovu, hata hivyo, inasemekana kwamba ndugu yake, Pala, alimwokoa asiadhibiwe.

      a Ona sanduku lenye kichwa, “Feliksi—Gavana wa Mkoa wa Yudea.”

      b Tertulo alimshukuru Feliksi kwa “amani nyingi” aliyoileta katika taifa hilo. Hata hivyo, ukweli ni kwamba amani iliyokuwa Yudea Feliksi akiwa gavana, ilikuwa ndogo ukilinganisha na amani nyingi iliyokuwako wakati wa wale magavana wengine waliotangulia mpaka uasi dhidi ya Roma ulipotokea. Pia, hakusema kweli alipotaja kwamba Wayahudi walitoa “shukrani nyingi sana” kwa marekebisho ambayo Feliksi alikuwa amefanya. Ukweli ni kwamba Wayahudi wengi walimchukia Feliksi kwa sababu ya kuwakandamiza na kuwatendea kikatili walipoasi.​—Mdo. 24:2, 3.

  • “Ninakata Rufaa kwa Kaisari!”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 25

      “Ninakata Rufaa kwa Kaisari!”

      Paulo aweka kielelezo katika kuitetea habari njema

      Matendo 25:1–26:32

      1, 2. (a) Paulo anajikuta katika hali gani? (b) Rufaa ya Paulo kwa Kaisari inatokeza swali gani?

      PAULO bado yuko chini ya ulinzi mkali jijini Kaisaria. Miaka miwili mapema alipokuwa amerudi Yudea, siku chache tu baada ya kufika kwake Wayahudi walijaribu kumuua mara tatu hivi. (Mdo. 21:27-36; 23:10, 12-15, 27) Kufikia sasa, adui zake hawajafanikiwa, hata hivyo, hawakati tamaa. Paulo anapoona kwamba huenda akakabidhiwa mikononi mwao, anamwambia Festo, Gavana Mroma: “Ninakata rufaa kwa Kaisari!”​—Mdo. 25:11.

      2 Je, Yehova aliunga mkono uamuzi wa Paulo wa kukata rufaa kwa maliki wa Roma? Jibu la swali hilo ni muhimu kwetu leo, sisi tunaotoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu. Tunahitaji kujua ikiwa tunaweza kuiga mfano wa Paulo “katika kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”​—Flp. 1:7.

      “Nimesimama Mbele ya Kiti cha Hukumu” (Mdo. 25:1-12)

      3, 4. (a) Kwa nini Wayahudi wanaomba Paulo apelekwe Yerusalemu, naye anaepuka kifo jinsi gani? (b) Kama alivyomtegemeza Paulo, Yehova huwategemeza jinsi gani watumishi wake leo?

      3 Siku tatu baada ya kuteuliwa, Festo, gavana mpya wa Roma katika mkoa wa Yudea, anaenda Yerusalemu.a Akiwa huko, anawasikiliza wakuu wa makuhani na wakuu kati ya Wayahudi wakitoa mashtaka mazito dhidi ya Paulo. Wanajua kwamba gavana huyo mpya anataka sana kudumisha amani kati yake nao na Wayahudi wengine wote. Kwa hiyo wanamwomba Festo ampeleke Paulo Yerusalemu, na kumhukumu huko. Hata hivyo, adui hao walikuwa wamepanga njama ya kumuua Paulo akiwa njiani kutoka Kaisaria kwenda Yerusalemu. Festo akataa ombi lao na kusema: “Wale walio na mamlaka kati yenu washuke pamoja nami [mpaka Kaisaria] na kumshtaki, ikiwa kwa kweli mtu huyu amefanya kosa lolote.” (Mdo. 25:5) Hivyo, kwa mara nyingine tena, Paulo anaepuka kifo.

      4 Katika kesi zote za Paulo, Yehova alimtegemeza kupitia Bwana Yesu Kristo. Kumbuka kwamba katika maono, Yesu alimwambia mtume wake: “Jipe moyo!” (Mdo. 23:11) Leo, watumishi wa Mungu hukabili upinzani na vitisho. Yehova hatulindi kutokana na kila tatizo, lakini hutupatia hekima na nguvu za kuvumilia. Sikuzote tunaweza kutegemea “nguvu zinazopita zile za kawaida” ambazo Mungu wetu mwenye upendo hutoa.​—2 Kor. 4:7.

      5. Festo alishughulikiaje kesi ya Paulo?

      5 Siku kadhaa baadaye, Festo “akaketi kwenye kiti cha hukumu” jijini Kaisaria.b Paulo na wanaomshitaki walikuwa wamesimama mbele yake. Akijibu mashtaka yao yasiyo na msingi, Paulo akasema: “Sijatenda dhambi yoyote dhidi ya Sheria ya Wayahudi wala dhidi ya hekalu wala dhidi ya Kaisari.” Mtume huyo hakuwa na hatia na alistahili kuachiliwa huru. Festo atatoa uamuzi gani? Akitamani kukubaliwa na Wayahudi, anamuuliza Paulo: “Je, ungependa kupanda kwenda Yerusalemu ukahukumiwe huko mbele yangu kuhusu mambo haya?” (Mdo. 25:6-9) Pendekezo la kipumbavu sana. Ikiwa Paulo angerudishwa Yerusalemu, watu wanaomshtaki ndio ambao wangemhukumu, na bila shaka angeuawa. Katika kisa hiki, Festo alikuwa akihangaikia manufaa yake ya kisiasa badala ya kuzingatia haki. Pontio Pilato, gavana aliyemtangulia, alitenda vivyo hivyo katika kesi iliyomhusu Yesu. (Yoh. 19:12-16) Leo pia, huenda mahakimu wakatenda isivyo haki ili kuwapendeza wanasiasa. Kwa hiyo, tusishangae mahakama zinapotoa uamuzi usiopatana hata kidogo na ushahidi uliotolewa katika kesi zinazowahusu watu wa Mungu.

      6, 7. Kwa nini Paulo alikata rufaa kwa Kaisari, naye aliwawekea Wakristo wa kweli leo mfano gani?

      6 Tamaa ya Festo ya kuwapendeza Wayahudi ingeweza kufanya Paulo auawe. Kwa hiyo, Paulo akatumia haki yake akiwa raia wa Roma. Alimwambia Festo: “Mimi nimesimama mbele ya kiti cha hukumu cha Kaisari, ambapo ninapaswa kuhukumiwa. Sijawakosea Wayahudi, nawe pia umegundua jambo hilo. . . . Ninakata rufaa kwa Kaisari!” Baada ya rufaa kukatwa, lazima ingesikilizwa. Festo alikazia hilo kwa kusema: “Umekata rufaa kwa Kaisari; nawe utaenda kwa Kaisari.” (Mdo. 25:10-12) Paulo aliwawekea Wakristo wa kweli leo mfano wa kuiga. Wapinzani wanapojaribu kutunga “matatizo kwa kutumia sheria,” Mashahidi wa Yehova hutumia maandalizi ya kisheria yaliyopo ili kuitetea habari njema.c—Zab. 94:20.

      7 Hivyo, baada ya kufungwa kwa zaidi ya miaka miwili kwa sababu ya makosa ambayo hakuwa amefanya, Paulo alipewa nafasi ya kujitetea jijini Roma. Hata hivyo, kabla ya kuondoka, mtawala mwingine alitaka kumwona.

      Watu wakiwa mahakamani baada ya hukumu kutolewa. Ndugu, wanasheria wake, na Mashahidi wengine walio mahakamani wakiwa wamevunjika moyo. Watu wasio Mashahidi wana furaha na wanawapongeza wanasheria walioshinda kesi dhidi ya ndugu.

      Tunapohukumiwa isivyofaa, tunakata rufaa

      “Sikukosa Kutii” (Mdo. 25:13–26:23)

      8, 9. Kwa nini Mfalme Agripa alienda Kaisaria?

      8 Siku kadhaa baada ya Paulo kumwambia Festo kwamba anakata rufaa kwa Kaisari, Mfalme Agripa na dada yake, Bernike walifika kwa “ziara ya kumsalimia” gavana huyo mpya.d Katika siku za Waroma, ilikuwa kawaida kwa maofisa kuwatembelea magavana wapya. Kwa kumpongeza Festo, ni wazi kwamba Agripa alikuwa akijaribu kujenga urafiki wa kibinafsi na kisiasa kati yao kwa ajili ya wakati ujao.​—Mdo. 25:13.

      KUKATA RUFAA KWA AJILI YA IBADA YA KWELI LEO

      Nyakati nyingine, Mashahidi wa Yehova wamekata rufaa katika mahakama kuu wakitumaini vizuizi viondolewe ili waendelee kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Fikiria mifano miwili ifuatayo:

      Mnamo Machi 28, 1938, Mahakama Kuu ya Marekani ilibatilisha maamuzi ya mahakama ya jimbo na kuondolea hatia kikundi cha Mashahidi waliokuwa wamekamatwa kwa sababu ya kugawa vitabu na magazeti ya Biblia jijini Griffin, katika jimbo la Georgia, nchini Marekani. Rufaa hiyo ilikuwa ya kwanza kati ya nyingi zilizokatwa katika mahakama hiyo kuu kuhusu haki ya Mashahidi ya kuhubiri habari njema.g

      Kesi nyingine ilimhusu Shahidi mmoja nchini Ugiriki, Minos Kokkinakis. Katika kipindi cha miaka 48, alikamatwa zaidi ya mara 60 akishtakiwa kwa kosa la “kugeuza imani ya watu.” Alifikishwa mahakamani mara 18. Alifungwa gerezani kwa miaka mingi naye alipelekwa uhamishoni katika visiwa vya mbali katika Bahari ya Aegea. Mara ya mwisho aliposhtakiwa, mnamo mwaka wa 1986, mahakama kuu za Ugiriki zilimhukumia hatia Ndugu Kokkinakis. Kisha akatafuta msaada kupitia Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR). Mnamo Mei 25, 1993, Mahakama hiyo ilifikia uamuzi kwamba nchi ya Ugiriki imekiuka uhuru wa kuabudu wa Ndugu Kokkinakis.

      Mashahidi wa Yehova wamekata rufaa katika Mahakama Kuu ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu katika kesi mbalimbali, nao wamepata ushindi katika kesi nyingi. Hakuna tengenezo lingine lolote, la kidini au lingine lolote, ambalo limefanikiwa kiasi hicho katika kutetea haki za msingi za kibinadamu mbele za Mahakama hiyo.

      Je, wengine hunufaika kutokana na ushindi huo wa Mashahidi wa Yehova? Msomi Charles C. Haynes aliandika: “Sote tunapaswa kuwashukuru Mashahidi wa Yehova. Haidhuru ni mara ngapi wanatukanwa, wanafukuzwa mjini, au kupigwa, wao huendelea kupigania uhuru wao wa dini (na wetu pia). Na wanaposhinda, sote tunashinda.”

      g Ona simulizi la uamuzi wa Mahakama Kuu ya Marekani kuhusu uhuru wa kusema, katika gazeti la Amkeni! la Januari 8, 2003, ukurasa wa 3-11.

      9 Festo alimwambia mfalme kumhusu Paulo, naye Agripa akataka kumwona. Siku iliyofuata, watawala hao wawili wakaketi juu ya kiti cha hukumu. Hata hivyo, jambo la kuvutia zaidi lilikuwa maneno ya mfungwa aliyekuwa mbele yao wala si nguvu au fahari yao.​—Mdo. 25:22-27.

      10, 11. Paulo alimwonyesha Agripa heshima kwa njia gani, na Paulo alimwambia nini mfalme kuhusu maisha yake ya awali?

      10 Paulo alimshukuru kwa heshima Mfalme Agripa kwa kumpa nafasi ya kujitetea, akikiri kwamba mfalme ana ujuzi juu ya desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kisha, Paulo akasimulia maisha yake ya wakati uliopita: “Niliishi nikiwa Farisayo kulingana na madhehebu yetu yenye msimamo mkali zaidi katika ibada yetu.” (Mdo. 26:5) Akiwa Farisayo, Paulo alitazamia kuja kwa Masihi. Sasa akiwa Mkristo, alimtambulisha kwa ujasiri Yesu Kristo kuwa yule aliyekuwa akisubiriwa kwa muda mrefu. Paulo alishtakiwa kwa sababu ya jambo ambalo yeye na wale waliokuwa wakimshtaki waliamini, lile tumaini la ahadi ya Mungu kwa mababu zao. Maelezo ya Paulo yalimchochea Agripa atake kusikia zaidi.e

      11 Akikumbuka jinsi alivyokuwa akiwatendea Wakristo kwa ukatili hapo awali, Paulo alisema: “Mimi niliamini kwamba ninapaswa kufanya matendo mengi ili kulipinga jina la Yesu Mnazareti . . . kwa sababu nilikuwa nimewakasirikia sana [wafuasi wa Kristo], nilifikia hatua ya kuwatesa hata katika majiji yaliyo mbali.” (Mdo. 26:9-11) Paulo hakuwa akitia chumvi. Watu wengi walijua jinsi alivyokuwa amewatendea Wakristo kwa ujeuri. (Gal. 1:13, 23) Huenda Agripa alitaka kujua: ‘Ni nini kilichombadili mtu huyu?’

      12, 13. (a) Paulo alieleza jinsi gani kugeuzwa kwake? (b) Ni kwa njia gani Paulo alikuwa ‘akiipiga teke michokoo’?

      12 Maneno yafuatayo ya Paulo yanatoa jibu: “Nikiwa safarini kwenda Damasko pia nikiwa na mamlaka na maagizo kutoka kwa wakuu wa makuhani, katikati ya mchana niliona barabarani, ewe Mfalme, nuru kutoka mbinguni inayozidi mwangaza wa jua ikimulika kunizunguka mimi na wale waliokuwa wakisafiri pamoja nami. Sisi sote tulipoanguka chini, nikasikia sauti ikiniambia katika lugha ya Kiebrania: ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa? Kuendelea kuipiga teke michokoo kunafanya iwe vigumu kwako.’ Lakini nikauliza: ‘Wewe ni nani Bwana?’ Naye Bwana akajibu: ‘Mimi ni Yesu, ambaye unamtesa.’”f—Mdo. 26:12-15.

      13 Kabla ya tukio hilo lisilo la kawaida, Paulo alikuwa ‘akiipiga teke michokoo.’ Kama vile mnyama wa kubeba mizigo angejiumiza kwa kupiga teke sehemu yenye ncha kali ya mchokoo, Paulo alijiumiza kiroho kwa kupinga mapenzi ya Mungu. Kwa kumtokea Paulo barabarani alipokuwa akielekea Damasko, Yesu aliyekuwa amefufuliwa alimchochea mtu huyo mnyoofu aliyetenda bila kujua, abadili maoni yake.​—Yoh. 16:1, 2.

      14, 15. Paulo alisema nini kuhusu mabadiliko aliyokuwa amefanya maishani?

      14 Bila shaka Paulo alifanya mabadiliko makubwa maishani. Alimwambia Agripa: “Mimi sikukosa kutii maono hayo kutoka mbinguni, lakini kwanza kwa wale walio huko Damasko kisha kwa wale walio Yerusalemu, na katika nchi yote ya Yudea, na pia kwa mataifa, nilikuwa nikipeleka ujumbe kwamba wanapaswa kutubu na kumgeukia Mungu kwa kufanya matendo yanayoonyesha toba.” (Mdo. 26:19, 20) Kwa miaka mingi, Paulo alikuwa akitimiza mgawo ambao Yesu Kristo alimpatia katika maono hayo aliyopata katikati ya mchana. Alipata matokeo gani? Waliokubali habari njema aliyohubiri Paulo, walitubu mwenendo wao mpotovu na usio mnyoofu, kisha wakamgeukia Mungu. Watu hao wakawa raia wazuri, wanaoheshimu sheria na mamlaka.

      15 Hata hivyo, matokeo hayo hayakuwa na maana yoyote kwa Wayahudi waliompinga Paulo. Paulo alisema hivi: “Hiyo ndiyo sababu Wayahudi walinikamata hekaluni na kujaribu kuniua. Hata hivyo, kwa sababu nimepata msaada kutoka kwa Mungu, mpaka leo hii ninaendelea kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia.”​—Mdo. 26:21, 22.

      16. Tunaweza kumwigaje Paulo tunapozungumza na mahakimu na watawala kuhusu imani yetu?

      16 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunapaswa ‘sikuzote kuwa tayari kuitetea’ imani yetu. (1 Pet. 3:15) Tunapozungumza na mahakimu na watawala kuhusu imani yetu, huenda ikafaa kuiga njia ambayo Paulo alitumia alipokuwa akizungumza na Agripa na Festo. Kwa kuwaeleza kwa heshima jinsi kweli za Biblia zimebadili maisha ya watu—yetu wenyewe na ya wale ambao wamekubali ujumbe wetu—huenda tukagusa mioyo ya watu hao wenye mamlaka.

      “Ungenishawishi Niwe Mkristo” (Mdo. 26:24-32)

      17. Baada ya kumsikiliza Paulo, Festo alisema nini, na ni mtazamo gani kama huo unaoonekana leo?

      17 Walipokuwa wakisikiliza ushahidi wenye kusadikisha wa Paulo, watawala hao wawili walichochewa sana. Ona jinsi mambo yalivyokuwa: “Paulo alipokuwa akijitetea kwa kusema mambo hayo, Festo akasema kwa sauti kubwa: ‘Unarukwa na akili, Paulo! Kusoma kwingi kunafanya urukwe na akili!’” (Mdo. 26:24) Huenda maneno ya Festo yanalingana sana na mtazamo unaoonekana leo. Machoni mwa wengi, wale wanaofundisha kweli za Biblia wamerukwa na akili. Wenye hekima ya ulimwengu huona vigumu kukubali fundisho la Biblia kuhusu ufufuo wa wafu.

      18. Paulo alimjibuje Festo, na hilo lilimfanya Agripa aseme nini?

      18 Hata hivyo, Paulo alimjibu gavana huyo: “Mimi sirukwi na akili, ewe Mtukufu Festo, bali ninasema maneno ya kweli na ya akili timamu. Kwa kweli, mfalme ninayezungumza naye kwa uhuru anajua vizuri mambo haya . . . Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii? Ninajua unawaamini.” Agripa akamwambia Paulo: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” (Mdo. 26:25-28) Maneno hayo, yawe yalitoka moyoni au la, yanaonyesha kwamba ushahidi wa Paulo ulikuwa na matokeo makubwa kwa mfalme.

      19. Festo na Agripa walifikia mkataa gani kuhusu Paulo?

      19 Kisha Agripa na Festo wakasimama, kuonyesha kwamba mahojiano yamefikia mwisho. “Walipokuwa wakiondoka wakaanza kuambiana: ‘Mtu huyu hafanyi lolote linalostahili kifo au vifungo vya gereza.’ Kisha Agripa akamwambia Festo: ‘Mtu huyu angefunguliwa kama hangekuwa amekata rufaa kwa Kaisari.’” (Mdo. 26:31, 32) Walijua kwamba mtu aliyesimama mbele yao hakuwa na hatia. Huenda tangu wakati huo na kuendelea wangekuwa na maoni yanayofaa kuhusu Wakristo.

      20. Ushahidi ambao Paulo alitoa mbele ya watu wenye mamlaka ulikuwa na matokeo gani?

      20 Hakuna yeyote kati ya watawala hao wawili wenye nguvu aliyekubali habari njema ya Ufalme wa Mungu. Je, kulikuwa na manufaa yoyote kwa Paulo kujitetea mbele ya watu hao? Ndiyo. Kwa kuwa Paulo ‘alipelekwa mbele ya wafalme na magavana’ huko Yudea, habari njema iliwafikia maofisa Waroma ambao huenda hawangehubiriwa kamwe. (Luka 21:12, 13) Pia, mambo yaliyompata na uaminifu wake chini ya majaribu yaliwatia moyo ndugu na dada zake Wakristo.​—Flp. 1:12-14.

      21. Tunaweza kupata matokeo gani mazuri tukiendelea na kazi yetu ya Ufalme?

      21 Ndivyo ilivyo leo. Tukiendelea na kazi ya Ufalme licha ya majaribu na upinzani, tunaweza kupata matokeo mazuri. Huenda tukawahubiria maofisa ambao hawapatikani kwa urahisi. Kuvumilia kwetu kwa uaminifu kunaweza kuwatia moyo ndugu na dada zetu Wakristo na kuwachochea wawe na ujasiri zaidi katika kazi ya kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu.

      PORKIO FESTO—GAVANA WA ROMA KATIKA MKOA WA YUDEA

      Habari kumhusu Porkio Festo, zinapatikana tu katika kitabu cha Matendo ya Mitume na maandishi ya Flavio Yosefo. Festo aliwekwa kuwa gavana wa Yudea baada ya Feliksi, mwaka wa 58 hivi W.K., na huenda alikufa akiwa gavana baada ya kutawala kwa miaka miwili au mitatu tu.

      Porkio Festo.

      Kwa ujumla, yaonekana Festo alikuwa gavana mwenye busara na uwezo, tofauti na Feliksi, gavana aliyemtangulia, na pia Albino, gavana aliyemfuata. Mwanzoni mwa utawala wa Festo, kulikuwa na wezi wengi Yudea. Yosefo alisema: “Festo . . . aliazimia kuwaadhibu wale waliosababisha usumbufu nchini. Hivyo, alikamata wezi wengi na wengi wao aliwaua.” Wakati wa utawala wake, Wayahudi walijenga ukuta ili kumzuia Mfalme Agripa asione kilichokuwa kikiendelea katika eneo la hekalu. Mwanzoni, Festo aliamuru ukuta huo ubomolewe. Hata hivyo, Wayahudi walipomwomba asiubomoe, aliwaruhusu wawasilishe ombi hilo kwa Nero, Maliki wa Roma.

      Inaonekana Festo alichukua hatua kali dhidi ya wahalifu na waasi. Hata hivyo, ili kuwafurahisha Wayahudi, alikuwa tayari kutotenda kwa haki—hasa aliposhughulika na mtume Paulo.

      MFALME HERODE AGRIPA WA PILI

      Agripa anayezungumziwa katika Matendo sura ya 25 ni Mfalme Herode Agripa wa Pili, mwana wa mjukuu wa Herode Mkuu na mwana wa Herode ambaye alikuwa ameshambulia kutaniko la Yerusalemu miaka 14 iliyopita. (Mdo. 12:1) Agripa alikuwa wa mwisho katika ukoo wa wana wa Herode.

      Mfalme Herode Agripa wa Pili.

      Baba yake alipokufa mwaka wa 44 W.K., Agripa alikuwa na umri wa miaka 17 naye alikuwa Roma, akisoma katika makao ya Maliki Mroma, Klaudio. Washauri wa maliki walimwona Agripa kuwa mchanga sana asiweze kumrithi baba yake; hivyo, gavana Mroma akachaguliwa badala yake. Hata hivyo, kulingana na Flavio Yosefo, Agripa akiwa bado Roma, aliendelea kuwasaidia Wayahudi na kutetea haki zao.

      Mwaka wa 50 W.K., Klaudio alimweka Agripa kuwa mtawala wa Chalcis na mwaka wa 53 W.K., akampa mamlaka juu ya Iturea, Trakoniti, na Abilene. Pia, Agripa alipewa wadhifa wa kusimamia hekalu la Yerusalemu, naye alikuwa na mamlaka ya kuwateua makuhani wakuu wa Wayahudi. Nero, aliyetawala baada ya Klaudio alipanua eneo la utawala wa Agripa likatia ndani sehemu za Galilaya na Perea. Alipokutana na Paulo, Agripa alikuwa Kaisaria pamoja na dada yake Bernike, aliyekuwa amemwacha mume wake, mfalme wa Kilikia.​—Mdo. 25:13.

      Mwaka wa 66 W.K., Agripa aliposhindwa kuzuia uasi wa Wayahudi dhidi ya Roma, aliamua kujiunga na Waroma kwa kuwa waasi hao walitaka kumshambulia. Baada ya kuzuia uasi wa Wayahudi, maliki mpya, Vaspasiani, alimshukuru Agripa kwa kumwongezea maeneo ya utawala.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Porkio Festo—Gavana wa Roma Katika Mkoa wa Yudea.”

      b “Kiti cha hukumu” ni kiti kilichokuwa juu ya jukwaa lililoinuliwa. Kwa kuwa kiti hicho kilikuwa juu, basi ilionekana kana kwamba uamuzi wa hakimu unapaswa kuheshimiwa na hauwezi kupingwa. Pilato aliketi juu ya kiti hicho aliposikiliza kesi ya Yesu.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Kukata Rufaa kwa Ajili ya Ibada ya Kweli Leo.”

      d Ona sanduku lenye kichwa “Mfalme Herode Agripa wa Pili.”

      e Akiwa Mkristo, Paulo aliamini kwamba Yesu ndiye Masihi. Wayahudi, waliomkataa Yesu, walimwona Paulo kuwa mwasi imani.​—Mdo. 21:21, 27, 28.

      f Kuhusu kusafiri kwa Paulo “katikati ya mchana,” msomi mmoja wa Biblia anasema hivi: “Isipokuwa iwe kwamba msafiri alikuwa na jambo la dharura sana, alipumzika mchana wakati ambao joto lilikuwa kali sana. Hivyo, Paulo alifanya jitihada nyingi sana ili kuwatesa Wakristo.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki