-
“Kuna Uzuri Upande wa Mkono Wako wa Kuume Milele”Mnara wa Mlinzi—2012 | Machi 15
-
-
TWAFANYA UPAINIA
Mwaka mmoja baadaye, mnamo 1959, tulikuwa tukifanya upainia na kuishi kwenye mlima fulani huko Saskatchewan katika nyumba ndogo inayokokotwa na gari. Ungeweza kuona mbali sana, na baadhi ya sehemu hizo zilikuwa eneo letu.
Siku moja, tulipata barua yenye kufurahisha kutoka ofisi ya tawi. Nilienda haraka mahali ambapo John alikuwa akirekebisha trekta. Ilikuwa barua ya kutualika kuwa mapainia wa pekee huko Red Lake, Ontario. Kwa kuwa hatukujua eneo hilo, basi tulichukua haraka ramani na kutafuta eneo hilo.
Eneo hilo lilikuwa tofauti kama nini na nyanda pana zenye majani! Sasa tuliishi katika eneo lenye misitu mikubwa na miji midogo iliyojengwa karibu na machimbo ya dhahabu. Siku ya kwanza tulipokuwa tukitafuta mahali pa kulala, msichana mdogo alisikia tulipokuwa tukizungumza na jirani yao. Msichana huyo alikimbia nyumbani kumwambia mama yake tulikuwa tukitafuta mahali pa kulala. Mama huyo alitukaribisha kwa fadhili tulale kwao usiku huo. Kitanda tulicholalia kilikuwa katika nyumba ndogo ya udongo. Siku iliyofuata, tulipata mahali pa kuishi, nyumba yenye vyumba viwili iliyojengwa kwa magogo ambayo haikuwa na mabomba ya maji wala fanicha, ilikuwa tu na jiko la mabati lililotumia kuni. Tulipata vitu vingine vichache katika duka linalouza vitu vilivyotumiwa na punde si punde tulikuwa na vitu vingi tulivyohitaji.
Hakukuwa na kutaniko umbali wa kilomita 209. Wafanyakazi wengi katika machimbo ya dhahabu walitoka Ulaya, na walituuliza ikiwa tungeweza kuwapelekea Biblia katika lugha yao. Baada ya muda mfupi, tulikuwa na mafunzo 30 mazuri sana ya Biblia. Katika muda wa miezi sita, kutaniko dogo lilianzishwa.
Mume wa mwanamke fulani ambaye tulijifunza naye Biblia alimpigia kasisi wao simu na kumwambia aje kumrekebisha mke wake. Wakati wa makabiliano hayo, kasisi huyo alisema kwamba kati ya mambo mengine, tunapaswa kuwafundisha watu kuhusu Utatu. Mwanamke huyo alichukua Biblia yao ya Kikatoliki na kumwomba kasisi huyo athibitishe mambo aliyokuwa akisema. Kasisi huyo aliitupa kwa nguvu Biblia hiyo mezani, akisema kwamba hakuhitaji kuthibitisha jambo lolote. Alipokuwa akiondoka, kasisi huyo alisema katika Kiukrainia kwamba tunapaswa kufukuzwa kutoka katika nyumba hiyo na tusiruhusiwe kamwe kurudi. Hakujua kwamba John alielewa Kiukrainia!
Muda mfupi baadaye, tuliondoka eneo la Red Lake kwa sababu John alipaswa kuzoezwa kuwa mwangalizi wa mzunguko. Hata hivyo, baada ya mwaka mmoja hivi, John alipokuwa akitoa hotuba ya ubatizo katika kusanyiko la wilaya, mume huyo alikuwa kati ya watu ambao walikuwa tayari kubatizwa! Yale makabiliano na kasisi yalimfanya aanze kuichunguza Biblia yeye mwenyewe.
-
-
“Kuna Uzuri Upande wa Mkono Wako wa Kuume Milele”Mnara wa Mlinzi—2012 | Machi 15
-
-
[Picha katika ukurasa wa 4]
Nilipokuwa painia wa pekee huko Red Lake, Ontario
-